Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Amkeni! Lenye Sura Mpya Jana usiku nilimaliza kusoma Amkeni! la Januari 2006. Ninapendezwa sana na sura yake mpya! Sasa Amkeni! ni gazeti ambalo mtu anapaswa kujifunza kwa makini, nalo limetayarishwa kwa njia inayomchochea msomaji kutafakari. Katika gazeti lote nimeona jinsi Yehova anavyoongoza mambo ili kutusaidia kukua kiroho.
B. N., Kanada
Nina miaka 16. Mambo mapya katika Amkeni! yatatusaidia sana kujifunza Biblia. Makala nyingine zina maswali ili kumsaidia msomaji atafakari mambo aliyosoma. Ninafurahia kutumia Amkeni! kwa ajili ya migawo yangu ya shule. Ninatumaini mtaendelea kuchapisha makala nzuri kama hizo zenye kuelimisha.
S. N., Namibia
Imani Yangu Yaniimarisha—Kuishi na Ugonjwa wa ALS (Januari 2006) Baada ya kusoma simulizi la Jason Stuart, matatizo yangu yote yamekuwa kama si kitu. Nimetambua kwamba Yehova anathamini utumishi tunaomtolea kulingana na hali zetu. Nimevutiwa sana na mke wa Jason, kwa kujidhabihu kwake na imani yake kwa Yehova. Daima simulizi hilo litabaki moyoni mwangu na litanisaidia kukabiliana na matatizo ambayo yatazuka baadaye.
C.R.S., Peru
Mara baada ya kusoma simulizi la Jason nililia, si kwa sababu tu niliguswa moyo niliposoma kuhusu masaibu yake lakini pia kama Shahidi wa Yehova, ninaona fahari sana kuwa na ndugu wa kiroho kama yeye. Makala hiyo ilinionyesha umuhimu wa kujitayarisha kwa ajili ya majaribu, kwani “wakati na tukio lisilotazamiwa” linaweza kumpata yeyote kati yetu.—Mhubiri 9:11.
T. A., Hungaria
Mama yangu alikufa kwa sababu ya ALS. Hivyo simulizi la Jason lilinigusa moyo sana. Mfano wake ulinichochea kujitahidi niwezavyo katika utumishi. Ninasali kwamba Yehova aendelee kumtia nguvu ndugu huyo na mke wake.
L.Z.G., Paraguai
Kujua kwamba Jason alipokuwa na afya alitumia wakati wake mwingi kujifunza kibinafsi na hivyo akawa na nguvu za kiroho za kumtegemeza alipozihitaji, kulinifanya nifikiri. Kujua hilo kuliimarisha azimio langu la kuwa na bidii zaidi katika funzo langu la kibinafsi la Biblia.
Y. M., Japani
Vijana Huuliza—Kwa Nini Mimi Hujiumiza? (Januari 2006) Nikiwa kijana nilihangaishwa na dawa za kulevya na pombe, lakini tatizo gumu zaidi nililokabili lilikuwa kujiumiza. Nimekuwa nikipambana nalo, lakini kusoma makala kama hiyo kumenipa nguvu za kuendelea kuvumilia. Ninashukuru sana.
E. C., Marekani
Nimekuwa nikijiumiza mwenyewe tangu nilipokuwa kijana. Sasa nina miaka 56. Niliacha tabia hiyo ya kujiumiza miaka minne iliyopita, lakini wakati mwingine matatizo yangu ni mengi na hivyo ninatamani kujiumiza tena. Makala hiyo imeugusa moyo wangu. Itawaimarisha watu kama mimi kuendelea kukabiliana na maisha kila siku.
Jina limebanwa, Uholanzi
Nina miaka 17, na ningependa kuwashukuru kwa makala hiyo. Nina tatizo la kujiumiza. Hivi karibuni nilijikata tena. Baada ya hapo nilimwomba mama asali pamoja nami. Ijapokuwa nina tatizo hilo, nimejifunza kwamba Yehova ananipenda. Makala yenu imenisaidia sana, na ninamshukuru Mungu kwa sababu hiyo!
N. M., Jamhuri ya Cheki
“Hili haliwezekani!” Nilisema hivyo nilipoona makala hiyo. Nina umri wa miaka 18 na nimekuwa nikijiumiza. Maumivu hunisaidia kudhibiti hisia zangu. Mara nyingi mimi hutaka kujiumiza na sijui jinsi ya kushinda hisia hizo. Nilishangazwa sana kuona makala hiyo. Macho yangu yalijawa na machozi nami nikamshukuru Yehova katika sala. Unaweza kupata kitulizo kama hicho katika tengenezo la Yehova tu!
A. P., Urusi
Nilipokuwa na miaka 14, nilianza kutuliza maumivu ya kihisia kwa kujiumiza. Hata wakati fulani nililazimika kwenda hospitalini kwa sababu ya jambo hilo. Kuweka kumbukumbu kumenisaidia sana kudhibiti dalili za tatizo hilo. Pia, ninapotamani kujiumiza, mimi humwita rafiki anayejali. Sala imenisaidia sana. Na ninapohisi sistahili kusali, marafiki na wazee wa kutaniko husali pamoja nami. Ni pambano kali, lakini nimejifunza jinsi ya kushughulika nalo na kukubali msaada wowote unaoweza kupatikana ili nisijiumize.
N. W., Ujerumani
Katika ukurasa wa kwanza wa makala hiyo kuna picha ya msichana anayevuta nywele zake, na makala inamtaja “Sara,” aliyekuwa akivuta nywele zake ili kujiadhibu. Binti yangu ana tatizo linalojulikana kama trichotillomania, tatizo linalomfanya mtu avute nywele zake. Hali hiyo inahusishwa na tatizo la kushindwa kudhibiti mawazo na misukumo. Tatizo hilo hutokana na msukumo fulani wala si tamaa ya kujiumiza. Kuzivuta nywele hakumfanyi mtu aanze kujikata-kata.
M. H., Marekani
“Amkeni!” linajibu: Neno trichotillomania, ambalo lilianza kutumiwa mwishoni mwa karne ya 19, linarejelea tatizo la kitabia linaloambatana na tamaa isiyozuilika ya mtu kuvutavuta nywele zake. Kama picha yetu ilivyokuwa ikijaribu kuonyesha, watu fulani wamevuta nywele zao ili wajiumize. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba kila mtu aliye na tabia ya kuvuta nywele ana tatizo la kujiumiza lililozungumziwa katika makala yetu. Kama msomaji wetu alivyoonyesha hapo juu, wakati mwingine tabia hiyo inahusishwa na tazizo la kushindwa kudhibiti mawazo na misukumo.
Vyovyote vile, wataalamu wanaeleza kuwa jambo linalomfanya mtu avute nywele linapaswa kufikiriwa ili mgonjwa apewe matibabu yanayomfaa. Hivyo huenda ikafaa wote ambao wana tatizo hilo wapate ushauri wa wataalamu wa tiba ili wafanyiwe uchunguzi na kutibiwa.
Ungejibuje? (Januari 2006) Nimependezwa sana na sehemu hii mpya! Tunawafundisha wajukuu wetu , na huu utakuwa msaada mkubwa katika usomaji wao wa Biblia kila siku na makala za Amkeni! wanazosoma kama sehemu ya migawo yao ya shule. Asanteni sana kwa kuwajali vijana.
B. E., Marekani
Sehemu hii inachemsha ubongo, lakini ninapopata jibu ninafurahi! Jana jioni nilisoma ukurasa huo nao ulinipendeza sana! Nitakapokuwa mtu mzima, ningependa kusaidia kutayarisha gazeti hili ili wengine wajifunze kuhusu Yehova!
D. H., Marekani
Nina miaka minane. Familia yetu ilitumia sehemu hiyo kwenye funzo letu la familia. Tunafurahia utafiti ambao tunapaswa kufanya. Ile sehemu “Mimi Ni Nani?” ni ngumu, lakini tunapenda kuchemsha ubongo. Endeleeni kuchapisha makala hizo nzuri.
C. W., Marekani