Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 6/22 kur. 16-19
  • Waaltai—Watu Tuliopata Kuwapenda

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Waaltai—Watu Tuliopata Kuwapenda
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nchi na Dini Yao
  • Matokeo ya Uwasiliani-Roho
  • Ibada ya Kikristo Yasitawi
  • Kushiriki Katika Huduma
  • Tulipokuwa Tukirudi
  • Kutafuta Hazina Kwenye Milima Maridadi ya Altay
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Hazina Iliyofichika Yafunuka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Nilifurahia Kufanya Mengi Zaidi
    Amkeni!—2005
  • Warusi Wathamini Sana Uhuru wa Kuabudu
    Amkeni!—2000
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 6/22 kur. 16-19

Waaltai—Watu Tuliopata Kuwapenda

Katika karne iliyopita, kasisi wa kanisa la Othodoksi ya Urusi Archimandrite Makarios alitafsiri Biblia ya “Agano la Kale” katika Kirusi. Hata hivyo, kabla ya kufanya hivyo, alitumwa na sinodi ya kanisa awafundishe Waaltai Ukristo. Waaltai ni nani? Wanaishi wapi? Nao wanaishije?

WAALTAI wapatao 40 walihudhuria mojawapo ya mikusanyiko ya wilaya ya Mashahidi wa Yehova iliyofanywa Urusi mwezi wa Julai mwaka uliopita. Ulifanyiwa Barnaul, jiji kuu zaidi katika Altay Kray huko Urusi. Mkusanyiko huo ulihudhuriwa na watu 1,730. Nilisafiri kwa ndege pamoja na marafiki wangu kutoka St. Petersburg umbali wa kilometa zipatazo 6,500, ili kuhudhuria mkusanyiko huo wa siku tatu.

Siku chache tulizokuwa Barnaul, tulipata kuwajua na kuwapenda sana Waaltai tuliokutana nao. Tulisisimuka sana hasa tulipojulishwa kwamba wengi wao walikuwa wamesafiri kwa basi kilometa zipatazo 650 kupitia barabara za mlimani na kwamba hata mwamba ulipoanguka na kupasua kioo cha basi lao, hawakufikiria kurudi. Tulipojifunza juu ya nchi yao na utamaduni wao, tulikuwa na hamu ya kuwatembelea nyumbani na vijijini mwao. Hivyo baada ya mkusanyiko, tulifunga safari yenye kusisimua sana ya zaidi ya kilometa 1,500 katika nchi ya Waaltai.

Nchi na Dini Yao

Wengi wa wakazi wa Altai wa awali wapatao 70,000, huishi katika maeneo ya mlimani karibu na mpaka wa Kazakhstan, China, na Mongolia. Mandhari ya eneo hilo ilikuwa yenye kutia kicho—maridadi na yenye milima-milima, mito yenye maji safi sana na maua mengi. Wakazi wa eneo hili hukusanya mizizi mbalimbali ambayo wanaitumia kutengenezea chai tamu yenye harufu nzuri. Wao pia hupenda kula kokwa za msonobari.

Baadhi ya Waaltai humiliki mashamba. Shahidi mmoja alisema kwamba yeye pamoja na jamaa zake wana ng’ombe 75, na kondoo 80. Wao huuza nyama, na kubadilishana sufu ili wapate unga na sukari. Dada mwingine Mkristo aliniambia kuwa aliuza wana-kondoo wanne ili yeye na bintiye waweze kuhudhuria mkusanyiko. Watu wengine saba waliandamana naye, mafunzo yake ya Biblia! Mmoja wao aliniambia hivi tulipokuwa mkusanyikoni: “Tuna njia moja tu ya maisha—njia ya Mungu.”

Ijapokuwa hili ni eneo la mbali sana lenye uzuri wa ajabu—wageni huliita Alp nyingine ya Uswisi—maisha yamebadilika sana hapa pia. Mtu mmoja mzee-mzee alituambia hivi: “Kama ningeambiwa na mtu fulani miaka kadhaa iliyopita kwamba ningehitaji kufunga kibanda changu kabla ya kulala, singemwamini. Lakini sasa nafanya hivyo kila usiku.” “Nyakati [hizi] za hatari” zimechochea wengi kuchunguza unabii wa Biblia.— 2 Timotheo 3:1-5.

Kwa kawaida Waaltai hujivunia mapokeo yao ya kale na ibada yao. Wengi wao huamini roho zilizo mtoni na mlimani—kwao mlima ni ishara ya miungu yao. Wao pia huabudu wanyama, na hata huchora mfano wa sungura kwenye kitambaa cheupe na kukiangika katika ukuta wa kibanda chao. Mvua ya radi ya kwanza katika msimu wa mvua inyeshapo, wao hutekeleza desturi fulani mbele ya mfano huo wa sungura, wakiunyunyizia chai, maziwa, au kinywaji chenye kulevya kinachoitwa arrack. Lakini wanaabudu hasa zile wanazoamini kuwa roho za wafu.

Viongozi wao wa kidini huitwa mashamani. Wakati wa masika na majani yanapopukutika, mashamani hutekeleza desturi katika ‘sehemu takatifu’ juu ya milima au kwenye miteremko ya milima. Mashamani hufunga vitambaa vidogo vyeupe kwenye matawi ya miti, huku wakifunika miti mingi, watekelezapo desturi hizo. Wanaamini kuwa roho za mlimani zitafurahi wafanyapo hivyo na kwamba roho hizo zitawalinda na aksidenti wanaposafiri.

Matokeo ya Uwasiliani-Roho

Hata hivyo, kilichonivutia zaidi pamoja na marafiki wangu ni watu hao wachangamfu na wenye moyo mweupe. Tulikutana na Svetlana na bintiye Tulunai katika Barnaul na tukafurahia ukaribishaji-wageni wao katika kijiji cha Ustʹ-Kan, chenye wakazi wapatao 3,000. Kulingana na mapokeo yao, nyanya yake Svetlana ndiye aliyemlea kwa kushirikiana kwa ukaribu na mashamani. Kwa hakika, Svetlana alijifunza kuwasiliana na zile zilizodaiwa kuwa roho za wafu. Kama tokeo la ujuzi wake wa pekee, Svetlana alipewa wadhifa mkubwa aliofurahia.

Lakini alianza kupatwa na matatizo mengi. “Niliteswa na roho-waovu,” akaniambia. “Singeweza kulala vema usiku.” Nyakati nyingine, angekuwa katika hali ya kupumbaa akili. “Wakati mmoja,” yeye aeleza, “nilimwona binti yangu Tulunai mwenye umri wa miezi sita akifanana na mwana-nguruwe aliyekuwa akitambaa kunijia. Nilitaka kumnyonga. Lakini Tulunai akaanza kulia kwa sauti. Nilishtuka niliporudiwa na fahamu na kutambua kwamba karibu nimuue binti yangu.” Svetlana alianza kufikiria hawa roho waovu ni nani.

Ndipo mwanamke mmoja Mwaltai akapeleka fasihi kadhaa za Biblia zinazochapwa na Mashahidi wa Yehova huko Ustʹ-Kan mnamo mwaka wa 1991. Kila mara Svetlana alipoanza kusoma broshua “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya,” angeshikwa na usingizi. “Ningecheka-cheka,” yeye akasema, “na kusema kwamba Mashahidi walinipa kitu bora kuliko dawa yoyote ya usingizi.” Lakini bado alipata maono ya kusumbua usiku na kwa hivyo akatoa sala ya kutoka moyoni: “Yehova, ikiwa wewe ni mwenye nguvu nyingi, tafadhali nisaidie niepuke ndoto hizi za kuogofya.” Baada ya muda mfupi, hali ikawa bora naye akahisi vema.

Svetlana alianza kusali kabla ya kulala usiku, naye alishangaa kwamba angelala upesi. “Inashangaza kwamba ningeweza kulala kama mtu wa kawaida,” akasema. Aliamua kujifunza Biblia kwa bidii kwa msaada wa vichapo vya Watch Tower Society, na mnamo mwaka wa 1992 alionyesha wakfu wake kwa Yehova Mungu kwa ubatizo wa maji. “Nilijifunza kwamba ukimtumaini Yehova kikamili, hakuna jambo lisilowezekana,” yeye akaniambia.—Wafilipi 4:13.

Ibada ya Kikristo Yasitawi

Mwaka wa 1993 kutaniko la Mashahidi wa Yehova lilianzishwa katika Ustʹ-Kan, na watu 70 walikuwa wakihudhuria mikutano huko. Katika Aprili mwaka wa 1998, watu 120 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kijiji cha Yakonur, kilichoko kilometa chache kaskazini ya Ustʹ-Kan, wakati mmoja kilionwa kuwa kitovu cha ushamanisti. Lakini mtu aitwaye Shamyt alisema kwamba Mashahidi walipoanza kuhubiri huko, mashamani walianza kupoteza mamlaka yao. Sasa kuna kikundi cha Mashahidi wenye bidii katika kijiji hicho, na watu wengi wanapendezwa na Biblia.

Inasemekana kuwa wengi wa wakazi wapatao 500 wa kijiji cha Chagan-Uzun, kilichoko kilometa zipatazo 90 kutoka mpaka wa Mongolia, husoma vichapo vyetu. Na katika Gorno-Altaysk, mji mkuu wa Jamhuri ya Altay, kuna makutaniko mawili yenye Mashahidi 160 hivi.

Hata hivyo, mapema mwaka wa 1994 Mashahidi wengi kutia na wale wa Ustʹ-Kan, waliitwa kortini huko Gorno-Altaysk. Walishtakiwa kwa makosa mabaya kama vile zoea la kuwadhabihu watoto. Kwa sababu ya upinzani huo, baadhi ya Mashahidi walifutwa kazi na kufukuzwa Altay. Lakini baada ya muda ikawa wazi kwamba mashtaka yaliyotolewa dhidi ya Mashahidi yalikuwa bandia. Hivyo, katika Mei 1994, idara ya Sheria ya Jamhuri ya Altay ilisajili kihalali jumuiya ya Mashahidi wa Yehova katika Gorno-Altaysk. Leo Mashahidi pamoja na fasihi zao za Biblia zinajulikana kotekote katika Altay.

Kushiriki Katika Huduma

Tulipozuru Ustʹ-Kan, tuliweza kushiriki huduma ya peupe pamoja na Mashahidi wa huko. Kwa kweli, kulikuwa na uvumi kwamba wageni walikuwa wakija. Kwa hiyo ripota mmoja wa gazeti la huko alipotuona tukihubiri alikaribia kikundi chetu na kusema: “Nilisikia kwamba watu fulani mashuhuri walikuwa wakizuru eneo hili. Naweza kuwaonaje?”

Alishangaa kama nini alipoambiwa kuwa sisi ndio watu waliodhaniwa kuwa mashuhuri! Alishangaa kwamba tukiwa pamoja na wakazi wa eneo hilo tulikuwa tukizuru makao ya majirani wake. Tulipozungumza naye alisema: “Naona kwamba hakuna mabwana wakubwa miongoni mwenu. Nyinyi ni watu wa kawaida tu wasiojiona kuwa wa pekee. Kwa kweli hili linastaajabisha! Nyinyi ni Wakristo halisi, nami napenda kazi yenu.”

Kwa kusikitisha ziara yetu ikaisha haraka. Tulipokuwa tukiondoka, rafiki zetu walilia machozi. Walisimama pamoja karibu-karibu, na kutuzingira. Hii ndiyo njia ya kawaida ya Waaltai ya kuwaaga marafiki wao wapendwa. Siku chache tulizokuwa nao, tulisitawisha shauku yenye kina kirefu kwa mmoja na mwenzake. Tulipata kuwa marafiki wa kweli. Kwa nini? Kwa sababu aliyetuunganisha ni Yehova, Mungu asiyebagua.—Matendo 10:34.

Tulipokuwa Tukirudi

Tulipokuwa tukirudi Barnaul, tulisimama penye duka moja katika kijiji kidogo mlimani. Muuzaji aliyekuwa peke yake alifurahi kutuona. Baada ya kuzungumza naye kwa muda, nilimuuliza: “Je, umewahi kusikia jina Makarios?”

“La, sijawahi,” yeye akajibu, baada ya kutua kidogo.

Kwa hiyo nikamwonyesha nakala ya tafsiri ya Biblia ya Makarios na kueleza hivi: “Makarios aliitafsiri Biblia hii karne iliyopita, katika nchi hii ya Altay.” Kisha, nilimpa Biblia hiyo kama zawadi.

Tulipoendelea kutazama huku na huku, yule mwanamke alianza kuisoma mara moja. Kwa ghafula, tuliona uso wake uking’aa kwa tumaini. Tulipokuwa tukiondoka, alituambia kwamba ana marafiki wengi na watu wa ukoo ambao watapendezwa na Biblia hiyo. Kwa hiyo kabla ya kumuaga kabisa, tulimwachia fasihi kadhaa za Biblia.

Ni jambo lenye kuthawabisha kama nini kujua kwamba ijapokuwa miaka 150 imepita tangu Makarios alipoishi na Waaltai na kuitafsiri Biblia yake, Waaltai wengi wananufaishwa na Biblia hiyo leo!—Imechangwa.

[Ramani katika ukurasa wa 17]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

URUSI

Altay

Gorno-Altay

Kazakhstan

China

Mongolia

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Waaltai wakiwa kwenye mkusanyiko huko Barnaul

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Mandhari katika Altay

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wengi huamini kwamba vipande hivi vya vitambaa huwalinda wasafiri

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuhubiri katika Ust’-Kan

[Picha katika ukurasa wa 18]

Svetlana na bintiye

[Picha katika ukurasa wa 19]

Biblia ya Makarios

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki