Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 8/1 kur. 8-12
  • ‘Acha Kuendelea Kwako Kuwe Dhahiri’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Acha Kuendelea Kwako Kuwe Dhahiri’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wakati wa Kujichunguza
  • “Vitabia vya Kitoto”
  • Jinsi Ambavyo Kuendelea Kwawa Dhahiri
  • Kukazania Ukomavu wa Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • ‘Dhihirisha Kuendelea Kwako’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Je, Wewe Ni Mkristo “Aliyekua Kabisa”?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Dhihirisha Maendeleo Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 8/1 kur. 8-12

‘Acha Kuendelea Kwako Kuwe Dhahiri’

“Sasa maadam mimi ni mtu mzima, mambo ya [vitabia vya, NW] kitoto nimeyaacha.”—1 WAKORINTHO 13:11, HNWW.

1. Ukuzi ni ushuhuda wa ajabu ya uumbaji kwa jinsi gani?

KUTOKA kwa yai dogo sana hivi kwamba laweza kuonwa tu chini ya hadubini (mikroskopu), nyangumi aweza kukua akawa kiumbe mwenye urefu wa mita zaidi ya 30 na kuwa na mwenye uzito wa tani zaidi ya 80. Vivyo hivyo, kutoka kwa mojawapo ya mbegu ndogo zaidi, ule mti mrefu sana uitwao Sekuoia waweza kukua ukawa na urefu wa juu wa mita zaidi ya 90. Kwa kweli, ukuzi ni mojawapo ya maajabu ya uhai. Kama mtume Paulo alivyosema, sisi twaweza kupanda na kutia maji, bali ni “Mungu akuzaye.”—1 Wakorintho 3:7.

2. Ni aina gani ya ukuzi iliyotabiriwa katika Biblia?

2 Hata hivyo, kuna aina nyingine ya ukuzi inayostaajabisha jinsi hiyo hiyo. Ni ile iliyotabiriwa na nabii Isaya: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; Mimi BWANA [Yehova, New World Translation], nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isaya 60:22) Unabii huo wahusu ukuzi wa watu wa Mungu, nao unatimizwa kwa ukubwa katika siku yetu.

3. Ripoti ya mwaka wa utumishi ya 1991 ilionyeshaje kwamba Yehova anaihimiza kazi ya watu wake?

3 Ripoti ya mwaka wa utumishi wa 1991 ya utendaji wa ulimwenguni pote wa Mashahidi wa Yehova huonyesha kwamba idadi ya wahubiri wa Ufalme ulifika kilele kipya cha 4,278,820, na jumla ya watu 300,945 wakabatizwa katika mwaka huo. Kukiwa na mwingio wa watu wengi wapya jinsi hiyo, makundi 3,191 mapya yalifanyizwa, pamoja na idadi inayopatana na hiyo ya mizunguko na wilaya. Hiyo ni zaidi ya makundi nane mapya kwa siku, karibu mzunguko mmoja mpya kila siku mbili. Huo ni ukuzi wa ajabu kama nini! Kwa wazi, Yehova anahimiza mambo, na baraka yake iko juu ya jitihada za watu wake.—Zaburi 127:1.

Wakati wa Kujichunguza

4. Ni lazima maswali gani yafikiriwe tutazamapo kwenye wakati ujao?

4 Ingawa inachangamsha moyo, baraka hiyo huleta madaraka fulani pia. Je! kutakuwako watu mmoja mmoja wa kutosha walio wakomavu na wenye nia watakaotunza mahitaji ya kiroho ya hao wapya wote? Tutazamapo mbele kwenye wakati ujao, inaduwaza kufikiria idadi ya mapainia, watumishi wa huduma, wazee, na waangalizi wasafirio watakaohitajiwa kuutunza ukuzi na upanuzi, pamoja na idadi ya wafanyakazi wa hiari watakaohitajiwa katika ofisi za tawi na Makao ya Betheli kotekote ulimwenguni kuitegemeza kazi hiyo. Watu hao wengi watatoka wapi? Hakuna shaka kwamba mavuno ni mengi. Lakini ni nani leo walio na uwezo wa kuwatunza wale wafanyakazi wote wanaohitajiwa ili kuvuna mavuno hayo?—Mathayo 9:37, 38.

5. Kuna hali zipi katika maeneo fulani kwa sababu ya ukuzi wa haraka?

5 Kwa mfano, imeripotiwa kwamba katika sehemu nyinginezo za ulimwengu, kuna makundi yenye wahubiri wa Ufalme wafikao mia moja wanaotumikiwa na mzee mmoja tu pamoja na watumishi wa huduma mmoja au wawili. Nyakati nyingine mzee mmoja anahitaji kutumikia makundi mawili. Kwingineko uhitaji wa wahudumu Wakristo wanaostahili kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani ni mkubwa sana hivi kwamba walio wapya wanahitaji kuandikwa kwenye orodha ya wale wanaomnjogea mtu awafunze. Katika maeno mengine bado, makundi mapya yanafanyizwa kwa mwendo wa kasi sana hivi kwamba makundi matatu, manne, au hata matano yanahitaji kushiriki Jumba la Ufalme moja. Labda umeona ukuzi kama huo katika eneo lenu wenyewe.

6. Ni kwa nini kujichunguza wenyewe ni kwa wakati ufaao kwa upande wetu?

6 Yaliyotangulia yanatuambia nini? Kwamba kulingana na nyakati, sisi sote twahitaji kuzichunguza hali zetu tuone ikiwa tunatumia wakati na mali zetu vizuri tuwezavyo ili kuuitikia uhitaji huo. (Waefeso 5:15-17) Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo Waebrania wa karne ya kwanza: “Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi mmekuwa mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu.” (Waebrania 5:12) Kama vile maneno hayo yanavyoonyesha, Wakristo mmoja mmoja wanahitaji pia kukua. Na kuna hatari halisi kwamba mtu aweza kusitasita katika utoto wa kiroho badala ya kufanya maendeleo ya kufikia ukomavu wa Kikristo. Kwa kupatana na hilo, Paulo atusihi hivi: “Jijaribuni wenyewe kwamba mmekuwa katika imani; jithibitisheni wenyewe.” (2 Wakorintho 13:5) Je! wewe umejichunguza mwenyewe uone ikiwa umekuwa ukikua kiroho tangu wakati wa ubatizo wako? Au, umekuwa ukisimama mahali pamoja? Lakini, mtu aweza kujuaje?

“Vitabia vya Kitoto”

7. Ili kuendelea kiroho kuwe dhahiri, ni lazima tufanye nini?

7 “Nilipokuwa mtoto mchanga nilisema kitoto, nilifahamu kitoto, nilifikiri kitoto. Lakini sasa, maadam mimi ni mtu mzima, mambo ya [vitabia vya, NW] kitoto nimeyaacha,” akasema mtume Paulo. (1 Wakorintho 13:11, HNWW) Katika ukuzi wa kiroho, wakati mmoja sisi sote tulikuwa kama watoto katika kufikiri na vitendo vyetu. Hata hivyo, ili kuendelea kuwe dhahiri, ni lazima tuiondolee mbali “vitabia vya kitoto,” kama alivyosema Paulo. Ni gani baadhi ya vitabia hivyo?

8. Kulingana na maneno ya Paulo kwenye Waebrania 5:13, 14, ni nini kitabia kimoja cha mtoto mchanga wa kiroho?

8 Kwanza, ona maneno ya Paulo kwenye Waebrania 5:13, 14: “Kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” Je! ‘unajua sana neno la haki’? Je! unalijua Neno la Mungu, Biblia, vya kutosha kuweza kulitumia “kupambanua mema na mabaya”? Paulo alisema kwamba watu wakomavu wanaweza kufanya hivyo kwa sababu wao hutwaa ndani “chakula kigumu” kwa ukawaida. Hivyo, tamaa au hamu ya mtu ya kupata chakula cha kiroho ni wonyesho mzuri wa kama mtu huyo amekua kiroho au angali mtoto mchanga wa kiroho.

9. Hamu ya mtu ya kiroho ni wonyesho wa maendeleo ya kiroho kwa jinsi gani?

9 Kwa hiyo, hamu yako ya kiroho ikoje? Wewe huonaje ule ugavi mwingi wa chakula cha kiroho unaoandaliwa na Yehova kwa ukawaida kupitia vichapo vyenye msingi wa Biblia na mikutano na makusanyiko ya Kikristo? (Isaya 65:13) Bila shaka unashangilia sana ikiwa vichapo vipya vinatolewa kwenye mikusanyiko ya wilaya ya kila mwaka. Lakini wewe hufanya nini navyo unapofika nyumbani? Wewe hufanya nini wakati toleo jipya la gazeti Mnara wa Mlinzi au Amkeni! linapowasili? Je! wewe huchukua wakati wa kuvisoma vichapo hivyo, au wewe huvipitia tu ili kuyaona mambo makuu na kisha kuviongezea vingine kwenye kabati yako ya kuwekea vitabu? Maswali kama hayo yangeweza kuulizwa kuhusu mikutano ya Kikristo. Je! wewe huhudhuria mikutano yote kwa ukawaida? Je! wewe hujitayarisha kwa ajili yao pamoja na kushikiri ndani yamo? Yaonekana wengine wametumbukia katika mazoea malegevu ya kujilisha kiroho, kana kwamba, kusoma kijuujuu tu na kula kwa haraka. Ilikuwa tofauti jinsi gani na mtunga zaburi, aliyesema hivi: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.” Zaidi ya hayo, Mfalme Daudi alisema hivi: “Nitakushukuru katika kusanyiko kubwa; nitakusifu kati ya watu wengi.” (Zaburi 35:18; 119:97) Kwa wazi, kadiri tunavyothamini maandalizi ya kiroho ni wonyesho wa maendeleo yetu ya kiroho.

10. Ni kitabia gani cha mtoto mchanga wa kiroho kinachoonyeshwa kwenye Waefeso 4:14?

10 Paulo alionyesha kitabia kingine cha mtoto mchanga wa kiroho alipoonya hivi: “Tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu.” (Waefeso 4:14) Kama vile wazazi wajuavyo vema, watoto ni wadadisi kuhusu kila jambo. Kwa njia fulani hicho ni kitabia chanya kwa sababu kinawawezesha wachunguze na kujifunza na polepole kukua wakawa watu wakomavu. Hata hivyo, hatari huwa katika kule kukengeushwa kwao fikira kwa urahisi na jambo moja baada ya jingine. Lililo baya zaidi, kwa sababu ya kutokuwa na ujuzi, udadisi huo mara nyingi huwaongoza katika matatizo mazito, hata wakijihatarisha wenyewe na wengine. Hali ni hivyo pia kwa watoto wachanga wa kiroho.

11. (a) Paulo alimaanisha nini kwa kutumia maneno “kila upepo wa elimu”? (b) Tunakabiliana na ‘pepo’ zipi leo?

11 Lakini, Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba watoto wachanga wa kiroho walitupwa huku na huku, “na kila upepo wa elimu”? Hapa, “upepo” linatafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki aʹne·mos, ambalo International Critical Commentary huonelea kwamba laonekana “limechaguliwa kufaa lile wazo la ubadilifu.” Hilo laonyeshwa vizuri kwa maneno ya Paulo yanayofuata, “kwa hila ya watu.” Neno “hila” katika lugha ya awali lamaanisha kwa msingi “dadu” au “kucheza dadu,” yaani, mchezo wa nasibu. Jambo ni kwamba twakabiliwa daima na mawazo na mambo mapya ya kufuatia ambayo huenda yakaonekana kutodhuru, yenye kushawishi, hata yanayofaa. Maneno ya Paulo hutumika hasa kuhusu mambo yanayohusu imani yetu—harakati zinazoendeleza umoja wa makanisa ulimwenguni, miradi ya kijamii na ya kisiasa, na mambo kama hayo. (Linganisha 1 Yohana 4:1.) Lakini kanuni hiyo yafaa kwa habari ya desturi na mitindo ya ulimwengu ibadilikayo kila wakati—mitindo ya nguo, vitumbuizo, vyakula, afya au mazoezi ya mwili, na kadhalika. Kwa sababu ya ukosefu wa ujuzi na uamuzi mzuri, mtoto mchanga wa kiroho huenda akakengeushwa fikira kupita kiasi na mambo ya jinsi hiyo na hivyo huenda akazuiwa asifanye maendeleo ya kiroho wala kutimiza wajibu wake mbalimbali wa Kikristo ulio wa umaana zaidi.—Mathayo 6:22-25.

