Vijana Huuliza . . .
Naweza Kuwaje Mwenye Urafiki Zaidi?
“Sijawahi kuwa mzungumzaji. Nilihisi kwamba watu wangeniepuka kabisa endapo ningesema neno fulani. Mama yangu ni mwenye haya sana, na nadhani ndiyo sababu nikawa mwenye haya.”—Artie.
JE, WEWE huhisi nyakati nyingine ingelikuwa heri kama hungelikuwa na haya sana yaani ungekuwa mwenye urafiki zaidi na mchangamfu? Kama makala iliyotangulia katika mfululizo huu ilivyoonyesha, haya ni tatizo la kawaida.a Kwa hiyo, si kosa kubwa sana iwapo una mwelekeo wa kukaa kimya, kuwa asiyecheka, au mwenye kujitenga. Lakini haya inayopita kiasi inaweza kuwa tatizo kubwa. Mbali na mambo mengine, inaweza kukuzuia kufurahia urafiki. Na inaweza pia kukufanya ukose starehe unapokuwa katikati ya watu.
Watu wazima pia hupambana na haya. Barryb ni mzee katika kutaniko la Kikristo. Lakini yeye hukaa kimya akiwa katika kikundi cha watu. Yeye akiri: “Naona kwamba sina uwezo wa kusema jambo lolote la maana.” Mke wake, Diane, ana tatizo hilohilo. Yeye hulitatuaje? Asema hivi: “Mimi hupenda kuwa miongoni mwa watu wenye urafiki kwa sababu naona kwamba wanaweza kuendeleza mazungumzo.” Ni baadhi ya njia zipi zinazoweza kukusaidia wewe uwe mwenye urafiki zaidi?
Koma Kujishushia Hadhi
Kwanza, utahitaji kuchunguza tena jinsi unavyojiona. Je, wewe hujishushia hadhi daima, ukifikiri kwamba wengine hawatakupenda au kwamba huwezi kusema jambo lolote la maana? Kuwa na maoni yasiyofaa juu yako mwenyewe kwaweza tu kukuzuia kuwa mwenye urafiki zaidi. Kwa vyovyote, Yesu alisema: “Lazima upende jirani yako kama wewe mwenyewe”—si badala yako mwenyewe! (Mathayo 19:19) Kwa hiyo kujipenda mwenyewe kwa kadiri inayofaa ni jambo bora na linalofaa. Kutakupa ujasiri ambao huenda ukahitaji ili uwafikie wengine.
Ikiwa unasumbuliwa na hisia za kutojistahi, huenda ukanufaika kusoma sura ya 12, “Kwa Nini Mimi Sijipendi?,” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi.c Habari hiyo yaweza kukusaidia kung’amua kwamba una sifa na uwezo unaokufanya uwe mwenye thamani na mwenye kuvutia. Kwani, jambo la kwamba wewe ni Mkristo huonyesha kwamba Mungu huona sifa fulani ya thamani ndani yako! Kwa vyovyote, Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.”—Yohana 6:44.
Pendezwa na Wengine
Andiko la Mithali 18:1 huonya hivi: “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe.” Ndiyo, ukijitenga na wengine, yaelekea kwamba utapendezwa sana na masilahi yako mwenyewe. Andiko la Wafilipi 2:4 hututia moyo ‘tufulize kuangalia, si masilahi ya kibinafsi ya mambo yetu wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.’ Unapokazia uangalifu masilahi na mahitaji ya wengine, hujifikirii sana. Na kadiri unavyozidi kuwajali wengine, ndivyo utakavyoelekea kuchukua fursa ya kwanza ya kupata kuwajua.
Kwa kielelezo, mfikirie Lidia, mwanamke ambaye amekuja kuonwa kuwa mfano wa urafiki na ukaribishaji-wageni. Biblia hutueleza kwamba baada ya kusikiliza mambo yaliyosemwa na mtume Paulo na kubatizwa, alisema hivi kwa kumsihi sana Paulo na waandamani wake: “Ikiwa nyinyi watu mmenihukumu mimi kuwa mwaminifu kwa Yehova, ingieni ndani ya nyumba yangu.” (Matendo 16:11-15) Ajapokuwa mwamini mpya, Lidia alichukua hatua ya kupata kuwajua ndugu hao—na bila shaka alipokea baraka nyingi kama tokeo. Baada ya Paulo na Sila kufunguliwa kutoka gerezani, walienda wapi? Jambo la kupendeza ni kwamba, walienda tena nyumbani mwa Lidia!—Matendo 16:35-40.
Hali kadhalika, utaona kwamba watu wengi wataitikia upendezi unaowaonyesha. Utaanzaje kupendezwa nao? Hapa pana madokezo machache yanayosaidia.
● Anza kwa mambo madogo-madogo. Kuwa mwenye urafiki zaidi hakumaanishi kuwa mcheshi kupita kiasi au mwenye kujishughulisha mno na mambo ya kijamii. Jitahidi kuzungumza na mtu mmoja-mmoja, peke yake. Waweza kuweka mradi wa kuzungumza na angalau mtu mmoja kila mara unapohudhuria mkutano wa Kikristo. Jaribu kutabasamu. Jizoeze kumtazama mtu kwenye macho.
● Anza urafiki. Huenda ukauliza ‘jinsi gani?’ Kwa kweli, ukipendezwa kikweli na wengine, haiwi vigumu kupata mambo ya kuzungumzia. Kijana mmoja huko Hispania anayeitwa Jorge asema: “Nimegundua kwamba kuuliza tu wengine jinsi walivyo au kuwauliza kazi yao ilivyo kunakusaidia upate kuwajua vema zaidi.” Kijana aitwaye Fred adokeza hivi: “Ikiwa hujui la kusema, anza tu kuuliza watu maswali.” Bila shaka, hutaki watu wahisi kwamba wanahojiwa. Ikiwa mtu aonekana kuwa mgumu kujibu maswali, jaribu kumweleza habari fulani juu yako mwenyewe.
Mary, mzazi wa kijana mmoja asema: “Nimegundua kwamba njia bora ya kuwastarehesha watu ni kuwaruhusu wajieleze.” Kate mchanga aongezea hivi: “Kuwasifu watu kuhusu mavazi yao au jambo jingine kunasaidia. Unawafanya wahisi kwamba wanapendwa.” Bila shaka, sema kwa unyofu, na epuka usemi usiofaa wa kurai. (1 Wathesalonike 2:5) Kwa kawaida watu wataitikia maneno ya moyo mweupe yenye fadhili na yanayopendeza.—Mithali 16:24.
● Uwe msikilizaji mzuri. ‘Uwe mwepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema,’ yasema Biblia. (Yakobo 1:19) Kwa vyovyote, maongezi ni kati ya watu wawili—si ya mtu mmoja. Kwa hiyo, ikiwa una mwelekeo wa kuona haya unapozungumza, huenda hilo likakusaidia sana! Watu huthamini wasikilizaji wazuri.
● Jiunge na maongezi. Ukisha kuwa stadi katika maongezi na mtu mmoja, songa kwenye maongezi ya kikundi. Mikutano ya Kikristo ni mahali panapofaa pa kujifunzia ustadi huu pia. Njia rahisi ya kujiunga na maongezi nyakati nyingine ni kujiunga na kikundi kinachoongea. Bila shaka, utambuzi na adabu nzuri ni muhimu katika maongezi haya. Usiingilie mazungumzo ambayo pasipo shaka ni ya faragha. Lakini iwapo wazi kwamba kikundi fulani kina maongezi ya kawaida, jaribu kujiunga nacho. Uwe mwenye busara; usikatize wala kujaribu kutawala mazungumzo. Jaribu kusikiliza kwa muda. Unapostarehe, huenda ukaelekea kutoa maelezo machache.
● Usitarajie kwamba hutakosea. Nyakati nyingine vijana huhofu kukosea katika usemi. Msichana mmoja huko Italia anayeitwa Elisa akumbuka: “Sikuzote nilihofu kwamba ikiwa ningesema jambo, ningelisema kwa njia mbaya.” Hata hivyo, Biblia hutukumbusha kwamba sote hatujakamilika, kwa hiyo hatuwezi kuwa na usemi mkamilifu. (Waroma 3:23; linganisha Yakobo 3:2.) Elisa asema: “Niling’amua kwamba hao ni marafiki wangu. Kwa hiyo endapo nitakosea katika usemi watanielewa.”
● Uwe mcheshi. Kwa wazi, kusema jambo lisilofaa bila kukusudia hutahayarisha. Lakini kama anavyosema Fred, “ukiwa mtulivu na ukijichekelea, punde si punde kipindi hicho hupita. Unafanya tatizo hilo liwe kubwa zaidi unapohangaika-hangaika, kuvunjika moyo, au unapokuwa na wasiwasi.”
● Uwe mwenye subira. Fahamu kwamba si kila mtu atakayeitikia mara moja. Kukosea kidogo katika maongezi hakumaanishi kwamba mtu hakupendi au kwamba unapaswa kuacha kujitahidi kuongea. Nyakati fulani watu huwa tu na shughuli nyingi—au huwa wenye haya kama wewe. Katika hali kama hizo, huenda ikasaidia kumpa muda zaidi wa kustarehe.
● Jaribu kuzungumza na watu wazima. Nyakati nyingine watu wazima, hasa Wakristo wakomavu huwasikitikia sana vijana wanaopambana na haya. Kwa hiyo, usihofu kuanzisha mazungumzo na mtu mwenye umri mkubwa zaidi. Kate asema: “Naweza kustarehe panapo watu wazima kwa sababu najua kwamba watu wazima hawawezi kunihukumu, kunidhihaki, au kunichambua kama vijana wa rika langu wawezavyo kufanya.”
Kuchochewa na Upendo
Ingawa madokezo hayo yaweza kusaidia, hakuna mbinu maalumu iliyo rahisi ya kushinda haya. Baada ya muda, utapata kwamba kushinda haya hakutegemei mbinu fulani ya werevu au utaratibu fulani maalumu. Hutegemea hasa ‘kumpenda jirani yako kama wewe mwenyewe.’ (Yakobo 2:8) Ndiyo, jifunze kuwajali watu wengine—hasa ndugu na dada zako Wakristo. (Wagalatia 6:10) Ukiwa na upendo halisi moyoni mwako, utashinda hofu na hisia ya kukosa usalama na utajitahidi kuwasiliana na wengine. Sawa na alivyosema Yesu, “kwa maana kutoka katika wingi wa moyo kinywa husema.”—Mathayo 12:34.
Barry, aliyetajwa mwanzoni asema: “Kadiri nipatavyo kuwajua watu wengine, ndivyo iwavyo rahisi kwangu kuzungumza nao.” Yaani, kadiri uzoeavyo kuwa mwenye urafiki zaidi, ndivyo itakavyokuwa rahisi kwako. Na unapoendelea kupata marafiki wapya na kuhisi kwamba wengine wanakupenda, bila shaka utaona kwamba jitihada yako haikuwa ya bure!
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Nisiwe Mwenye Urafiki Zaidi?” katika toleo letu la Oktoba 22, 1999.
b Baadhi ya majina yamebadilishwa.
c Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Chukua hatua ya kujiunga na maongezi!y