Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 11/12 kur. 12-15
  • Biblia—Kitabu cha Unabii Sahihi Sehemu ya 7

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Biblia—Kitabu cha Unabii Sahihi Sehemu ya 7
  • Amkeni!—2012
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwisho wa Uovu
  • Unabii wa Biblia Unategemeka
  • Babiloni Mkubwa Ni Nani?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Ufalme Umesimamishwa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Kumtambulisha “Babiloni Mkubwa”
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Unabii Mwingi Uliotimizwa
    Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2012
g 11/12 kur. 12-15

Biblia​—Kitabu cha Unabii Sahihi Sehemu ya 7

“Ule Mwisho Utakuja”

Katika mfululizo huu wa makala nane, gazeti la “Amkeni!” litazungumzia jambo la pekee kuhusu Biblia—unabii wake, au utabiri. Makala hizi zitakusaidia kujibu maswali haya: Je, unabii wa Biblia ulibuniwa na wanadamu werevu? Au kuna mambo yanayoonyesha kwamba uliongozwa na roho ya Mungu? Tunakukaribisha uchunguze uthibitisho.

JE, hukasirika unapoona serikali zenye ufisadi zikiwakandamiza na kuwapunja raia wake? Je, unaudhika unapoona ukosefu wa haki wakati biashara kubwa zinapozidi kuwatajirisha matajiri huku maskini wakizidi kukandamizwa? Je, unakasirika unapoona viongozi wa kidini wakiwatapeli waumini wao au kuwafundisha uwongo mtupu? Ikiwa unahisi hivyo, huenda ukapendezwa kujua kwamba Biblia pia inashutumu maovu hayo. Makala hii itazungumzia (1) unabii wa Biblia unaotabiri mwisho wa uovu na watu waovu na (2) kwa nini tunapaswa kuamini kabisa unabii huo.

Mwisho wa Uovu

[Picha katika ukurasa wa 12]

Makala iliyopita ya mfululizo huu, ilizungumzia ile ishara yenye mambo mengi ambayo Yesu alitoa kuonyesha kwamba mwisho wa ulimwengu huu uko karibu. Ishara hiyo inatia ndani kutangazwa ulimwenguni pote kwa habari njema ya Ufalme wa Mungu, yaani, serikali ya Mungu ambayo hivi karibuni itatawala dunia yote. (Danieli 2:44; Mathayo 24:3, 14) Yesu alisema kwamba kazi hiyo itakapomalizika, ‘ule mwisho utakuja.’ Huenda ukashangaa kujifunza kwamba kitu cha kwanza ambacho Mungu ataondoa ni dini ya uwongo ambayo haiwafundishi watu ukweli kumhusu. Katika Biblia, dini ya uwongo inafananishwa na kahaba anayeitwa “Babiloni Mkubwa.”​—Ufunuo 17:1, 5

Unabii wa 1:

“Mapigo yake [Babiloni Mkubwa] yatakuja, kifo na kuomboleza na njaa, naye atateketezwa kabisa kwa moto, kwa sababu Yehova Mungu, aliyemhukumu, ni mwenye nguvu.”​—Ufunuo 18:2, 8.

Utimizo: Biblia inafunua kwamba kwa wakati wake uliowekwa, Mungu atafanya serikali za ulimwengu zimshambulie Babiloni Mkubwa na kumwangamiza. Zitamfanya “kuwa ukiwa na uchi” na zitakula “sehemu zake zenye nyama.” (Ufunuo 17:16) Hilo linamaanisha kwamba zitafunua mwenendo wake wa aibu na kupora utajiri wake mwingi. Uharibifu wake utafanyika haraka na utakuwa kamili hivi kwamba hakuna sehemu yoyote yake itakayobaki.​—Ufunuo 18:21.

Watawala wa serikali hizo watadhani kwamba wao ndio waliotunga wazo hilo. Hata hivyo, kutimizwa kwa unabii huo wenye kustaajabisha kutathibitisha kwamba uharibifu wa Babiloni ulisababishwa na Mungu. Yeye ndiye ‘atalitia hilo ndani ya mioyo yao ili kutekeleza wazo lake.’​—Ufunuo 17:17.

Unabii wa 2:

“Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme. . . . Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [za wanadamu], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”​—Danieli 2:44.

Utimizo: Baada ya kuondoa dini ya uwongo, Mungu atageuza fikira zake kwa mashirika mengine​—ya kisiasa na ya kibiashara—​na pia watu waovu. (Methali 2:22; Ufunuo 19:17, 18) Kama vile mwenye nyumba anavyowafukuza wapangaji waharibifu, Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ Atawaharibu wale ambao wameijaza dunia jeuri na matendo mapotovu ya kingono.​—Ufunuo 11:18; Waroma 1:18, 26-29.

Ni nani watakaookoka? Biblia inajibu: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”​—Zaburi 37:11; 72:7.

Je, tunaweza kuamini unabii wa Biblia? Je, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu ataondoa uovu na kuteseka na kuwakomboa waadilifu? Ndiyo!

Unabii wa Biblia Unategemeka

[Picha katika ukurasa wa 14]

Ufalme wa Mungu utakomesha dini zote za uwongo, serikali zenye ufisadi, na biashara zenye pupa

Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Yehova Mungu ndiye Mtungaji wa Biblia na kwamba atatimiza kila ahadi ambayo ametoa. (2 Timotheo 3:16) Je, inapatana na akili kuamini hivyo?

Ikiwa mtu fulani amekuwa rafiki yako kwa muda mrefu na anakupenda sana na hajawahi kukudanganya, je, utamwamini akiahidi atakutendea jambo fulani jema na unajua kwamba ana uwezo wa kutimiza alichoahidi? Bila shaka utamwamini. Mungu ni bora kuliko rafiki yeyote wa kibinadamu tunayeweza kuwa naye. “Mungu . . . hasemi uongo.”​—Tito 1:2, Biblia Habari Njema.

Mungu hataki tuamini tu mambo bila kuwa na msingi wowote. Kwa sababu hiyo, alitumia roho yake kuwaongoza waandikaji wa Biblia waandike unabii mwingi ambao ni yeye tu akiwa Mweza-Yote anayeweza kuutimiza. Baadhi ya unabii huo na jinsi ulivyotimizwa kwa njia yenye kushangaza ulizungumziwa katika sehemu sita za kwanza za mfululizo wa makala hizi. Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atatimiza unabii unaohusu wakati wetu ujao, kutia ndani unabii uliotajwa katika makala hii.

Kwa kweli, Muumba atakomesha dini ya uwongo, utawala wenye kukandamiza, na biashara zenye pupa za ulimwengu huu. Ungependa kujifunza mengi kuhusu yale yatakayofuata baada ya mambo hayo kutukia? Toleo lifuatalo la Amkeni! litakusaidia. Litakuwa na makala ya mwisho ya mfululizo huu.

KUMTAMBULISHA BABILONI MKUBWA

Tunajuaje kwamba mwanamke wa mfano anayeitwa Babiloni Mkubwa katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo anafananisha dini zote za uwongo? Fikiria uthibitisho ufuatao:

  • Hawezi kuwa mwanamke halisi kwa sababu kitabu cha Ufunuo kinataja mambo kwa njia ya “ishara,” au mifano.​—Ufunuo 1:1.

  • Babiloni Mkubwa anaketi juu ya maji, ambayo yanawakilisha “vikundi vya watu na umati na mataifa.” (Ufunuo 17:1, 5, 15) Mwanamke halisi hawezi kufanya hivyo. Hata hivyo, dini ya uwongo inategemezwa na wafuasi wake wengi.

  • Mwanamke huyo wa mfano ni “jiji kubwa lililo na ufalme juu ya wafalme wa dunia.” Yaani, yeye ni shirika lenye uvutano ulimwenguni pote.​—Ufunuo 17:18.

  • Kahaba huyo wa kiroho, Babiloni Mkubwa, anafanya mapatano na “wafalme wa dunia.” Isitoshe, wafalme hao wanaomboleza kuharibiwa kwake. (Ufunuo 17:1, 2; 18:9) Kwa hiyo, hawezi kuwa tengenezo la kisiasa.

  • Wanabiashara pia wanaomboleza kuharibiwa kwake. (Ufunuo 18:15) Kwa hiyo, hawezi kuwa milki ya kibiashara.

  • Biblia inaeleza kwamba kuchanganya ibada ya Mungu na kuupenda ulimwengu ni uzinzi wa kiroho. (Yakobo 4:4) Ufafanuzi huo unamfaa Babiloni Mkubwa. Pia anaendeleza mazoea ya kuwasiliana na pepo, ambayo ni mazoea ya kidini.​—Ufunuo 18:23.

  • Jiji la kale la Babiloni, ambalo Babiloni Mkubwa ameitwa, lilikuwa jiji lenye dini nyingi sana.​—Isaya 47:1, 12, 13; Yeremia 50:1, 2, 38.

Kwa hiyo, tunaweza kusema kwa uhakika kwamba Babiloni Mkubwa anawakilisha dini zote za uwongo ulimwenguni.

UNABII ULIOTIMIZWA

Ifuatayo ni orodha ya unabii wa Biblia uliozungumziwa katika sehemu sita za kwanza za mfululizo huu. Kama makala hizo zilivyoonyesha, unabii huo umethibitika kuwa sahihi!

UNABII KUHUSU ABRAHAMU NA WAZAO WAKE

  • Wazao wa mwanamume mwaminifu Abrahamu wangekuwa taifa kubwa, ambalo lilikuja kuitwa taifa la Israeli.​—Mwanzo 12:1, 2.

  • Wazao wa Abrahamu wangerudi katika nchi ya Kanaani baada ya kuishi katika nchi ya kigeni kwa vizazi vinne.​—Mwanzo 15:13, 16.

  • Wazao wa Abrahamu wangeimiliki “nchi yote ya Kanaani.”​—Mwanzo 17:8.

  • Kwa sababu Waisraeli walimwasi Mungu, angeruhusu washindwe na kuchukuliwa mateka.​—Yeremia 25:8-11.

  • Mungu angewarudisha Wayahudi nchi ya nyumbani kwao baada ya kuwa utekwani kwa miaka 70.​—Yeremia 25:12; 29:10.

  • Serikali kubwa ya ulimwengu ya Babiloni ingepinduliwa, na baada ya muda Babiloni lingekuwa magofu.​—Isaya 13:19, 20.

UNABII KUMHUSU MASIHI NA WAFUASI WAKE

  • Masihi, au Kristo angetokea kutoka kwa uzao wa Mfalme Daudi.​—Isaya 9:7.

  • Masihi huyo angezaliwa Bethlehemu.​—Mika 5:2.

  • Masihi angetokea miaka 483 baada ya “kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu.” Amri hiyo ilitolewa katika mwaka wa 455 K.W.K.​—Danieli 9:25.

  • Kabla ya kuuawa, Masihi angepigwa mijeledi.​—Isaya 50:6.

  • Masihi angeuawa kama mhalifu aliyedharauliwa, hata hivyo, angezikwa pamoja na “jamii ya matajiri.”​—Isaya 53:9.

  • Wafuasi wa Kristo wangeeneza ujumbe wake kotekote katika Yudea, Samaria, na katika sehemu nyingine za ulimwengu wa wakati huo.​—Matendo 1:8.

  • Wakristo wangeteswa.​—Marko 13:9.

  • Watu wadanganyifu na wenye kukandamiza wangetokea katika kutaniko la Kikristo, na kufanya wengi wawe waasi-imani.​—Matendo 20:29, 30; 2 Petro 2:1, 2.

UNABII KUHUSU SIKU ZA MWISHO

Katika siku za mwisho kutakuwa na

  • Kuhubiriwa kwa “habari njema ya Ufalme [wa Mungu]” ulimwenguni pote.​—Mathayo 24:14.

  • Vita ulimwenguni pote.​—Mathayo 24:7; Ufunuo 6:4.

  • Upungufu wa chakula.​—Mathayo 24:7.

  • Matetemeko makubwa ya nchi.​—Luka 21:11.

  • Magonjwa mabaya.​—Luka 21:11.

  • Chuki na jeuri.​—Mathayo 24:10, 12.

  • Watu wenye pupa na ubinafsi, na wanaopenda pesa.​—2 Timotheo 3:1-5

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki