Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 5/1 kur. 4-7
  • Je! Jina Lenyewe Linapasa Kutumiwa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Jina Lenyewe Linapasa Kutumiwa?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Habari Zinazolingana
  • Jina Lililo Kuu Kupita Majina Yote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Kwa Nini Ni Lazima Tujue Jina la Mungu
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Liheshimu Jina Kuu La Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Jina la Mungu—Maana na Matumizi
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 5/1 kur. 4-7

Je! Jina Lenyewe Linapasa Kutumiwa?

WATU wengi wanajisikia wakiwa na wasiwasi wa kutumia jina takatifu la Mungu. Wayahudi wenye kufuata sana dini yao wanaliona jina hilo katika Biblia zao, lakini maoni yao ni kwamba halipasi kutamkwa. Wanadini wengine wengi wanasitasita kulitumia.

Lakini, wakati mmoja taifa zima la Israeli lilimsikia Mungu akitaja jina lake. Walilisikia likitamkwa kwa usahihi. Wakiwa kwenye Mlima Sinai walilisikia mara nane katika yale Maneno Kumi, au Amri Kumi, ambazo walisikia zikinenwa kutoka mbinguni.—Kutoka 20:2-17.

Ikiwa mtafsiri wa nakala yako ya Biblia alitumia jina la Mungu mahali linapoonekana katika Kiebrania cha kwanza kabisa, utaona kwamba amri hizo zilianza kwa kutaja maneno haya: “Mimi ni Yehova Mungu wako, ambaye amekuleta kutoka nchi ya Misri, kutoka nchi ya watumwa. Ni lazima usiwe na miungu mingine yo yote dhidi ya uso wangu.” Tafsiri ya The Living Bible inatafsiri maneno hayo hivi: “Mimi ni Yehova Mungu wako . . . Huna ruhusa kuabudu mungu mwingineye yote isipokuwa mimi.” (Kutoka 20:2, 3) Ikiwa watafsiri wa Biblia yako hawakutumia jina la Mungu, huenda wakawa waliliandika neno “BWANA” katika herufi kubwa ili kuonyesha kwamba Jina Lenyewe linaonekana katika kifungu cha yale maneno ya kwanza kabisa, ya huko nyuma.

Hakuna jambo lo lote katika Maandiko linalosema kwamba jina hilo halipasi kutumiwa. Mungu alisema jina lake lisitajwe “bure.” Lakini hiyo haimaanishi kwamba haitupasi kulitumia jina hilo. Bali, maana yake ni kwamba haiwapasi watumishi wa Yehova kufanya mambo yanayoleta sifa mbaya juu ya jina lake.—Kutoka 20:7.

Musa, aliyetumiwa kuiandika amri hiyo katika Biblia, hakuielewa kuwa na maana ya kwamba jina la Mungu halipasi kutumiwa, kwa maana yeye aliliandika jina hilo mara mia nyingi katika ile Pentateuko, yaani, vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. Badala ya kuepuka kutumia jina hilo, Musa alisema hivi: “Sikiliza, O Israeli: Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja. Na wewe lazima upende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na nafsi yako yote na nguvu zote za uhai ulizo nazo.” —Kumbukumbu la Torati 6:4, 5, NW.

Biblia haionyeshi kwamba jina hilo lilibaki likiwa limefichwa au likiwa halitamkwi. Badala yake, inaonyesha kwamba kwa kipindi cha karne nyingi lilitumiwa kwa wingi. Biblia inamtaja Hawa kuwa alilitumia. (Mwanzo 4:1, NW ) Musa anasema kwamba Abrahamu mwadilifu alilitumia, kwamba Abrahamu aliita “jina la Yehova yule Mungu mwenye kudumu kwa wakati usiojulikana,” ingawa uhakika huo umefichwa katika tafsiri nyingi za kisasa za Biblia.—Mwanzo 21:33, NW.

Abrahamu alitumia jina la Yehova katika kuongea na mfalme wa Sodoma. Sara alilitumia katika maongezi pamoja na Abrahamu. Mtumishi wa Abrahamu alilitumia kwa ukawaida. Yakobo, Raheli mke wake na baba ya Raheli, Labani, wote walitumia jina la Mungu. —Mwanzo 14:22; 16:2; 24:35, 42, 44; 28:16; 30:24, 27, 30, NW.

Musa aliamriwa atumie jina la Mungu. Musa na Haruni walilitumia katika kusema na Farao asiyeamini, naye Farao alilitumia katika kujibu. Alisema: “Yehova ni nani, ili kwamba mimi nipaswe kutii sauti yake niagize Israeli waende zao? ”—Kutoka 5:1-3; 3:15, NW.