12. Watoto wachanga hutofautianaje na watu wazima kwa habari ya madaraka?

12 Kitabia kingine cha watoto wachanga ni uhitaji wao wa daima wa kupata msaada na uangalifu. Hawatambui wala hawahangaikii madaraka; utoto ni wakati wa maisha ambapo karibu kila jambo ni lenye kufurahisa. Kama Paulo alivyosema, wao ‘husema kitoto, hufahamu kitoto, hufikiri kitoto.’ Wao husadiki kwamba wengine watawashughulikia. Lilo hilo laweza kusemwa kuhusu mtoto mchanga wa kiroho. Mtu mpya anapotoa hotuba ya Biblia yake ya kwanza au aanzapo huduma ya shambani kwa mara ya kwanza, mzazi wa kiroho hufurahi kufanya yoyote awezayo kusaidia. Namna gani ikiwa mtu huyo mpya aendelea kuutegemea msaada huo na athibitika kutoweza kukubali lile daraka la kujitegemea mwenyewe? Kwa wazi huo ungekuwa wonyesho wa ukosefu wa kujitahidi.

13. Kwa nini ni lazima kila mmoja ajifunza jinsi ya kuuchukua mzigo wake mwenyewe?

13 Kwa habari hiyo kumbuka himizo la mtume Paulo kwamba ingawa twapaswa ‘kuchukuliana mizigo,’ bado “kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe.” (Wagalatia 6:2, 5) Bila shaka, inachukua wakati na bidii ili mtu ajifunze kujichukulia madaraka yake ya Kikristo, na huenda ikamaanisha kufanya dhabihu katika mambo fulani. Hata hivyo, ingekuwa kosa zito kwa mtu kujiruhusu mwenyewe ajihusishe mno katika mambo ya maisha yenye kufurahisha, yawe ni tafrija, safari, vidude-vidude, au hata ufuatiaji wa kazi ya kimwili usiohitajiwa, hivi kwamba mtu awa kana kwamba ni mtazamaji tu, bila tamaa yoyote ya kuongeza kushiriki kwake katika kazi ya kufanya wanafunzi au kufikilia maendeleo na madaraka ya kiroho. “Iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu,” akasihi mwanafunzi Yakobo.—Yakobo 1:22; 1 Wakorintho 16:13.

14. Kwa nini tusitosheke na kuonyesha vitabia vya mtoto mchanga wa kiroho?

14 Naam, kuna vitabia vingine viwezavyo kutambuliwa kwa urahisi ambavyo hutofautisha kati ya mtoto na mtu mzima. Hata hivyo, jambo la maana kama alivyosema Paulo, ni kwamba tuondolee mbali polepole vitabia vya kitoto na kukua. (1 Wakorintho 13:11; 14:20) Ama sivyo, huenda tukawa mapunguani katika maana ya kiroho. Lakini mtu aweza kufanyaje maendeleo? Ni nini kinachohusika katika kudumisha ukuzi wa kiroho kufikia ukomavu?

Jinsi Ambavyo Kuendelea Kwawa Dhahiri

15. Ni nini hatua za msingi katika taratibu ya ukuzi?

15 Ukuzi hutukiaje katika ulimwengu wa asili? “Kila mtu huanza uhai akiwa chembe moja,” chaeleza The World Book Encyclopedia. “Chembe hiyo hutwaa ndani viasili mbalimbali na kuvigeuza kuwa visehemu vya kujengea inayohitaji ili kukua. Hivyo, chembe hiyo moja hukua kutoka ndani. Chembe hiyo yaweza kuongezeka na kujigawanya kufanyiza chembe nyinginezo. Taratibu ya kujenga, kuongezeka, na kujigawanya ni ukuzi.” Jambo kuu hapa ni kwamba ukuzi hutukia kutoka ndani. Vyakula vinavyofaa vinapotwaliwa ndani, kusagwa-sagwa, na kutumiwa, ukuzi hutokea. Hilo laonekana wazi kwa habari ya kitoto kilichozaliwa karibuni. Kama tujuavyo, kitoto kilichozaliwa karibuni hula ugavi wa kawaida wa chakula kilichofanyizwa kipekee, maziwa, yaliyojaa mafuta na protini, viasili vinavyohitajiwa kwa ajili ya ukuzi. Tokeo ni nini? Kiasi cha ukuzi kwa habari ya uzani na urefu wa juu ambao kitoto hupata katika mwaka wa kwanza hauna kifani katika mwaka mwingine wowote wa ukuzi wa kawaida katika maisha yake yanayobaki.

16. Ni aina gani ya ukuzi inayoonwa katika wanafunzi wengi wa Biblia, na hiyo hufanywaje iwezekane?

16 Kuna mengi ambayo twaweza kujifunza kutokana na taratibu ya ukuzi ya asili ambayo twaweza kutumia kwa habari ya maendeleo yetu ya kiroho kutoka kwa mambo ya msingi hadi ukomavu. Kwanza, programu ya kawaida ya kujilishi ni ya muhimu. Fikiri nyuma kwa wakati ulipoanza kujifunza Biblia kwa mara ya kwanza. Ikiwa wewe ni kama wengine wengi, labda hukujua mengi juu ya Neno la Mungu. Lakini juma kwa juma ulitayarisha masomo yako ukawa na funzo lako la Biblia na kwa muda mfupi kwa kulinganisha, ulipata kuelewa mafundisho yote ya msingi ya Maandiko. Ni lazima ukubali kwamba hilo lilikuwa ukuzi wa ajabu, na yote hayo yakiwa tokeo la kujilisha Neno la Mungu kwa ukawaida!

17. Kwa nini programu ya kujilisha kiroho ya ukawaida ni ya lazima?

17 Lakini, namna gani sasa? Je! wewe bado hufuata programu ya kujilisha ya ukawaida? Mtu hapaswi kamwe afikiri kwamba kwa sababu tu amebatizwa, hakuna uhitaji tena kuwa na funzo la kawaida la utaratibu la kutwaa ndani chakula cha kiroho chenye kukuza. Hata ingawa Timotheo alikuwa mwangalizi Mkristo mkomavu, Paulo alimsihi hivi: “Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.” (1 Timotheo 4:15) Kila mmoja wetu ahitaji kufanya hivyo kwa kadiri kubwa kama nini! Ikiwa unapendezwa kufanya kuendelea kwako kiroho kuwe dhahiri, jitihada hizo ni za lazima.

18. Kuendelea kwa mtu kiroho kunadhihirikaje?

18 Kuacha kuendelea kwa mtu kuwe dhahiri hakumaanishi kufanya jitihada ya pekee kuonyesha yale ambayo mtu ajua au kujaribu kuwavutia wengine. Yesu alitaarifu hivi: “Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima” na “kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake.” (Mathayo 5:14; 12:34) Mioyo na akili zetu zinapojawa na mambo mema ya Neno la Mungu, hatuna la kufanya ila kudhihirisha hilo katika yale tunayofanya na kusema.

19. Twapaswa kuazimia kufanya nini kuhusu maendeleo yetu ya kiroho, ili kuwe na tokeo gani?

19 Kwa hiyo swali ni: Je! wewe hujifunza Biblia kwa ukawaida na kuhudhuria mikutano ya Kikristo ili kutwaa ndani habari yenye kukuza iwezayo kuchochea ukuzi wako wa kiroho, wa ndani? Usiridhike na kuwa mtazamaji asiyetenda kwa habari ya ukuzi wa kiroho. Chukua hatua chanya za kuhakikisha kwamba unatumia kikamili kile chakula kingi cha kiroho ambacho Yehova huandaa. Ikiwa wewe ni mmoja ambaye ‘hupendezwa na sheria ya Yehova, na huitafakari sheria yake mchana na usiku,’ basi yaweza kusemwa hivi juu yako: “Naye atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa. (Zaburi 1:2, 3) Lakini, ni jambo gani liwezalo kufanywa ili kuhakikisha kwamba utaendelea kufanya maendeleo ya kiroho? Hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.

Je! Waweza Kujibu?

◻ Kwa nini wakati wafaa wa kuchunguza kuendelea kwetu kiroho?

◻ Ukuzi wa kiroho unahusianaje na hamu ya kiroho?

◻ Ni nini kinachomaanishwa na “kila upepo wa elimu”?

◻ Kwa nini ni lazima kila mtu auchukue mzigo wake mwenyewe?

◻ Kuendelea kwa kiroho kunatimizwaje?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je! wewe huchukua wakati kusoma vichapo vyenye msingi wa Biblia?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki