Hatimaye Wakati Ujao Ulio Salama!
“Dunia yote inastarehe na kutulia; hata huanzilisha kuimba.”—ISAYA 14:7.
“WETU ni ulimwengu wa majitu walio wajuzi wa nyuklia lakini vitoto vichanga katika kufuata tabia zifaazo. Sisi twajua mengi zaidi kuhusu vita kuliko yale tuyajuayo kuhusu amani, mengi zaidi kuhusu kuua kuliko yale tuyajuayo kuhusu kuishi.” Maneno hayo yaliyosemwa na jenerali wa Kijeshi wa Marekani mnamo 1948, hutukumbusha maoni yanayopatikana katika Biblia: ‘Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9) Wanadamu wanapokuwa na silaha za nyuklia, wanaweza kusababisha madhara zaidi kuliko kuwajeruhi tu wanadamu wenzao; wanaweza kuwaangamiza!
Watu wengi wanaamini kwamba kuwa na silaha za nyuklia na kuzitumia ni kosa la kiadili. Kwa mfano, jenerali mstaafu wa Jeshi la Wanaanga la Marekani George Lee Butler alisema: “Mtu anapokuwa na silaha za nyuklia akibani anatoa ujumbe kwamba tunaweza kuwazia hali ambazo . . . kwa njia fulani tunaweza kufikiria kutumiwa kwa silaha hiyo. Hilo ni kosa kabisa.”
Hata hivyo, mwandishi wa makala za gazeti Mwingereza Martin Woollacatt asema: “Bado silaha za nyuklia zinapendeza, bila kujali wataalamu na watu wenye kutetea maadili wanasemaje kuhusu kutofaa na hatari zake. Serikali zinaamini kwamba zinahitaji silaha hizo kwa sababu ya kujilinda; pia wanazing’ang’ania kwa sababu bila shaka silaha za nyuklia zina uvutano mbaya ambao wanasiasa na majeshi hutambua na kutaka kuwa nao.”
Ni kweli kwamba kwa miongo mitano iliyopita, kwa njia fulani mwanadamu amefaulu kuepusha vita vya nyuklia. Lakini katika kipindi hichohicho, silaha za kawaida zimetumiwa kuua maelfu yasiyojulikana ya watu. Kwa kufikiria historia ya binadamu, ni jambo linalofaa kudhania kwamba pindi moja, silaha hizi za nyuklia zenye kuogofya zitatumiwa.
Sababu za Msingi
Je, mielekeo ya mwanadamu ya kupenda vita inaweza kuzuiwa? Watu fulani wanadai kwamba wanadamu hupigana kwa sababu ya upumbavu, ubinafsi, na uchokozi unaofaa. “Ikiwa hizi ndizo sababu za msingi za vita,” asema msomi Kenneth Waltz, “basi kukomeshwa kwa vita kwapaswa kutokana na kuboresha hali ya wanadamu na kuwaelimisha.”
Wengine wanasema kwamba visababishi vya vita vyategemea sera za siasa za kimataifa. Kwa sababu kila nchi inayojitawala hufuatia mapendezi yake yenyewe, mapambano hayawezi kuepukwa. Kwa kuwa hakuna njia yenye kutegemeka ya kutatua matatizo, vita huzuka. William E. Burrows na Robert Windrem waandika hivi katika kitabu chao Critical Mass: “Jambo gumu ni la kisiasa. Hakuna usimamizi wenye udhibiti unaowezekana bila kuwa na azimio la msingi la kisiasa la kukomesha na hata kutangua kuenea kwa silaha za nyuklia.”
Fikiria majadiliano yanayoendelea ya kutekeleza Mkataba wa Kukomesha Kabisa Majaribio. Gazeti la Guardian Weekly liliyafafanua kuwa “kipindi cha majadiliano makali kati ya mataifa yenye uwezo wa nyuklia na mataifa ambayo tayari yana silaha za nyuklia kisiri au yaliyo na tekinolojia ya kuzitengeneza haraka.” Makala hiyohiyo inakiri: “Hakuna [kikundi] chochote kilicho na mpango wa kuacha silaha zake au uwezo wake wa nyuklia, au kuboresha ama silaha zake ama uwezo wake.”
Bila shaka, ushirikiano wa kimataifa wahitajiwa ikiwa vitisho vyote vya nyuklia vitaondolewa kabisa. Kitabu Critical Mass chasema: “Kuaminiana lazima kuchukue mahali pa kuangamizana wenyewe kwa wenyewe kila mahali, . . . au baada ya pindi fulani msiba mkubwa utatokea.” Kwa kusikitisha, uhusiano wa kimataifa leo na majadiliano mara nyingi unafanana na kile nabii Danieli alichokifafanua karne 26 zilizopita: ‘Wanasema uongo wakiwa katika meza moja.’—Danieli 11:27, Byington.
Ushirikiano wa Tufeni Pote Chini ya Serikali ya Ulimwengu
Hata hivyo, Biblia hutuhakikishia kwamba Mungu mwenyewe anakusudia kuwepo kwa ushirikiano wa kweli tufeni pote chini ya serikali ya ulimwengu itakayoleta matokeo makubwa. Pasipo kujua mamilioni wamesali kwa ajili ya serikali hiyo wanaposema Sala ya Bwana: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:10) Ufalme ni serikali. Na Mkuu wa Ufalme huo ni Mkuu wa Amani, Yesu Kristo. Neno la Mungu latuhakikishia hivi: “Maongeo ya enzi [yake] na amani hayatakuwa na mwisho kamwe . . . Wivu wa BWANA wa majeshi ndio utakaotenda hayo.” (Isaya 9:6, 7) Biblia inatoa ahadi hii kuhusu serikali hiyo chini ya Yesu: “Utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu,” au serikali za kibinadamu.—Danieli 2:44.
Serikali hiyo ya ulimwengu italeta amani na usalama wa kweli—lakini si kwa kuzuia silaha za nyuklia au kupitia mikataba isiyotegemeka. Zaburi 46:9 inatoa unabii kwamba Yehova Mungu “avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.” Hatua nusunusu hazitafaa. Ufalme wa Mungu chini ya Kristo utafanya mengi zaidi kuliko kupunguza silaha za nyuklia—itaziondoa kabisa pamoja na silaha zote za vita.
Hakutakuwa na tisho la nyuklia kwa sababu hakutakuwa tena mataifa yenye uwezo mkubwa, mataifa makaidi, wala magaidi. Amani ya kweli itaenea: “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake, wala hapana mtu atakayewatia hofu, kwa kuwa kinywa cha BWANA wa majeshi kimesema hivi.” Maneno haya yaliyopuliziwa yanatoka kwa Mungu ambaye hawezi kusema uwongo.—Mika 4:4; Tito 1:2.
Kulingana na Zaburi 4:8, amani na usalama wa kweli zaweza kupatikana tu ndani ya mpango wa Yehova Mungu: “Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, maana Wewe, BWANA, peke yako, ndiwe unijaliaye kukaa salama.” Kama ilivyothibitishwa na historia ya mwanadamu kwa njia yenye kuhuzunisha, ahadi zozote za “amani na usalama” isipokuwa kupitia kwa Ufalme wa Yehova zitakuwa bandia tu.—Linganisha 1 Wathesalonike 5:3.
‘Utulivu na Usalama’
Lakini vipi juu ya asili ya binadamu ya kupenda vita? “Watu wakaao duniani hujifunza haki.” (Isaya 26:9) Mafundisho hayo kuhusu uadilifu yatakuwa na matokeo makubwa kwa asili ya binadamu na hali za ulimwengu: “Na kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini [“usalama,” NW] daima.” (Isaya 32:17) Msukumo wowote wa uchokozi au mtazamo wa jeuri utabadilishwa na upendo wa jirani na kuhangaikia hali njema ya wote. Wakazi wa dunia “watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:4.
Katika lugha ya unabii Isaya alitabiri kwamba watu wenye mielekeo kama ya wanyama watabadilishwa. Alisema juu ya wakati ambapo “dunia itajawa na kumjua BWANA.” Tokeo litakuwa, “mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza. . . . Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu.”—Isaya 11:6-9.
Itikadi katika ahadi hizo za Mungu imewapa Mashahidi wa Yehova mtazamo unaofaa kuhusu maisha. Tunapotazama wakati ujao, hatuoni dunia iliyoharibiwa kabisa na nyuklia. Badala ya hivyo, tunaona utimizo wa ahadi ya Biblia: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) Huenda wengine wakaiita imani hiyo kuwa ya ujinga na isiyo halisi. Lakini kwa kweli ni nani aliye mjinga? Je, ni mtu anayejenga imani katika ahadi ya Mungu au mtu anayeamini bila kutilia shaka ahadi zisizo za kweli za wanasiasa? Jibu ni wazi kwa wale wanaopenda amani kwelikweli.a
[Maelezo ya Chini]
a Mashahidi wa Yehova wamesaidia mamilioni ya watu kukubali ujumbe wa Biblia wenye tumaini kupitia funzo la Biblia la nyumbani bila malipo. Unaweza kupanga wakutembelee kwa kuwasiliana na wachapishaji wa gazeti hili au kwa kuzuru Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwenu.
[Blabu katika ukurasa wa 11]
“Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:4
[Picha katika ukurasa wa 9]
Katika ulimwengu mpya wa Mungu, familia ‘zitakaa salama,’ na silaha za aina zote zitaondolewa
[Picha katika ukurasa wa 10]
Watu wanapojifunza Neno la Mungu Biblia na kulitumia, wanaacha tabia za kupenda vita