Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 7/22 kur. 21-23
  • Kwa Nini Mama Ni Mgonjwa Sana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Mama Ni Mgonjwa Sana?
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Mzazi Wangu Ni Mgonjwa?
  • Hisia Zinazoumiza
  • Jambo Unaloweza Kufanya
  • Kudumisha Usawaziko wa Kiroho
  • Nishughulikeje na Mzazi Wangu Aliyeondoka Nyumbani?
    Amkeni!—1992
  • Naweza Kumsaidiaje Mzazi Wangu Aliye Peke Yake?
    Amkeni!—1992
  • Nini Ikiwa Mzazi Wangu ni Mraibu wa Dawa za Kulevya au Pombe?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Namna Gani Ikiwa Mzazi Wangu Hatimizi Matakwa ya Kimungu?
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 7/22 kur. 21-23

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Mama Ni Mgonjwa Sana?

Babake Al alikufa kutokana na kansa.a Akiwa amefundishwa ahadi ya Biblia ya ufufuo, kwa njia fulani Al aliweza kukabiliana na msiba wake. Lakini mama yake alipopimwa na kupatikana kuwa ana kansa, wasiwasi na hofu ilianza kwa mara nyingine tena. Wazo la kumpoteza mzazi mwingine lilimwogofya Al. ‘Kwa nini iwe ni mama yangu ndiye mgonjwa?’ angejiuliza swali hilo kwa uchungu.

KULINGANA na Dakt. Leonard Felder, “kuna Wamarekani zaidi ya milioni sitini ambao . . . wanakabili ugonjwa au kulemaa kwa mmoja wa wapendwa wao.” Felder aongezea hivi: “Katika siku fulani hususa, takriban mfanyakazi Mmarekani mmoja kati ya wanne ana daraka la ziada la kuhangaikia mahitaji ya mzazi anayeugua” au ya mpendwa mwingine. Ikiwa uko katika hali hiyo, hauko peke yako. Hata hivyo, kumwona mtu fulani unayempenda akiugua ni jambo linalotisha na kuhuzunisha. Unaweza kukabilianaje na hali hiyo?

Kwa Nini Mzazi Wangu Ni Mgonjwa?

Mithali 15:13 husema: “Bali kwa huzuni ya moyo roho hupondeka.” Ni jambo la kawaida kupatwa na hisia nyingi sana mzazi wako anapokuwa mgonjwa. Kwa mfano, huenda ukahisi kuwa na hatia juu ya hali mbaya ya mzazi wako. Labda wewe na mzazi wako mmekuwa na ugumu wa kupatana. Huenda mliwahi kubishana vikali mara kadhaa. Sasa kwa kuwa mzazi wako ni mgonjwa, huenda ukahisi kwamba kosa ni lako. Lakini ingawa mabishano ya familia yaweza kusababisha mkazo, ni nadra sana yatokeze ugonjwa mbaya. Mikazo na kutokubaliana kwa mambo madogo kwaweza kutokea hata katika nyumba za Kikristo zenye upendo. Kwa hiyo huhitaji kuhisi kuwa na hatia, kana kwamba ulipasa kulaumiwa kwa matatizo ya afya ya wazazi wako.

Kwa msingi, mama au baba yako ni mgonjwa kwa sababu ya dhambi ya wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. (Waroma 5:12) Kwa sababu ya dhambi hiyo ya kwanza, “viumbe vyote vinafuliza kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja hadi sasa.”—Waroma 8:22.

Hisia Zinazoumiza

Ijapokuwa hivyo, huenda ukawa na wasiwasi na mahangaiko. Mamake Terri anaugua ugonjwa wa mapaku-mekundu, wenye madhara mabaya sana. Terri akiri hivi: “Wakati wowote ninapokuwa mbali na nyumbani, ninakuwa na wasiwasi, nikijiuliza ikiwa mama yuko sawa. Mimi huona ugumu wa kukaza fikira. Hata hivyo, kwa kuwa sitaki awe na wasiwasi, ninaficha hisia zangu.”

Mithali 12:25 husema: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha.” Ni jambo la kawaida kwa vijana kupatwa na mshuko-moyo wanapokuwa katika hali hii. Terri asema kwamba lilikuwa jambo lenye kuhuzunisha sana alipoona kwamba mama yake hangeweza kufanya kazi rahisi. Jambo linaloongezea mkazo ni uhakika wa kwamba vijana—hasa wasichana—mara nyingi hulazimika kubeba madaraka zaidi. Kulingana na Profesa Bruce Compas, “wasichana hutwikwa mzigo wa madaraka ya familia kama vile kutunza nyumba na kutunza ndugu na dada zao wachanga, mambo ambayo yanazidi uwezo wao na ambayo huvuruga ukuzi wao wa kawaida wa jamii.” Vijana fulani hujitenga, wakisikiliza muziki wenye huzuni na unaovunja moyo.—Mithali 18:1.

Kuhofu kwamba huenda mzazi akafa ni jambo la kawaida pia. Terri ni mtoto pekee, na mama yake ni mzazi mmoja. Terri alijipata akilia kila wakati mama yake alipoenda hospitalini, akihofu kwamba hangerudi kamwe. Terri asema hivi: “Tulikuwa wawili tu. Sikutaka kumpoteza rafiki yangu aliye bora.” Vivyo hivyo kijana mmoja anayeitwa Martha alikiri hivi: “Nina umri wa miaka kumi na minane, lakini bado ninaogopa kuwapoteza wazazi wangu. Kuwapoteza kungetokeza hali ya kujihisi mpweke kwelikweli.” Maitikio ya kawaida mzazi anapokuwa mgonjwa huwa kuvurugika kwa usingizi, ndoto mbaya, na matatizo ya kula.

Jambo Unaloweza Kufanya

Hata mambo yaonekane kuwa magumu hivi sasa, unaweza kukabiliana na hali hiyo! Anza kwa kuwaeleza wazazi wako hofu na mahangaiko yako. Hali ya mzazi wako ni mbaya kadiri gani? Kuna uwezekano gani kwamba atapona? Ni mipango gani ambayo imefanywa ya kukutunza endapo mzazi wako hatapona? Je, kuna uwezekano kwamba utapatwa na hali hiyo baadaye maishani? Ingawa ni vigumu kwa wazazi kuzungumza juu ya mambo hayo, ukiwaomba msaada kwa utulivu na kwa staha, yaelekea watafanya yote wawezayo kukusaidia na kukutegemeza.

Pia waeleze hisia zako zinazofaa. Al akumbuka jinsi alivyoshindwa kufanya hivyo alipopata habari kwamba mama yake angekufa kutokana na kansa. Asema: “Sikumwambia kadiri nilivyompenda. Nilijua kwamba alitaka kunisikia nikisema hivyo, lakini nikiwa kijana nilihisi ugumu wa kumweleza hisia za namna hiyo. Alikufa muda mfupi baada ya hapo, na sasa nahisi hatia kwa sababu nilipokuwa na fursa ya kufanya hivyo sikuitumia. Najutia jambo hilo kwa sababu alikuwa mtu wa maana zaidi maishani mwangu.” Usijizuie kuwaeleza wazazi wako kadiri unavyowapenda.

Ikiwezekana, jifunze habari zinazohusu ugonjwa wa mzazi wako. (Mithali 18:15) Labda daktari wa familia yenu anaweza kukusaidia katika habari hii. Unapojua mambo unaweza kuonyesha hisia-mwenzi zaidi, saburi, na uelewevu. Pia kwaweza kukusaidia ujitayarishie mabadiliko yoyote ya kimwili yanayoweza kuwapata wazazi wako, kama vile makovu, kupoteza nywele, au uchovu.

Je, mzazi wako yuko hospitalini? Basi unapomzuru uwe mchangamfu na mwenye kujenga. Endeleza mazungumzo yakiwa machangamfu kadiri iwezekanavyo. Mweleze juu ya kazi yako ya shule na utendaji wa Kikristo. (Linganisha Mithali 25:25.) Ikiwa unaishi katika nchi ambayo watu wa jamaa wanatarajiwa kumwandalia mgonjwa chakula na huduma nyinginezo, fanya kazi yako bila malalamiko. Unapovalia vizuri na kwa njia nadhifu hautamchangamsha tu mzazi wako bali pia utawavutia wafanyakazi wa hospitali na madaktari. Jambo hilo lingeweza kufanya mzazi wako apewe utunzaji bora.b

Je, mzazi wako anapona akiwa nyumbani? Basi fanya lolote uwezalo kusaidia katika kumtunza. Jitolee kufanya kazi za kila siku kwa kiasi kikubwa. Jaribu kumwiga Yehova kwa kujitoa mwenyewe ‘kwa ukarimu na bila kushutumu.’ (Yakobo 1:5) Fanya yaliyo bora uwezavyo ili kuonyesha mtazamo usio wa kulalamika wa kutumainia mema, na unaofaa.

Bila shaka, bado una kazi ya shule. Jaribu kutenga wakati kwa ajili yake, kwa kuwa bado elimu yako ni muhimu. Ikiwezekana, tenga wakati kwa ajili ya mapumziko na tafrija. (Mhubiri 4:6) Jambo hilo litakuburudisha na kukusaidia uwategemeze wazazi wako kwa njia bora. Mwishowe, epuka kujitenga. Jinufaishe kwa utegemezo wa Wakristo wenzi. (Wagalatia 6:2) Terri asema: “Kutaniko lilikuwa familia yetu. Wazee walikuwa tayari sikuzote kuongea nami na kunitia moyo. Sitasahau jambo hilo kamwe.”

Kudumisha Usawaziko wa Kiroho

Jambo lililo la maana zaidi ni kudumisha usawaziko wa kiroho. Jishughulishe na mambo ya kiroho, kama vile kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano, na kuhubiria wengine. (1 Wakorintho 15:58) Wakati wa miezi ya kiangazi, Terri angeongeza utendaji wake wa kueneza evanjeli akiwa painia-msaidizi. Aongezea hivi: “Sikuzote mama alinitia moyo kutayarisha na kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Jambo hilo lilitunufaisha sote. Kwa kuwa hangeweza kuhudhuria kila mkutano kama alivyotaka, nilisikiliza kwa makini kuliko kawaida ili niweze kumweleza juu yake baadaye. Alinitegemea nimwandalie chakula cha kiroho wakati ambapo hangeweza kuwapo.”

Makala moja katika The New York Times ilitoa muhtasari mzuri iliposema juu ya mfanyakazi mmoja wa huduma za jamii ambaye amekuwa “akishangazwa daima na jinsi watoto wanavyoweza kukua na hata kusitawi licha ya vurugu ya ugonjwa wa mzazi.” Asema: “Wanasitawisha stadi fulani ambazo hawakujua wanazo . . . Ikiwa wanaweza kukabili hali hii, wanaweza kukabili mambo mengi.”

Wewe pia unaweza kukabili kipindi hiki kilicho kigumu. Kwa kielelezo, mamake Terri sasa amepata nafuu vya kutosha kujitunza mwenyewe. Labda, baada ya muda, mzazi wako pia atapona. Lakini kwa wakati uliopo, usisahau kwamba Rafiki yako wa kimbingu Yehova, anakutegemeza. Yeye ni “Msikiaji wa sala” na atasikiliza kilio chako cha kutaka msaada. (Zaburi 65:2, NW) Atakupa wewe—pamoja na mzazi wako mwenye kumhofu Mungu—“nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” kusudi uweze kukabili hali hiyo.—2 Wakorintho 4:7; Zaburi 41:3.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Makala “Visiting a Patient—How to Help,” katika toleo la Amkeni! la Machi 8, 1991 la Kiingereza lina madokezo kadhaa yanayotumika.

[Blabu katika ukurasa wa 22]

“Wakati wowote ninapokuwa mbali na nyumbani, ninakuwa na wasiwasi, nikijiuliza ikiwa mama yuko sawa”

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Kujifunza habari zinazohusu ugonjwa wa mzazi wako kwaweza kukutayarisha vema kutoa msaadya

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki