Sehemu ya 5
Ukweli Kuhusu Uchawi na Ulozi
1. Imani kwamba kuna uchawi na ulozi imeenea kadiri gani?
“BARANI Afrika, haina haja kuuliza kama kuna wachawi,” chasema kitabu African Traditional Religion, na kuendelea kusema kwamba “Waafrika wa hali zote huamini sana uchawi.” Watu wasio na elimu na hata wenye elimu ya juu huamini kwamba kuna uchawi na ulozi. Viongozi wa dini ya Kiislamu na wa Jumuiya ya Wakristo pia huamini kuna uchawi na ulozi.
2. Watu wengi wanaamini nguvu za uchawi hutoka wapi?
2 Watu wengi barani Afrika wanaamini kwamba kuna nguvu fulani ya kiroho yenye uwezo sana. Wanaamini kwamba Mungu anaidhibiti nguvu hiyo. Viumbe wa roho na wazazi wa kale wanaweza kuitumia. Na watu fulani pia wanajua jinsi ya kupata sehemu ya nguvu hiyo na kuitumia katika uchawi unaotoa ulinzi au uchawi unaodhuru.
3. Uchawi unaodhuru ni nini, na watu huamini unaweza kufanya nini?
3 Uchawi unaodhuru, hutumiwa kwa maadui. Inaaminika kwamba wale wanaoutumia wana nguvu za kutuma popo, ndege, nzi, na wanyama wengine wakashambulie watu. Watu wengi huamini kwamba uchawi husababisha mapigano, utasa, magonjwa, na hata kifo.
4. Watu wengi wanaamini nini kuhusu wachawi, nao wanatoa sababu gani ya kuamini hivyo?
4 Katika sehemu nyingi za Afrika, watu wengi wanaamini kwamba binadamu anaweza kubadilika au kubadilishwa na kuwa mnyama. Wengi wanaamini kuwa wachawi wana uwezo wa kubadilika kuwa chui au nyoka. Hali kadhalika, watu wengi huhofu kwamba mchawi anaweza kuwabadili watu wengine kuwa wanyama. Katika Afrika magharibi, inaaminiwa kwamba wachawi wanaweza kutuma roho za wanadamu kupitia ndege au wanyama wengine ili kuwadhuru watu wengine. Waafrika wengi huhisi kwamba mabadiliko hayo ya mtu kuwa mnyama yamethibitishwa na watu fulani waliojionea kwa macho. Wao hudai kwamba zile hadithi nyingi zinazosimuliwa na watu wenye akili timamu haziwezi kuwa mambo ya kukisia tu.
5. Uchawi unaoaminiwa kuleta ulinzi ni nini, nao hutumiwaje?
5 Uchawi unaoaminiwa kutoa ulinzi unasemekana kwamba hukinga mtu na mabaya. Wale wanaotumia uchawi huo huvaa pete au bangili za uchawi. Wao hunywa dawa fulani ya uchawi au kuipaka mwilini ili kujikinga. Nyumbani kwao au chini ya ardhi, wao huficha vitu ambavyo wanaamini vina nguvu za kuwalinda. Wanatumainia hirizi zenye maandiko ya Qurani au ya Biblia.
Uwongo na Udanganyifu
6. Shetani na roho wake waovu walifanya nini zamani, nasi tunapaswa kuzionaje nguvu zao?
6 Ni kweli kwamba Shetani na roho wake waovu ni maadui hatari wa wanadamu. Wana nguvu za kudhibiti akili na maisha ya watu, na zamani hata waliwapagaa wanadamu na wanyama. (Mathayo 12:43-45) Ingawa hatupaswi kupuuza nguvu zao, hatupaswi pia kuziona kuwa kubwa mno.
7. Shetani anataka tuamini nini, na ni mfano gani unaoonyesha jambo hilo?
7 Shetani ni mdanganyifu stadi. Yeye huwapumbaza watu wafikiri kwamba ana nguvu nyingi kuliko ilivyo kwa kweli. Kwa mfano: Wakati wa vita vya hivi karibuni katika nchi moja ya Afrika, askari-jeshi walitumia vikuza sauti ili kuwaogopesha maadui wao. Kabla ya kushambulia, askari hao walikuwa wakivumisha mlio mkubwa wa mizinga na bunduki uliokuwa umerekodiwa. Walitaka maadui wao wafikiri kwamba wanashambuliwa na jeshi lenye silaha nzito-nzito. Kwa njia hiyohiyo, Shetani hutaka watu waamini kwamba ana nguvu kubwa mno. Kusudi lake ni kuogopesha watu wasifanye mapenzi ya Yehova bali wafanye mapenzi yake. Na tuone aina tatu za uwongo ambao Shetani hutaka watu waamini.
