Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 2/8 kur. 7-9
  • Kumtambua Mungu wa Pekee wa Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumtambua Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jina la Kumtambua
  • Je, Ni Yehova au Ni Yahweh?
  • Je, Kweli Ni Jambo la Maana?
  • Sifa za Mungu wa Kweli
  • Mungu wa Kweli Afunuliwa
  • Yehova
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Jina la Mungu—Maana Yalo na Linavyotamkwa
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Yehova Ni Nani?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Kwa Nini Tulitumie Jina la Mungu Ikiwa Hatujui Linavyopaswa Kutamkwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 2/8 kur. 7-9

Kumtambua Mungu wa Pekee wa Kweli

KARIBU muda wote wa kuwapo kwa wanadamu, wamekuwa na miungu mingi. Miungu hiyo imekuwa mingi sana hivi kwamba ni vigumu kutaja idadi kamili ya miungu na miungu ya kike ambayo imeabudiwa duniani pote—lakini inafikia mamilioni kadhaa.

Baada ya kuthibitisha kwamba kuna Mungu fulani, sasa twajiuliza, Kati ya miungu mingi ambayo imeabudiwa duniani pote sasa na wakati uliopita, ni yupi Mungu wa kweli? Jambo linaloonyesha kwamba kuna Mungu mmoja tu wa kweli anayeweza kutambuliwa linatajwa waziwazi katika Biblia kwenye Yohana 17:3: “Hii [yamaanisha] uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”

Jina la Kumtambua

Lingekuwa jambo la kufikiri kuzuri kwamba mungu yeyote aliye na utu angehitaji kuwa na jina la kibinafsi ili kumtambulisha na miungu mingine iliyo na majina yao. Ingekuwa afadhali jina hilo liwe limeteuliwa na mungu mwenyewe, badala ya jina lililotungwa na waabudu wake.

Hata hivyo, kuhusiana na habari hii, kuna jambo lenye kutatanisha. Ingawa dini nyingi zaidi zilizoimarishwa hupatia miungu yao majina ya kibinafsi, Wayahudi na makanisa makubwa-makubwa ya Jumuiya ya Wakristo yameshindwa kumtambulisha mungu wanayeabudu kwa jina la kibinafsi. Badala yake, wanatumia mitajo ya cheo kama vile Bwana, Mungu, Mweza Yote, na Baba.

Akiandika katika kichapo Theology, mwandishi David Clines alisema mambo yafuatayo: “Mahali fulani kati ya karne ya tano na ya pili K.W.K. Mungu alipatwa na aksidenti yenye kuhuzunisha: alipoteza jina lake. Kisahihi zaidi, Wayahudi waliacha kutumia jina la Mungu la kibinafsi Yahweh, na wakaanza kumrejezea Yahweh kwa kutumia maneno mbalimbali ya mkato: Mungu, Bwana, Jina, Aliye Mtakatifu, Kuwapo, hata Mahali. Hata mahali ambapo jina Yahweh lilionekana katika maandishi ya Kibiblia, wasomaji walitamka jina hilo kuwa Adonai. Hekalu lilipoanguka mara ya mwisho, hata katika pindi zilizokuwa nadra sana za kawaida za kidini ambapo jina hilo lilitumiwa ziliisha, na hata ujuzi wa kutamka jina hilo ukasahauliwa.” Hata hivyo, hakuna mtu awezaye kusema kwa uhakika ni wakati gani hasa Wayahudi wenye imani ya kidesturi walipoacha kutamka jina la Mungu kwa sauti na badala yake wakaanza kutumia maneno tofauti ya Kiebrania kwa Mungu na Bwana Mwenye Enzi Kuu.

Basi, inaonekana kwamba jambo muhimu la kwanza kabisa katika utafutaji wowote wa kutambua “Mungu wa pekee wa kweli” lingekuwa kumjua kwa jina. Utafutaji huo si mgumu hata kidogo, kwa kuwa jina la Mungu Mweza Yote, Muumba, linatajwa waziwazi na kwa njia sahili kwenye Zaburi 83:18: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.”

Je, Ni Yehova au Ni Yahweh?

Ingawa jina Yehova huonekana katika tafsiri ya King James Version na tafsiri nyinginezo za Biblia, wengine hupendelea kutumia jina Yahweh badala ya Yehova. Ni jina lipi lililo sahihi?

Hati za Biblia za kale zaidi ziliandikwa katika lugha ya Kiebrania. Katika Maandiko ya Kiebrania, jina la Mungu huonekana karibu mara 7,000 na linaandikwa kwa konsonanti nne—YHWH au JHVH. Maneno haya yenye konsonanti nne kwa kawaida huitwa Tetragramatoni, au Tetragramu, yanayotokana na maneno mawili ya Kigiriki yanayomaanisha “herufi nne.” Sasa swali linalohusu matamshi sahihi lazuka kwa sababu maandishi ya Kiebrania ya mapema yalikuwa na konsonanti bila vokali za kumwongoza msomaji. Hivyo, kama matamshi ya Tetragramatoni yatakuwa Yahweh au Yehova itategemea ni vokali zipi ambazo msomaji ataongezea kwenye konsonanti hizo nne. Leo, wasomi wengi wa lugha ya Kiebrania hupendelea Yahweh kuwa matamshi sahihi.

Hata hivyo, kwa ajili ya upatano ni afadhali kutumia Yehova. Katika njia gani? Matamshi Yehova yamekubaliwa katika lugha ya Kiswahili kwa miongo mingi. Wale wanaokataa kutumia matamshi haya wanapaswa pia kukataa kutumia matamshi yanayokubalika ya Yeremia na hata Yesu. Yeremia lingehitaji kubadilishwa kuwa Yir·meyahʹ au Yir·meyaʹhu, matamshi ya awali ya Kiebrania, na Yesu lingekuwa Ye·shuʹaʽ (Kiebrania) au I·e·sousʹ (Kigiriki). Kwa sababu hiyo, wanafunzi wengi wa Biblia, kutia ndani Mashahidi wa Yehova, huhisi kwamba upatano huunga mkono matumizi ya jina “Yehova” ambalo tayari linajulikana vizuri katika lugha ya Kiswahili na tafsiri yake katika lugha nyinginezo.

Je, Kweli Ni Jambo la Maana?

Huenda wengine wakabisha kwamba kwa kweli si jambo la maana kama unamtaja Mungu Mweza Yote kwa jina la kibinafsi au la, na wanaridhika kuzungumza juu ya Mungu na kumtaja kuwa Baba au kwa usahili tu kuwa Mungu. Hata hivyo, hayo maneno yote mawili ni majina ya cheo bali si majina na si ya kibinafsi wala ya kutofautisha. Katika nyakati za Biblia neno Mungu (Kiebrania, ʼElo·himʹ) lilitumiwa kufafanua mungu yeyote—hata mungu wa Wafilisti wapagani aliyeitwa Dagoni. (Waamuzi 16:23, 24) Hivyo, kwa Mwebrania kumwambia Mfilisti kwamba yeye, Mwebrania, anaabudu “Mungu” hakungemtambulisha Mungu wa kweli aliyeabudu.

Tunapendezwa na maelezo katika The Imperial Bible-Dictionary ya mwaka wa 1874: “Kila mahali mtajo [Yehova] ni jina halisi, likionyesha Mungu wa kibinafsi na yeye peke yake; ilhali Elohim kwa kiwango kikubwa ni nomino ya kawaida, ambayo kwa kawaida inaonyesha, kwa kweli, lakini si kwa lazima wala kwa upatano, Mkuu Kuliko Wote. . . . Mwebrania aweza kusema yule Elohim, Mungu wa kweli, katika kupinga miungu yote isiyo ya kweli; lakini hawezi kusema kamwe yule Yehova, kwa kuwa Yehova ni jina la Mungu wa kweli peke yake. Husema tena na tena Mungu wangu . . . ; lakini hasemi kamwe Yehova wangu, kwa kuwa asemapo Mungu wangu, humaanisha Yehova. Husema juu ya Mungu wa Israeli, lakini hasemi kamwe Yehova wa Israeli, kwa kuwa hakuna Yehova mwingine. Husema juu ya Mungu aishiye, lakini hasemi kamwe juu ya Yehova aishiye, kwa kuwa hawezi kudhania Yehova kuwa asiye hai.”

Sifa za Mungu wa Kweli

Bila shaka, kujua jina tu la mtu fulani, hakumaanishi kwamba tunamjua kwa undani. Wengi wetu tunajua majina ya wanasiasa mashuhuri. Hata twaweza kujua vizuri majina ya wanaume na wanawake mashuhuri katika nchi nyingine. Lakini kujua tu majina yao—hata namna ya kuyatamka ifaavyo—hakumaanishi tunawajua kibinafsi au kujua wao ni watu wa aina gani. Vivyo hivyo, ili kujua Mungu wa pekee wa kweli, tunahitaji kujua na kuthamini sifa zake.

Ingawa ni kweli kwamba wanadamu hawatapata kumwona Mungu wa kweli, kwa fadhili ameturekodia mambo mengi kuhusu utu wake katika Biblia. (Kutoka 33:20; Yohana 1:18) Manabii fulani Waebrania walionyeshwa maono yaliyopuliziwa ya ua wa kimbingu wa Mungu Mweza Yote. Wanayofafanua hayaonyeshi tu adhama kubwa na ukuu wenye kutisha na nguvu bali pia hali tulivu, utaratibu, uzuri, na hali yenye kupendeza.—Kutoka 24:9-11; Isaya 6:1; Ezekieli 1:26-28; Danieli 7:9; Ufunuo 4:1-3.

Yehova Mungu alimwonyesha Musa baadhi ya sifa zake zenye kuvutia na kupendeza, kama zilivyorekodiwa kwenye Kutoka 34:6, 7: “BWANA, BWANA, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi.” Je, hukubali kwamba kupata kujua juu ya sifa hizi za Mungu hutuvuta kwake na kutufanya tutake kujua mengi zaidi kumhusu akiwa mtu?

Ingawa hakuna mtu atakayepata kumwona Yehova Mungu katika utukufu wake wenye kung’aa, imerekodiwa kwamba wakati Yesu Kristo alipokuwa mwanadamu duniani, kwa kweli alidhihirisha utu wa Yehova Mungu, Baba yake wa kimbingu. Pindi moja Yesu alisema: “Mwana hawezi kufanya hata kitu kimoja kwa uanzisho wake mwenyewe, ila tu kile atazamacho Baba akifanya. Kwa maana mambo yoyote yale Huyo hufanya, mambo hayo Mwana pia hufanya kwa namna kama hiyo.”—Yohana 5:19.

Kwa hiyo, kutokana na ithibati iliyopo, tunaweza kufikia mkataa wa kwamba fadhili za Yesu, huruma, upole, na uchangamfu na vilevile upendo wake mkubwa kwa uadilifu na kuchukia uovu, hizo zote ni sifa ambazo Yesu aliona katika Baba yake, Yehova Mungu, wakati Yesu alipokuwa pamoja naye katika nyua za kimbingu kabla hajawa mwanadamu duniani. Hivyo, tunapomjua kikweli kwa kuelewa maana kamili ya jina Yehova, kwa hakika tuna sababu za kumpenda na kubariki jina hilo takatifu, kulisifu na kulihimidi, na kuliitibari.

Kumjua Mungu wa pekee wa kweli katika njia hii kwa kweli ni hatua isiyokoma, kama ionyeshwavyo waziwazi katika fasili ya Yohana 17:3 katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hapa, njeo sahihi ya kitenzi “kujua” inasaidia sana, kwa kuwa njeo ya wakati uliopo na yenye kuendelea inatumiwa badala ya njeo ya wakati uliopo tu. Kwa sababu hiyo twasoma: “Hii [yamaanisha] uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” Naam, kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu wa pekee wa kweli, Yehova, na Mwana wake, Yesu Kristo, ni hatua ambayo haipaswi kukoma.

Mungu wa Kweli Afunuliwa

Hivyo, Mungu wa kweli hutambulishwa kwa urahisi kutoka kwa miungu mingi isiyo ya kweli. Yeye ndiye Muumba mweza yote wa ulimwengu wote mzima, kutia ndani sayari Dunia na wanadamu walio juu yake. Ana jina la kibinafsi na la kipekee—Yehova, au Yahweh. Yeye si sehemu ya miungu watatu wa kifumbo, au Utatu. Yeye ni Mungu wa upendo, naye huwatakia mema tu uumbaji wake wa kibinadamu. Lakini pia yeye ni Mungu mwenye haki, na hatawavumilia milele wale wanaosisitiza kuiharibu dunia na kuchochea vita na jeuri.

Yehova amefunua azimio lake si la kuondoa tu uovu na kuteseka duniani, bali pia kuifanya iwe paradiso ambapo watu wenye kufuatia haki wanaweza kuishi milele kwa furaha. (Zaburi 37:10, 11, 29, 34) Sasa Mungu Mweza Yote amemtawaza Mwana wake, Yesu, kuwa Mfalme wa kimbingu wa Ufalme wa Mungu, na karibuni Yesu ataleta ulimwengu huo wenye uadilifu na kurudisha hali za Kiparadiso kwenye dunia yetu.—Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.

Tunatumaini kwamba sasa unaweza kujibu kwa urahisi swali hili, Je, kweli Mungu yuko? na kumtambua Mungu wa kweli.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yesu Kristo alimtambulisha Yehova kuwa Mungu wa pekee wa kweli

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki