Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g05 9/8 kur. 26-27
  • Je, Usali kwa Bikira Maria?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Usali kwa Bikira Maria?
  • Amkeni!—2005
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Tufundishe Jinsi ya Kusali”
  • Namna Gani Rozari?
  • Kumheshimu Maria
  • Jukumu la Maria Katika Kusudi la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Mfano wa Maria Unatufundisha Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Je! Wakristo Wapaswa Kutumia Tasbihi (Rozari)?
    Amkeni!—1990
  • “Tazama! Kijakazi wa Yehova!”
    Igeni Imani Yao
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2005
g05 9/8 kur. 26-27

Maoni ya Biblia

Je, Usali kwa Bikira Maria?

MARIA anajulikana sana na watu wengi wanaojua Ukristo. Maandiko yanasema kwamba Mungu Mweza Yote alimbariki hasa mwanamke huyo kijana kwa kumchagua awe mama ya Yesu. Kuzaliwa kwa Yesu kulikuwa kwa pekee kwa kuwa Maria alikuwa bikira alipopata mimba yake. Kwa muda mrefu, makanisa fulani yanayojiita ya Kikristo yamemheshimu Maria kwa njia ya pekee. Katika mwaka wa 431 W.K., Baraza la Efeso lilimtangaza kuwa “Mama ya Mungu,” na leo watu wengi wanafundishwa wasali kwake.a

Waabudu wanyoofu wanajua kwamba wanapaswa kuelekeza sala zao kwa mtu anayefaa. Biblia inafundisha nini kuhusu jambo hilo? Je, Wakristo wasali kwa Bikira Maria?

“Tufundishe Jinsi ya Kusali”

Simulizi la Injili ya Luka linasema kwamba mmoja wa wanafunzi wa Yesu alimwomba hivi: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.” Yesu alimjibu: “Wakati wowote mnaposali, semeni, ‘Baba, jina lako na litakaswe.’” Wakati wa Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu aliwaagiza wafuasi wake wasali vivyo hivyo: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.”—Luka 11:1, 2; Mathayo 6:9.

Hivyo, jambo la kwanza tunalojifunza ni kwamba sala, au maneno ya ibada yanapaswa kuelekezwa kwa Baba ya Yesu, yaani, Yehova. Biblia haituruhusu tusali kwa mtu mwingine yeyote. Jambo hilo linafaa kwa sababu Musa alipopewa zile Amri Kumi, aliambiwa kwamba Yehova ni “Mungu anayetaka watu wajitoe kikamili.”—Kutoka 20:5.

Namna Gani Rozari?

Watu wengi wanaosali kwa Maria wamefundishwa kwamba watapata baraka wakirudia-rudia maneno yaleyale katika sala kama vile Maria Mtakatifu, Baba Yetu, na sala nyingine. Kitabu Symbols of Catholicism kinasema kwamba kwa Wakatoliki, “bila shaka, rosari ndiyo ibada ya Maria iliyoenea sana.” Rozari ni desturi ya kidini ya kumheshimu Bikira Maria. Pia neno hilo linarejelea ushanga unaotumiwa kuhesabu sala. Kitabu hicho kinaeleza kwamba, “vikundi 5 vya shanga 10 zilizogawanywa na ushanga mmoja tofauti ni sala 50 za ‘Mtakatifu Maria’, 5 za ‘Baba Yetu’, na 5 za ‘Utukufu kwa Baba.’” Je, Mungu husikiliza sala hizo zinazotolewa kwa kutumia rozari?

Kwa mara nyingine, maagizo ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake yanatupa jibu lenye kutegemeka. Alisema: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa wanavyofanya, kwa maana wao huwaza watasikiwa kwa kutumia maneno mengi.” (Mathayo 6:7) Hivyo Yesu aliwaambia kihususa wafuasi wake wasirudie-rudie maneno yaleyale katika sala zao.