8. Ni uwongo gani ambao Shetani huendeleza?
8 Uwongo mmoja ambao Shetani huendeleza ni huu: Hakuna jambo lolote baya linalotukia tu; kila jambo baya husababishwa na mtu fulani au na nguvu zisizo za kawaida. Kwa mfano, tuseme mtoto amekufa kwa ugonjwa wa malaria. Huenda mama yake anajua kwamba malaria ni ugonjwa ambao huenezwa na mbu. Lakini huenda pia akaamini kwamba mtu fulani alitumia uchawi kutuma mbu aje kumwuma mtoto wake.
9. Biblia inaonyeshaje kwamba Shetani hasababishi kila tatizo?
9 Ingawa Shetani ana nguvu za kusababisha matatizo fulani, ni kosa kuamini kwamba ana nguvu za kusababisha kila tatizo. Biblia inasema: “Si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” NW] huwapata wote.” (Mhubiri 9:11) Mkimbiaji mmoja anaweza kukimbia kwa kasi kushinda wengine, lakini asishinde. ‘Tukio fulani lisilotazamiwa’ linaweza kumfanya asishinde. Labda anajikwaa na kuanguka au anapatwa na tatizo la misuli. Mambo hayo yanaweza kumpata yeyote. Si lazima yawe yanasababishwa na Shetani au uchawi; yanatukia tu.
10. Ni nini ambacho husemwa kuwahusu wachawi, na tunajuaje kwamba huo ni uwongo?
10 Uwongo wa pili ambao Shetani huendeleza ni huu: Wachawi wanaweza kubadilika au kubadilishwa kuwa wanyama ili kuwadhuru wengine. Hebu jiulize: ‘Ikiwa wachawi wanaweza kufanya hivyo, ni nini hasa hutoka katika mwili na kuingia ndani ya mwili wa mnyama?’ Kama tulivyoona, roho si kitu kinachoweza kuuacha mwili wa mtu. Roho ni nguvu ya uhai ambayo huutia mwili nguvu lakini haiwezi kufanya chochote bila mwili. Kubadilika na kuwa mnyama ni kinyume cha sheria za maumbile zilizoanzishwa na Yehova Mungu. Bila shaka, Mungu hangepuuza sheria zake kwa kuwapa wanadamu uwezo wa kujibadili na kuwa wanyama wasio na akili.
11. Tunajuaje kwamba wachawi hawawezi kuiacha miili yao au kujibadili kuwa wanyama, na je, wewe unaamini hilo?
11 Roho haiwezi kuuacha mwili na kwenda kufanya jambo lolote baya au zuri. Hivyo, wachawi hawawezi kuiacha miili yao au kujibadili kuwa wanyama. Kwa kweli hawafanyi mambo wanayodai au wanayofikiri wamefanya.
12. Ni kwa njia gani Shetani huwafanya watu waamini kwamba wamefanya mambo ambayo hawakufanya?
12 Tunaweza kuelezaje mambo ambayo wale waliokuwa wachawi wanakiri kwamba walifanya? Shetani anaweza kufanya watu waamini kwamba wameona mambo ambayo hawakuona. Kupitia maono, Shetani anaweza kufanya watu wafikiri kwamba wameona, kusikia, au kufanya mambo ambayo hawakufanya. Kwa njia hiyo, Shetani anatarajia kugeuza watu wamwache Yehova na kuwafanya wafikiri kwamba Biblia si ya kweli.
13. (a) Je, uchawi unaoaminiwa kuleta ulinzi unafaa? (b) Biblia inasema nini kuhusu uchawi?
13 Uwongo wa tatu ni huu: Uchawi unaoaminiwa kutoa ulinzi unafaa kwa kuwa inaaminika kwamba unaweza kuumaliza nguvu ule uchawi unaodhuru. Biblia haitofautishi kati ya uchawi unaotoa ulinzi na uchawi unaodhuru. Inashutumu uchawi wa aina zote. Ona sheria ambazo Yehova alipatia taifa la Israeli kuhusu uchawi na wale wanaoutumia:
● ‘Msifanye uchawi.’—Mambo ya Walawi 19:26, Biblia Habari Njema.
● “Mtu mume au mtu mke aliye na pepo, au aliye mchawi, hakika atauawa.”—Mambo ya Walawi 20:27.
● “Asionekane kwako . . . mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi.”—Kumbukumbu la Torati 18:10-14.
14. Kwa nini Yehova alitunga sheria za kupinga uchawi?
14 Sheria hizo zinaonyesha wazi kwamba Mungu hakutaka watu wake wawe wachawi. Yehova aliwapa watu wake sheria hizo kwa sababu aliwapenda na hakutaka wawe watumwa wa woga na ushirikina. Hakutaka wakandamizwe na roho waovu.
15. Biblia inaonyeshaje kwamba Yehova ana nguvu nyingi zaidi kuliko Shetani?
15 Ingawa Biblia haizungumzii kwa undani mambo ambayo roho waovu wanaweza kufanya na wasiyoweza kufanya, inaonyesha kwamba Yehova Mungu ana nguvu nyingi zaidi kuliko Shetani na roho wake waovu. Yehova alimfanya Shetani atupwe kutoka mbinguni. (Ufunuo 12:9) Ona pia kwamba Shetani aliomba ruhusa ya kumjaribu Yobu naye alitii amri ya Mungu ya kutomwua Yobu.—Ayubu 2:4-6.
16. Tunapaswa kumtegemea nani atulinde?
16 Andiko la Mithali 18:10 linasema: “Jina la BWANA ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia, akawa salama.” Hivyo tunapaswa kumtegemea Yehova atulinde. Watumishi wa Mungu hawategemei hirizi au dawa za uchawi ziwalinde dhidi ya matendo maovu ya Shetani na roho wake waovu, wala hawaogopi walozi. Watumishi wa Mungu huamini yale ambayo Biblia inasema: “Macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.”—2 Mambo ya Nyakati 16:9.
17. Andiko la Yakobo 4:7 linatuhakikishia nini, lakini tunapaswa kufanya nini?
17 Wewe pia unaweza kuwa na uhakika huo ikiwa unamtumikia Yehova. Andiko la Yakobo 4:7 linasema: “Jitiisheni wenyewe kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia.” Ikiwa unamtumikia Mungu wa kweli na kujitiisha kwake, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakulinda.
Je, Wachawi Wanaweza Kudhibiti Radi?
Mapema mwaka wa 1977, wachawi 14 waliuawa kwa kuchomwa moto karibu na Pietersburg, Afrika Kusini. Gazeti la Drum la Afrika Kusini lilisema hivi kuhusu tukio hilo: “Wanaume na wanawake wameshikwa na woga. Wanaogopa kulogwa na kupigwa kwa radi . . .
“Ni lazima hatua fulani ichukuliwe . . . Kwa sababu hiyo, gazeti DRUM linawatolea wachawi wote mwito huu: Kuna pesa kiasi cha Randi 5 000 [sawa na dola 5,750 (za Marekani) wakati huo] kwenye ofisi zetu zitakazopewa yeyote ambaye katika mwezi wa Machi 1977, ataweza kumpiga na kumwua Stanley Motjuwadi kwa radi. Ikiwa hamwezi kufanya hivyo, basi acheni kila mtu ajue kwamba kule kujifanya kwamba mnaweza kudhibiti radi ni upumbavu na upuuzi mtupu.
“Kwa hiyo, enyi wachawi waongo, anzeni kujitayarisha. Mpigeni na kumwua Stanley Motjuwadi kwa radi ikiwa mnaweza.”
Je, wachawi hao waliweza kumpiga Stanley Motjuwadi kwa radi? Hapana, hawakuweza. Bw. Motjuwadi, mmoja wa waandishi wa Drum, hakufa bali alifanikiwa sana katika kazi yake na mwishowe akawa mhariri wa gazeti hilo.
Sanduku: Mwandishi mmoja nchini Afrika Kusini aliwatolea wachawi mwito gani, na matokeo yakawaje?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Wachawi hawawezi kujibadili kuwa wanyama
[Picha katika ukurasa wa 17]
Mara kwa mara, mambo mabaya hutokea tu