Tisho la Nyukilia—Laondolewa Milele!
MUNGU hataki wanadamu waishi kwa hofu kuu. Akiwa “Mungu mwenye furaha,” yeye anawataka wafurahie amani na kuishi kwa salama—kwa ufupi, wawe na furaha. (1 Timotheo 1:11, New World Translation) Lakini ni wazi kwamba jambo hilo haliwezekani kabisa katika ulimwengu uliojaa matisho ya nyukilia.
“Amani na Salama”—Ya Bandia
Inapasa kuwa wazi kwamba tisho la nyukilia halijamalizika kamwe. Lakini bado yaonekana kwamba mataifa kwa ujumla yana matazamio mazuri ijapokuwa mivurugo ya kisiasa, kiuchumi, na ya kijamii. Jitihada inayoendelea ya kuondoa hatari hiyo imeonekana wazi tangu ule Mwaka wa Amani ya Kimataifa wa UM katika 1986.
Gazeti The Bulletin of the Atomic Scientists limegeuza ile saa yalo ya uangamizo katika karne hii—njia yalo ya kuonyesha uwezekano wa kutokea kwa vita vya nyukilia—kutoka dakika 3 kabla ya maangamizo ya nyukilia hadi dakika 17 kabla ya maangamizo hayo. Mnamo 1989, Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Amani ya Stockholm ilisema kwamba “tumaini la kupata suluhisho la amani lina msingi bora zaidi kuliko katika mwaka mwingine wowote tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu 2.”
Katika miaka ya karibuni shirika la Umoja wa Mataifa limeimarishwa ili kushughulikia maeneo ya kimataifa yenye mizozo. Ufanisi walo, ambalo si kamili, umetosha kutokeza roho ya ujumla ya kuwa na matazamio mazuri. Huenda wakati ujao ukatokeza mafanikio mengine zaidi. Labda matangazo ya “amani na salama” yatatangazwa zaidi na zaidi na kwa bidii sana. Huenda hata yakaonekana kuwa yastahili.
Lakini jihadhari! “Wakati wasemapo, Kuna amani na salama,” Biblia yaonya, “ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.” Kwa hiyo, matangazo ya “amani na salama” yatakuwa ishara ya wakati wa Mungu “kuwaharibu hao waiharibuo nchi [kupitia uchafuzi, nyukilia na vinginevyo].”—1 Wathesalonike 5:3, 4; Ufunuo 11:18.
Ona kwamba Biblia haisemi mataifa yatapata “amani na salama.” Kwa wazi watakuwa wakisema kuzihusu kwa njia ya kipekee sana, inayoonyesha matazamio mazuri na usadikisho ambao haujapata kuonekana hapo awali. Uwezekano wa kupata amani na salama utaonekana kuwa karibu kuliko wakati mwingine wowote. Lijapokuwapo tisho la nyukilia linaloendelea, mataifa yatadanganywa na hisia-bandia ya salama.
Lakini, Wakristo wa kweli hawatadanganywa. Kwa upendezi wenye makini wao watatazamia kitu bora zaidi kuliko amani na salama ya kibinadamu!
Amani na Salama—Ya Kweli
Kulingana na Zaburi 4:8, amani na salama ya kweli itapatikana tu katika mpango wa Yehova Mungu: “Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, maana Wewe, BWANA, peke yako, ndiwe unijaliaye kukaa salama.” Tangazo lolote la “amani na salama” litangazwalo bila mpango wa Ufalme wa Yehova ni la bandia tu. Haliwezi kutimiza chochote chenye kudumu.
Ufalme wa Mungu ukiwa chini ya Kristo hautasuluhisha mambo nusu-nusu. Serikali hiyo ya kimungu itafanya mengi zaidi ya kupunguza tu silaha za nyukilia; itaziondoa kabisa pamoja na silaha nyinginezo zote za vita. Zaburi 46:9 laahidi hivi: “Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.”
Vivyo hivyo, matisho ya nyukilia yatokezwayo na kasoro za mitambo ya nyukilia au yatokezwayo na takataka zenye mnururisho yatakuwa mambo yaliyopita. Ama sivyo maneno haya hayangekuwa ya kweli: “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha BWANA wa majeshi kimesema hivi.” Mungu hawezi kusema uongo. Hatuna sababu ya kutilia shaka maneno yake.—Mika 4:4; Tito 1:2.
Je! ungefurahi kuwa na tazamio la kuishi katika ulimwengu ambamo tisho la nyukilia limeondolewa milele? Unaweza, kwa kuwa Neno la Mungu laeleza waziwazi matakwa yanayohitajika. Kwa kujifunza juu ya matakwa hayo na kwa kuishi kupatana nayo, huenda siku moja ukawa na shangwe ya kusema kwa faraja: “Tisho la nyukilia—limekwisha hatimaye!”
[Picha katika ukurasa wa 7]
Amani itakuwapo kwa wingi katika ulimwengu mpya wa Mungu bila matisho yoyote ya nyukilia
[Hisani]
M. Thonig/H. Armstrong Roberts
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]
Picha ya U.S. National Archives