Mazungumzo Ni Usanii
KULA, kulala, kufanya kazi, haya ni mahitaji ya msingi ya binadamu. Na bado, uhitaji mwingine wataka kutoshelezwa. Ni nini huo?
Fikiria maneno ya mwanamume mmoja aliyekaa miaka mitano katika kizuizi cha kufungiwa peke yake, akinyimwa moja ya mahitaji ya msingi yenye thamani ya maisha. “Nilitamani sana uandamani, mtu wa kuongea naye, kuzungumza naye,” yeye akiri. “Nilianza kutambua ilinilazimu kufanya jambo fulani ili kushinda upweke huo. Katika upweke wangu na unyamavu, akili yangu ingeathiriwa.”
Ndiyo, tuna uhitaji wa kiasili wa kuwasiliana. Mazungumzo husaidia kutosheleza uhitaji huo. Watafiti Dennis R. Smith na L. Keith Williamson watoa maelezo hivi: “Twahitaji kuwa na watu ambao twaweza kuwaambia yote yaliyo mioyoni mwetu kwa unyofu, ambao twaweza kushiriki nao shangwe zetu kubwa zaidi na hofu zetu zinazosumbua zaidi, ambao twaweza kuongea nao.”
Twahitaji Kuongea!
Binadamu wamejaliwa zawadi ya ajabu ya usemi. Ndiyo, tumebuniwa ili tuzungumze. Mwanamume mmoja alionelea hivi: “Tuliumbwa na Mungu tuwe wenye kuishi pamoja. Ikiwa huna fursa ya kuongea, au ikiwa mtu fulani akuondolea uwezo wako wa kuwasiliana, ni kama adhabu. Unapozungumza, jambo la maana hutukia. Wahisi vizuri zaidi kujihusu, na wafaidika kutokana na kujua yale ambayo wengine wanafikiri na kuhisi.”
Elaine, mke wa mhudumu asafiriye, asema: “Maneno huonyesha hisia. Hatuwezi kudhania kwamba mwenzi wetu ajua jinsi alivyo mwenye thamani kwetu. Ni lazima isemwe; sikio lahitaji kusikia maneno. Twahitaji kuzungumza.”
David, mwana wa mzee Mkristo, ajieleza hivi: “Nyakati fulani navunjika moyo na sijui kwa kweli jinsi ninavyohisi. Mwelekeo wangu wa kwanza ni kukimya, halafu msongo wa kihisia-moyo unaongezeka ndani. Napata kwamba ikiwa naongea na mtu, ni kama tundu la kutoa nje msongo huo. Ninapokuwa nikiongea, nina nafasi ya kupata kujua jinsi ninavyojihisi kikweli na naweza kushughulika na hilo na kutafuta suluhisho.”
Vizuizi kwa Mazungumzo
Kwa kweli, mazungumzo hutosheleza uhitaji. Hata hivyo, kuna vizuizi kwa mazungumzo. Kwa wengine, hakika, mazungumzo yanakuwa mng’ang’ano—utendaji wa kuepukwa.
“Sehemu kubwa ya maisha yangu,” asema Gary, “napata ikiwa rahisi kuepuka mazungumzo na watu wengine.” Yeye aeleza hivi: “Sababu ya msingi kufanya hivyo ni ukosefu wangu wa matumaini. Bado napatwa na hofu ya kwamba ninapozungumza na watu, ninasikika mpumbavu au huenda mtu fulani akanidhilisha kwa yale ambayo nimesema.”
Elaine hueleza ugumu wake wa kuongea kuwa haya. Yeye aeleza hivi: “Nililelewa katika familia ambamo hatukuwa na maongezi muhimu. Baba yangu alikuwa mwenye kuogofya mno. Kwa hiyo nilipokuwa nikikua, nilihisi kwamba sikuwa na chochote kilichostahiki kunenwa.” Ndiyo, haya yaweza kutokeza vizuizi vikubwa kwa ufurahiaji wa mazungumzo. Kwani yaweza kukuzuia ndani ya kuta za unyamavu!
“Ni kama pigo,” asema John, mzee Mkristo anayekubali kujikakamua kushinda hisia ya kukosa utoshelevu. “Ukijiacha ushindwe na haya, wajitenga mwenyewe. Hata kuwe na watu mia moja katika chumba, hutazungumza. Na kama tokeo, utaumia!”
Kwa upande mwingine, mzee aitwaye Daniel ana hili la kusema: “Sina tatizo lolote kuhusu kuongea. Lakini kabla sijatambua, nimemkatiza mtu fulani na kumiliki mazungumzo. Nafahamu hili ninapoona ile sura ya kufadhaika katika uso wa mke wangu, nami nafikiria, ‘Mambo gani haya, nilimiliki mazungumzo tena.’ Ninajua kwamba shangwe yake inapotea kwa sehemu yote iliyobaki ya mazungumzo.”
Je, vizuizi hivi vya mazungumzo na vinginevyo vyaweza kushindwaje? Ni sifa gani zilizo za lazima katika usanii huu? Zaweza kutumiwaje?
‘Naweza Kusema Nini?’
‘Naweza kuongea kuhusu nini?’ ‘Sijui lolote.’ ‘Hakuna yeyote anayetaka kusikia lile ninalotaka kusema.’ Ingawaje huenda ukawa na mawazo hayo, yaelekea si ya kweli. Wewe wajua mengi zaidi ya unavyotambua, na baadhi ya habari hiyo yaelekea itakuwa yenye kupendeza kwa wengine. Kwa kielelezo, labda ulisafiri mahali fulani hivi karibuni. Huenda watu wakataka kujua jinsi mahali huko kunavyolingana na mahali wanapoishi.
Kwa kuongezea, waweza na wapaswa kuongeza ujuzi wako wa habari tofauti-tofauti kwa kusoma. Ni zoea zuri kuchukua wakati ili kusoma kitu fulani kila siku. Fasihi ya Mashahidi wa Yehova huwa na habari juu ya Biblia na vilevile juu ya habari za upendezi wa kawaida. Kwa kadiri unavyopata habari, ndivyo uwezavyo kuishiriki. Kielelezo bora ni kijitabu cha andiko la kila siku Kuyachunguza Maandiko Kila Siku kama kinavyotumiwa na Mashahidi wa Yehova. Kila siku, kijitabu hicho hukupa jambo tofauti la kufikiria na la kutumia katika mazungumzo.
Kujihusisha katika mazungumzo hakumaanishi kwamba mtu apaswa kuongea mambo yote. Wote wapaswa kujieleza wenyewe. Ruhusu mtu yule mwingine aseme. Ikiwa yuko kimya, waweza kumtia moyo kwa maswali yenye busara. Wazia unaongea na mtu mwenye umri mkubwa zaidi. Ungeweza kumwuliza kuhusu matukio ya wakati uliopita na jinsi ulimwengu au maisha ya familia yamegeuka tangu alipokuwa kijana. Utafurahia kumsikiliza na utajifunza.
Uwe Msikilizaji Mwema
Kusikiliza kwa uangalifu ni kitu cha thamani katika mazungumzo. Jinsi tunavyowasikiliza wengine kwaweza kutegemeza wale wajitahidio kupata msaada kwa mahangaiko yao. Mwanamume mmoja, aliyejiona kuwa ‘miongoni mwa wasiostahiki kitu,’ alikuwa akihisi huzuni na akampigia rafiki simu ili amsaidie. Ijapokuwa ulikuwa wakati usiofaa kabisa, rafiki huyo alisikiliza kwa fadhili—kwa muda wa saa mbili! Mwanamume huyo sasa aona kwamba mazungumzo hayo yalikuwa ni badiliko kubwa katika maisha yake. Ni nini kilichochangia kufaulu? “Ni kuwa tu msikilizaji mwema,” akubali rafiki huyo mwenye kusikiliza kwa makini. “Sikumbuki nikisema maneno yoyote ya hekima. Niliuliza maswali yafaayo tu, ‘Kwa nini wahisi hivyo?’ ‘Kwa nini hilo lakusumbua?’ ‘Ni nini chaweza kusaidia?’ Alijibu maswali yake yote mwenyewe alipojibu yangu!”
Watoto huhazini wazazi ambao huweka wakati wa kuzungumza nao. Mvulana mmoja aitwaye Scott atoa maelezo hivi: “Ni vema wazazi wako wakujiapo na kutaka kujua mahangaiko yako. Baba amekuwa akifanya hivyo karibuni, na inasaidia kwa sababu kuna mambo fulani ambayo huwezi kuyakabili peke yako.”
“Ni lazima ufanyize mazingira ambayo katika hayo watoto wako wataongea nawe,” adokeza mwanamume mmoja. Yeye hutumia wakati kwa ukawaida akiwa na kila mmoja wa watoto wake wanne kwa sababu ahisi kwamba usikivu wa wazazi wenye umakini na huruma ni wa muhimu ikiwa vijana watakuza nyutu zilizorekebishwa ifaavyo. Pendekezo lake ni nini? Fursa zinapotokea na mtoto ataka kuongea, uwe tayari kusikiliza. “Hata iwe umechoka au umelemewa kadiri gani, usiwakandamize kamwe! Sikiliza,” yeye asema.
Upendezi wa Moyo Mweupe Hupata Itikio
Watu wengi wanahitaji utegemezo wa kihisia-moyo ili waweze kuwasiliana na kujieleza wenyewe katika mazungumzo. Mwanamume mmoja kijana aliomboleza hivi: ‘Nahitaji kuongea na mtu, lakini niende kwa nani? Si rahisi kwangu kuongea. Nahitaji mtu fulani ambaye atapendezwa nami!’ Upendezi wa kweli na wa moyo mweupe waweza kufanyiza hali yenye kutumaini na salama ambayo katika hiyo ni rahisi kwa mtu kuongea na kufunua moyo wake kwa mwingine.
Mwanamume mmoja aelezea: “Miaka kadhaa iliyopita, nilipokuwa na magumu katika kushughulikia hali za familia, nilijaribu kuzungumza na rafiki. Aliyosema tu ni, ‘Vumilia hali hiyo isiyofurahisha na uwe thabiti na kila kitu kitakuwa shwari.’ Hakukuwa na masemezano, wala mazungumzo, na haikusaidia. Kwa hakika ilinirudisha tu katika hali ileile ya unyamavu na kutowasiliana. Kinyume na hilo, niliongea na mwangalizi fulani wa Mashahidi wa Yehova baadaye. Kwa mtazamo wake, wonyesho wake wa usoni, na tabia yake ya upole, nilijua kwamba alikuwa mwenye huruma. Kama tokeo, nilijipata nikiweza kuwasiliana na kuzungumza zaidi kwa kuwa alipendezwa kwa moyo mweupe. Yeye alisema hivi: ‘Tutafanya lolote tuwezalo ili kukuunga mkono katika hali yako.’ Je, wewe huitikia watu kwa njia hiyo!”
Je, wengi wetu twaweza kufungua mioyo yetu na kuvuta wengine kwenye mazungumzo yenye maana? Tuonapo mtu fulani ameachwa nje katika mazungumzo ya kikundi, mwenye haya mno kuzungumza, je, sisi hujaribu kumtia ndani mtu huyo katika mazungumzo yetu? Asema John, aliyetajwa mapema: “Naweza kuhisi hisia hiyo ya unyamavu kwa sababu najiona katika hali yake, nami naugua pamoja naye!” Yeye aongeza hivi: “Jinsi ilivyo muhimu kuvutwa kumkaribia na kumhusisha. Twaweza hata kusema sala ya kimya kuhusu jambo hilo.”
Dan asema kuhusu rafiki fulani: “Roy alikosa utumainifu katika uwezo wake wa kuzungumza na watu hivi kwamba wakati kikundi kingekuwa kikizungumza, yeye angesimama hatua kadhaa nyuma. Hivyo ningemuuliza swali, ‘Aise, Roy, nini kile ulichokuwa ukisema kuhusu hili au lile?’ Halafu angeanza kuongea. Kama tokeo, wengine waliona sehemu ya utu wake waliyokuwa hawajui.” Dan ahimiza: “Usikate tamaa wakati mtu anapokuwa mgumu kuongea au kukueleza jambo. Fikiria ndani yako kwamba kuna mtu wa ndani atakaye kuzungumza. Endelea kumfanya aongee kwa uhuru na uendelee kufanyia hilo kazi.”
Kwa kukuza upendezi wenye upendo na wa moyo mweupe kuelekea wengine, wewe pia wanufaika—hata ikiwa una tatizo la haya. John alipata kwamba hili lilimsaidia kushinda tatizo la kujitenga mwenyewe. “Upendo hautafuti mambo yake,” yeye aeleza. (1 Wakorintho 13:5) “Ili kufanya jambo la upendo ni lazima uongee na kuulizia habari za wengine. Kujiacha ushindwe na mapungukio yako hakuwi na maana yoyote. Waweza kupitia sala kushinda mielekeo yako.” Yeye aongeza hivi: “Kuna thawabu kubwa sana katika kufanya jambo hilo. Unapoona wengine wakiitikia na kutambua jinsi wanavyojengwa, wajengwa hata wewe pia. Na hilo lapaswa kukutia ujasiri wa kukaribia mtu mwenye haya wakati ujao tena na tena.”
Hisia-Mwenzi—Msingi wa Mazungumzo
Miongoni mwa vitabia vya binadamu vinavyothaminiwa sana ni hisia-mwenzi. Lakini hisia-mwenzi ni nini? Dakt. Bernard Guerney wa Chuo Kikuu cha Pennsylvania State asema kwamba ni ‘uwezo wa kufahamu kwa umakini hisia za mtu mwingine na maoni yake—iwe wakubaliana naye au la.’ Hisia-mwenzi ni ya maana kadiri gani katika mazungumzo? “Hiyo ndiyo jiwe la msingi! Hiyo ndiyo msingi ambao juu ya huo vitu vingine vyote hujengwa.”
Dakt. Guerney aeleza kwamba mazungumzo ni ya lazima katika mahusiano yote mema. Bila shaka, tofauti za maoni huwa za kawaida. Ili kushughulika nazo kwa mafanikio na kudumisha uhusiano, lazima tuwe na nia ya kuongea kuhusu tatizo. Wengi huepuka kufanya hilo kwa sababu hawajui jinsi ya kuongea bila kumfanya mtu yule mwingine awe mwenye kutetea udhaifu wake na kumkasirisha. Kulingana na Dakt. Guerney, “watu wengi hushindwa kupambanua kati ya uthamini na staha kwa cheo cha yule mtu mwingine na kukubali cheo hicho. Kama tokeo, wanapokosa kukubaliana, hawaonyeshi wepesi wa kufahamu na staha. Hisia-mwenzi hukuruhusu utambue tofauti kati ya kukubali na uthamini.”
Kwa kujiweka kiakili katika hali ya mtu mwingine, wahisi na kufikiri kama afanyavyo. Chini ya hali kama hizo, utapata kwamba uelewevu, uthamini, na staha zitakua, hata ikiwa mwakosa kukubaliana.
Fikiria Janet, mama ya watoto wanne. Wakati mmoja alikuwa mwenye kukata tamaa na kuhisi akiwa bure. Sasa yeye ajua jinsi hisia-mwenzi ni muhimu katika kusaidia mtu fulani. Yeye asimulia hivi: “Nakumbuka mume wangu akiongea nami na kueleza njia zote tofauti nilizokuwa mwenye kusaidia, ilhali niliwazia kwamba matendo yangu yalijumlika kutokuwa chochote kabisa. Yeye kwa upendo alinisikia hata nilipokuwa nikilia, halafu akanijenga. Lakini ikiwa angedhilisha kufikiri kwangu au kusema ‘Ah, huo ni upuzi,’ au kusema kitu kama hicho, ningekuwa mnyamavu sana na ningalienda kivyangu. Badala yake, jioni hiyo tulikuwa na mazungumzo marefu, yenye maana.”
‘Hisia-mwenzi huonyesha kwamba wahisi upendezi na una ufikirio. Hilo huchochea uwasiliano, aina ya mbadilishano uliopanuka ambao watu wengi hutamani na kuhitaji,’ amalizia Dakt. Guerney.
Wewe Unaweza Kufanya Hilo!
Unaweza kuwa mzungumzaji mwema. Tumechunguza baadhi ya mambo muhimu ili kujua vizuri usanii wa mazungumzo, lakini kuna mengine mengi. Hayo yatia ndani urafiki, ucheshi, na busara, kutaja machache tu. Lakini kama msanii, ambaye kupitia kujifunza na mazoezi hutumia kwa ustadi burashi yake kwenye kitambaa ili kubuni mchoro wenye kupendeza, twahitaji kujitahidi sana kukuza sifa hizi zihitajiwazo.
Kwa kielelezo, Daniel amekuwa mzungumzaji mwema. Jinsi gani? Kwa kujifunza kudhibiti mwelekeo wake wa kukatiza na kumiliki mazungumzo. Yeye akubali: “Ni lazima nifanye jitihada nyingi ili nisimiliki mazungumzo. Kwangu hilo lamaanisha kuuzuia ulimi wangu. Ninapojikuta nikitaka kuongezea visehemu vidogo, ninajisimamisha kiakili! Nikiona kwamba elezo litageuza mwendo wa mazungumzo au kuondoa uwezo wa mtu wa kuzungumza, naacha kusema tu!”
Ni nini kilichomsaidia Elaine? Baada ya kupata ujuzi sahihi wa Biblia, alitambua alikuwa na jambo la thamani na linalostahiki kuzungumzia. Yeye asema: “Napata kwamba nikiondoa uangalifu kwangu na kuzungumza kuhusu mambo ya kiroho na wengine, naweza kustareheka zaidi kuzungumza. Inasaidia pia kusoma fasihi inayotegemea Biblia tunayopokea kwa ukawaida. Ninapoendelea kuwa wakati mmoja nayo, ninakuwa na jambo jipya na la karibuni kushiriki na naweza kuzungumza kwa urahisi zaidi.”
Jaribu kukuza sifa hizi muhimu katika mazungumzo yako. Ndipo hata wewe unaweza kuleta kiburudisho na raha kwa wengine na kuwa na uradhi wa kujua vizuri usanii ambao kwa kweli hutimiza uhitaji wa binadamu.