Huenda mtu akauliza, ‘Lakini, si Yesu aliwafundisha wanafunzi wake warudie sala ya Baba Yetu, ambayo ni sehemu ya rozari?’ Inakubaliwa kwamba Yesu alifundisha sala ya kielelezo, ambayo ilijulikana kama Baba Yetu, au Sala ya Bwana. Hata hivyo, tunapaswa kukumbukwa kwamba alifanya hivyo punde tu baada ya kuonya kwamba tusiseme “mambo yaleyale tena na tena.” Ili kuonyesha kwamba hakunuia sala ya kielelezo ikaririwe, Yesu alitumia maneno tofauti katika visa viwili alipowafundisha wanafunzi wake kusali. (Mathayo 6:9-15; Luka 11:2-4) Katika visa vyote viwili, Yesu alieleza wazo lilelile kwa kutumia maneno tofauti. Hilo linafanya tukate kauli kwamba Yesu alikuwa tu akitoa vielelezo au mifano ya jinsi ambavyo wafuasi wake wanaweza kusali na mambo yanayofaa ambayo wanaweza kusali juu yake. Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba, maneno yake yalionyesha yule ambaye sala zinapaswa kuelekezwa kwake.

Kumheshimu Maria

Ingawa Maandiko hayawafundishi Wakristo kusali kwa Maria, hilo halimaanishi kwa njia yoyote kwamba yanapuuza yale ambayo alifanya katika kutimizwa kwa makusudi ya Mungu. Baraka ambazo zitaletwa kupitia Mwana wake zitawanufaisha wanadamu wote watiifu. Maria mwenyewe alisema: “Vizazi vyote vitanitangaza kuwa mwenye furaha.” Naye Elisabeti, binamu yake alisema kwamba Maria alikuwa “mbarikiwa kati ya wanawake.” Na kwa kweli alibarikiwa. Lilikuwa pendeleo kubwa kwa Maria kuchaguliwa kumzaa Masihi.—Luka 1:42, 48, 49.

Hata hivyo, si Maria peke yake anayetajwa katika Biblia kuwa mwanamke aliyebarikiwa. Kwa sababu ya yale ambayo alifanya kwa manufaa ya taifa la kale la Israeli, Yaeli pia anatajwa kuwa ‘alibarikiwa zaidi kati ya wanawake.’ (Waamuzi 5:24) Kwa kweli, tunapaswa kuwaiga wanawake kama Yaeli, Maria, na wengine wengi waliomwogopa Mungu ambao wanatajwa katika Biblia, lakini hatupaswi kuwaheshimu kupita kiasi.

Maria alikuwa mfuasi mwaminifu wa Yesu. Alikuwepo pindi mbalimbali wakati wa huduma yake hapa duniani na hata Yesu alipokufa. Baada ya Yesu kufufuliwa, Maria pamoja na ndugu za Yesu walikuwa “wakidumu katika sala.” Jambo hilo linatupa sababu ya kuamini kwamba yeye pamoja na ndugu za Yesu walitiwa mafuta kwa roho takatifu Pentekoste 33 W.K., na kwa hiyo alikuwa na tumaini la kuwa sehemu ya jamii ya bibi-arusi ambayo itatawala pamoja na Kristo mbinguni.—Mathayo 19:28; Matendo 1:14; 2:1-4; Ufunuo 21:2, 9.

Ingawa hivyo, hatupaswi kusali kwa Maria. Sala ya kutoka moyoni ni sehemu muhimu ya ibada, na Wakristo wanatiwa moyo ‘wadumu katika sala.’ (Waroma 12:12) Hata hivyo, sala zote zinapaswa kuelekezwa kwa Yehova peke yake, kupitia Yesu Kristo.—Mathayo 4:10; 1 Timotheo 2:5.

[Maelezo ya Chini]

a Wazo la kwamba Maria ni mama ya Mungu linategemea fundisho la Utatu lisilopatana na Maandiko, ambalo husema kwamba Yesu ni Mungu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki