Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 12/12 kur. 16-18
  • Ni Nini Humfanya Mtu Kuwa Mwanamume Halisi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nini Humfanya Mtu Kuwa Mwanamume Halisi?
  • Amkeni!—2012
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Acha Kuendelea Kwako Kuwe Dhahiri’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Akina Baba Wanawezaje Kuwa na Uhusiano wa Karibu na Wana Wao?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Je, Sisi Ni Marafiki Tu—Au Ninavutiwa Naye Kimahaba?, Sehemu ya 2
    Amkeni!—2012
  • Je, Ananifaa?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2012
g 12/12 kur. 16-18

Vijana Huuliza

Ni Nini Humfanya Mtu Kuwa Mwanamume Halisi?

“Baba yangu alikufa nilipokuwa na umri wa miaka mitatu. Nyakati nyingine mimi huwaonea wivu wavulana ambao wamelelewa na baba zao. Wao huonekana wakiwa na sifa ya kujiamini kuliko mimi.”​—Alex.a

“Uhusiano kati yangu na baba yangu si mzuri. Kwa hiyo nimelazimika kujifunza mimi mwenyewe jinsi ya kuwa mwanamume halisi.”​—Jonathan.

[Picha katika ukurasa wa 17]

JE, UMEWAHI kuhisi kama vijana hao ambao wamenukuliwa hapo juu? Je, una wasiwasi kwamba hutajua jinsi ya kuwa mwanamume halisi? Ikiwa ndivyo, usikate tamaa!

Fikiria jinsi unavyoweza kushinda vikwazo viwili ambavyo hutokea mara kwa mara.

KIKWAZO CHA 1: Maoni yasiyofaa kuhusu sifa za mwanamume halisi

Mambo ambayo wengine husema:

  • Wanaume halisi ni sugu; hawapaswi kulia.

  • Wanaume halisi hawakubali yeyote awaongoze.

  • Wanaume ni bora kuliko wanawake.

Maoni yanayofaa: Kuna tofauti kubwa kati ya mwanamume halisi na mvulana. Lakini hilo halimaanishi kwamba mwanamume ni bora kuliko mwanamke. Unakuwa mwanamume halisi unapoacha tabia za kitoto. Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa nikisema kama mtoto, nikifikiri kama mtoto, nikiwaza kama mtoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za mtoto.” (1 Wakorintho 13:11) Kwa maneno mengine, kadiri unavyoacha kufikiri, kuzungumza, na kutenda kama mtoto na kuanza kufikiri, kuzungumza, na kutenda kama mtu mkomavu ndivyo unavyozidi kuthibitisha kwamba wewe ni mwanamume halisi.b

Jaribu kufanya hivi: Chukua karatasi na uandike majibu ya maswali yafuatayo:

  1. Ni katika njia gani tayari mimi nimefanya maendeleo katika kuondolea mbali “tabia za mtoto”?

  2. Ni mambo gani ninayoweza kufanyia maendeleo zaidi?

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa: Luka 7:36-50. Ona jinsi ambavyo Yesu alijithibitisha kuwa mwanamume halisi kwa (1) kutetea mambo ya kweli na (2) kuwatendea wengine​—kutia ndani wanawake—​kwa heshima.

“Ninavutiwa na sifa za rafiki yangu, Ken. Yeye ni mwanamume imara​—kimwili, kihisia, na kiroho—​lakini pia ni mtu mwenye fadhili. Mfano wake umenifundisha kwamba mwanamume halisi hawavunjii wengine heshima ili tu yeye aonekane kuwa bora zaidi.”​—Jonathan.

KIKWAZO CHA 2: Kulelewa bila baba

Mambo ambayo wengine husema:

  • Ikiwa hukulelewa na baba, hutawahi kamwe kujifunza jinsi ya kuwa mwanamume halisi.

  • Ikiwa baba yako alikuwa mtu mwenye sifa mbaya, lazima wewe pia utakuwa hivyo.

Maoni yanayofaa: Hata ikiwa hukuwa na baba au hakukuwekea mfano mzuri, hilo halimaanishi huwezi kuwa mwanamume halisi! Unaweza kushinda vikwazo hivyo. (2 Wakorintho 10:4) Unaweza kuchagua kufuata ushauri ambao Mfalme Daudi alimpa mwanaye Sulemani: “Uwe na nguvu na ujionyeshe kuwa mwanamume.”​—1 Wafalme 2:2.

Kusema kweli, inaweza kuwa vigumu kuishi na baba ambaye hakujali​—au hata bila baba kabisa. “Mtu anapolelewa bila baba anakuwa na pengo kubwa maishani,” anasema Alex, aliyenukuliwa kwenye utangulizi wa makala hii. “Nina umri wa miaka 25, lakini ninahisi kana kwamba sasa ninajifunza mambo ambayo nilipaswa kujifunza nilipokuwa bado mvulana mdogo.” Ikiwa wewe pia unahisi kama Alex, unaweza kufanya nini?

Jaribu kufanya hivi: Tafuta mtu ambaye atakuwa mshauri wako—mtu aliye na sifa za mwanamume halisi.c Muulize ni sifa gani ambazo anaona mwanamume halisi anapaswa kuwa nazo. Kisha muulize jinsi wewe unavyoweza kuiga sifa hizo pia.​—Methali 1:5.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa: Methali sura ya 1-9. Jaribu kutambua ushauri unaoweza kusaidia mvulana akue na kuwa mwanamume wa kiroho na mwenye hekima.

“Ninafurahi kwamba nimeanza kuwa mwanamume halisi. Ingawa natamani baba yangu angenisaidia kufanya maendeleo, bado nina uhakika kuwa nitafaulu kusitawisha sifa ninazohitaji. Si lazima nishindwe.”​—Jonathan.

Baada toleo la Amkeni! la Desemba 2012, makala za “Vijana Huuliza” zitapatikana tu katika Tovuti

a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

b Ona sanduku lenye kichwa “Tofauti Kati ya Mwanamume Halisi na Mvulana.”

c Wazee katika kutaniko la Kikristo wanaweza kuwa washauri wazuri.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Ian​—Kuwa mwanamume hakumaanishi kwamba unapaswa tu kujiendesha kwa njia ya kiume bali pia kunamaanisha unapaswa kuwa na bidii, udhibiti hisia zako, na ukubali kuwajibika kwa sababu ya matendo yako.

TOFAUTI KATI YA MWANAMUME HALISI NA MVULANA

Huenda mvulana akawa . . .

  • mkaidi.

  • mbinafsi.

  • anayefikiria kujifurahisha tu.

  • anaongozwa na hisia zake.

Mwanamume halisi hujitahidi . . .

  • kuwa mwenye heshima.​—Waroma 12:10.

  • kujitolea kuwasaidia wengine.—1 Wakorintho 10:24.

  • kuwa mwenye kutegemeka.—Wagalatia 6:5.

  • kudhibiti hisia zake.​—Methali 16:32.

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Unafikiri ni sifa gani zinazomtambulisha mwanamume halisi? Kwa sasa nimekomaa kwa kadiri gani?

TAARIFA KWA WAZAZI

AKINA BABA​—

Kwa kiwango kikubwa, kijana wako ataiga mfano wako akijiambia kwamba kufanya hivyo kutamsaidia kuwa mwanamume halisi. Ikiwa unamtendea mke wako kwa heshima, utakuwa unamfundisha mwana wako kuwatendea wanawake kwa heshima. Ikiwa unafanya kazi kwa bidii kuandalia familia yako​—hata ikiwa kufanya hivyo kunamaanisha kufanya kazi za hali ya chini au zenye kuchosha—​unamfundisha mwana wako kufanya kazi kwa bidii na kuwa mwenye kutegemeka.​—1 Timotheo 5:8.

Huenda uhusiano wako na baba yako haukuwa mzuri. Huenda pia baba yako hakuwa na uhusiano mzuri na baba yake. Lakini kumbuka: Una nafasi ya kuzuia hali hiyo isijirudie tena. Usipoteze fursa hiyo! Chagua kuwa na uhusiano wa karibu na mwana wako.d Uwe mfano mzuri kwa kijana wako ili aweze kukua na kuwa mwanamume halisi—mtu ambaye atakufanya ujivunie kuwa baba yake.​—Methali 23:24.

AKINA MAMA​—

Mnawezaje kuwasaidia wana wenu waje kuwa wanaume halisi? Epuka kumlinganisha na mume wako kwa njia isiyofaa. Kwa mfano, labda mwana wako anafanya kosa linalokukumbusha kuhusu tabia ya mume wako. Huenda ukaropoka: “Acha! Wewe ni kama baba yako!” Ni kweli kwamba una haki ya kumshauri mwana wako anapofanya makosa. Lakini kumbuka: Ikiwa maneno au matendo yako yanaonyesha kwamba kila jambo ambalo mume wako anafanya ni kosa, bila kujua utakuwa unazuia kijana wako kukua na kuwa mtu mzima, yaani, mwanamume halisi.

Muunge mkono mume wako anapojitahidi kumsaidia kijana wenu. Watie moyo watumie wakati pamoja, na tafuta fursa za kutaja sifa nzuri za mume wako na mambo mazuri anayofanya. Je, mume wako hufanya kazi kwa bidii ili kuandalia familia? Je, yeye huwa na wakati wa kuwa pamoja na watoto? Je, yeye huwatendea wengine kwa heshima? Acha mwana wako ajue jinsi unavyothamini mambo hayo. Maneno yako yatamsaidia mwana wako kujifunza kutokana na mfano mzuri wa baba yake.

d Kwa habari zaidi, ona makala yenye kichwa “Akina Baba Wanawezaje Kuwa na Uhusiano wa Karibu na Wana Wao?” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 2011, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki