Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 9/22 kur. 13-15
  • Mvua Ikosapo Kunyesha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mvua Ikosapo Kunyesha
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mashahidi Wenzi Waitikia kwa Upendo
  • Furaha Katika Kutoa na Kupokea Msaada
  • Suluhisho Lenye Kudumu
  • Ukame Wenye Uharibifu Mkubwa Kusini mwa Afrika
    Amkeni!—1994
  • Kukua Pamoja Katika Upendo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kutoa Msaada kwa Walioathiriwa na Misiba
    Jinsi Michango Yako Inavyotumiwa
  • Yehova Aandaa Msaada
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 9/22 kur. 13-15

Mvua Ikosapo Kunyesha

NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA BRAZILI

MWAKA uliopita, ukame mkubwa sana uliharibu kabisa sehemu kubwa ya kaskazini-mashariki mwa Brazili. Kulingana na gazeti la Veja, mamia ya maelfu ya wanordestino, kama waitwavyo wakazi wa sehemu ya kaskazini-mashariki mwa nchi hiyo, walijikuta katika “hatari ya kukumbwa na ukame.” Ukame huo uliharibu mpunga, maharagwe, na mahindi na kusababisha njaa iliyoenea kila mahali—kali zaidi kwa miaka 15. Katika sehemu nyingine, hata hakukuwa na maji ya kunywa ya kutosha.

Wabrazili wanafahamu ukame. Mnamo mwaka wa 1877, watu wapatao 500,000 walikufa njaa kutokana na ukame uliokuwa mbaya zaidi katika nchi hiyo. Wakati huo maliki wa Brazili, Dom Pedro wa Pili, aliapa kwamba angepata suluhisho la ukame hata kama ingemaanisha kuuza vito vyote vilivyokuwa kwenye taji lake ili kufanya hivyo! Hiyo ilikuwa zaidi ya miaka 100 iliyopita; na bado hata leo, tatizo hilo lingalipo. Ilikadiriwa kwamba ukame uliotokea mwaka jana, ungeathiri watu wapatao milioni kumi wanaoishi katika majiji 1,209 yaliyoko kaskazini-mashariki mwa Brazili.

Mashahidi Wenzi Waitikia kwa Upendo

Ripoti za ukame zilipofika kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Brazili, hatua ilichukuliwa mara moja. Wawakilishi wasafirio walitumwa kwenye sehemu zilizoathiriwa zaidi katika majimbo ya Bahia, Ceará, Paraíba, Pernambuco, na Piauí ili kukagua mweneo wa tatizo hilo. Waangalizi wasafirio walipata kwamba Mashahidi 900 na wanafunzi wa Biblia waliokuwa wakiishi katika sehemu hiyo walikuwa na uhitaji mkubwa. Baadhi yao walikuwa wakijikimu kwa viazi vikuu; wengine walikula tu wali. Familia moja haikuwa na chakula chochote ila maziwa tu ya kunywa wakati wa kifungua-kinywa, chakula cha mchana, na chakula cha jioni. Dada Mkristo aliye na kansa alilazimika kuuza kitanda chake ili anunue chakula kidogo. Familia moja ya washiriki sita ilikuwa imekula chakula ambacho walifikiri kuwa mlo wao wa mwisho wakati walipopokea msaada kutoka ndugu zao Wakristo.

Halmashauri za kutoa msaada zilipangwa mara moja ili kugawanya chakula na misaada mingineyo. Mashahidi kutoka Recife na kutoka majiji yaliyo karibu walichanga kwa ukarimu kwa wale waliokuwa na uhitaji. Lakini msaada zaidi ulipohitajika, Wakristo kutoka Rio de Janeiro pia walijiunga kuwasaidia ndugu zao. Katika muda mfupi, Mashahidi walikuwa wamechanga tani 34 za chakula na walikuwa wamelipa gharama za kusafirisha misaada hiyo kilometa 2,300 hadi Recife.

Katika miji mikuu ya majimbo ya Piauí na Paraíba, tani sita za chakula zilikusanywa mara moja. Jumba la Ufalme katika jiji la Fortaleza lilichaguliwa kuwa mahali pa muda pa kuhifadhi chakula kilichotolewa. Lakini kulikuwa na tatizo. Mashahidi wangesafirishaje chakula hadi mahali kilipotakikana? Mtu mmoja ambaye si Shahidi wa Yehova alitoa kwa fadhili lori lake litumiwe. Hata hivyo, msafara uliokuwa ukibeba chakula na misaada mingineyo ulikuwa ukizuiwa njiani na kuporwa. Je, vitu vilivyotolewa vingefika mahali vilipotakikana? Mashahidi walikuwa wameazimia kugundua jambo hilo. Wakiwa na imani kamili katika Yehova, waliendesha lori lililokuwa limepakiwa chakula hadi kwenye eneo hilo. Misaada hiyo ilifika salama na kupokewa kwa shukrani.

Furaha Katika Kutoa na Kupokea Msaada

Mashahidi waliopanga kutolewa kwa misaada walisisimuliwa na fursa ya kuwasaidia ndugu zao. Mzee mmoja wa kutaniko anayeishi São Paulo alisema: “Mara ya mwisho kulipokuwa na njaa, hatukualikwa kutoa chakula. Tunashukuru kama nini kwamba wakati huu tulialikwa!” Mashahidi katika Fortaleza waliandika: “Tunafurahi sana kwamba tumeweza kuwasaidia ndugu zetu, hasa kwa sababu tuna hakika kwamba tumefanya moyo wa Yehova ufurahi. Hatusahau kamwe maneno ya Yakobo 2:15, 16.” Mistari hiyo ya Biblia inasema: “Ikiwa ndugu au dada yumo katika hali ya uchi na anakosa chakula cha kutosha kwa siku, lakini mtu fulani kati yenu awaambia wao: ‘Nendeni kwa amani, fulizeni kujipasha moto na kulishwa vizuri,’ lakini nyinyi hamwapi mahitaji ya lazima ya mwili wao, ina manufaa gani?”

Nyakati nyingine Mashahidi waliokuwa wakitoa misaada waliweka jumbe zenye kutia moyo kwenye vifurushi vya chakula. Ujumbe mmoja ulisema: “Kumbukeni ahadi inayopatikana kwenye Zaburi 72:16 kwamba karibuni, katika ulimwengu mpya wa Mungu, kutakuwepo wingi wa nafaka.” Bila shaka, Mashahidi walioathiriwa na njaa walishukuru sana kwa ajili ya fadhili waliyoonyeshwa na ndugu zao. Shahidi mmoja ambaye familia yake ilipokea msaada iliyohitaji sana iliandika hivi kwa uthamini: “Mimi na familia yangu tunaona tendo hili kuwa udhihirisho ulio wazi wa upendo wa Mungu wetu na Baba mwenye rehema, Yehova, na hangaiko lenye upendo la tengenezo lake na washiriki wake. Jambo hilo limetufanya tuhisi kuwa karibu zaidi naye na watu wake.”

Suluhisho Lenye Kudumu

Kinyume na hilo, hakuna ukosefu wa maji katika sehemu ya kaskazini-mashariki mwa Brazili; kuna maji baridi mengi sana chini ya udongo, na vilevile maji mengi katika mabwawa. Ikiwa ingewezekana kuwapatia watu wote maji haya, nchi hiyo ingetokeza mazao mengi sana kupitia kilimo.

Karibuni, tatizo lililomtesa Maliki Dom Pedro wa Pili litatatuliwa daima. Siku hiyo itafika wakati Ufalme wa Mungu kupitia Yesu Kristo utakapotatua matatizo yote ya dunia, kutia ndani njaa. Kisha ardhi iliyokumbwa na ukame itapata utimizo wa unabii wa Isaya: “Katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani. Na mchanga ung’aao mfano wa maji utakuwa ziwa la maji, na nchi yenye kiu itakuwa chemchemi za maji.”—Isaya 35:1, 2, 6, 7.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

“Tufanye Lililo Jema Kuelekea Wote”

Mtume Paulo aliwashauri waamini wenzi: “Acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Ukame uliotokea Brazili hivi karibuni uliwapa Mashahidi wa Yehova fursa ya kutumia shauri hilo kwa njia yenye kutumika. Walionyesha hangaiko lenye upendo si kwa waamini wenzao tu bali pia kwa wengineo. Tokeo ni kwamba watu fulani waliokuwa wakipinga kazi ya Mashahidi wa Yehova hapo awali wameanza kufikiria upya maoni yao kuwaelekea.

Mwanzoni mwanamume fulani alikasirika sana mke wake alipoamua kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Baada ya muda, mke alianza kushiriki itikadi mpya pamoja na wengine. Wakati njaa ilipokuwa imepamba moto Mashahidi wa hapo wakawasili nyumbani mwa wenzi hao wakiwa na chakula, mwanamume huyo alivutiwa sana hivi kwamba akaamua kufanya jambo alilokuwa ameapa kutofanya kamwe—kuhudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme la mahali hapo. Ijapokuwa bado alikuwa na shaka fulani kuhusu upulizio wa Biblia, mwanamume huyo aliyekuwa mpinzani hapo awali alikubali funzo la Biblia la nyumbani.

Mahali penginepo Mashahidi waliripoti: “Tulishangaa kwamba misaada ilifika haraka sana. Kiasi cha chakula kilichotolewa kilikuwa kikubwa kuliko tulivyotarajia. Kwa hiyo baada ya kuhangaikia mahitaji ya ndugu zetu na familia zao, tuliwapa wanafunzi wa Biblia chakula, jamaa zao na pia majirani wa Mashahidi wa Yehova.”

Mashahidi fulani walioishi katika kijiji kimoja waliwapa baadhi ya majirani wao vifurushi vya chakula. Mwenye nyumba mmoja mwenye uthamini alisema: “Nyinyi watu mnafanya yale aliyofundisha Kristo; mnatoa bila kutarajia kurudishiwa chochote.”

[Picha katika ukurasa wa 14]

Matokeo ya ukame

[Picha katika ukurasa wa 13]

UN/DPI Photo by Evan Schneider

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki