Maoni ya Biblia
Je, Unaweza Kuwasaidia Wafu?
“Tangu mwanzo Kanisa . . . limekuwa likitoa sala kwa ajili ya [wafu] . . . ili, wakiisha kutakaswa, waweze kumwona Mungu kihalisi.”—Kitabu “Catechism of the Catholic Church.”
WATU katika jamii zote huhangaikia sana hali ya wafu. Labda umehuzunika na kujihisi mpweke baada ya kufiwa na mpendwa wako. Huenda ukajiuliza ikiwa wafu wanaendelea kuishi, ikiwa wanateseka au wana amani, na ikiwa kuna jambo lolote unaloweza kufanya ili kuwasaidia.
Watu wengi wa kidini huamini kwamba wanaweza kuwasaidia wafu. Kwa mfano, Wahindu huamini kwamba wakichoma mwili wa mpendwa wao kwenye ukingo wa Mto Ganges na kutawanya majivu juu ya maji yake, wanaweza kuhakikisha kwamba nafsi ya aliyekufa itakuwa na furaha ya milele. Kule Mashariki, Wabudha huchoma karatasi zilizoundwa kwa mfano wa gari, nyumba, nguo, na pesa, kwa kuwa wao huamini aliyekufa anaweza kutumia vitu hivyo katika maisha mengine ambayo sasa anaishi. Barani Afrika, vileo humwagwa kaburini eti kufanya hivyo kutamsaidia aliyekufa.
Wakatoliki hufundisha kwamba mtu akifa bila kutubu “dhambi ya mauti,” amejiondolea kibali cha Mungu. Hali hiyo “inaitwa ‘moto wa mateso.’” Kwa upande mwingine, wanafundisha kwamba mtu aliye na kibali cha Mungu anaweza kuwa na tumaini la kupata “furaha kuu na kamili” pamoja na Mungu mbinguni, lakini si kabla ya kutakaswa kabisa. Ili atakaswe huenda akahitaji kukaa purgatori kwa muda fulani ili ateseke katika “moto wa kutakasa” unaotolewa kama nidhamu kwa ajili ya makosa yake ambayo anaweza kusamehewa. Hata hivyo, anapokuwa purgatori, mtu huyo anaweza kusaidiwa kwa kuombewa na Kanisa na vilevile kwa Misa zinazofanywa kwa niaba yake. Kwa kawaida, ibada kama hizo hulipiwa na marafiki na watu wa ukoo wa aliyekufa.
Ni jambo la kawaida kwa mtu kutaka kufanya jambo lolote ili wapendwa wake wasiteseke. Ikiwa tungeweza kuwasaidia, je, Mungu hangetueleza jambo tunalopaswa kufanya? Na tuone Biblia inafundisha nini kuhusu kuwasaidia wafu.
Hali ya Wafu
Desturi zote zilizotajwa zinategemea imani kwamba nafsi haiwezi kufa, yaani, sehemu fulani ya mtu huendelea kuishi baada ya mwili wake kufa. Je, Biblia inafundisha hivyo? Biblia inasema hivi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe, wala hawana malipo tena, kwa maana kumbukumbu lao limesahauliwa. Pia, upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari zimepotea, na mpaka wakati usio na kipimo hawana fungu lolote tena katika chochote ambacho kitafanywa chini ya jua. Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote, kwa maana hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi, mahali unapokwenda.”—Mhubiri 9:5, 6, 10.
Mtunga-zaburi aliyeongozwa kwa roho aliandika hivi kuhusu athari za kifo: “Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.”—Zaburi 146:4.
Maneno ya Biblia yana mamlaka nayo yanapatana na akili. Unafikirije? Je, baba mwenye upendo anaweza kuwatesa watoto wake kwa sababu ya mwelekeo wao wa kutenda dhambi ambao wamerithi? (Mwanzo 8:21) Bila shaka la. Kwa hiyo, Baba yetu wa mbinguni angewezaje kufanya jambo kama hilo? Watu fulani katika Israeli la kale walipoanza kufuata desturi ya kipagani ya kuwachoma watoto wao ili kuwatolea dhabihu miungu bandia, Yehova alishutumu zoea hilo lenye kuchukiza, akisema kwamba lilikuwa ‘jambo ambalo hakuwa ameamuru wala halikuingia moyoni mwake.’—Yeremia 7:31.
Dhambi za wanadamu hutokeza kifo, bali si kuteswa katika maisha baada ya kifo. “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” Maandiko yanasema, na “yeye ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.”—Waroma 5:12; 6:7, 23.
Wafu hawateseki. Badala yake, ni kana kwamba wamelala usingizi mzito, bila kuwa na fahamu yoyote, nzuri au mbaya. Hivyo, hakuna shaka kwamba jitihada zozote za watu za kuwasaidia wafu hupingana na mafundisho ya Biblia.
Kuna Tumaini Gani kwa Waliokufa?
Hilo halimaanishi kwamba wapendwa wako waliokufa wataendelea kuwa bila fahamu milele. Tofauti na hilo, kuna tumaini zuri kwa waliokufa.
Kabla ya kumfufua rafiki yake mpendwa Lazaro, Yesu alisema kwamba anaenda “kumwamsha kutoka usingizini.” (Yohana 11:11) Katika pindi nyingine alisema kwamba “wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Wanaofufuliwa watakuwa tayari wamesamehewa dhambi zao za awali na hivyo hawatahitaji kuteseka kwa ajili ya mambo waliyofanya walipokuwa hai. Watakuwa na nafasi ya kujifunza kufurahia maisha chini ya hali kamilifu. Hilo ni taraja zuri kama nini!
Ikiwa taraja hilo linakuvutia, usisite kuchunguza ikiwa ni za hakika. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.
JE, UMEJIULIZA HIVI?
◼ Je, wafu wanajua jambo lolote?—Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5, 6, 10.
◼ Je, Mungu anaweza kuruhusu wafu wateseke katika moto wa mateso?—Yeremia 7:31.
◼ Je, kuna tumaini kwa waliokufa?—Yohana 5:28, 29.