Karne nyingi baadaye watu walikuwa bado hawalioni jina la Yehova kuwa lisilopasa kutajwa. Walilitumia katika kuongea na Samweli, naye alilitumia katika kujibu. (1 Samweli 12:19, 20, NW ) Mfalme Daudi mwenye uadilifu aliimba jina hilo mbele ya watu, akisema: “Mimi nitatangaza jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya kundi nitakusifu wewe. Ninyi waogopaji wa Yehova, sifuni yeye! ”—Zaburi 22:22, 23, NW.

Yule nabii mkuu Isaya hakuwa na fikiria ya kwamba jina hilo linapasa kuachiliwa mbali. Yeye alilitumia mara zaidi ya 400 katika kitabu cha Biblia kinachoitwa kwa jina lake.

Isaya hakuwaambia Wayahudi wenye kusoma maandishi yake wasitumie jina la Mungu. Bali, yeye alisema hivi: “Mpeni Yehova shukrani, enyi watu! Iteni jina lake. Julisheni miongoni mwa makundi ya watu shughuli zake. Tajeni kwamba jina lake linawekwa juu. Fanyieni Yehova muziki wenye michanganyiko ya sauti tamu, kwa maana yeye amefanya mambo yanayozidi mengineyo yote. Jambo hilo linajulishwa katika dunia yote.”—Isaya 12:4, 5, NW.

Je! lo lote la maneno hayo linasikika kama kwamba jina hilo lililo kuu sana lilipasa kufichwa? lisitumiwe? mahali palo pachukuliwe na neno jingine la namna fulani? Ni wazi kwamba watafsiri wanaoondoa jina la Mungu katika kitabu chake mwenyewe hawana uthamini wa jina hilo kama ule waliokuwa nao watu wenye kumwogopa Mungu, Abrahamu, Sara, Yakobo, Musa, Haruni, Samweli, Daudi na Isaya.

Wala manabii wa nyakati zilizofuata hawakulificha jina hilo, kuliona kuwa takatifu mno wasiweze kulitumia wala kuwa na maoni ya kwamba waandikaji wa Biblia waliowatangulia walikosea na hivyo kuwa na fikira ya kwamba mahali pa jina hilo panapasa kuwekwa neno fulani la namna nyingine. Ujumbe wao mbalimbali ulijawa na semi kama hizi: “Sikieni neno la Yehova.” “Hivi ndivyo Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, amesema.” “Hivi ndivyo Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu amesema.”—Yeremia 2:4; 19:15; Ezekieli 21:28, NW.

Wala jina hilo halikutumiwa kuhusiana na mambo ya kidini tu. Zaidi ya kutumiwa na walimu, jina la Mungu lilitumiwa na watu wa kawaida katika maongezi yale ya kikawaida, Biblia inasema kwamba Boazi aliwaambia hivi wafanya kazi wenzake: “Yehova na awe nanyi.” Wao walikuwa wakijibu: “Yehova na akubariki wewe.”—Ruthu 2:4, NW.

Wachimbuzi wa vitu vya kale katika ardhi wamepata uthibitisho wenye maneno ya Biblia yanayoonyesha kwamba watu walitumia jina hilo. Katika miaka ya 1930 waligundua zile Barua za Lakishi, ambazo ni vyungu vinavyoaminiwa kuwa vya kuanzia wakati ule wa ushindi wa Kibabuloni katika karne ya saba K.W.K. Barua hizo zinarudia-rudia matumizi ya semi zilizo kama huu: “YHWH [Yahweh, au Yehova] na afanye bwanangu asikie leo hii hii habari za wema! ”

Hata watu wasiokuwa Waisraeli walilijua jina la Mungu na wakalitumia. Wagibeoni walimwambia Yoshua hivi: “Watumishi wako wamekuja kwa kuheshimu jina la Yehova Mungu wako kwa sababu sisi tumesikia habari za sifa yake na za yote aliyotenda katika Misri.” (Yoshua 9:9; NW ) Katika karne ya kumi kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, Mesha, mfalme wa Moabu, aliyekuwa adui wa Israeli aliagiza jina hilo liandikwe juu ya Jiwe la Moabi, ambalo liligunduliwa tena mwaka wa 1868 na sasa limewekwa katika mahali pa kuonwa na watu katika jumba la kuhifadhia vitu vya kihistoria la Louvre huko Paris.

Mambo hayo ya hakika hayapasi kuwa ya kushangaza. Badala ya kutokeza kiwazo cha kwamba jina hilo lilikuwa la siri ambalo halikupasa kutumiwa, Musa alikuwa amewaambia watu hivi: “Na makundi yote ya watu wa dunia yatalazimika kuona kwamba jina la Yehova limeitwa juu yenu ninyi.” (Kumbukumbu la Torati 28:10, NW ) Jambo hilo lingewezekanaje ikiwa hata waabudu hawakulitumia jina lake?

Badala ya kuwa lisilotajika, jina lenyewe lilitukuzwa, likapendwa, likaheshimiwa. Maeneo fulani yaliitwa kwa jina hilo, na hata katika kuwapa watu majina. Abrahamu alipaita mahali alikokwenda kumtoa Isaka awe dhabihu “Yehova-yire.” (Mwanzo 22:14) Na yanayofuata ni mengine kati ya majina yaliyomo katika Biblia yanayojulikana sana ambayo maana yayo yanahusu Yehova, au Yah, ile namna fupi zaidi ya kishairi ya jina la Yehova: Hezekia, Isaya, Yosia, Nehemia, Obadia, Zekaria na Sefania. Watu wanatumia jina la Mungu kuwapa watoto majina leo. Kwa kweli, jina zuri ajabu la Mungu huenda likawa limetiwa katika jina lako mwenyewe! Je! unajua mtu ye yote anayeitwa Yoeli? Jina lake linamaanisha, “Yehova ni Mungu.” Namna gani Yonathani? Maana yake ni “Yehova ametoa.” Yoshua maana yake ni “Yehova ni wokovu.” Na mtu ye yote aliye na lile jina wanaloitwa watu wengi, John (Yohana), jina lake linamaanisha “Yehova amekuwa mwenye neema.”

Kwa hiyo ijapokuwa watu wengine wana imani ya kwamba jina la Mungu ni takatifu mno lisiweze kutajwa, na ijapokuwa wengine wana imani ya kwamba linapasa kuachiliwa mbali, hakuna njia iwayo yote ambayo kwayo linaweza kuachwa liwe nje ya Biblia. Jina hilo limetiwa ndani ya majina yote hayo ya Kibiblia yaliyotumiwa wakati wa zile karne nyingi ambazo, zaidi ya kujua jina takatifu la Mungu YEHOVA, watu walilitumia pia katika sala, ibada na maongezi ya kikawaida.

Lakini namna gani Maandiko ya Kikristo, ambayo mara nyingi yanaitwa Agano Jipya? Jina Yehova limetiwa ndani ya majina ya Yesu na Yohana, na katika neno “Haleluya,” lakini kwa sababu gani halionekani mara nyingi zaidi ya zile linaonekana? Jibu la ulizo hilo la maana ndilo litazungumzwa sasa.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

Jina Lenyewe Linatamkwa Namna Gani?

Kwa sababu ya kuacha kutumiwa kidini, tamko lile la kwanza kabisa la neno la Kiebrania יהוה limepotezwa. Wanachuo wengine wanapendelea zaidi kusema “Yahweh,” lakini hakuna njia ya kujua ni tamko gani lililo sahihi.

Lakini, mara nyingi majina yanatamkwa kwa njia tofauti katika lugha tofauti-tofauti. Katika Kiswahili tunamwita yule Mkristo aliyekuwa wa kwanza kufa,Stefano, lakini Wafaransa wanamwita Étienne. Katika Kiebrania Yesu aliitwa Ye·shuʹaʽ, au Yehohshuʹaʽ, na katika Kigiriki akaitwa I·e·sousʹ.

Uhakika wa kwamba hatutamki jina la Yesu—au jina la mtu mwingine ye yote—sawasawa kabisa na lilivyotamkwa katika lugha ya kwanza kabisa hautufanyi tuache kulitumia. Jambo tunalofanya ni kulitamka kama linavyotamkwa katika lugha yetu.

Hivyo, kitabu Aid to Bible Understanding kinasema hivi: “Kwa kuwa uhakika wa tamko lenyewe hauwezi kupatikana sasa, inaelekea kuwa hakuna sababu ya kuacha katika Kiingereza kuitumia namna inayojulikana sana ya kusema ‘Jehovah’ kwa kupendelea zaidi tamko la namna nyingine linalopendekezwa. . . .Katika Kiingereza jina ‘Jehovah’ linamtambulisha Mungu wa kweli, nalo linapitishia watu wazo hilo kwa njia ya kutosheleza zaidi leo kuliko lo lote la maneno yale yanayopendekezwa yatumiwe badala yalo.”—Ukurasa wa 885.

[Picha katika ukurasa wa 6]

HAWA WALIMWITA MUNGU KWA JINA LAKE

Abrahamu

Sara

Raheli

Daudi

Samweli

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki