Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 6/8 kur. 14-20
  • Kuokolewa Kutoka Kwenye Dhoruba Yenye Kufisha!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuokolewa Kutoka Kwenye Dhoruba Yenye Kufisha!
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kimbunga Mitch Chashambulia Honduras
  • El Salvador Yahisi Kiruu cha Kimbunga Mitch
  • Kimbunga Mitch Chapitia Nikaragua
  • Ghasia Katika Guatemala
  • Matokeo ya Baadaye ya Kimbunga Mitch
  • Kukua Pamoja Katika Upendo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kitu Kisichoweza Kuharibiwa na Dhoruba
    Amkeni!—2003
  • Kazi ya Kutoa Msaada
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Udugu Wenye Umoja Usioweza Kuvunjwa
    Amkeni!—2001
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 6/8 kur. 14-20

Kuokolewa Kutoka Kwenye Dhoruba Yenye Kufisha!

Uharibifu uliosababishwa na Kimbunga Mitch mwaka jana ulikuwa kwenye vichwa vya habari vya magazeti ulimwenguni pote. Hata hivyo, mara nyingi jitihada kubwa sana ambazo zimefanywa na Mashahidi wa Yehova ili kusaidia watu waliokumbwa na dhoruba hii yenye kufisha, zimepewa uangalifu mdogo. Ripoti ifuatayo yaonyesha kwa njia yenye kuvutia mno jinsi Ukristo wa kweli na udugu uwezavyo kushinda, hata chini ya hali mbaya kabisa.

KATIKA Oktoba 22, 1998, bahari ya kusini-magharibi ya Karibea ilitokeza dhoruba yenye kufisha. Ilijitokeza kama upunguaji wa kanieneo ya angahewa ya kitropiki. Katika muda wa saa 24, ilipata nguvu zaidi na kuwa dhoruba ya kitropiki hivyo ikapewa jina litakalokumbukwa kwa muda mrefu kwa hofu na huzuni—Mitch. Kimbunga Mitch kilikuwa kikipata nguvu kikilielekea upande wa kaskazini. Kufikia Oktoba 26, kilikuwa kimbunga Aina namba 5, kikitokeza pepo zenye kuendelea zinazosafiri kilometa 290 kwa saa moja na dharuba za ghafula zinazosafiri mwendo wa zaidi ya kilometa 320 kwa saa moja.

Hapo kwanza, kimbunga Mitch kilikuwa tayari kukumba Jamaika na Visiwa vya Cayman. Lakini dhoruba hiyo yenye kufisha iligeuka upande wa magharibi na kuelekea moja kwa moja hadi Belize, kwenye pwani ya Amerika ya Kati. Ingawa hivyo, badala ya kushambulia, Mitch ilizunguka-zunguka kwa kuogofya kando ya pwani ya kaskazini ya Honduras. Kisha, kwa ghafula dhoruba yenye kufisha ikaanza mwendo. Katika Oktoba 30, Mitch ilivamia Honduras, na kutokeza kifo na uharibifu.

Kimbunga Mitch Chashambulia Honduras

Kimbunga Mitch kilianza kujitokeza kufuatia mvua nyingi sana. “Karibu saa saba za usiku Jumamosi, Oktoba 31,” akumbuka Víctor Avelar, mweneza-evanjeli wa wakati wote anayeishi Tegucigalpa, “tulisikia kelele kama radi kubwa mno. Kile kilichokuwa kijito kidogo sasa kikawa mto uliochafuka! Mkondo huo ulibeba nyumba mbili, huku wakazi wake wakipiga mayowe wakiwa wamenaswa ndani.” Katika sehemu nyingine ya jiji, watu 32 walikufa katika maporomoko ya matope, kutia ndani watu 8 waliokuwa wakijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, hakuna Shahidi aliyebatizwa aliyeangamia.

Maofisa wa Honduras walishughulikia tatizo hilo upesi, wakijenga vibanda vya wakimbizi. Pia, kikundi cha kimataifa cha kutoa msaada kutoka zaidi ya makumi ya nchi kilijihusisha katika shughuli hiyo. Hali kadhalika, Mashahidi wa Yehova walichukua uongozi katika jitihada za kutoa msaada, wakikumbuka maneno ya Biblia: “Acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Hivyo halmashauri za kutoa msaada wa dharura zilianzishwa. Wakitambua jinsi hali ilivyokuwa yenye kutamausha katika miji ya pwani, Mashahidi walipanga kazi ya uokoaji.

