Maoni ya Biblia
Ni Nini Husababisha Uchawi?
“WACHAWI.” Neno hilo huleta picha gani akilini mwako? Je, ni picha ya maajuza wenye sura mbaya wanaodhuru kwa ulozi au ni ya wanawake wasio na adili wakiwasiliana na Shetani? Kinyume cha dhana hiyo, watu wengi wa kisasa wanaodai kuwa wachawi huwa sawa tu na watu wa kawaida. Baadhi yao ni wataalamu wenye kuheshimiwa, kama vile wanasheria, waalimu, waandishi, na wauguzi. Harakati za kidini zimeibuka ulimwenguni pote ambazo yaelekea zinahusiana na mizungu, kama vile dini za mambo ya asili na upagani-mpya.a “Popote unapozuru katika Urusi siku hizi unapata kwamba uchawi ni jambo la kawaida maishani,” akasema ofisa mmoja wa polisi katika nchi hiyo. Marekani ina takriban wachawi 50,000 hadi 300,000, au “Wiccan,”b kama wanavyojiita wengine wao.
Leo neno “mchawi” ambalo kwa kawaida hutumiwa kiholela-holela laweza kuwa na maana tofauti kwa watu tofauti. Kuenea kwa uchawi katika nyakati za kisasa yaonekana kunahusiana hasa na ibada fulani ya mungu-mke, dini inayotegemea mambo ya asili yenye kuitikadi sana uwezo wa maono. Baadhi ya wachawi wamejitenga—wanafanya uchawi peke yao, wakichunguza mabadiliko ya majira, sura ya mwezi, na matukio mengine ya kiasili. Wengine huabudu na kuloga wakiwa kikundi, ambacho kwa kawaida huwa na wachawi 13.
Ni kweli kwamba mtazamo wa umma katika nchi za Magharibi kuelekea uchawi leo, ni tofauti sana na mitazamo iliyotia moyo kuchomwa kwa wachawi katika Enzi za Kati. Hata hivyo, mara kwa mara kunakuwa na visa vya jeuri mbaya dhidi ya wachawi. Kwa mfano, mapema mwezi wa Oktoba 1998 huko Indonesia, genge lenye mapanga liliua zaidi ya watu 150 waliotuhumiwa kuwa wachawi. Katika Afrika Kusini zaidi ya visa 2,000 vya jeuri dhidi ya wachawi, kutia ndani visa 577 vya mauaji viliripotiwa kati ya mwaka wa 1990 na 1998. Kwa sababu ya mitazamo hiyo mbalimbali—kutoka kupendezwa na uchawi hadi chuki kuelekea wachawi—Wakristo wanapaswa kuonaje suala hilo?
Mahitaji Yasiyotimizwa
Ni nini kinachowasukuma watu wazoee uchawi katika nyakati za kisasa? Wanadai kwamba sababu moja ni staha kwa mambo ya asili na kwa uhai. Kwa kweli, wengine hueleza kwa msisimuko kwamba ibada yao haihusishi desturi za kudhabihu wanyama. Wengine husema kwamba wao hujidukiza katika uchawi ikiwa njia ya kutafuta watu wanaoweza kuwa huru nao, kutumainiana, na walio na mapendezi sawa ya kiroho. “Kila mtu ninayemjua katika harakati za kipagani ni mnyoofu na mwenye urafiki sana . . . Ni watu wazuri ajabu,” asema mchawi mmoja wa kisasa. Wengi wao hukana dai la kujihusisha na Shetani, wakisisitiza kwamba katika muundo wao wa kidini hakuna mungu aliye mwovu kikamili.
Sababu ya msingi inayowafanya wengi wao wawe wachawi ni hisi ya utupu wa kiroho na kupoteza imani kwa dini zinazopendwa. Akizungumza juu ya kundi lao la wachawi, Phyllis Curott, kuhani wa kike wa cheo cha juu wa Wiccan, asema: “Sote tulikosa kuridhika na mafundisho na mazoea ya dini tulimolelewa.” Wachawi wa kisasa, aeleza Curott, hujaribu kujibu maswali kama vile, ‘Tunaweza kuvumbuaje upya mambo matakatifu?’ Lakini je, uchawi unaweza kutokeza hali ya kiroho ya kweli?
Hali ya Kiroho ya Kweli—Hutokana na Nini?
Biblia huonyesha wazi kwamba Yehova ndiye Mungu pekee wa kweli na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima. (Zaburi 73:28; 1 Petro 1:15, 16; Ufunuo 4:11) Anawaalika watu wote wamtafute yeye “na kwa kweli wampate.” (Matendo 17:27) Kwa hiyo, hali ya kiroho ya kweli yaweza kutokana tu na kutwaa ujuzi sahihi juu ya Mungu wa kweli, Yehova. Hili laweza kutimizwa kwa kujifunza Neno lake, Biblia Takatifu. “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia,” mwandikaji wa Biblia Yakobo atuhakikishia.—Yakobo 4:8.
Ingawa hivyo, Neno la Mungu hutuonya dhidi ya chanzo hatari cha hali ya kiroho iliyo mbovu. (1 Yohana 4:1) Humtambulisha Shetani Ibilisi, yule adui mkubwa wa Yehova, na roho wake waovu kuwa vyanzo vya hali ya kiroho iliyopotoka iliyoenea leo.c Kulingana na Biblia, Shetani “amepofusha akili” za wengi. Kwa kweli yeye ‘anaongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa na watu,’ kutia ndani wale wanaojihusisha na uchawi—wawe wanadai kumwabudu Ibilisi au la. Mbona iwe hivyo?—2 Wakorintho 4:4; Ufunuo 12:9.
Mazoea mengi na desturi nyingi za uchawi wa kisasa zinashabihi sana mazoea ya kiajabu ya Ibada ya Shetani. Kwa sababu hiyo, hata ule unaoitwa eti udadisi wenye madhumuni yanayofaa waweza kwa urahisi kuongoza kwa mambo ya mizungu. Kwa kweli, wengi wamenaswa na uvutano mwovu wa Shetani kwa njia hiyo.
Jambo lisilopasa kupuuzwa ni uhakika wa kwamba mara kwa mara wachawi wengi wa kisasa hujihusisha na zoea hilo kwa sababu ya tamaa ya utawala au ya kulipa kisasi. “Kuna watu wawezao kujiita wachawi na kutumia dai hilo kwa makusudi ya kikatili,” akasema Jennifer, mchawi wa kisasa. Kwa vyovyote vile, wale wanaozoea uchawi kwa sababu zinazofaa au kwa kulipa kisasi wako katika hatari ya kudhibitiwa na Shetani na roho wake waovu. Huenda baadhi ya wachawi wakakana kuwapo kwa viumbe wa kiroho walio waovu, lakini hilo huwatia katika hatari zaidi ya kunaswa na udanganyifu wao.—Linganisha 1 Wakorintho 10:20, 21.
Biblia hushutumu uaguzi, uchawi, zoea la mizungu, ulozi, na jaribio lolote la kuwasiliana na wafu. Hutaarifu waziwazi: “Mtu atendaye hayo ni chukizo kwa BWANA.” (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Bila shaka, Wakristo wameazimia ‘kufanya lililo jema kuelekea wote,” na katika huduma yao wamewasaidia wengi kuwa huru kutokana na namna zote za uwasiliani-roho. (Wagalatia 6:10; Matendo 16:14-18) Hata hivyo, Wakristo wa kweli huepuka kabisa kujihusisha kwa njia yoyote na ibada bandia, kutia ndani uchawi wa aina yoyote.—2 Wakorintho 6:15-17.
[Maelezo ya Chini]
a Usemi “dini ya mambo ya asili” hurejezea itikadi ya kwamba dunia na vitu vyote vilivyo hai ni sehemu ya uungu na huwa na kani-uhai ileile; “upagani-mpya” hurejezea ibada ya miungu ya kabla ya Ukristo.
b Kwa mujibu wa The American Heritage College Dictionary, Wawiccan ni wafuasi wa Wicca, ambayo ni “dini ya kipagani ya mambo ya asili iliyoanzia magharibi mwa Ulaya kabla ya Ukristo.”
c Mfululizo wa makala “Maoni ya Biblia” katika Amkeni! umejibu maswali kama vile “Je! Kweli Kuna Ibilisi?” (Novemba 8, 1990, ukurasa wa 26-27) na “Je, Roho Waovu Ni Halisi?” (Aprili 8, 1998, ukurasa wa 18-19).
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
Picture Book of Devils, Demons and Witchcraft/Ernst and Johanna Lehner/Doveyr