Maoni ya Biblia
Je, Mungu Anaunga Mkono Vita Leo?
MFALME Daudi alisema hivi kuhusu jukumu lake akiwa shujaa wa vita: “[Mungu] anaifundisha mikono yangu kupigana vita, na mikono yangu imepinda upinde wa shaba.”—Zaburi 18:34.
Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo: “Ingawa tunatembea katika mwili, hatupigi vita kulingana na tulivyo katika mwili. Kwa maana silaha za vita vyetu si za kimwili.”—2 Wakorintho 10:3, 4.
Je, maandiko hayo mawili yanapingana? Au je, kulikuwa na sababu nzuri kwa nini Mungu aliwaruhusu Waisraeli wa kale waende vitani lakini akawakataza Wakristo kufanya hivyo? Je, maoni ya Mungu kuhusu vita yamebadilika? Tunapata majibu tunapochunguza tofauti tatu kubwa kati ya Israeli na kutaniko la Wakristo wa kweli.
Tofauti Tatu Kubwa
1. Israeli la kale lilikuwa taifa lenye mipaka iliyowekwa na Mungu, na lilizungukwa na majirani waliokuwa na uhasama. Kwa sababu hiyo, Mungu aliwaamuru watu wake wailinde nchi yao, na hata akawapa ushindi dhidi ya maadui wao. (Waamuzi 11:32, 33) Kwa upande mwingine, kutaniko la Kikristo halina mipaka halisi, na washiriki wake wanapatikana katika kila nchi. Kwa hiyo, ikiwa wafuasi wa Kristo katika nchi moja wangeshiriki katika vita dhidi ya nchi nyingine, wangekuwa wanapigana dhidi ya waamini wenzao—ndugu na dada zao wa kiroho—ambao wameaamuriwa wawapende na hata wafe kwa ajili yao.—Mathayo 5:44; Yohana 15:12, 13.
2. Israeli la kale lilikuwa na mfalme wa kibinadamu ambaye alitawala kutoka Yerusalemu. Hata hivyo, Wakristo wa kweli wanatawaliwa na Yesu Kristo, ambaye sasa ni kiumbe wa roho mwenye nguvu anayetawala kutoka mbinguni. (Danieli 7:13, 14) Yesu mwenyewe alisema hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Hivyo, hakuna ufalme au utawala wowote wa kisiasa hapa duniani unaoweza kudai kwamba unatokana na Kristo. Kwa nini hilo ni muhimu kwa “watumishi,” au wafuasi wa Yesu? Jambo la tatu linaeleza.
3. Kama mataifa mengine, taifa la Israeli la kale liliwatuma wawakilishi, ambao leo tunawaita mabalozi au wajumbe. (2 Wafalme 18:13-15; Luka 19:12-14) Kristo pia amewatuma mabalozi lakini mambo mawili yanawafanya wawe tofauti. Kwanza, wafuasi wake wote ni mabalozi au wajumbe. Kwa sababu hiyo, mtume Paulo angeweza kuandika hivi kwa niaba ya Wakristo wenzake: “Kwa hiyo sisi ni mabalozi walio badala ya Kristo.” (2 Wakorintho 5:20) Wakiwa mabalozi wenye amani, hawakubeba silaha. Pili, wafuasi wa Yesu wanawahubiria wote wanaotaka kusikiliza ujumbe wao. Yesu alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Alisema hivi pia: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—Mathayo 28:19, 20.
Kwa kusikitisha, watumishi wa Kristo hawakaribishwi kila wakati. Kwa sababu hiyo Paulo alimwandikia hivi Mkristo Timotheo aliyekuwa mweneza-injili: “Ukiwa askari-jeshi mwema wa Kristo Yesu shiriki sehemu yako katika kuvumilia uovu.” (2 Timotheo 2:3) Bila shaka silaha za vita za Timotheo zilikuwa za kiroho na zilitia ndani Neno la Mungu lililoandikwa, ambalo linaitwa “upanga wa roho.”—Waefeso 6:11-17.
Kwa Nini Mungu Aliliacha Taifa la Israeli na Kuanzisha Kutaniko la Kikristo?
Kwa miaka 1,500 hivi, taifa la Israeli lilikuwa na uhusiano wa pekee na Mungu, na msingi wake ulitegemezwa na agano, au makubaliano fulani. (Kutoka 19:5) Agano hilo ambalo lilipatanishwa na Musa, lilitia ndani zile Amri Kumi na sheria nyingine, ambazo zilihakikisha kwamba taifa hilo lilishikamana na ibada ya kweli na viwango vya juu vya maadili. (Kutoka 19:3, 7, 9; 20:1-17) Hata hivyo, inasikitisha kwamba Waisraeli wakiwa taifa walikosa kuwa waaminifu kwa Mungu na hata wakawaua baadhi ya manabii wake.—2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16; Luka 11:47, 48.
Mwishowe, Yehova alimtuma Mwana wake, Yesu Kristo, ambaye alizaliwa akiwa Myahudi. Badala ya kumpokea akiwa Masihi, taifa lote la Kiyahudi lilimkataa. Kwa sababu hiyo, Mungu alivunja agano lake la muda mrefu pamoja na Israeli, na ule ukuta wa mfano ambao uliwatenganisha Wayahudi na watu wasio Wayahudi ukaondolewa.a (Waefeso 2:13-18; Wakolosai 2:14) Karibu na wakati huo, Mungu alianzisha kutaniko la Kikristo, na akamweka rasmi Yesu awe Kichwa cha kutaniko hilo. Isitoshe, kabla ya mwisho wa karne ya kwanza, kutaniko hilo lilifanyizwa na watu kutoka mataifa mbalimbali. “Katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa [Mungu] na kutenda uadilifu anakubalika kwake,” akasema Petro, mtume Myahudi.—Matendo 10:35.
Mashahidi wa Yehova hufuata kielelezo cha Wakristo wa mapema. Kwa hiyo, Mashahidi wanajulikana kwa kazi yao ya kuhubiri hadharani, na msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote wa kisiasa au wa vita. (Mathayo 26:52; Matendo 5:42) Naam, hawaruhusu kitu chochote kiwakengeushe kutoka kwa kazi yao ya kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu, ambayo ndiyo serikali pekee itakayoondoa kabisa uovu na kuleta amani ya kudumu duniani. Akiwa na tumaini hilo zuri akilini, mtume Paulo aliandika hivi: “Kama walio badala ya Kristo tunaomba: ‘Mpatanishwe pamoja na Mungu.’” (2 Wakorintho 5:20) Maneno hayo yana umaana mkubwa sana leo kwa kuwa tunakaribia mwisho wa “siku za mwisho” za ulimwengu huu mwovu.—2 Timotheo 3:1-5.
[Maelezo ya Chini]
a Mwanzoni jina “Myahudi” lilitumiwa kurejelea watu waliokuwa wa kabila la Yuda la Israeli. Baadaye, jina hilo lilirejelea Waebrania wote.—Ezra 4:12.
JE, UMEJIULIZA HIVI?
● Ni sifa gani muhimu ambayo Wakristo wanapaswa kuonyeshana?—Yohana 13:34, 35.
● “Silaha” kuu ya Mkristo wa kweli ni nini?—Waefeso 6:17.
● Wawakilishi wa Kristo hutangaza ujumbe gani muhimu?—Mathayo 24:14; 2 Wakorintho 5:20.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mashahidi wa Yehova ni undugu wa mataifa mbalimbali na hawaungi mkono upande wowote wa vita