Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 8/22 kur. 12-14
  • Je, Kuna Hatari Yoyote Katika Michezo Inayokufanya Uwe Mhusika-Mkuu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Kuna Hatari Yoyote Katika Michezo Inayokufanya Uwe Mhusika-Mkuu?
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ujeuri na Mizungu
  • Mambo Mengine
  • Ndoto Tu au Uhalisi?
  • Je, Nicheze Michezo ya Kompyuta?
    Amkeni!—2008
  • Nicheze Michezo ya Kompyuta?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Je, Nicheze Michezo ya Kompyuta au ya Vidio?
    Amkeni!—1996
  • Je, Kuna Hatari kwa Wachezaji?
    Amkeni!—2002
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 8/22 kur. 12-14

Vijana Huuliza . . .

Je, Kuna Hatari Yoyote Katika Michezo Inayokufanya Uwe Mhusika-Mkuu?

“Yote ni mambo ya kuwaziwa tu. Pindi moja wewe ni mfanya-mizungu. Pindi nyingine wewe ni mpiganaji. Unaweza kuwa aina mbalimbali za watu ambao unatamani. Hakuna kikomo.”—Christophe.

“KUWA kila kitu ambacho maishani huwezi kuwa.” Gazeti moja lilinukuu shime hiyo lilipokuwa likifafanua mchezo mmoja wa kubuniwa unaopendwa sana. Mamilioni ya vijana huvutiwa sana na michezo isiyo halisi ambamo wao ndio wahusika-wakuu. Lakini, ni michezo gani hii inayokufanya uwe mhusika-mkuu?

Kulingana na kitabu Jeux de rôle (Michezo Inayokufanya Uwe Mhusika-Mkuu), “kila mchezaji hujifanya kuwa mtu fulani mashuhuri ambaye ana utume fulani au anafuatilia jambo fulani na ajitayarisha kupata magumu katika ulimwengu unaowaziwa tu.” Lengo la mchezo huo ni kusitawisha mtu huyo wa kuwaziwa kwa kupata ujuzi, fedha, silaha, au uwezo wa kufanya mizungu unaohitajiwa kutekeleza utume huo.

Michezo inayokufanya uwe mhusika-mkuu ilipendwa sana katika miaka ya 1970 kwa mchezo ulioitwa Dungeons and Dragons.a Tangu wakati huo, michezo hiyo imekuwa biashara inayochuma mamilioni ya dola, ikitia ndani michezo ya meza, michezo fulani ya kadi, michezo kwenye vitabu, michezo ya kompyuta, na hata michezo halisi ambayo washiriki ndio wanakuwa wahusika-wakuu. Yaonekana kwamba kuna wachezaji wa kawaida zaidi ya milioni sita nchini Marekani na mamia ya maelfu katika Ulaya. Nchini Ufaransa, shule nyingi za sekondari zina klabu za michezo inayokufanya uwe mhusika-mkuu, na nchini Japani hiyo ndiyo michezo ya vidio ipendwayo zaidi.

Watetezi husema kwamba michezo hiyo huchochea akili, husitawisha stadi za kuweza kusuluhisha matatizo, na kuendeleza ushirikiano katika kikundi. Hata hivyo wapinzani wamedai kuwa michezo hiyo imechangia ujiuaji, mauaji, ubakaji, kuharibiwa kwa makaburi, na ibada ya Shetani. Kule Madrid, Hispania, vijana wawili walikamatwa, wakishukiwa kuwa walimwua mtu mmoja mwenye umri wa miaka 52 walipokuwa wakirudia kutenda kihalisi sehemu moja ya mchezo fulani uliowafanya wawe wahusika-wakuu. Nchini Japani tineja mmoja aliwaua wazazi wake kisha akajikata vifundo vya mikono akiiga mwisho wa mchezo unaomalizika kwa njia hiyo. Ni kweli kwamba hivi ni visa vyenye kupita kiasi—na wachezaji wengi wana akili na huchangamana na jamii. Lakini, Wakristo wachanga hufanya vema kujiuliza, ‘Je, nicheze michezo inayonifanya niwe mhusika-mkuu? Je, kuna haja ya kutahadhari?’

Ujeuri na Mizungu

Michezo ya mhusika-mkuu hutofautiana sana. Hata hivyo, kuna ujeuri katika mingi ya michezo hiyo. Kwa hakika, katika ulimwengu wa kuwaziwa tu katika michezo hiyo, mara nyingi ujeuri ni sehemu kubwa ya kufanya maendeleo—au kusalimika. Basi, kucheza michezo kama hiyo kunaweza kupatanaje na shauri la Biblia? Mithali 3:31 yasema: “Usimhusudu mtu mwenye jeuri, wala usiichague mojawapo ya njia zake.” Biblia pia inatuhimiza ‘tutafute sana amani na kuifuatia’—wala si ujeuri.—1 Petro 3:11.

Hangaiko jingine ni kwamba mizungu huonyeshwa mara nyingi katika michezo mingi. Mara nyingi, wachezaji wanaweza kucheza wakiwa wachawi au kucheza kama watu wanaofanya mizungu. Kisha vizuizi au maadui hushindwa kwa kufanyiwa mizungu. Inaripotiwa kwamba katika mchezo mmoja upendwao “wachezaji hucheza fungu la ama Malaika ama Mashetani wanaotumikia Malaika Wakuu ama Mashetani Wakuu . . . Maneno ya kukufuru hufanya michezo hiyo ipendeze.” Mchezo mmoja wa kompyuta hata humwezesha mchezaji awe mwenye nguvu zote kwa kuchapa tu neno “Shetani.”

Vijana fulani Wakristo wamesababu kwamba hakuna ubaya wowote kucheza michezo inayokufanya uwe mhusika-mkuu maadamu hutumii wakati mwingi mno kuucheza. “Ni mchezo tu,” kijana mmoja asema. Labda. Lakini Mungu aliwaonya Waisraeli wasijihusishe na mambo ya mafumbo. Sheria ambayo Musa alipewa ilitangaza kwamba ‘mtu atazamaye bao, mtu atazamaye nyakati mbaya, mwenye kubashiri, msihiri, mtu alogaye kwa kupiga mafundo, mtu apandishaye pepo, mchawi ni chukizo kwa BWANA.’—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

Basi, je, ni jambo la hekima kucheza michezo inayoendeleza mafumbo? Je, kucheza kama mwenye uwezo wa mizungu si kuingilia “mambo yenye kina kirefu ya Shetani”? (Ufunuo 2:24) Kijana mmoja akiri hivi: “Baada ya kuwa mhusika-mkuu katika mchezo mchana kutwa, niliogopa kuondoka nyumbani. Nilihisi nitashambuliwa na mtu fulani.” Je, chochote kinachotokeza hofu mbaya kama hiyo kinaweza kufaa?

Mambo Mengine

“Wakati ubakio umepunguzwa,” lasema andiko la 1 Wakorintho 7:29. Basi, hangaiko jingine kubwa katika michezo inayokufanya uwe mhusika-mkuu ni wakati mwingi ambao michezo hiyo huchukua. Michezo fulani huchukua muda wa saa nyingi, siku nyingi au hata majuma mengi. Isitoshe, mchezo huo unaokufanya uwe mhusika-mkuu waweza kunasa mtu sana, au hata kuwa yenye uraibu hivi kwamba kila kitu kingine kinawekwa kando. “Niliposhinda kila hatua ya mchezo,” akiri kijana mmoja, “nilitaka hali ngumu zaidi iliyo halisi zaidi. Nikawa nimenaswa kabisa.” Uraibu kama huo waweza kuathirije masomo ya shule na utendaji wa kiroho wa kijana?—Waefeso 5:15-17.

Kijana mmoja wa Japani akumbuka hivi: “Sikuzote nilikuwa nikiwazia hatua nitakayochukua kwenye mchezo, hata wakati ambapo sikuwa nacheza. Shuleni na mikutanoni, nilikuwa nikifikiria tu mchezo. Ikafikia hatua ambapo sikuweza kufikiria kitu kingine chochote. Hali yangu ya kiroho ilikuwa imeharibika kabisa.” Christophe, aliyetajwa mapema, asema jinsi “alivyokuwa amepotoka.” Ni kweli kwamba kuna ‘wakati wa kucheka na wakati wa kucheza,’ lakini, je, tafrija inapasa kuchukua mahali pa utendaji wa kiroho?—Mhubiri 3:4.

Ebu fikiria pia roho ambayo mchezo huo hukuza. Gazeti moja nchini Ufaransa latangaza mchezo unaokufanya uwe mhusika-mkuu kwa maneno yafuatayo: “Utapata mambo mengi maovu, yasiyofaa, na mapotovu, ambayo yamepangwa ili kukutia hofu na kubadilisha kabisa mtazamo wako wa ulimwengu.” Je, roho kama hiyo inapatana na shauri la Biblia la kuwa “watoto wachanga sana kuhusu ubaya”? (1 Wakorintho 14:20) Hatimaye Christophe akafikia uamuzi wa kwamba michezo aliyokuwa akicheza “haipatani na maadili ya Kikristo.” Aongezea kusema: “Niliona siwezi kuendelea kuhubiri, kuhudhuria mikutano, na kujifunza mambo mazuri, kama vile upendo wa Kikristo, na huku ninacheza mchezo ambao hauhusiki hata kidogo na Ukristo. Jambo hilo halifai hata kidogo.”

Ndoto Tu au Uhalisi?

Vijana wengi huvutiwa na michezo hiyo ili wasahau uhalisi wa maisha. Lakini, je, inafaa kujitumbukiza katika ndoto za mchana? Mwanasosholojia Mfaransa Laurent Trémel aeleza: “Ulimwengu halisi, ukiwa umejaa ukosefu wa hakika, . . . watofautiana kabisa na ulimwengu wa kuwaziwa unaoonyeshwa kuwa halisi, ambako hatimaye unadhibiti sheria na ambako unaweza kufanyiza mhusika-mkuu afanane na wewe au kile ambacho ungependa uwe.” Mtaalamu mmoja wa akili Etty Buzyn aongezea kusema: “Wanapocheza, vijana wanawazia kwamba wanaishi maisha hatari, wanafanyiza upya ulimwengu, lakini kihalisi, hawakabili hatari yoyote. Wao wanatoroka jamii na vikwazo vyake.”

Hatimaye, hali hiyo ya kuepuka uhalisi wa maisha yaweza tu kutokeza mfadhaiko, kwa kuwa baada tu ya kila mchezo mtu hurudia uhalisi wa maisha. Ni lazima ukabili uhalisi wa maisha. Kwa kweli, hakuna mafanikio yoyote au msisimko wowote katika mchezo ambao unaweza kusaidia mtu ashindwapo maishani au kuboresha hali ya maisha. Jambo la busara kufanya ni kukabiliana na uhalisi wa maisha—ana kwa ana! Boresha uwezo wako wa utambuzi kwa kukabili uhalisi wa maisha. (Waebrania 5:14) Sitawisha sifa za kiroho ambazo zitakuwezesha kukabiliana na matatizo yako. (Wagalatia 5:22, 23) Kufanya hivyo kunaridhisha na kuthawabisha zaidi kuliko kucheza mchezo wowote.

Hatumaanishi kwamba michezo yote inayokufanya uwe mhusika-mkuu inadhuru. Tangu nyakati za Biblia, watoto wachanga walikuwa wakicheza michezo ambayo ina kadiri fulani ya kuwazia tu mambo na iliyowafanya wawe wahusika-wakuu, kama Yesu mwenyewe alivyosema. (Luka 7:32) Na Yesu hakushutumu tafrija isiyo na madhara. Lakini, ni lazima vijana Wakristo, pamoja na wazazi wao ‘wafulize kuhakikisha ni nini lililo lenye kukubalika kwa Bwana.’ (Waefeso 5:10) Unapofikiria mchezo fulani, jiulize, ‘Je, mchezo huo unaonyesha “kazi za mwili”? Je, utazuia uhusiano wangu na Mungu?’ (Wagalatia 5:19-21) Kwa kufikiria mambo kama hayo, unaweza kufanya uamuzi wenye hekima kuhusu michezo inayokufanya uwe mhusika-mkuu.

[Maelezo ya Chini]

a Ona Amkeni! la Machi 22, 1982, ukurasa wa 26-27, Kiingereza.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Baadhi ya michezo inayokufanya uwe mhusika-mkuu husitawisha roho ya aina gani?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki