Mkutano Wenye Kutokeza Kuhusu Upasuaji Bila Damu Wafanywa Moscow
VIBADALA VYA UTIAJI-DAMU MISHIPANI KATIKA UPASUAJI ndilo lililokuwa jina la mkutano wa kimataifa wa kitiba uliofanywa Moscow, Urusi, mnamo Oktoba 6, 1998. Madaktari zaidi ya 800 walikuwako kwenye Taasisi ya Upasuaji ya Vishnevskij kwa ajili ya mfululizo, uliotolewa na pia Kongamano la Sita la Urusi la Wataalamu wa Nusukaputi na wa Wagonjwa Mahututi.
Profesa Andrey Ivanovich Vorobiev, ambaye sasa anatumikia akiwa msimamizi wa tawi la biolojia inayohusika na damu kwenye Taasisi ya Sayansi ya Kitiba ya Urusi, katika Moscow, aliwakaribisha madaktari kwa kile alichokiita “mfululizo huu kwa madhumuni ya kutafuta vibadala vya utiaji-damu mishipani.”
Akifafanua kwa nini mkutano huo ulikuwa muhimu, Vorobiev alisimulia “misiba mibaya sana ya utiaji-damu mishipani.” Alidai kwamba likiwa tokeo la utiaji-damu mishipani, watoto wengi walio na ugonjwa wa kutoganda kwa damu katika nchi kama vile Marekani, Japani, na Ujerumani wamepata UKIMWI. Kisha, baada ya kuandaa takwimu kuhusu kuenea kwa mchochota wa ini kupitia kutiwa damu mishipani, aliomboleza hivi: “Takwimu hizi zinashangaza kabisa. Karibu wagonjwa wote wenye tatizo la kutoganda kwa damu wana mchochota wa ini.”
Vorobiev alitaja kwamba, maoni ya kitiba yalikuwa, ikiwa mtu “alipoteza lita moja ya damu, basi anapaswa kutiwa damu lita moja.” Lakini “hilo ni kosa!” akatangaza. Akimalizia maelezo yake ya kufungua, alisema: “Tuliunga mkono utiaji-damu mishipani, na sasa kwa pamoja tutafutilia mbali maoni ya kale.”
Wataalamu wengi wa kitiba waliofuatia katika programu hiyo walitoka Urusi, lakini kulikuwako pia wasemaji kutoka Ufaransa, Sweden, Ubelgiji, na Marekani. Mbali na kufafanua maendeleo katika kushughulikia upotezaji damu kwa kutumia vibadala vya utiaji-damu mishipani, madaktari walitaja hatari za utiaji-damu mishipani, kutia ndani hatari za athari za kinga-maradhi.
Taarifa za Televisheni
Kituo cha televisheni cha umma cha Urusi, ambacho matangazo yake hufikia watu milioni 235, kiliandaa ripoti nzuri kuhusu mkutano huo. Msimamizi, Elena Malysheva, alieleza: ‘Madaktari-Wapasuaji, madaktari-nusukaputi, na wataalamu wa biolojia inayohusu damu wanaojulikana vizuri na walio mashuhuri ulimwenguni pote, walikusanyika Moscow kujibu swali moja: Je, upasuaji unaweza kufanywa bila damu?’
Elena aliwaarifu watazamaji wa televisheni kuhusu maradhi yanayoweza kupitishwa kupitia damu na kueleza hivi: “Jambo hili ndilo lililowafanya madaktari watafute njia badala. Na ilipatikana. Iliitwa upasuaji bila damu. Kila mtu atakayefanyiwa upasuaji anaweza kuzungumza na daktari wake kuhusu njia za upasuaji bila damu.”
Wakati Andrey Vorobiev alipotokea kwenye tangazo la televisheni, alisema: ‘Damu iliyotolewa ina protini ambazo ni geni kwa mwili na zinaweza kusababisha athari zisizoweza kutabiriwa na zisizoepukika. Kwa kuongezea, hata tujaribu namna gani, mwenye kutoa damu anaweza kumwambukiza mgonjwa virusi alivyo navyo na tusivyoweza kugundua.’ Hivyo alimalizia: ‘Tunahitaji kupunguza kuwatia wagonjwa damu mishipani.’
Pia kwenye programu kulikuwa na Jean-François Baron, msimamizi wa unusukaputi na utunzaji wa wagonjwa mahututi kwenye Hospitali ya Broussais, Paris, Ufaransa. Alieleza kwamba: “Katika taasisi yangu tulivumbua umajimaji wa pekee unaoweza kubeba oksijeni. Umajimaji wote una uwezo wa kubeba oksijeni na damu lakini hauna chembe nyekundu za damu [zinazoweza kupitisha maradhi]. Katika wakati ujao karibuni,” alitabiri, “umajimaji huu utatumiwa kwa ukawaida.”
Jambo hili lilimchochea msimamizi wa programu aeleze kuhusu profesa Mrusi Felix F. Beloyartsev, aliyetokeza umajimaji unaobeba oksijeni kuwa kibadala cha damu miaka 20 hivi iliyopita. Alisema kwamba wakati huo, uvumbuzi wa Beloyartsev haukukubaliwa na jumuiya ya kitiba na kwamba “alijiua kufuatia mnyanyaso usiokoma uliompata kwa sababu ya uvumbuzi huo.”
Taarifa Katika Majarida ya Kitiba
Pia gazeti la habari za kitiba Meditsinskaya Gazeta lilitoa ripoti kuhusu mkutano huo. “Umalizio wa Mfululizo huo,” lilisema, “waweza kutajwa kuwa: Ni lazima kutumia vibadala vya utiaji damu mishipani katika visa vyote inapowezekana na kuamua kutumia damu baada tu ya kufikiria kwa uangalifu kiwango cha hatari ya kibinafsi kwa kila mgonjwa katika hali zenye kutishia uhai peke yake.”
Pia gazeti hilo la habari za kitiba lilirejezea nia ya madaktari fulani ya kutotaka kufuata uamuzi wa mgonjwa wa kukataa damu. Kwa kielelezo, Mashahidi wa Yehova, hawakubali kutiwa damu mishipani kwa sababu ya agizo la Biblia la ‘kujiepusha na damu.’ (Matendo 15:28, 29) Hata hivyo, kuhusu jambo hili, Michel de Guillenchmidt, profesa wa sheria kutoka Ufaransa, alinukuliwa akisema:
‘Tunapaswa kuwashukuru Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya kuzusha suala hili, hawakuvuta uangalifu kwenye haki zao tu bali pia wamesaidia jumuiya yote ya kitiba kuelewa hatari za utiaji-damu mishipani. Jambo hili, hatimaye huwatia moyo wanasayansi watafute njia za hali ya juu za kufanya upasuaji bila damu.’
Makala moja katika Meditsinskaya Gazeta ilianza kwa kusema: “Imesemwa kwamba kutiwa damu mishipani ni sawa na ndoa: Hakuna mtu anayejua litakalofuata.” Kisha, baada ya kusema kwamba ‘damu ya binadamu ni kama alama za kidole za binadamu—hakuna alama mbili zinazofanana,’ gazeti hilo la habari liliuliza: “Je, inawezekana leo kutoa uhakikisho kamili kwamba mgonjwa hatapatwa na maambukizo kama tokeo la kutiwa damu mishipani?” Likajibu: ‘Hata katika nchi ambazo zimepata mafanikio makubwa ya kitiba, hakuna njia yenye matokeo ya kudhibiti vitu vilivyotengenezwa kwa damu.’
‘Hivyo, kwa kutegemea watu waliokuwa wamejaa kwenye ukumbi wa mkutano huo na upendezi dhahiri wa wajumbe katika matatizo yaliyozungumziwa,’ makala hiyo ilimalizia kwa kusema, ‘badiliko la maoni linatukia miongoni mwa madaktari.’
Kuandaa Utumishi
Nje ya jumba la mkutano, Mashahidi wa Yehova walikuwa na kibanda ambapo waliwatolea madaktari kifurushi chenye makala kutoka majarida ya kitiba kuhusu matumizi ya njia badala za kushughulikia kupotezwa kwa damu. Mamia ya madaktari walipokea makala hizi kwa mteremo.
Kwa wazi, wataalamu wa kitiba walioelimika wanafanya maendeleo kuelekea kupunguza matumizi ya damu katika tiba.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Mashahidi wa Yehova waliwatolea mamia ya madaktari makala zenye utafiti wa karibuni kuhusu damu