Maoni ya Biblia
Je, Ni Kosa Kutamka Jina la Mungu?
KWA karne nyingi Dini ya Kiyahudi imefunza kwamba jina la Mungu, Yehova, ni takatifu sana kutamkwa.a (Zaburi 83:18) Wanatheolojia wengi wamesababu kwamba ni utovu wa heshima kumwita Muumba mwenye utukufu kwa njia hiyo ya kawaida na hata kwamba kufanya hivyo kunavunja amri ya tatu kati ya zile Amri Kumi, inayokataza ‘kulitaja bure jina la Bwana.’ (Kutoka 20:7) Katika karne ya tatu W.K., Mishnah ilitangaza kwamba “yule anayelitamka Jina la Mungu kama ambavyo limeandikwa” ni mtu ambaye “hana urithi katika ulimwengu ujao.”—Sanhedrini 10:1.
Kwa kupendeza, wasomi wengi katika Jumuiya ya Wakristo hufuata desturi hii ya Dini ya Kiyahudi wanapotafsiri Biblia. Kwa mfano, The New Oxford Annotated Bible husema hivi kwenye dibaji: “Tumizi la jina halisi lo lote kwa ajili ya Mungu mmoja na pekee, kana kwamba kulikuwako miungu mingine ambayo yeye alipaswa kujitofautisha nayo, liliachwa katika dini ya Kiyahudi kabla ya wakati wa Kikristo na halifai kabisa kwa imani ya Kanisa la Kikristo ya ulimwengu wote mzima.” Kwa hiyo, katika tafsiri hiyo neno “BWANA” limetumiwa badala ya jina la Mungu.
Mungu Ana Maoni Gani?
Lakini je, maoni ya watafsiri hao na wanatheolojia hao yanapatana na maoni ya Mungu? Mungu hakuchagua kuwaficha kamwe wanadamu jina lake; badala yake, aliwafunulia. Katika Maandiko ya Kiebrania ya Biblia, ambayo kwa kawaida huitwa Agano la Kale, jina la Mungu, Yehova, lapatikana zaidi ya mara 6,800. Rekodi ya Biblia huonyesha kwamba wale wanadamu wa kwanza wawili, Adamu na Hawa, walikuwa miongoni mwa wale waliolijua na kulitumia jina la Mungu. Hawa alipomzaa mwana wa kwanza, alisema: “Nimepata mtoto mwanamume kwa BWANA [“Yehova,” NW].”—Mwanzo 4:1.
Karne nyingi baadaye, Mungu alipomwita Musa aongoze taifa la Israeli kutoka utumwani Misri, Musa alimwuliza Mungu: “Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia, Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n’nani? niwaambie nini?” Huenda Musa alikuwa akifikiria iwapo Mungu angejijulisha kwa jina jingine jipya. Mungu akamwambia Musa: “Waambie wana wa Israeli maneno haya, BWANA [“Yehova,” NW], Mungu wa baba zenu, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu; hili ndilo jina langu hata milele, nalo ni kumbukumbu langu hata vizazi vyote.” (Kutoka 3:13, 15) Ni dhahiri kwamba Mungu wa kweli hakuhisi kuwa jina lake ni takatifu sana kwa watu wake kulitamka.
Kwa kweli, watumishi waaminifu wa Mungu katika kila kizazi wamelitamka jina la Mungu kwa uhuru na kwa heshima. Boazi, mtumishi mwaminifu-mshikamanifu wa Mungu, aliwaamkua kwa ukawaida wafanyakazi wake shambani kwa maneno haya, “BWANA [“Yehova,” NW] akae nanyi.” Je, wafanyakazi wake walishtuka kwa sababu ya maamkuzi hayo? La. Andiko lasema: “Wakamwitikia, BWANA [“Yehova,” NW] na akubariki.” (Ruthu 2:4) Badala ya kuiona salamu hiyo kuwa chukizo kwa Mungu, waliiona kuwa njia ya kumtukuza Mungu na kumheshimu katika shughuli zao za kila siku. Kwa kusudi kama hilo, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe.”—Mathayo 6:9.
Ile Amri ya Tatu
Namna gani lile katazo linalotajwa katika Amri ya tatu kati ya zile Amri Kumi? Andiko la Kutoka 20:7 lasisitiza hivi: “Usilitaje bure jina la BWANA [“Yehova,” NW], Mungu wako, maana BWANA [“Yehova,” NW] hatamhesabia kuwa hana hatia mtu alitajaye jina lake bure.”
Kulitaja jina la Mungu “bure” kwamaanisha nini hasa? Kitabu The JPS Torah Commentary, kilichochapishwa na Jewish Publication Society, chaeleza kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa kuwa “bure”(lash·shaw’ʹ) laweza kumaanisha “kwa uongo” au “bila sababu.” Kichapo hicho chaendelea kusema: “Maana nyingi ya [neno hilo la Kiebrania] yatia ndani kuzuia kutekelezwa kwa haki na wahusika wakuu katika mashtaka, kuapa kwa uongo, na kutumia Jina la Mungu isivyo lazima au isivyofaa.”
Ufafanuzi huo wa Kiyahudi wakazia kwa usahihi kwamba ‘kulitaja jina la Mungu bure’ kwahusisha kulitumia jina hilo katika njia isiyofaa. Lakini je, kulitamka jina la Mungu unapowafundisha wengine juu yake au unapomfikia Baba yetu wa kimbingu katika sala kwaweza kwa haki kutajwa kuwa kulitumia jina hilo “isivyo lazima au isivyofaa”? Yehova hueleza maoni yake kwa maneno ya Zaburi 91:14: “Kwa kuwa amekaza kunipenda, nitamwokoa; na kumweka palipo juu, kwa kuwa amenijua Jina langu.”
Je, Ni Jambo la Maana Kutamka Jina la Mungu?
Tafsiri ya Kiingereza cha kisasa yenye kichwa The Five Books of Moses, iliyoandikwa na Everett Fox, haifuati mapokeo. Tafsiri hii haitumii neno la kawaida “BWANA,” bali hutumia “YHWH” kuliwakilisha jina la Mungu “ili kuonyesha jinsi ambavyo jina hilo lingeonekana kwa msomaji wa lugha ya Kiebrania.” Fox akazia hivi: “Msomaji atatambua mara moja kwamba jina la kibinafsi la Mungu wa Biblia laonekana katika buku hili kwa herufi ‘YHWH.’” Yeye akiri kwamba kuonekana kwa jina la Mungu huenda “kukamshtua” msomaji. Lakini baada ya kuchukua hatua inayostahili sifa ya kutolificha jina la Mungu katika kutafsiri, aongeza hivi: “Ningependekeza utumizi wa jina la kawaida ‘BWANA’ wakati wa kusoma kwa sauti, lakini huenda wengine wakapenda kufuata desturi yao wenyewe.” Hata hivyo, je, hilo ni jambo la kujiamulia mwenyewe, mapokeo, au kufuata desturi?
La hasha. Biblia haipendekezi tu utumizi mzuri wa jina la Mungu bali inaamuru jina hilo litumiwe! Kwenye Isaya 12:4a, watu wa Mungu wanaonyeshwa wakipaza sauti waziwazi: “Mshukuruni BWANA [“Yehova,” NW], liitieni jina lake.” Kwa kuongezea, mtunga zaburi husema juu ya wale wanaostahili kupata hukumu kali ya Mungu: “Ukali wako uwamwagie mataifa wasiokujua, na falme za hao wasioliitia jina lako.”—Zaburi 79:6; ona pia Mithali 18:10; Sefania 3:9.
Kwa hiyo, hata ingawa watu wengine hukataa kulitamka jina tukufu la Yehova kwa sababu ya kutofahamu ile amri ya tatu, wale wanaompenda Mungu kikweli wanataka kuliitia jina lake. Ndiyo, kwa kila fursa inayofaa, ‘wanayatangaza matendo yake kati ya mataifa, wakilitaja jina lake kuwa limetukuka’!—Isaya 12:4b.
[Maelezo ya Chini]
a Katika Maandiko ya Kiebrania ya Biblia (Agano la Kale), jina la Mungu linawakilishwa na herufi nne, ambazo zinaweza kunukuliwa kuwa YHWH. Ingawaje matamshi kamili ya jina la Mungu hayajulikani, kwa kawaida jina hilo linatamkwa “Yehova” katika lugha ya Kiswahili.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Sehemu ya kitabu cha Zaburi ya Hatikunjo za Bahari ya Chumvi. Jina la Mungu, Yehova (YHWH), huonekana katika maandishi ya kale zaidi ya Kiebrania kuliko katika hatikunjo nyingine
[Hisani]
Courtesy of the Shrine of the Book, Israel Museum, Jerusalemyy