Shahidi mmoja anayeitwa Edgardo Acosta akumbuka hivi: “Jumamosi, Oktoba 31, tulipata mashua ndogo na kuelekea eneo lililokuwa na mafuriko. Ijapokuwa tuliweza kuokoa ndugu wawili,a tulitambua kwamba tulihitaji mashua kubwa zaidi ikiwa tungetoa ndugu wote. Hivyo tulipata mashua ya kuwindia nyangumi na kuanza safari ya pili mapema asubuhi ya Jumapili. Hatimaye, tulihamisha kila mshiriki wa kutaniko, pamoja na majirani wao wengine—jumla ya watu 189.”

Juan Alvarado alisaidia katika shughuli za uokoaji karibu na La Junta. Akumbuka: “Tungeweza kusikia watu wakilia, ‘Tusaidieni! Tuokoeni!’ Hilo lilikuwa jambo baya zaidi ambalo nimepata kuona. Akina ndugu walikuwa wamenaswa kabisa. Wengi walikuwa juu kwenye paa.” Aeleza mwokokaji anayeitwa María Bonilla: “Maji yaliyotuzunguka yalikuwa kama bahari. Sote tulikuwa tukilia.” Lakini jitihada za uokoaji zilifanikiwa. Mwokokaji Humberto Alvarado asema hivi: “Akina ndugu hawakutuokoa tu bali pia walitupatia makao, chakula, na nguo.” Humberto azidi kukumbuka hivi: “Mtu mmoja aliyejionea shughuli ya uokoaji alituambia kwamba hakuna mtu yeyote wa kanisa lake aliyejaribu kumtoa—ni Mashahidi wa Yehova peke yao waliofanya hivyo. Sasa amesadiki kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wenye dini ya kweli!”

Katika mji mmoja unaoitwa La Lima, kikundi cha Mashahidi walinaswa ndani ya nyumba. Huku maji yaliyowazunguka yakizidi kuongezeka, walifanyiza mwanya kwenye dari na kupanda juu ya mihimili ya dari. Shahidi anayeitwa Gabi asimulia: “Tulikuwa na maandalizi ambayo yangetutosha kwa siku chache. Yalipoisha, mmoja wa akina ndugu alihatarisha uhai wake kwa kutoka nje kwenye maji akaokote nazi. Ili kupunguza msononeko tuliokuwa nao, tuliimba nyimbo za Ufalme.” Juan ambaye ni mtumishi wa huduma akumbuka hivi: “Hatukufikiri tungeokoka. Hivyo tuliamua kujifunza jarida la Biblia la Mnara wa Mlinzi. Sote tulianza kulia, tukifikiri kwamba hii ilikuwa mara ya mwisho ambayo tungejifunza pamoja. Funzo hilo lilituimarisha kuvumilia.” Walivumilia kwa siku nane mpaka hatimaye walipookolewa na vikundi vya waokoaji.

Ingawa walikuwa salama na hai, waokokaji wengi wa furiko walihitaji kukabili ukweli mchungu. Shahidi mmoja anayeitwa Lilian akiri hivi: “Ni jambo lenye kuhuzunisha sana kupoteza vitu vya kibinafsi kama vile mavazi, fanicha, na picha za familia. Nilipoona nyumba yangu imejaa matope, takataka, na hata nyoka, iliogopesha kwelikweli!” Ingawa hivyo, kwa mara nyingine tena, udugu wa Kikristo ulithibitika kuwa wenye thamani kweli kweli. “Akina ndugu walikuja kusaidia,” akumbuka Lilian. “Mume wangu ambaye si Shahidi, aliuliza, ‘Tutawalipa nini kwa ajili ya kazi yao yote?’ Mmoja wa akina dada alijibu kwa kuniambia, ‘Huhitaji kunishukuru. Mimi ni dada yako!’”

El Salvador Yahisi Kiruu cha Kimbunga Mitch

Kimbunga Mitch kilipokuwa kikisonga upande wa magharibi kuelekea El Salvador, kilipoteza kiasi fulani cha nguvu yake. Lakini bado kilikuwa na uwezo wa kuua. Wakati huo Mashahidi wa Yehova katika El Salvador walikuwa na shughuli nyingi wakipanga Mkusanyiko wa Wilaya wa “Njia ya Mungu ya Maisha.” Walitarajia hudhurio la watu 40,000. Kwa kuwa kimbunga Mitch kilikuwa kinakaribia, haikuwa rahisi ndugu wote kuhudhuria mkusanyiko huo. Mito ilifurika, ikifunika mazao, barabara kuu, na nyumba. Milima ilitokeza maporomoko makubwa sana ya matope baada ya kudhoofishwa na kuanguka kwa miti.

Nelson Flores ndiye aliyekuwa mwangalizi-msimamizi wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova katika mji wa Chilanguera. Jumamosi asubuhi, Oktoba 31, aliamka na kuona kwamba ng’ambo ya mto mahali palipokuwa na mji wa Chilanguera, hapakuwa na kitu chochote! Nyumba mia tano zilikuwa zimefagiliwa mbali! Akihofia uhai wa ndugu zake wa kiroho, na bila kujali sana usalama wake mwenyewe, Nelson alijitumbukiza ndani ya mto uliokuwa umefurika. “Nilipofika upande ule mwingine,” akumbuka Nelson, “nilisimama na kujaribu kufikiria mahali nilipokuwa. Nilikuwa nimepita katika eneo hili kila siku, nikihubiri nyumba hadi nyumba, lakini singeweza kupata alamardhi hata moja niliyoijua!”

Watu takriban 150 walikuwa wamekufa usiku huo katika Chilanguera. Miongoni mwao kulikuweko watu kadhaa waliokuwa wakijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, hakuna Mashahidi waliobatizwa ambao walikufa.

Punde si punde jitihada za uokoaji zikaanza. Arístedes Estrada, aliyesaidia kupanga shughuli hizi, aeleza hivi: “Hatukuruhusiwa kwenda Chilanguera. Maji yalikuwa yanazidi kuongezeka! Sitasahau kamwe kuona watu waliokuwa wakiomba msaada lakini wakaachwa na waokoaji waliolazimika kutoroka kwa sababu ya uhai wao wenyewe.” Hata hivyo, baada ya muda, ndugu wote walihamishwa kwa njia salama. Majumba ya Ufalme yalitumika kuwa vituo vya wakimbizi. Kwa kuongezea, Mashahidi walipelekwa hospitalini, shuleni, na sehemu nyinginezo ambapo wangeweza kukagua orodha ya waliojeruhiwa na walioachwa bila makao ili kupata majina ya Mashahidi. Makutaniko ya mahali hapo yaliandaa upesi vitu vilivyohitajiwa.

Hata hivyo, haikuwa rahisi sikuzote kupeleka vitu vilivyohitajiwa kwenye vituo vya ukusanyaji. Akina ndugu kutoka mji unaoitwa Corinto walifunga safari wakiwa wamebeba mazao kutoka kwenye mashamba yao, lakini wakakabili maporomoko ya ardhi yaliyofunga njia. Suluhisho lilikuwa nini? Walichimba maporomoko na kupita katikati! Hapo kwanza wapita-njia walitazama wakiwa na shaka. Lakini baada ya muda, walichochewa kujiunga katika jitihada hiyo ya kusaidia kufungua barabara. Akina ndugu kutoka Corinto walifika mwisho wa safari yao wakiwa wamejaa matope lakini wakiwa na furaha kwa mchango waliotoa.

Ofisi ya tawi ya Watch Tower Society ilitumika kuwa mojawapo ya vituo vya ukusanyaji. Gilberto, mfanyakazi aliyesaidia kugawanya misaada, akumbuka hivi: “Ilikuwa ajabu sana! Magari mengi sana yaliwasili hivi kwamba wafanyakazi wa kujitolea walipewa mgawo wa kuyaelekeza kwenye sehemu ya maegesho na kwenye barabara iliyoko upande wa mbele wa ofisi ya tawi.” Inakadiriwa kwamba tani 25 za mavazi na tani 10 za chakula zilichangwa. Iliwachukua wafanyakazi wa kujitolea 15 muda wa juma moja kuchagua nguo na kuzipeleka.

Kimbunga Mitch Chapitia Nikaragua

Kimbunga Mitch kilipita karibu sana na mpaka wa Nikaragua na kusababisha mvua yenye kuleta uharibifu katika nchi hiyo pia. Maelfu ya nyumba zilifagiliwa mbali, pamoja na barabara kuu. Karibu na mji wa Posoltega, maporomoko ya matope yalizika vijiji vizima-vizima—na watu zaidi ya 2,000.

Mashahidi katika Nikaragua walipopata habari kuhusu msiba huo, shirika kubwa sana la kutoa msaada lilianzishwa. Wafanyakazi wa kujitolea walitumwa kufanya kazi ya rehema yenye kuchosha na iliyo hatari—kuwatafuta ndugu zao! Vikundi viwili vya Mashahidi, kimoja kutoka León (mji ulioko kusini ya Posoltega) na kimoja kutoka Chichigalpa (mji ulioko upande wa kaskazini), viliondoka kuelekea Posoltega, kila ndugu akibeba kifurushi kikubwa sana cha misaada. Waokoaji walitoa onyo kwamba njia ilikuwa karibu haipitiki, lakini akina ndugu walikuwa wameazimia.

Mapema asubuhi ya Jumatatu, Novemba 2, akina ndugu kutoka León walipakia maandalizi kwenye lori na kuliendesha hadi mahali ambapo daraja lilikuwa limefagiliwa mbali. Baada ya kupakua mizigo kutoka kwenye lori hilo, akina ndugu waliunda vikundi viwili vya waendesha-baiskeli: Kimoja kielekee Posoltega, na kingine kwenye mji uliokumbwa na mafuriko unaoitwa Telica. Akina ndugu walitoa sala kwanza. “Baada ya sala,” asema mwokoaji mmoja, “tulipata nguvu nyingi kwelikweli.” Wangeihitaji. Walilazimika kuvuka mitaro mikubwa, nyakati nyingine kwa kuteleza juu ya matope na nyakati nyingine kwa kubeba baiskeli mabegani. Mara nyingi miti iliyoanguka iliziba njia. Na walilazimika kuvumilia kuona mambo yenye kutisha, maiti zikielea katika vidimbwi vya maji.

Kwa kushangaza, waendesha-baiskeli kutoka León na Chichigalpa waliwasili Posoltega karibu wakati mmoja! Nerio López, mshiriki wa kikundi cha waokoaji, akumbuka hivi: “Magurudumu ya baiskeli yangu yalikuwa yameisha. Nilifikiri yangetumika tu kwa mwendo wa kilometa moja au mbili.” Lakini, kwa njia fulani baiskeli iliendelea na mwendo. Wakati wa safari ya kurudi ndipo magurudumu yote mawili yalipopasuka. Kwa vyovyote vile, akina ndugu ndio waliokuwa wa kwanza kuwasili kati ya wafanyakazi wa kutoa msaada. Walihisi furaha kama nini walipokutana na kikundi cha akina ndugu na dada Wakristo wa mahali hapo! “Namshukuru sana Yehova na ndugu zetu kwa sababu wametutegemeza na kutusaidia,” akasema dada mmoja. “Hatukuwazia kamwe kwamba ndugu zetu wangekuja kutusaidia upesi namna hiyo.”

Hii ilikuwa safari ya kwanza kufanywa kwa baiskeli kati ya safari kadhaa zilizofanywa kuelekea miji iliyokumbwa na mafuriko, na katika visa vingi akina ndugu walikuwa wa kwanza kuwasili kati ya wafanyakazi wa kutoa msaada. Mji wa Larreynaga ulishuhudia kioja cha akina ndugu 16 waliowasili kwa baiskeli! Akina ndugu wa mahali hapo walitokwa na machozi kwa kuona jitihada zao. Nyakati fulani waendesha-baiskeli walilazimika kubeba mizigo ya kilogramu 20 migongoni mwao. Ndugu wawili walibeba misaada yenye uzito uzidio kilogramu 100 hadi kwenye mji wa El Guayabo! Mwendesha-baiskeli mmoja akiwa amebeba mzigo mkubwa kadiri alivyoweza, alifarijika kwa kutafakari andiko la Biblia kwenye Isaya 40:29: “[Yehova] huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo.”

Mashahidi katika mji wa Tonalá walituma mjumbe kupeleka ripoti kwa akina ndugu wenye madaraka kwamba walikuwa karibu kuishiwa na chakula. Mjumbe huyo alipowasili, alishangaa kuona kwamba misaada ilikuwa imepelekwa tayari! Na alipowasili nyumbani, alipata chakula kikiwa kimefika tayari. Marlon Chavarría, aliyesaidia kupeleka misaada kwenye eneo lililokumbwa na mafuriko kuzunguka Chinandega, akumbuka hivi: “Katika mji mmoja kulikuweko familia 44 za Mashahidi. Hata hivyo, familia 80 zilinufaika kwa sababu akina ndugu waliwagawia wenzao chakula.”

Wenye mamlaka walitambua jitihada za kutoa msaada. Meya wa mji wa Wamblán aliwaandikia Mashahidi, akisema: “Tunawaandikia kuhusu uwezekano wa kupokea msaada fulani. . . . Tunaona jinsi ambavyo mmekuwa mkiwasaidia ndugu na dada zenu hapa katika Wamblán, na tunataka kujua ikiwa mnaweza kutusaidia pia.” Mashahidi wa Yehova waliitikia kwa kupeleka chakula, dawa, na mavazi.

Ghasia Katika Guatemala

Punde tu baada ya kimbunga Mitch kuondoka Honduras na El Salvador, kilikumba Guatemala. Sara Agustín, Shahidi anayeishi kusini ya Guatemala City, aliamshwa na mvumo wa maji yaliyokuwa yamechafuka. Bonde alilokuwa akiishi lilikuwa limegeuzwa kuwa mto wenye kunguruma. Mara nyingi, alikuwa amebisha milango ya majirani wake ili kushiriki kweli ya Biblia. Sasa alienda mlango hadi mlango akijaribu kuwaamsha akiwa tayari kufanya lolote! Baadaye maporomoko ya matope yaliteremka kwa kasi kutoka mlimani, yakifunika nyumba nyingi za majirani wake. Akiwa ameshikilia sepetu, Sara alianza kusaidia waokoaji, kuchimbua chini ili kutoa watoto wadogo saba kwenye matope. Sara ambaye alifanya kazi ya ukunga, alikuwa amesaidia kuzalisha mmoja wa watoto hawa. Kwa kusikitisha, msichana mchanga aliyeitwa Vilma alikuwa miongoni mwa waliokufa. Sara alikuwa amemwangushia fasihi ya Biblia punde kabla ya hapo.

Ingawa kimbunga Mitch kilikuwa kimepungua nguvu, mvua iliyozidi kunyesha iliharibu sana mazao, madaraja, na nyumba. Misaada mingi ilipelekwa kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Guatemala, na ikaamuliwa kwamba misaada hii ingetumiwa kwa njia ifaayo zaidi kusaidia akina ndugu katika Honduras. Kwa kuwa madaraja mengi yalikuwa yamebomoka na uwanja wa ndege ulikuwa umefurika, baadhi ya misaada hiyo ilihitaji kupelekwa kupitia bahari. Frede Bruun, kutoka ofisi ya tawi, aeleza hivi: “Tulikodi mashua yenye bodi la mseto wa glasi na nyuzi yenye urefu wa meta nane na kuanza safari tukiwa tumebeba takriban tani moja ya dawa na chakula. Baada ya safari yenye kuogofya katika bahari iliyochafuka, hatimaye tulifika kwenye bandari ya Omoa, tukiwa tumelowa chepechepe.”

Matokeo ya Baadaye ya Kimbunga Mitch

Kimbunga Mitch kilionekana kuwa kinapungua nguvu upande wa kusini-mashariki mwa Mexico. Hata hivyo, katika jaribio lake la mwisho, kimbunga Mitch kilielekea upande wa kaskazini-mashariki na kukumba kwa kishindo Florida, iliyoko kusini mwa Marekani. Lakini kimbunga Mitch kikapungua nguvu. Kilirudi kuelekea Atlantiki na kikaanza kuchanguka upesi. Kufikia Novemba 5, maonyo yote kuhusu dhoruba ya kitropiki yalikuwa yamekomeshwa.

Wataalamu fulani wamekiiita Mitch kuwa “kimbunga chenye kufisha zaidi kilichowahi kukumba Kizio cha Magharibi katika karne mbili zilizopita!” Huenda idadi kamili ya vifo ikafikia 11,000; maelfu ya watu bado hawajapatikana. Zaidi ya milioni tatu waliachwa bila makao au angalau wakaathiriwa vibaya sana. Rais wa Honduras, Carlos Flores Facusse, aliomboleza: “Tumepoteza vitu tulivyojenga, pole kwa pole, kwa miaka 50.”

Wengi wa Mashahidi wa Yehova walipoteza makao yao kimbunga Mitch kilipowakumba. Kwa kusikitisha, katika visa vingi, ardhi ambayo nyumba zao zilikuwa zimejengwa juu yake ilioshwa na maji! Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova walifanya mipango ya kusaidia wengi warekebishe au wajenge upya nyumba zao.

Misiba yenye kuhuzunisha kama vile Kimbunga Mitch ni kikumbusha chenye kuhofisha kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5) Ulinzi halisi kutokana na misiba ya namna hiyo utapatikana tu wakati Ufalme wa Mungu utakapoanza kusimamia mambo katika sayari hii. (Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 21:3, 4) Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wanashukuru kwamba hakuna mmoja wa ndugu zao aliyepoteza uhai wake kama tokeo la moja kwa moja la kimbunga Mitch.b Kutii amri za kuhama na utaratibu mzuri wa makutaniko ya mahali hapo kulisaidia wengi wahamie mahali palipokuwa salama mbali na hatari hiyo.

Katika miezi michache iliyopita, Mashahidi wa Yehova katika nchi zilizoathiriwa wamefanya kazi kwa bidii ili kurudia utaratibu wao wa kawaida wa mambo ya kiroho. Kwa mfano, katika El Salvador, mipango ilifanywa kusaidia waliokumbwa na dhoruba hiyo wahudhurie mkusanyiko wa wilaya uliofanywa siku chache tu baada ya kutokea kwa kimbunga Mitch. Mabasi yalikodishwa ili kuandaa usafiri, na mahali pa kulala pakapatikana. Hata mipango ilifanywa ya kutibu walio wagonjwa ili wao pia waweze kuhudhuria! Mkusanyiko ulifana, kukiwa na kilele cha wahudhuriaji 46,855—wengi zaidi ya ilivyotazamiwa. “Tulibabaishwa sana na mambo yaliyotupata,” akiri José Rivera, ndugu kutoka El Salvador aliyepoteza nyumba na biashara yake wakati wa kimbunga Mitch. “Lakini tulitoka katika kusanyiko hilo, tukiwa tumebadilishwa kwa sababu ya kushuhudia ukaribishaji-wageni kutoka kwa akina ndugu.” Inaripotiwa kwamba hudhurio la mikutano ya Mashahidi wa Yehova katika nchi hizo limeongezeka kwa njia yenye kutokeza—tokeo la moja kwa moja la watu walio nje kushuhudia jitihada zetu za uokoaji.

