Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 4
Muungano wa Umedi na Uajemi na Historia ya Biblia
Hii ni habari ya nne katika mfululizo wenye habari saba katika matoleo ya “Amkeni!” yenye kufuatana yanayozungumzia serikali saba kuu za ulimwengu zinazotajwa katika historia ya Biblia. Kusudi lake ni kuonyesha kwamba Biblia inategemeka na imeongozwa na roho ya Mungu na ujumbe wake unatoa tumaini kwamba mateso yanayosababishwa na utawala mkatili wa wanadamu yatakwisha.
MAGOFU ya majumba na makaburi ya wafalme yanatuonyesha kijuujuu tu utukufu, nguvu, na utajiri wa milki ya kale ya Muungano wa Umedi na Uajemi. Kabla ya falme hizo mbili kuungana, Umedi ndiyo iliyokuwa ufalme wenye nguvu zaidi. Lakini katika mwaka wa 550 K.W.K., Wamedi walianza kutawaliwa na Mfalme Koreshi wa Pili, ambaye baadaye alitawala Muungano wa Umedi na Uajemi. Milki hiyo ambayo kitovu chake kilikuwa katika eneo la kaskazini ya Ghuba ya Uajemi baadaye ilienea kutoka Bahari ya Aegea hadi Misri na kufikia kaskazini-magharibi mwa India kutia ndani Yudea.
Muungano wa Umedi na Uajemi ulitawala taifa la Kiyahudi kwa zaidi ya miaka 200—kuanzia kuanguka kwa Babiloni katika mwaka wa 539 K.W.K. hadi muungano huo wa Umedi na Uajemi uliposhindwa na Wagiriki katika mwaka wa 331 K.W.K. Vitabu kadhaa vya Biblia vinataja matukio muhimu yaliyotukia wakati huo.
Historia Inayotegemeka
Biblia inatuambia kwamba Mfalme Koreshi wa Pili aliwaachilia huru Wayahudi waliokuwa mateka huko Babiloni, akawaruhusu kurudi Yerusalemu na kujenga upya hekalu la Mungu ambalo Wababiloni waliharibu katika mwaka wa 607 K.W.K. (Ezra 1:1-7; 6:3-5) Simulizi hilo linaungwa mkono na maandishi yaliyoandikwa kwenye silinda ya udongo inayoitwa Cyrus Cylinder iliyopatikana kwenye magofu ya Babiloni la kale mwaka wa 1879. Maandishi hayo yanamtaja Koreshi kwa jina na kueleza sera yake ya kuwaruhusu mateka warudi nchini kwao pamoja na vyombo vyao vya kidini. Mwandikaji wa Biblia, Isaya, aliandika maneno ya Yehova ya kinabii kuhusu Koreshi: “‘Atatenda kikamilifu mapendezi yangu yote’; neno langu kuhusu Yerusalemu, ‘Atajengwa upya,’ na kuhusu hekalu, ‘Msingi wako utawekwa.’”—Isaya 44:28.
Hata Koreshi aliamuru kwamba pesa za kujenga upya hekalu ‘zitolewe kutoka katika nyumba ya mfalme,’ linasema andiko la Ezra 6:3, 4. Maneno hayo yenye kushangaza yanapatana na vitabu vya historia. “Lilikuwa jambo la kawaida kwa wafalme Waajemi kusaidia kujenga upya maeneo matakatifu katika milki yao,” kinasema kitabu Persia and the Bible.
Biblia inatuambia kwamba wapinzani wa Wayahudi baadaye walimwandikia barua Dario Mkuu (ambaye pia aliitwa Dario wa Kwanza) wakipinga madai ya Wayahudi kwamba Koreshi aliwaruhusu wajenge upya hekalu. Dario aliamuru hati hiyo ya awali itafutwe. Ni nini kilichopatikana? Kitabu cha kukunjwa kilichokuwa na amri ya Koreshi kilipatikana huko Ekibatana, uliokuwa mji mkuu. Dario aliwajibu wapinzani hao hivi: “Mimi, Dario, natoa agizo. [Hekalu lijengwe upya] mara moja.” Hivyo, upinzani dhidi ya ujenzi ukakoma.a—Ezra 6:2, 7, 12, 13.
Vitabu vya historia vinaunga mkono maelezo hayo. Kwanza, kwa sababu Koreshi aliishi huko Ekibatana wakati wa majira ya kiangazi, na huenda alitoa amri hiyo akiwa huko. Pili, vitu vilivyochimbuliwa vinaonyesha kwamba wafalme wa Muungano wa Umedi na Uajemi walipendezwa sana na mambo ya kidini ya milki yao na waliandika barua za kutatua mizozo.
Unabii Unaotegemeka
Katika ndoto iliyoongozwa kwa roho ya Mungu, nabii Danieli aliona wanyama wanne waliofuatana kutoka kwenye bahari, kila mnyama akiwalisha serikali kuu ya ulimwengu ambayo ingefuata. Mnyama wa kwanza, simba mwenye mabawa, aliwakilisha Babiloni. Wa pili ‘alikuwa kama dubu.’ Simulizi hilo linaendelea kusema: “Walikuwa wakimwambia hivi, ‘Simama, ule nyama nyingi.’” (Danieli 7:5) Dubu huyo mwenye kuogopesha alifananisha Muungano wa Umedi na Uajemi.
Kama Danieli alivyotabiri, milki ya Muungano wa Umedi na Uajemi ilikuwa na pupa ya ushindi. Muda mfupi baada ya maono ya Danieli, Koreshi alishinda Umedi, kisha akapigana na Lidia na Babiloni waliokuwa majirani wake. Mwana wake, Cambyses wa Pili alishinda Misri. Baadaye watawala wa Muungano wa Umedi na Uajemi walipanua milki hiyo zaidi.
Tuna uhakika gani kwamba ufafanuzi huo ni sahihi? Katika maono tofauti lakini yanayohusiana na hayo, Danieli aliona “kondoo-dume akisukuma kuelekea upande wa magharibi na wa kaskazini na wa kusini.” Unabii huo ulitimia wakati Muungano wa Umedi na Uajemi ‘uliposukuma’ mataifa mengine, kutia ndani taifa lenye nguvu la Babiloni. Malaika wa Mungu alifafanua maono hayo alipomwambia Danieli: “Yule kondoo-dume uliyemwona mwenye pembe mbili anawakilisha wafalme wa Umedi na Uajemi.”—Danieli 8:3, 4, 20.
Isitoshe, karne mbili hivi kabla ya kushindwa kwa Babiloni, nabii Isaya alitabiri jina la mfalme Mwajemi atakayelishinda—ambaye wakati huo alikuwa bado hajazaliwa—na mbinu ambayo angetumia kushinda Babiloni. Isaya aliandika hivi: “Yehova amemwambia hivi mtiwa-mafuta wake, Koreshi, ambaye mkono wake wa kuume nimeushika, ili kuyatiisha mataifa mbele yake, . . . nifungue mbele yake milango yenye pande mbili, hivi kwamba hata malango hayatafungwa.” (Isaya 45:1) Isaya na pia Yeremia walitabiri kwamba “mito,” au mifereji inayoingiza maji kutoka kwenye Mto Efrati, ambao ulikuwa handaki la maji lililotoa ulinzi, ingekaushwa. (Isaya 44:27; Yeremia 50:38) Wanahistoria Wagiriki, Herodotus na Xenophon, wanathibitisha kwamba unabii huo wa Biblia ni sahihi, kutia ndani unabii wa kwamba Wababiloni walikuwa na karamu usiku ule ambao Koreshi aliteka jiji hilo. (Isaya 21:5, 9; Danieli 5:1-4, 30) Baada ya kugeuza mkondo wa Mto Efrati, majeshi ya Koreshi yaliingia bila upinzani wowote kwenye jiji kupitia malango yaliyo kando ya mto huo yaliyokuwa yameachwa wazi. Babiloni lenye nguvu lilianguka katika usiku mmoja!
Tukio hilo lilifanya unabii mwingine utimie. Nabii Yeremia alikuwa ametabiri mapema kwamba watu wa Mungu wangekaa uhamishoni Babiloni kwa miaka 70. (Yeremia 25:11, 12; 29:10) Unabii huo ulitimia kwa wakati barabara, na wale waliokuwa uhamishoni waliruhusiwa kurudi katika nchi yao.
Tumaini Linalotegemeka
Muda mfupi baada ya Muungano wa Umedi na Uajemi kushinda Babiloni, Danieli aliandika unabii ambao unatusaidia kuelewa tukio muhimu sana katika kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu kwa wanadamu. Malaika Gabrieli alimwambia Danieli wakati hususa ambao Masihi—ule “uzao” ulioahidiwa kwenye Mwanzo 3:15—angekuja! Malaika wa Mungu alisema: “Tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62,” jumla ya majuma 69. (Danieli 9:25) Kipindi hicho kilichotabiriwa kilianza wakati gani?
Ingawa Koreshi aliwaruhusu Wayahudi warudi kwenye nchi yao baada tu ya Babiloni kuanguka, miaka mingi baadaye bado Yerusalemu na kuta zake hazikuwa zimerekebishwa. Katika mwaka wa 455 K.W.K., Mfalme Artashasta alimruhusu Nehemia, mnyweshaji wake Myahudi, arudi Yerusalemu na kuongoza kazi ya kulijenga upya. (Nehemia 2:1-6) Yale majuma 69 yalianza wakati huo.
Hata hivyo, majuma hayo 69 hayakuwa majuma halisi ya siku saba lakini yalikuwa majuma ya miaka. Kwa kweli, tafsiri fulani za Biblia zinasema “majuma ya miaka” badala ya kusema “majuma.”b (Danieli 9:24, 25) Masihi angekuja baada ya kipindi cha “majuma” 69, kila juma likiwa na urefu wa miaka 7—jumla ya miaka 483. Unabii huo ulitimizwa mwaka wa 29 W.K. Yesu alipobatizwa, miaka 483 ukihesabu kutoka mwaka wa 455 K.W.K.c
Kutimizwa kikamili kwa unabii wa Danieli kunathibitisha hata zaidi utambulisho wa Yesu. Uthibitisho huo pia unatupa uhakika kuhusu tumaini la wakati ujao. Yesu, akiwa Mfalme wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu, ataondoa utawala mkatili wa wanadamu. Kisha atatimiza unabii mwingine mwingi wa Biblia, kutia ndani unabii unaotabiri kufufuliwa kwa wafu ili waishi milele katika Paradiso duniani.—Danieli 12:2; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:3-5.
[Maelezo ya Chini]
a Wafalme watatu hivi wanaitwa kwa jina Dario.
b Biblia zifuatazo zinatumia usemi “majuma ya miaka”: Tanakh—A New Translation of the Holy Scriptures, The Complete Bible—An American Translation, na The Bible—Containing the Old and New Testaments, ya James Moffatt.
c Kwa habari zaidi kuhusu unabii huo, kutia ndani mchoro unaoonyesha kipindi cha majuma 69 ya miaka, ona ukurasa wa 197-199 katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
[Chati/Picha katika ukurasa wa 18]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
455 K.W.K. 29 W.K.
Kuanzia wakati amri ilitolewa ya kujenga upya Yerusalemu hadi kuja kwa Masihi, miaka 483 ilipita
[Picha katika ukurasa wa 16, 17]
Silinda inayoitwa Cyrus Cylinder inaeleza sera ya kuwarudisha mateka nchini kwao
[Picha katika ukurasa wa 17]
Bado kaburi la Koreshi linaweza kuonekana katika magofu ya mji wa kale wa Pasargadae, katika Iran ya leo
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 17]
Page 16, top, time line: Egyptian wall relief and bust of Nero: Photograph taken by courtesy of the British Museum; Persian wall relief: Musée du Louvre, Paris; bottom, Cyrus Cylinder: Photograph taken by courtesy of the British Museum; page 17, Cyrus’ tomb: © Richard Ashworth/age fotostock