Vijana Huuliza . . .
Kwa Nini Sipati Vitu Ninavyotaka?
“Kuna vitu vizuri kweli, na ningependa kuwa navyo; lakini wazazi wangu hawana uwezo wa kuvigharimia.”—Mike.
JE, KUNA vitu ambavyo unataka kuwa navyo sana lakini huwezi kuvipata? Labda unatamani sana kuwa na stirio ya karibuni zaidi, viatu vinavyofanana na vya watoto wengine, au suruali mpya ya jeans yenye chapa ya watengenezaji mashuhuri. Baadhi ya marika wako wana vitu hivyo na wanavionyesha kwa majivuno. Hivyo unapoambiwa kwamba wazazi wako hawana uwezo wa kuvigharimia, huenda ukatamauka.
Lakini ingawa kutaka kuwa na vitu fulani vya kimwili ni jambo la kawaida, kwa vijana wengi ile tamaa ya kuwa navyo inapita kiasi. Hii inasababishwa na propaganda zinazoenezwa na vyombo vya habari. Matangazo ya biashara yenye kuvutia katika televisheni, magazetini, na katika redio huwasilisha ujumbe wa kwamba usipovaa mavazi ya aina fulani, au usipotumia bidhaa zilizo na chapa fulani, basi wewe ni mtu bure. Kwani, matineja hutumia zaidi ya dola bilioni 100 kila mwaka Marekani peke yake!
Kisha kuna msongo wa marika. “Katika ulimwengu wa vijana ulio sahili na usio na huruma,” yasema makala moja katika gazeti Marketing Tools, “kuonekana ukiwa mshenzi na kikundi cha kirafiki unachokitamani si kushindwa tu kufikia kiwango cha marika zako, au hata kukataliwa: ni ishara ya kuwa Mshenzi.” Ni nini ufunguo wa kuonekana ukiwa “mstaarabu”? Kwa vikundi vingi vya kirafiki kunamaanisha kuwa na vitu vya kimwili vilivyo bora na vya kisasa. Na kama huna uwezo wa kuvigharimia? “Kwa kweli, ni vigumu sana kustahimili,” akiri kijana mmoja Mkristo. “Unapoenda shuleni na mavazi yasiyo na chapa ya watengenezaji mashuhuri, kila mtu anakutania.” Kijana mwingine akiri hivi, “Wakati mwingine mimi hujihisi sikubaliwi.”
Misongo kama hiyo yaweza ikahisiwa na vijana wanaoishi katika nchi zinazositawi, ambako watu hufanya kazi kwa muda mrefu kwa shida ili wapate mahitaji ya lazima ya maisha. Ikiwa hili ni kweli katika familia yenu, huenda ukatamani sana maisha bora kiasili. Baada ya kutazama maonyesho ya televisheni na sinema kutoka kwenye nchi tajiri, huenda pia ukawa umeanza kusitawisha tamaa ya kupata mavazi ghali sana, nyumba, na magari yaliyotangazwa katika maonyesho na filamu hizo. Huenda ukasononeka au kushuka moyo, kwa sababu vitu hivyo vyaonekana kuwa ghali sana usiweze kuvipata.
Kukasirika au kukata tamaa kwa sababu huwezi kupata vitu fulani kwaweza kukudhuru, uwe waishi katika nchi maskini au tajiri. Kwaweza pia kusababisha kubishana-bishana na wazazi wako sikuzote. Swali ni, Utakabilije tatizo hilo?
Maoni Yaliyosawazika ya Vitu vya Kimwili
Kwanza, ng’amua kwamba si tamaa ya Yehova Mungu kwamba watu wake waishi katika umaskini au wakose vitu wanavyohitaji sana. Kwa vyovyote, Mungu hakuwaweka Adamu na Hawa katika lundo la taka, bali katika bustani maridadi iliyojaa miti inayotamanika kwa macho. (Mwanzo 2:9) Baadaye zaidi, baadhi ya watumishi wa Mungu, kama vile Abrahamu, Yobu, na Solomoni, wakawa na vitu vingi vya kimwili. (Mwanzo 13:2; Ayubu 1:3) Kwani, Solomoni alikuwa na dhahabu nyingi sana hivi kwamba fedha “haikuhesabiwa kuwa kitu” wakati wa utawala wake!—1 Wafalme 10:21, 23.
Ingawa hivyo, kwa ujumla wengi wa watu wa Mungu wameishi maisha ya kiasi. Yesu Kristo alikuwa maskini; hakuwa na “mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 8:20) Ijapokuwa hivyo, husomi kamwe juu ya Yesu akilalamika kwamba hakuwa na uwezo wa kugharimia vitu alivyotaka. Badala ya hivyo, alifunza hivi: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tule nini?’ au, ‘Tunywe nini?’ au, ‘Tuvae nini?’ . . . Kwa maana Baba yenu wa kimbingu ajua mwahitaji vitu hivi vyote. Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.”—Mathayo 6:31-33.
Hii haimaanishi kwamba Mungu ana wajibu wa kutimiza tamaa ya mtu ya kupata mavazi ya kimtindo, au vifaa vya kielektroni. Mungu huandaa mahitaji yetu—si lazima viwe vitu tunavyotaka. Ndiyo sababu Biblia hutuhimiza turidhike na “riziki na cha kujifunika.” (1 Timotheo 6:8) Lakini tunapaswa kutambua kwamba, kuridhika si jambo rahisi. Kijana aitwaye Mike akiri hivi, “Una pambano la daima kati ya yale unayotaka na mahitaji yako.” Mbali na mwelekeo wetu wenyewe wa ubinafsi, lazima tupige vita dhidi ya uvutano wa adui mkuu wa Mungu, Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Na mojawapo ya mbinu zake za zamani ni kuwafanya watu wahisi kwamba kuna kitu fulani wanachokosa. Hawa alishawishiwa kufikiri kwamba alikuwa ananyimwa—hata ingawa alikuwa akiishi katika paradiso kamilifu!—Mwanzo 3:2-6.
Waweza kuepukaje hali hii ya kutoridhika? Huenda lisionekane kuwa jambo halisi, lakini kuna sababu nyingi sana za kufikiria baraka ulizo nazo. Usitatanishwe na mawazo yasiyofaa kuhusu vitu ambavyo huna. Fikiri kwa njia ifaayo, na ukumbuke vitu ulivyo navyo. (Linganisha Wafilipi 4:8.) Mike asema hivi: “Kuna vitu vingi ninavyovitaka sana, lakini sivikazii fikira sana.”
Inasaidia pia kushuku matangazo ya werevu yanayoamsha hisia-moyo zako.a (Mithali 14:15) Kabla hujafikia mkataa wa kwamba huwezi kuishi bila jozi ile mpya ya viatu vya michezo au bila mashine ya kuchezea CD, jaribu kuichanganua hali kwa utulivu. Jiulize: ‘Je, kweli ninahitaji kitu hiki? Je, kina kusudi la muhimu? Je, vitu nilivyo navyo tayari vyatosha?’ Jihadhari sana na matangazo ya kibiashara yanayokuza fahari ya umilikaji. Maneno ya mtume Yohana katika 1 Yohana 2:16 ni yenye kumfanya mtu afikiri: “Kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya kutegemeza maisha—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.”
Unapohitaji Sana Kitu Fulani
Namna gani ikiwa unahitaji kitu fulani kwa sababu nzuri? Kabla ya kuzungumza na wazazi wako juu ya kitu hicho, fikiria kimbele. Uwe tayari kueleza sawasawa sababu kwa nini unahitaji kitu hicho, namna utakavyokitumia, na kwa nini unahisi kwamba kitu hicho kitakufaa. Huenda wazazi wako wakatafuta njia ya kukiongeza katika bajeti ya familia. Lakini namna gani ikiwa hawataweza, angalau kwa wakati huu? Huenda usiwe na la kufanya isipokuwa kusubiri. (Mhubiri 7:8) Hizi ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na wazazi wengi hawana uwezo wa kugharimia vitu vyote ambavyo huenda watoto wao wakaomba. (2 Timotheo 3:1) Unaweza kuirahisisha kazi ngumu ya wazazi wako, kwa kuepuka kudai vitu visivyo vya maana.
Hata hivyo, huenda ikawa kwamba unaweza kuchukua hatua. Kwa mfano, je, wewe hupokea marupurupu? Basi jaribu kujifunza jinsi ya kupanga bajeti ya pesa zako kwa uangalifu ili uweze kuweka akiba ya kiasi fulani kila mwezi. Huenda hata ukaweza kufungua akaunti ya akiba katika benki iliyo karibu. (Linganisha Luka 19:23.) Hivyo ndivyo msichana mdogo aitwaye Abigail alivyofanya. Yeye asema: “Nilizitenga pesa zangu katika mafungu mawili—fungu moja ni la akaunti yangu ya benki na jingine ni la matumizi.” Ukiwa mwenye umri wa kutosha, unaweza kujaribu kufanya vibarua au kazi ya muda.b Kwa vyovyote vile, ikiwa wazazi wako wanaona kwamba kwa kweli unataka kununua kitu fulani na unajitahidi sana kuweka akiba ya pesa, huenda wakapendezwa kukusaidia kugharimia kitu hicho, iwapo inawezekana.
Kufanya mabadiliko fulani katika namna unavyonunua vitu kwaweza kuwa kwenye faida kwako. Kwa kielelezo, ikiwa kitu fulani ni ghali sana, unaweza kuomba upunguziwe bei. Usipofaulu, subiri uone kama kitu hicho kitauzwa kwa mnada. Tafuta kwenye maduka mengine uone kama unaweza kupata kitu kile-kile kwa bei nafuu. Jifunze kuchunguza vitu kwa uangalifu uone ubora wake; nyakati nyingine bidhaa za kawaida zinakuwa zenye thamani bora na bei nafuu kabisa.c
Jifunze Kuridhika
Mithali 27:20 huonya hivi: “Kuzimu na uharibifu havishibi; wala macho ya wanadamu hayashibi.” Ndiyo, kama vile kaburi lisivyotosheka, watu fulani hutaka vitu zaidi na zaidi sikuzote—bila kujali wana vitu vingapi tayari. Epuka kigezo hicho cha kufikiri kilicho cha ubinafsi. Hatimaye, pupa husababisha kukata tamaa na kukosa furaha. Kijana aitwaye Jonathan asema hivi: “Ikiwa furaha yako yategemea kuwa na vitu, hutakuwa kamwe mwenye furaha. Sikuzote utataka kitu fulani kipya. Unahitaji kujifunza kuwa mwenye furaha na vitu ulivyo navyo.”
Ukiridhika, unaweza kushughulikia msongo wa marika. Vincent mchanga asema: “Kwa sababu tu nimemwona mtu fulani akiwa amevalia viatu vya michezo vyenye chapa ya watengenezaji haimaanishi kwamba lazima niende nikajinunulie jozi yangu.” Bila shaka, mara kwa mara, huenda ukahangaika usipoweza kupata unachokitaka. Lakini usisahau kamwe kwamba Yehova anajua mahitaji yako. (Mathayo 6:32) Na katika wakati ujao ulio karibu, ‘atashibisha kila kilicho hai matakwa yake.’—Zaburi 145:16.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala mfululizo “Matangazo ya Biashara—Yanakuathirije?,” katika toleo la Amkeni! la Agosti 22, 1998.
b Ona makala “Vijana Huuliza . . . Naweza Kuchumaje Pesa?,” katika toleo letu la Agosti 22, 1998.
c Kwa madokezo zaidi yenye msaada, ona makala “Vijana Huuliza . . . Naweza Kuboreshaje Jumla ya Mavazi Yangu?,” katika toleo letu la Januari 22, 1995.
[Blabu katika ukurasa wa 13]
“Unapoenda shuleni na mavazi yasiyo na chapa ya watengenezaji mashuhuri, kila mtu anakutania”
[Picha katika ukurasa wa 14]
Unaweza kuwa mwenye furaha bila kuwa na vitu vyote unavyotaka