Lakini labda Mashahidi ndio waliopata athari kubwa zaidi kuhusiana na tukio hilo. Carlos, mwokokaji wa furiko katika Honduras, asema: “Sijawahi kuona jambo kama hilo. Nimehisi upendo na shauku ya akina ndugu kibinafsi.” Naam, madhara yaliyosababishwa na Kimbunga Mitch siku moja yatasahauliwa. Lakini upendo ulioonyeshwa na Mashahidi wa Yehova, ambao wengi wao walihatarisha uhai na viungo vyao vya mwili ili kuwasaidia ndugu zao, hautasahauliwa kamwe.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa kawaida Mashahidi wa Yehova huitana “ndugu” na “dada.”

b Baada ya dhoruba, visa vya maradhi ya kuambukiza vilizidi. Shahidi mmoja katika Nikaragua alikufa kutokana nayo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

Mashahidi Jirani Watoa Msaada

WATABIRI waliposema kwamba Kimbunga Mitch kingekumba Belize, taifa lilijitayarishia athari hiyo. Kwa kuwa serikali ilikuwa imetoa amri watu wahame maeneo yote ya pwani na ya chini, Mashahidi wa Yehova walihamia kwenye jiji kuu, Belmopan, karibu kilometa 80 barani au hadi kwenye miji mingine iliyoko milimani.

Kwa uzuri, Belize haikupatwa na madhara ya Mitch. Lakini waliposikia juu ya hali mbaya ya ndugu zao katika Honduras, Nikaragua, na Guatemala, akina ndugu katika Belize walitoa chakula, mavazi, maji safi, na pesa.

Kwa kweli, akina ndugu katika nchi zilizo jirani waliitikia kwa njia hiyohiyo. Mashahidi katika Kosta Rika walipeleka kontena nne kubwa za chakula, mavazi, na dawa. Akina ndugu katika Panama walisimamisha vituo vinne vya kupokea, kuchagua, na kupakia vitu vilivyotolewa. Katika siku chache, misaada inayozidi kilogramu 20,000 ilikuwa imekusanywa. Mtu mmoja asiyekuwa Shahidi alisema hivi: “Nilifikiri kwamba majeshi ndiyo yaliyokuwa namba moja katika kupanga kazi ya kutoa msaada. Lakini sasa ninaona Mashahidi wa Yehova ndio wa kwanza.” Sasa Mashahidi wameanza kumtembelea mtu huyo kwa ukawaida ili kushiriki naye kweli za Biblia.

Ndugu mmoja anayefanya kazi katika shirika la usafiri alitoa trela ndogo na dereva (asiyekuwa Shahidi) kupeleka misaada huko Nikaragua. Maofisa katika Panama na Kosta Rika hawakudai ushuru wa forodha waliporuhusu lori hilo lipite kwenye mipaka yao. Kituo kimoja cha petroli kilitoa fueli ya kutosha kujaza matangi yote mawili ya lori hilo—iliyotosha safari ya kwenda na kurudi! Katika Nikaragua maofisa wa forodha vilevile hawakukagua vifurushi hivyo. “Ikiwa vitu hivi vinatoka kwa Mashahidi wa Yehova, hatuhitaji kuvikagua,” wakasema. “Hawatusumbui kamwe.”

Hata hivyo, usafiri wa barabarani hadi Honduras, haukuwezekana. Lakini dada Mkristo anayefanya kazi katika Ubalozi wa Honduras aliweza kufanya mipango kupitia kwa ubalozi huo kupeleka misaada kwa ndege bila malipo! Misaada inayozidi uzito wa kilogramu 10,000 iliweza kupelekwa kwa kutumia njia hii.

Kwa kupendeza, watu fulani wasiokuwa Mashahidi walivutiwa sana na kazi ya uokoaji ya Mashahidi. Makampuni fulani yalitoa masanduku ya kadibodi, tepu, na vyombo vya plastiki. Mengine yalitoa pesa na kupunguza bei za vitu. Wafanyakazi wa uwanja wa ndege katika Panama walivutiwa hasa kuona zaidi ya wafanyakazi wa kujitolea 20 waliokuwa Mashahidi wakisaidia kupakua misaada iliyotolewa kupelekwa Honduras. Siku iliyofuata, baadhi ya wafanyakazi hawa wa uwanja wa ndege walijitokeza wakiwa na michango waliyokuwa wamekusanya miongoni mwao wenyewe.

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

Kazi ya Kutoa Msaada Inayofanana na Hiyo Katika Mexico

MEXICO haikuathiriwa sana na Kimbunga Mitch. Lakini majuma kadhaa kabla tu kimbunga hicho chenye kufisha kukumba Amerika ya Kati, kulikuwa na furiko kubwa sana katika jimbo la Chiapas. Karibu jumuiya 350 ziliathiriwa; miji fulani mizima-mizima ilitoweka.

Bila shaka, furiko hilo lilisababisha magumu mengi kwa Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo. Hata hivyo, hatua ya haraka ya wazee wa kutaniko la mahali hapo mara nyingi ilisaidia kupunguza athari za dhoruba. Kwa mfano, katika jumuiya moja ndogo, wazee walizuru kila mshiriki wa kutaniko na kuwaonya wakimbilie kwenye Jumba la Ufalme ikiwa mvua ingeendelea kunyesha. Jumba hilo lilionwa kuwa jengo madhubuti zaidi katika jumuiya hiyo. Kwenye mapambazuko, mji huo ulikumbwa na kani kutoka mito miwili iliyokuwa imefurika! Mashahidi—pamoja na majirani kadhaa—waliokoka shambulizi hilo kwa kukimbia na kupanda kwenye paa ya Jumba la Ufalme. Hakuna Shahidi hata mmoja aliyekufa.

Hata hivyo, takriban Mashahidi 1,000 katika Mexico walilazimika kuhama kwenye makao ya serikali. Takriban nyumba 156 za Mashahidi ziliharibiwa kabisa, na 24 zikaharibiwa kwa kiasi fulani. Kwa kuongezea, Majumba ya Ufalme saba yaliharibiwa kabisa.

Hivyo, halmashauri sita za kutoa msaada zilipangwa ili kushughulikia mahitaji ya Mashahidi wa Yehova na majirani wao. Upesi, chakula, mavazi, blanketi, na vitu vinginevyo viligawanywa. Kwa hakika, wasimamizi wa mahali hapo walipoelezwa kadiri kazi ya uokoaji ilivyokuwa imefanywa, walisema: “Hata majeshi hayajawahi kufanya haraka namna hiyo.”

Kwa muda mrefu Mashahidi wa Yehova wamekuwa na sifa ya ufuatiaji haki, na mara nyingi jambo hilo limewanufaisha. Kwa mfano, kikundi cha watu fulani kilipoomba msaada kutoka kwa wasimamizi wa mahali hapo, waliulizwa ikiwa kulikuwa Shahidi wa Yehova yeyote katika jumuiya yao. Waliposema ndiyo, wasimamizi hao waliwaambia: “Basi leteni mmoja wao ili tumpe misaada!”

Mzee wa kutaniko mwenyeji aeleza kwa njia nzuri na kwa muhtasari jinsi mambo yalivyokuwa anapoandika: “Akina ndugu wamedumisha mtazamo mzuri licha ya msiba huo. Kwa kuhatarisha uhai wao wenyewe, ndugu wengi kutoka jumuiya za karibu walikuja kutusaidia wakiwa na chakula na vichapo vya Biblia ili kutuimarisha. Tuna mengi sana ya kumshukuru Yehova.”

Ramani/Picha katika ukurasa wa 14]

Mexico

Guatemala

El Salvador

Belize

Honduras

Nikaragua

Kosta Rika

[Picha katika ukurasa wa 15]

HONDURAS

◼ Mto Guacerique

[Picha katika ukurasa wa 16]

EL SALVADOR

◼ Barabara Kuu katika Chilanguera

◼ José Lemus na binti zake waliokoka, pamoja na Jumba la Ufalme

◼ José Santos Hernandez, akiwa mbele ya nyumba yake iliyoharibiwa

[Picha katika ukurasa wa 17]

NIKARAGUA

◼ Kikundi cha waendesha-baiskeli cha kwanza kuelekea Telica

◼ Mashahidi katika El Guayabo walipokea vifurushi vya chakula kwa furaha

[Picha katika ukurasa wa 18]

NIKARAGUA

◼ Wafanyakazi wa kujitolea wajenga upya nyumba ya kwanza kati ya zile nyingi

◼ Mashahidi kutoka makutaniko ya mahali hapo walisaidia kupakia vifurushi vya chakula

[Picha katika ukurasa wa 18]

GUATEMALA

◼ Sara alisaidia kuokoa watoto saba kutoka kwenye matope

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki