Hazina Iliyofichika Yafunuka
Simulizi juu ya Biblia ya Makarios
MWAKA wa 1993, mtafiti fulani alipata rundo la magazeti ya zamani ya Orthodox Review yaliyogeuka kuwa manjano katika Maktaba ya Kitaifa ya Urusi iliyoko St. Petersburg. Ndani ya kurasa za magazeti ya mwaka wa 1860 hadi wa 1867 palikuwa na hazina ambayo watu wa Urusi walikuwa wamefichwa kwa zaidi ya karne moja. Ilikuwa tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania yote, au “Agano la Kale,” ya Biblia katika lugha ya Kirusi!
Watafsiri wa hayo Maandiko walikuwa Mikhail Iakovlevich Glukharev, ajulikanaye kuwa Mwadhamu Makarios, na Gerasim Petrovich Pavsky. Wote wawili walikuwa washiriki mashuhuri wa Kanisa Othodoksi la Kirusi na vilevile wasomi wa lugha. Wanaume hawa walipoanza kazi yao mapema katika karne iliyopita, Biblia nzima ilikuwa bado haijatafsiriwa katika Kirusi.
Ni kweli, Biblia ilikuwa katika Kislavoni, lugha iliyotangulia Kirusi cha siku ya kisasa. Hata hivyo, kufikia katikati ya karne ya 19, lugha ya Kislavoni ilikuwa haitumiki ila katika ibada za kidini, ambako ilitumiwa na makasisi. Hali kama hiyo ilikuwako Magharibi, ambako Kanisa Katoliki ya Kiroma lilijaribu kuiweka Biblia katika Kilatini pekee lugha ambayo haikutumiwa katika uwasiliano wa kila siku.
Makarios na Pavsky walijaribu kuifanya Biblia ipatikane kwa watu wa kawaida. Kwa hiyo, uvumbuzi wa tafsiri yao iliyosahaulika kwa muda mrefu, umefanya iwezekane kurudisha sehemu ya maana ya urithi wa kifasihi na wa kidini wa Urusi.
Hata hivyo, Makarios na Pavsky walikuwa akina nani? Na kwa nini jitihada zao za kuitafsiri Biblia katika lugha ya kawaida ya watu zilikabili ukinzani wa namna hiyo? Simulizi juu yao ni lenye kuvutia sana na lenye kutia nguvu imani ya wale waipendao Biblia.
Kuhitajiwa kwa Biblia ya Kirusi
Makarios na Pavsky hawakuwa ndio watu wa kwanza kuona uhitaji wa Biblia katika lugha ya kawaida ya watu. Miaka 100 mapema, Zari wa Urusi, Peter wa Kwanza, au Peter Mkubwa, pia aliona uhitaji huo. La muhimu ni kwamba, alistahi Maandiko Matakatifu na anukuliwa akisema hivi: “Biblia ni kitabu ambacho chazidi kwa ubora vitabu vingine vyote, na kina kila kitu kinachohusiana na wajibu wa mwanadamu kwa Mungu na kwa jirani yake.”
Hivyo, mwaka wa 1716, Peter aliamuru watu wa nyumba yake ya kifalme waichape Biblia huko Amsterdam, kwa gharama zake mwenyewe. Ilibidi kila ukurasa uwe na safu ya maandishi ya Kirusi na safu ya maandishi ya Kiholanzi. Katika 1717, mwaka mmoja tu baadaye, sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au “Agano Jipya,” ilikuwa tayari.
Kufikia mwaka wa 1721 ile sehemu ya tafsiri ya Kiholanzi yenye mabuku manne ya Maandiko ya Kiebrania ilikuwa pia imechapwa. Safu moja iliachwa ikiwa tupu, ili ipate kujazwa baadaye na maandishi ya Kirusi. Peter alikabidhi hizo Biblia kwa “Sinodi Takatifu” ya Kanisa Othodoksi la Kirusi—ile mamlaka kuu ya kidini ya kanisa—ili itamatishe uchapaji na kusimamia ugawanyaji. Hata hivyo, sinodi haikukamilisha kazi hiyo.
Miaka ipunguayo minne baadaye, Peter alikuwa amekufa. Ni nini kilichozipata Biblia zake? Zile safu tupu zilizokusudiwa maandishi ya Kirusi hazikutumiwa kamwe. Hizo Biblia zilipangwa katika marundo makubwa katika chumba cha chini, ambamo zilioza—hakuna nakala hata moja ambayo ingepatikana baadaye ikiwa haijaharibika! Uamuzi wa sinodi ulikuwa ni “kuwauzia wafanya-biashara nakala zote zilizobaki.”
Jitihada za Kutafsiri Zaanza
Mwaka wa 1812, John Paterson, mshiriki wa British and Foreign Bible Society, alikuja Urusi. Paterson aliamsha upendezi wa watu wenye akili wa St. Petersburg kufanyiza sosaiti ya Biblia. Desemba 6, 1812—mwaka uleule ambao jeshi la Urusi lilirudisha nyuma askari wenye kuvamia wa Napoléon wa Kwanza—Zari Aleksandr wa Kwanza alikubali mkataba wa kufanyizwa kwa sosaiti ya Biblia ya Kirusi. Mwaka wa 1815 Zari aliamuru mwenyekiti wa hiyo sosaiti, Mwana-Mfalme Alexsandr Golitsyn, aidokezee sinodi yenye kuongoza kwamba “Warusi pia wapaswa kuwa na fursa ya kusoma Neno la Mungu katika lugha yao wenyewe.”
Jambo la kupongezwa ni kwamba, kibali kilitolewa cha kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika Kirusi moja kwa moja kutoka Kiebrania cha awali. Tafsiri ya kale ya Septuagint ya Kigiriki ilikuwa imekuwa msingi wa kutafsiriwa kwa Maandiko ya Kiebrania katika Kislavoni. Wale ambao wangeitafsiri Biblia katika Kirusi waliambiwa kwamba kanuni kuu za hiyo tafsiri zingekuwa usahihi, uwazi, na usafi. Ni nini kilichopata jitihada hizi za mapema za kuandaa Biblia katika lugha ya Kirusi?
Kutafsiriwa kwa Biblia Kwafikia Kikomo?
Wasiopendelea mabadiliko katika kanisa na katika serikali upesi wakawa na hadhari juu ya uvutano wa kidini na kisiasa wa kigeni. Zaidi, viongozi fulani wa kanisa walidai kwamba Kislavoni—lugha ya liturjia—ilionyesha ujumbe wa Biblia vizuri zaidi ya Kirusi.
Hivyo Russian Bible Society ilivunjwa mwaka wa 1826. Maelfu kadhaa ya nakala za tafsiri zilizotokezwa na hiyo sosaiti ya Biblia zilichomwa. Tokeo ni kwamba, Biblia ilichukua mahali pa pili baada ya desturi na pokeo. Ikifuata kiolezo kilichowekwa na Kanisa Katoliki la Kiroma, hiyo sinodi iliagiza hivi mwaka wa 1836: “Yaruhusika kwa mtu wa kawaida aliye mstahifu kusikia Maandiko, lakini hairuhusiki kwa yeyote kusoma sehemu fulani za Maandiko, hasa Agano la Kale, bila mwongozo.” Kutafsiriwa kwa Biblia kulionekana kuwa kumefikia kikomo.
Tafsiri ya Pavsky
Wakati huohuo, Gerasim Pavsky, profesa wa Kiebrania, alichukua daraka la kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika Kirusi. Mwaka wa 1821 alimaliza kutafsiri Zaburi. Zari aliikubali upesi, na kufikia Januari 1822 kitabu cha Zaburi kilikuwa kimetolewa kwa watu wote. Kilipokewa mara moja na ilibidi kichapwe tena mara 12—jumla ya nakala 100,000!
Jitihada za Pavsky za kisomi zilifanya aheshimiwe na wasomi wa lugha na wanatheolojia wengi. Afafanuliwa kuwa mtu mnyoofu na mwenye kufuata haki ambaye hakuathiriwa na njama zilizomzunguka. Kujapokuwa na upinzani wa kanisa dhidi ya hiyo Russian Bible Society na uhakika wa kwamba watu fulani walihisi iliwakilisha masilahi ya kigeni, Profesa Pavsky aliendelea kutafsiri mistari ya Biblia katika Kirusi kwenye mihadhara yake. Wanafunzi wake wenye kumsifu kwa kustaajabia waliandika kwa mkono fasili zake na, baada ya muda, wakaweza kukusanya tafsiri yake. Mwaka wa 1839 walijijasirisha na kuchapisha nakala 150 kwenye matbaa ya chuo—bila ruhusa ya wachujaji.
Tafsiri ya Pavsky iliwavutia sana wasomaji, na wenye kudai waipate wakafuliza kuongezeka. Lakini mwaka wa 1841 lalamiko kutoka chanzo kisichojulikana lilifanywa kwa sinodi kuhusu “hatari” ya tafsiri hiyo, likidai kwamba hiyo tafsiri ilipotea njia kutoka kwenye fundisho la Imani ya Kidesturi. Miaka miwili baadaye hiyo sinodi ilitoa agizo hili: “Twaeni na kuziharibu nakala zote zilizoko za tafsiri ya G. Pavsky ya Agano la Kale zilizoandikwa kwa mkono na kwa lithografia.”
Kulitukuza Jina la Mungu
Hata hivyo, Pavsky alikuwa amewasha tena upendezi katika kutafsiri Biblia. Alikuwa pia ameweka kielelezo cha maana kwa watafsiri wa wakati ujao kuhusiana na suala jingine la maana—Jina la Mungu.
Korsunsky, mtafiti Mrusi alieleza hivi: ‘Jina lenyewe la Mungu, lililo takatifu zaidi ya majina yake yote, lilitungwa kwa herufi nne za Kiebrania יהוה na sasa latamkwa Yehova.’ Katika nakala za kale za Biblia, jina hilo la pekee la Mungu laonekana maelfu ya mara katika Maandiko ya Kiebrania peke yake. Hata hivyo, Wayahudi walikuja kuamini kimakosa kwamba jina la Mungu lilikuwa takatifu mno lisiweze kuandikwa au kutamkwa. Kuhusu hilo, Korsunsky alisema hivi: ‘Katika kusema au kuandika, kwa kawaida mahali pake palichukuliwa na neno Adonai, ambalo kwa kawaida lilitafsiriwa “Bwana.”’
Kwa wazi, jina la Mungu liliacha kutumiwa kwa sababu ya hofu ya kishirikina—si kicho cha kimungu. Hakuna mahali popote ambapo Biblia hupinga matumizi ya jina la Mungu. Mungu mwenyewe alimwambia Musa hivi: “Waambie wana wa Israeli maneno haya, BWANA [“Yehova,” NW], Mungu wa baba zenu . . . amenituma kwenu; hili ndilo jina langu hata milele, nalo ni kumbukumbu langu hata vizazi vyote.” (Kutoka 3:15) Maandiko yawahimiza waabudu tena na tena hivi: “Mshukuruni BWANA [“Yehova,” NW], liitieni jina lake.” (Isaya 12:4) Hata hivyo, watafsiri walio wengi wa Biblia walichagua kufuata pokeo la Kiyahudi na kuepuka kulitumia jina la Mungu.
Hata hivyo, Pavsky hakufuata mapokeo hayo. Katika tafsiri yake ya Zaburi peke yake, jina Yehova laonekana zaidi ya mara 35. Ujasiri wake ungekuwa na uvutano wa maana juu ya mmojawapo wa watu walioishi siku yake.
Mwadhamu Makarios
Mtu huyo ambaye aliishi siku yake alikuwa Mwadhamu Makarios, mmishonari Mrusi mwenye imani ya kidesturi aliyekuwa na ustadi wa isimu wenye kutisha. Akiwa na umri mchanga wa miaka saba, angeweza kutafsiri maandishi mafupi ya Kirusi katika Kilatini. Kufikia wakati alipokuwa na umri wa miaka 20, alijua Kiebrania, Kijerumani, na Kifaransa. Hata hivyo, mtazamo wa unyenyekevu na hisi kali ya daraka lake mbele ya Mungu zilimsaidia kuepuka mtego wa kuwa na hakika kupita kiasi. Alitafuta tena na tena ushauri wa wana-isimu na wasomi wengine.
Makarios alitaka kurekebisha utendaji wa mishonari katika Urusi. Alihisi kwamba kabla ya kuupeleka Ukristo kwa Waislamu na Wayahudi walio Urusi, kanisa lilipaswa “kuelimisha umma kwa kuanzisha shule na kugawanya Biblia katika lugha ya Kirusi.” Katika Machi 1839, Makarios aliwasili St. Petersburg, akitumaini kupata ruhusa ya kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika Kirusi.
Makarios alikuwa tayari ametafsiri vitabu vya Biblia, cha Isaya na cha Ayubu. Hata hivyo, sinodi ilikataa kumpa ruhusa ya kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika Kirusi. Kwa kweli, Makarios aliambiwa asahau wazo la kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika lugha ya Kirusi. Sinodi ilitoa sheria, yenye tarehe ya Aprili 11, 1841, ikimwamuru Makarios “kutumikia muda wa kuonyesha toba ya kati ya majuma matatu hadi sita kwenye nyumba ya askofu fulani katika Tomsk ili asafishe dhamiri yake kupitia sala na kupiga magoti.”
Msimamo Wenye Ujasiri wa Makarios
Kuanzia Desemba 1841 hadi Januari 1842, Makarios alitimiza wonyesho wake wa toba kwa utii. Lakini mara jambo hilo lilipotimizwa, alianza mara moja kutafsiri sehemu iliyosalia ya Maandiko ya Kiebrania. Alikuwa amepata nakala ya tafsiri ya Pavsky ya Maandiko ya Kiebrania na kuitumia ili ahakiki fasili zake. Kama Pavsky, alikataa kuficha jina la Mungu. Kwa hakika, jina Yehova laonekana zaidi ya mara 3,500 katika tafsiri ya Makarios!
Makarios aliwapelekea marafiki wake wenye mtazamo ufaao nakala za tafsiri yake. Ingawa nakala chache zilizoandikwa kwa mkono ziligawanywa, kanisa liliendelea kuzuia kuchapishwa kwa tafsiri yake. Makarios alifanya mipango ya kuendeleza kazi yake ng’ambo. Siku ya kuamkia kuondoka kwake, akawa mgonjwa kisha akafa muda mfupi baadaye, mwaka wa 1847. Tafsiri yake ya Biblia haikuchapishwa kamwe katika muda wa maisha yake.
Yachapishwa Mwishowe!
Mwishowe, hali za kisiasa na za kidini zilibadilika. Hali mpya ya kupendelea maendeleo na mabadiliko ilikumba Urusi, na mwaka wa 1856 sinodi ikakubali kwa mara nyingine tena kutafsiriwa kwa Biblia katika Kirusi. Katika hali hii iliyoboreshwa, Biblia ya Makarios ilichapishwa sehemu-sehemu katika gazeti la Orthodox Review kati ya mwaka wa 1860 na wa 1867, chini ya kichwa An Experiment of Translation Into the Russian Language (Jaribio la Kutafsiri Katika Lugha ya Kirusi.)
Askofu mkuu Filaretwa wa Chernigov, msomi wa fasihi ya kidini ya Kirusi, alitoa kadirio hili juu ya Biblia ya Makarios: “Tafsiri yake yashikamana sana na maandishi ya Kiebrania, na lugha ya hiyo tafsiri ni safi na yaifaa hiyo habari.”
Hata hivyo, Biblia ya Makarios haikutolewa kamwe kwa watu wote kwa ujumla. Kwa kweli, ilisahaulika kabisa. Hatimaye, mwaka wa 1876 Biblia nzima, kutia na Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki, ilitafsiriwa katika Kirusi kwa kibali cha sinodi. Mara nyingi Biblia hiyo nzima huitwa tafsiri ya sinodi. Kinyume cha matazamio, tafsiri ya Makarios, pamoja na ya Pavsky, zilitumika zikiwa chanzo cha msingi cha tafsiri hiyo “rasmi” ya Kanisa Othodoksi la Kirusi. Lakini jina la Mungu lilitumiwa katika mahali pachache ambapo latumiwa katika Kiebrania.
Biblia ya Makarios Leo
Biblia ya Makarios ilibaki bila kuonekana hadi mwaka wa 1993. Kama ambavyo imetajwa katika utangulizi, wakati huo nakala moja yake ilipatikana katika gazeti la zamani la Orthodox Review katika sehemu ya vitabu-nadra ya Maktaba ya Kitaifa ya Urusi. Mashahidi wa Yehova walitambua thamani ya kufanya Biblia hiyo ipatikane kwa watu wote. Maktaba hiyo ililipa Shirika la Kidini la Mashahidi wa Yehova katika Urusi ruhusa ya kuwa na nakala moja ya Biblia ya Makarios ili iweze kutayarishwa kwa ajili ya kuchapishwa.
Kisha Mashahidi wa Yehova wakapanga nakala karibu 300,000 za Biblia hiyo zichapwe huko Italia ili zigawanywe kotekote Urusi na nchi nyingine nyingi ambako Kirusi husemwa. Kwa kuongezea tafsiri ya Makarios ya Maandiko ya Kiebrania karibu yote, chapa hii ya Biblia ina tafsiri ya Pavsky ya Zaburi na vilevile tafsiri ya sinodi ya Maandiko ya Kigiriki iliyoidhinishwa na Kanisa Othodoksi.
Katika Januari 1997, hiyo Biblia ilitolewa wakati wa mkutano baina ya waandishi wa habari katika St. Petersburg, Urusi. (Ona ukurasa wa 26.) Hakika wasomaji wa Kirusi wataelimishwa na kuadilishwa na Biblia hii mpya.
Hivyo kuchapishwa kwa Biblia hii ni ushindi wa kidini na wa kifasihi! Pia ni kikumbusha chenye kutia nguvu imani cha ukweli wa maneno haya ya Isaya 40:8: “Majani yakauka, ua lanyauka; bali neno la Mungu wetu litasimama milele.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]
Biblia Yasifiwa na Wachambuzi
“BADO nguzo nyingine ya fasihi imetolewa: Biblia ya Makarios.” Kwa utangulizi huo, gazeti la habari la Komsomolskaya Pravda lilitangaza kutolewa kwa Biblia ya Makarios.
Baada ya kutaja kwamba Biblia haikuwa imetokea katika lugha ya Kirusi hadi “miaka [ipatayo] 120 iliyopita” gazeti hilo liliomboleza hivi: “Kwa miaka mingi kanisa lilipinga kutafsiriwa kwa vitabu vitakatifu katika lugha iliyo rahisi kusomwa. Likiwa limekataa tafsiri kadhaa, kanisa mwishowe lilikubali mojawapo ya hizo tafsiri mwaka wa 1876, nayo ikaja kujulikana kuwa tafsiri ya sinodi. Hata hivyo, haikuruhusiwa makanisani. Hadi siku hii, Biblia pekee ambayo yatambuliwa katika Kanisa Othodoksi la Urusi ni ya Kislavoni.”
Gazeti la habari St. Petersburg Echo lilionyesha pia thamani ya kuchapisha Biblia ya Makarios, likisema hivi: “Wasomi wenye mamlaka kutoka Chuo Kikuu cha Serikali ya St. Petersburg, Chuo Kikuu cha Kiufundishaji cha Herzen, na kutoka Jumba la Makumbusho la Serikali la Historia ya Kidini walisifu sana chapa hii mpya ya Biblia.” Likitaja kutafsiriwa kwa Biblia katika Kirusi na Makarios na Pavsky katika nusu ya kwanza ya karne iliyopita, hilo gazeti la habari lilisema hivi: “Kufikia wakati huo, katika Urusi Biblia ingeweza kusomwa tu katika Kislavoni, lugha iliyoeleweka tu na makasisi.”
Kutolewa kwa Biblia ya Makarios na Mashahidi wa Yehova kuliripotiwa katika mkutano baina ya waandishi wa habari katika St. Petersburg mapema mwaka huu. Gazeti la kila siku la Nevskoye Vremya la mahali hapo lilisema hivi: “Wasomi wenye mamlaka . . . walikazia kwamba hiyo chapa yapasa kukadiriwa kuwa uhakika wa maana sana katika maisha ya kitamaduni ya Urusi na ya St. Petersburg. Hata iwe mtu afikiri nini juu ya utendaji wa shirika hili la kidini, bila shaka kuchapishwa kwa tafsiri hii ya Biblia ambayo mpaka sasa haikuwa ikijulikana bila shaka ni kwa manufaa makubwa.”
Hakika, wote wampendao Mungu hupendezwa wakati ambapo Neno lake lililoandikwa lafanywa lipatikane katika lugha ambayo watu wa kawaida waweza kusoma na kuelewa. Wapendao Biblia kila mahali wapendezwa kwamba tafsiri nyingine ya Biblia imefanywa ipatikane kwa mamilioni ya watu ulimwenguni pote ambao husema Kirusi.
[Picha]
Kutolewa kwa Biblia ya Makarios kulitangazwa kwenye mkutano huu baina ya waandishi wa habari
[Picha katika ukurasa wa 23]
Maktaba ya Kitaifa ya Urusi ambapo hazina iliyofichika ilipatikana
[Picha katika ukurasa wa 23]
Peter Mkubwa alijaribu kufanya Biblia ichapishwe katika Kirusi
[Hisani]
Corbis-Bettmann
[Picha katika ukurasa wa 24]
Gerasim Pavsky, aliyechangia kutafsiriwa kwa Biblia katika Kirusi
[Picha katika ukurasa wa 25]
Mwadhamu Makarios, ambaye jina lake lilipewa hiyo Biblia mpya ya Kirusi