Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 8/15 kur. 368-373
  • ‘Dhihirisha Kuendelea Kwako’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Dhihirisha Kuendelea Kwako’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUONGEZA UJUZI, UFAHAMU NA HEKIMA
  • KUZAA TUNDA LA ROHO
  • KUFANYA MAENDELEO KAMA JAMAA
  • Vijana—Fanyeni Maendeleo Yenu Yawe Wazi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Dhihirisha Maendeleo Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Uwe Mwenye Maendeleo
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Fanya Maendeleo Yako Yawe Dhahiri
    Huduma Yetu ya Ufalme—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 8/15 kur. 368-373

‘Dhihirisha Kuendelea Kwako’

1. Maneno ya mtume Paulo kwa Timotheo yanafunua nini juu ya kama Mkristo aliyekomaa kwa kiroho aweza kufanya maendeleo?

KUKOMAA kwa Kikristo hakumaanishi mwisho wa kuendelea kwa habari ya mtumishi wa Yehova Mungu aliyejitoa. Ni kwa Mkristo aliyekomaa, Timotheo, kwamba mtume Paulo aliandika hivi: “Ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha. . . . Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.”​—1 Tim. 4:13-15.

2. Mwendo wa mtu wa kawaida wa maisha unaonyeshaje kwamba kukomaa hakukomeshi maendeleo?

2 Kwamba kukomaa hakumaanishi mwisho wa kuendelea ni wazi kutokana na yale tunayoyaona katika maisha ya kila siku. Je! mwanamume aliyeoa mwenye jamaa yake mwenyewe haonwi kama mtu aliyekomaa? Lakini, je! yeye hawezi kuendelea kupata hekima kuu zaidi anapozidi kuchukua madaraka ya mtu mzima? Je! hawezi kujifunza kutokana na makosa yake na matokeo mema na makosa ya wengine? Bila shaka! Vile vile aweza kutazamia shauri na uongozi kutoka kwa baba yake na wazee wengine, akijua kwamba wao wana ujuzi zaidi na hekima.

3. Wakristo waliokomaa wanawezaje wakazidi kuendelea?

3 Ndivyo ilivyo na kwa Wakristo waliokomaa. Kwa kujifunza Neno la Mungu na kulitumia, wanaendelea kukua katika ujuzi na ufahamu. Wanafanya maendeleo katika kusitawisha roho njema kati ya washiriki wa jamaa na kuwafaidi watu wengine. Wakristo waliokomaa wanaweza kujifunza kwa mtu na mwenzake vile vile, kwa maana wanatofautiana katika kudhihirisha kwao sifa za kiroho. Yawezekana mtu asiwe na ujuzi mwingi. Mwingine aweza kuwa anajulikana sana kama mwenye fadhili au uvumilivu. Tena mwingine anaweza akawa na uamuzi mzuri zaidi au ufahamu juu ya matatizo. Mwingine anaweza akawa mkarimu zaidi sana au mkaribishaji. Tena mwingine anaweza akawa na uwezo mzuri zaidi wa kusimamia.

4. Kwa kuwa Wakristo waliokomaa wanaweza kuzidi kufanya maendeleo, ni sehemu gani tatu za maendeleo ambazo ingefaa waziangalie?

4 Kwa kuwa kuna nafasi ya kufanya maendeleo katika mambo mbalimbali ya maisha ya Kikristo, ingefaa mtumishi aliyekomaa wa Yehova Mungu atumie wakati akifikiri kama yeye anazidi kufanya maendeleo. Kuna sehemu tatu tunazoweza kuangalia: (1) kupata ujuzi mwingi zaidi, ufahamu na hekima, (2) kuzaa sana tunda la roho ya Mungu na (3) kutimiza madaraka kama mshiriki wa jamaa.

KUONGEZA UJUZI, UFAHAMU NA HEKIMA

5. Mtu awezaje kuchanganua kama anapata ujuzi zaidi, ufahamu na hekima?

5 Jiulize hivi: Je! furaha yangu ya kusoma na kujifunza Biblia inaongezeka kila mwaka upitapo? Je! nazidi kuifahamu na kuiona kuwa yenye maana zaidi kwangu? Je! mimi natumia maonyo ya Biblia kwa njia nzuri zaidi katika maisha yangu? Ikiwa waweza kujibu, Ndiyo, kwa maulizo haya, wewe unapata ujuzi zaidi, ufahamu na hekima. Lakini ukiona maendeleo machache imekupasa ufanye nini?

6. Twaweza kufanya nini tuhakikishe kwamba tunayoyasoma katika Neno la Mungu yanaivuta mioyo yetu iitikie kwa kuthamini?

6 Bila shaka utataka ujitahidi ujaze akili yako na moyo na hekima ipatikanayo katika Neno la Mungu. Bila ya kujali maendeleo tuliyoyafanya, kusoma Biblia tu na vitabu vinavyosaidia katika kujifunza Biblia hakutoshi kutuwezesha kuzidi kufanya maendeleo hata ikiwa hili linafanywa kwa kawaida. Lazima shauri la Biblia liufikie moyo, yaani, lazima moyo uvutwe kwa kuthamini. Ni wakati huo tu tutakapovutwa kutenda kwa hekima. (Zab. 119:11) Kwa hiyo, kuna haja ya kutafakari sana, kufikiria namna ambavyo maisha yetu yamepaswa yawe yakigeuzwa na mambo tunayoyasoma na kujifunza, na sababu yake. Unaposoma na kujifunza, waweza kufikiria maulizo kama haya: Habari inanisaidia kufahamu nini juu ya Yehova Mungu? Je! ninajitahidi kujipatanisha na utu wake, njia za matendo kama yanavyofunuliwa katika fungu la Maandiko linalosomwa? Je! habari ya Biblia yaonyesha udhaifu wo wote ndani yangu? Naweza kufanya nini niuondoe udhaifu huu?

7. Mikutano ya Kikristo inatuchocheaje “katika upendo na kazi nzuri”?

7 Kuhudhuria na kusikiliza kwa makini mikutanoni kunaongeza akiba yetu ya ujuzi vile vile, kunaongeza ufahamu wetu na kutuvuta tutende kwa hekima. Mikutano ya Kikristo inatuchochea “katika upendo na kazi nzuri.” (Ebr. 10:24, 25) Maelezo na hotuba zinazotolewa vyaweza kuichochea mioyo yetu tuendelee kuonyesha upendo kwa Mungu kwa kujipatanisha hata zaidi na Neno lake. Tunayoyasikia yanaweza kutia mradi wetu nguvu uwe bora katika kuacha upendo wa kujinyima uonyeshwe kabisa kwa waamini wenzetu, washiriki wa jamaa na wengine wa ulimwengu wa wanadamu. Kwa sababu ya yale tunayoyasikia, huenda nyakati nyingine tukaona kwamba kazi zetu katika sehemu fulani si ‘njema’ sana. (Mt. 5:16; Tito 3:8) Hii inatuweka katika hali ya kutumia mambo yaliyokaziwa fikira zetu na kutenda kwa hekima.

8. Kutayarisha mikutano kwawezaje kukatutanya tufanye maendeleo na kuwa chanzo cha kutia moyo kwa wengine?

8 Zaidi ya hayo, yale tunayoyafanya wenyewe kwa kutayarisha mikutano yanaweza yakatusaidia kufanya maendeleo. Habari ya Maandiko inakaziwa akilini mwetu na moyoni zaidi tunapoiangalia mapema kisha kuisikia ikirudiwa mikutanoni. Kutayarisha mapema kunatuweka katika hali bora ya kuzifahamu habari zote na kuhakikisha kama tulizifahamu habari zilivyo tulipoziangalia tukiwa peke yetu. Kwa sababu ya kutayarisha mapema, maelezo yetu yatakuwa ya maana zaidi. Tutaweza zaidi kutumia maneno yetu wenyewe na siyo kusoma mambo tu yaliyoandikwa bila ya kutangulia kufikiria maana yake kwa moyo. (Mit. 15:28) Hii yaweza kutufanya chanzo kikubwa zaidi cha kutia moyo kwa wengine, kwa maana maneno yetu ya moyoni yatawavuta zaidi wale wanaotusikia.

9. Kwa sababu gani kumwomba Yehova msaada wa roho yake kutatusaidia tufanye maendeleo?

9 Sala, vile vile, inasaidia sana katika kufanya maendeleo. Yesu Kristo alisema hivi: “Ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa [roho takatifu] hao wamwombao?” (Luka 11:13) Ni kwa njia ya roho hii kwamba Yehova Mungu anatuwezesha kulifahamu Neno lake na kulitumia inavyofaa. Roho takatifu inatumikia kama mkumbushaji na mwalimu. Kama mkumbushaji, inatukumbusha kanuni za Maandiko tunazozijua, na, kama mwalimu, inatusaidia kuyafahamu matumizi yake yafaayo. Kwa hiyo tunapopatwa na matatizo au inapokuwa lazima kufanya maamuzi mazito, twaweza kumwomba Yehova Mungu msaada. Ndipo roho yake itakapotusaidia tuyakumbuke tunayopaswa kuyajua na kutuzuia tusije tukapotoka kwa kutusaidia tuuone mwendo ufaao kufuata kwa msaada wa yale tuliyokumbushwa. Hii ni kulingana na maneno ya Yesu kwa wanafunzi wake: “Msaidizi, roho takatifu, . . . atawafundisheni mambo yote na kuwakumbusheni mambo yote niliyowaambieni.”​—Yohana 14:26, NW.

10. Sala zetu za kuomba msamaha wa dhambi zawezaje kutusaidia tuendelee kwa kiroho?

10 Kwa kuwa hatujakamilika, yatupasa kutafuta msamaha wa Mungu kwa dhambi zetu. Mtume Yohana aliwashauri waamini wenzake hivi: “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.” (1 Yohana 1:9) Tunaposema waziwazi katika sala zetu juu ya namna tulivyokosa, hii inakazia juu yetu uzito wa kile tulichokifanya. Hii yaweza kututia nguvu katika uamuzi wetu wa kufanya mema zaidi tunapoutafuta msaada wa roho ya Mungu ili tufanye maendeleo katika sehemu ambazo sisi tu dhaifu. Hivyo tunasaidiwa tutende kwa hekima.

11. Sala zetu zinaweza kufunua nini juu ya maendeleo yetu ya kiroho na ukamatano wetu na Yehova?

11 Namna ambavyo sisi tunasema katika sala kwa Yehova Mungu yaweza kuonyesha wazi kama tunafanya maendeleo katika ufahamu na matumizi ya Neno la Mungu katika maisha zetu. Namna gani juu ya sala zako? Je! zimepata kuwa zenye maana zaidi? Je! zinaonyesha kupendezwa kwingi na wanadamu wenzetu? Je! zinaonyesha mambo waziwazi? Je! zinaonyesha upendano kati yetu na Baba yetu wa kimbinguni? Je! unajikuta ukitaka kumgeukia kwa sala, kutoa shukrani yako kwa ajili ya fadhili zake za upendo? Ikiwa ukamatano wetu na Yehova ni wa karibu karibu, tutapendezwa kumfikia yeye katika sala. Uongozi wake utaonekana wazi sana kwa kujibu sala zetu. Hatutajiona kuzuiwa tusimfikie yeye kwa sala, tukiogopa kwamba yeye hatatusikia kwa sababu tunafikiri anatuchukia. Upendo mwingi kwa Yehova unaondoa hofu hiyo. Hilo ndilo alilolisema mtume Yohana wakati alipoandika hivi: “Katika pendo hamna hofu; lakini pendo lililo kamili huitupa nje hofu, kwa maana hofu ina adhabu; na mwenye hofu hakukamilishwa katika pendo.”​—1 Yohana 4:18.

KUZAA TUNDA LA ROHO

12. Kuacha tuongozwe na hekima ya Mungu na roho yake kutakuwa na matokeo gani mazuri juu yetu?

12 Tunapoyakubali maongozi ya hekima ya Mungu kama yalivyoandikwa katika Neno lake na uongozi wa roho yake, tutaona kwamba roho yetu au maoni yetu makuu yatatulazimisha tujipatanishe zaidi sana na kanuni ya Mungu ya utakatifu au usafi. Tutavutwa tutake kuziiga sifa zake njema​—⁠upendo wake, haki, hekima, rehema na uaminifu. Matokeo mema ya mazoezi na mafundisho yanayopokewa kwa funzo la kipekee na la kundi la Biblia yatadhihirishwa kwa watazamaji katika nia yetu, usemi na matendo. Ijapokuwa maelekeo yenye dhambi ya mwili usiokamilika yaweza kutuelekeza upande mbaya roho yetu au nia yetu kuu itashirikiana na uongozi wa roho ya Mungu na kuzizuia tamaa za mwili wetu. Kama vile mtume Paulo alivyosema katika barua yake kwa Wagalatia: “Enendeni kwa [roho], wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na [roho], na [roho] kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka.”​—Gal. 5:16, 17.

13. Twaweza kujiuliza maulizo gani tujue kama tunafanya maendeleo katika kuonyesha sifa za kimungu?

13 Unapoyatazama maisha yako kwa kusudi kama Mkristo, waona nini? Je! waiona nguvu hii nzuri au nia kuu ikitenda kazi ndani yako kwa kadiri kubwa zaidi kuliko wakati ulipokuwa “mtoto mchanga” tu wa kiroho? Je! Wakristo wenzako wanaona maendeleo yako ukidhihirisha zaidi sana tunda la roho, hasa katika wonyesho wako wa upendo wa kujinyima? Je! mwenendo wako wa kila siku unaonyesha kwamba maendeleo yanaonekana maishani mwako? Watu wanaona nini ndani yako​—katika nyumba yako, kazini pako, katika ujirani wako, katika ushirika wako na wengine? Je! mfano wako unamheshimu Yehova kwa kuonyesha kwake fadhili, uaminifu, upole na kujiweza? Je! unazidi kufanya maendeleo katika jambo hili?​—Gal. 5:22-26.

KUFANYA MAENDELEO KAMA JAMAA

14. Linapokuwa shauri la maendeleo ya kiroho, tamaa yetu imepaswa kuwa nini kama jamaa za Kikristo?

14 Imetupasa tuwe tofauti na ulimwengu wa wanadamu kama watumishi waliojitoa wa Yehova Mungu na kama vikundi vya jamaa. Je! ndivyo ilivyo jamaa yako? Je! wote katika jamaa wanayatambua madaraka yao waliyopewa na Mungu? Je! wanazidi kufanya maendeleo katika kutimiza matakwa ya kimungu yanayowapasa wao wenyewe?

15. Baba amepewa daraka gani zito, na imempasa baba wa Kikristo aige mfano wa nani katika kulitimiza?

15 Je! wewe ni baba? Basi unalo daraka zito la kutumia ukichwa ufaao. (1 Kor. 11:3) Je! wewe wautumiaje ukichwa huo? Je! unajipatanisha zaidi na zaidi na mfano wa Yesu Kristo, kichwa cha kundi la Kikristo? Je! wewe unamwiga yeye?​—Efe. 5:25-29.

16. Yesu alionyeshaje kupendezwa kwingi na faida za kiroho za wanafunzi wake?

16 Yesu Kristo alipendezwa kweli na hali njema ya kiroho ya wanafunzi wake. Hata wakati walipokawia kushika mambo, yeye hakushindwa kuwavumilia. Alitumia wakati kuwaonyesha mambo waziwazi naye alihakikisha kwamba walielewa kweli mafundisho yake. (Mt. 16:6-12; Yohana 16:16-30) Walipoendelea kuwa na ugumu katika kuwa na maoni yafaayo juu yao wenyewe, Yesu alirudia kutaja mambo juu ya haja ya kuhudumia wengine kwa unyenyekevu. (Marko 9:33-37; 10:42-44; Luka 22:24-27) Wakati wa usiku wake wa mwisho akiwa nao aliliimarisha jambo hili kwa kuwapa somo lenye mafundisho​—⁠kuosha miguu yao. (Yohana 13:14, 15) Vile vile Yesu alifikiria udhaifu wao naye hakuwapa habari zaidi kuliko ambazo wangeweza kuzifahamu.​—Yohana 16:4, 12.

17. Baba wa Kikristo awezaje kujihoji mwenyewe ahakikishe anauiga mfano wa Yesu anapoangalia hali ya kiroho ya jamaa yake?

17 Je! wewe kama baba unauiga mfano wa Yesu unapojifunza Biblia na jamaa yako? Je! unahakikisha wanaelewa kabisa? Je! unaufikiria udhaifu wao na kujihadhari usitazamie mengi mno kutoka kwao? Unapoona nia mbaya na matendo, je! unawaonyesha wazi washiriki wa jamaa yako sababu gani hasa wao wamekosa na sababu gani imewapasa watake kuwa vingine? Je! wewe unasimama imara kwa upande ya yaliyo haki na je! unatoa adhabu kwa upendo?

18. (a) Yesu alionyeshaje kupendezwa kwake na hali njema ya kimwili ya wanafunzi wake? (b) Baba wa Kikristo anawezaje kuuiga mfano wa Yesu katika hili?

18 Yesu Kristo alihangaikia hali njema ya kimwili ya wanafunzi wake. Hivyo, wakati mitume walipomrudia Yesu kutoka safari ya kuhubiri nao wakatoa habari za utendaji wao, aliwaambia hivi: “Njoni ninyi peke yenu kwa faragha, mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo.” (Marko 6:31) Kama kichwa cha jamaa, je! nawe ndivyo unavyoyajua mahitaji ya mke wako na watoto? Je! unamtendea mkeo kama “chombo kisicho na nguvu,” ukiufikiria udhaifu wake wa kimwili? (1 Pet. 3:7) Je! unahakikisha kwamba jamaa yako inapata wakati wa kujiburudisha kutoka kwa kawaida ya kila siku ya maisha?

19. Ni katika sehemu gani nyingine baba wa Kikristo aweza kujichunguza aone kama anaufuata mfano wa Yesu wa upendo wa kujinyima?

19 Yesu Kristo aliutoa uhai wake kwa hiari kama wonyesho wa upendo wake mwingi kwa wanafunzi wake. (Yohana 15:13) Je! wewe unaonyesha namna hii ya upendo kwa mkeo na watoto? Je! unayo nia ya kujinyima mapendezi fulani kwa ajili ya furaha ya jamaa yako? Je! unaonyesha upendo kwa mkeo kwa kumpa heshima na ubora nyumbani, kutokumdharau au kumfanya ajione hafifu? Je! unajitahidi kumfanya kila mshiriki wa jamaa ajisikie anatakiwa, kuthaminiwa na kuhitajiwa? Je! unatumia wakati kuwasikiliza, kujua maoni yao juu ya mambo na kuyafikiria unapofanya maamuzi?

20. Baba wa Kikristo aweza kujifunza nini kutokana na matumizi ya Yesu ya ukichwa juu ya kundi la Kikristo?

20 Yesu halitawali kundi la Kikristo anapotumia ukichwa wake. Yeye hafungi mshiriki mmoja mmoja kwa orodha ya amri nyingi lakini anawaruhusu watumie uwezo wao wa dhamiri. Kama vile Yesu, je! wewe unauvuta upendo wa haki wa jamaa yako na kujihadhari usifikilize madai yako kwa kulazimisha ati kwa sababu una mamlaka?

21. Mke wa Kikristo awezaje kuonyesha kwamba yeye anamtii mumewe kweli kweli?

21 Maandiko yanashauri wake hivi:“Watiini waume zenu, kama ipendezavyo katika Bwana.” (Kol 3:18) Ikiwa wewe u mke, je! unayategemeza maamuzi ya mumeo? Je! unatii hata maamuzi yanayotofautiana na mapendezi yako na kukipinga kishawishi cha kutumia maongozi ya kike ili mambo yafanywe unavyotaka? Mke anayemtii mumewe kweli kweli anaijua nia yake na hali ya kuwaza mambo. Kwa hiyo, yeye anaangalia mambo ya jamaa kwa njia ambayo haitapingana na maoni ya mumewe. Ikiwa hana uhakika juu ya maoni yake ya utendaji fulani au kitu fulani kikubwa cha kununuliwa, yeye (mke) hakifanyi, bali anamwuliza yeye, kwa njia hiyo akiepuka matatizo. Nyakati zote anajaribu kutimiza kazi zake kama mke kwa njia ambayo itampendeza mumewe isimfanye alalamike.

22. Ni baraka gani zinazomjia mke wa Kikristo aliye mtiifu kwa mumewe?

22 Mke anayefanya kupatana na ukichwa wa mumewe anapata hali ya heshima na ubora katika jamaa. Kama vile Mithali 31:11, 28 isemavyo juu ya mke afaaye: “Moyo wa mumewe humwamini, . . . Wanawe huondoka na kumwita heri; mumewe naye humsifu.” Mumewe anasadiki kwamba yeye hatatenda kwa upumbavu na kuhatirisha hali njema ya jamaa. Akijua kwamba mkewe hatayapuza maoni yake ya mambo kwa makusudi, mume anayemwiga Kristo hataona lazima ya kutoa usimamizi mkali sana juu ya matendo ya mke hata yeye (mke) asiweze kujiona huru kutumia akili yake mwenyewe. Hii inafanya iwe vyepesi kwa mke kuangalia madaraka yake nayo inaongeza furaha ya jamaa nzima. Kama mke, je! wewe unazidi kufanya maendeleo katika kutaka kujua mume wako anavyoona mambo na kuacha hili liongoze maamuzi yako unapoangalia mambo ya jamaa?

23. Maendeleo ya mke wa Kikristo yaweza kuonekanaje anapochagua mavazi na mapambo?

23 Sehemu nyingine ambayo katika hiyo Biblia inashauri wake ni mapambo na mavazi. “Kujipamba kwenu, kusiwe kujipamba kwa nje, yaani, kusuka nywele; na kujitia dhahabu, na kuvalia mavazi; bali kuwe utu wa moyoni usioonekana, katika mapambo yasiyoharibika; yaani, roho ya upole na utulivu.” (1 Pet. 3:3, 4; linganisha Mithali 31:30.) Hii haimaanishi kwamba haimpasi mwanamke kujali sura yake ya nje​—sivyo hata kidogo. Wanawake wanaonywa katika Maandiko “wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi.” (1 Tim. 2:9) Lakini, linalopaswa kukaziwa fikira ni sifa za moyo, nayo mapambo ya nje yamepaswa yaionyeshe sifa njema ya adabu. Je! wewe kama mke umefanya maendeleo katika hili? Je! unaona kwamba huvutwi sana na mitindo ya karibuni kama ulivyokuwa ukivutwa wakati fulani uliopita? Je! unaelekea zaidi kuchagua yaliyo ya adabu? Je! umefanya maendeleo katika kujipamba kwa kuonyesha “roho ya upole na utulivu,” yaani, ukionyesha maoni makuu ya utulivu na hata upole ijapokuwa hali zisizopendeza zaweza kutokea?

24. Ni katika sehemu gani ambazo watoto wanaweza kufanya maendeleo?

24 Ijapokuwa kwa kawaida hawafikiriwi kama Wakristo walio komaa, watoto, vile vile, wanaweza kudhihirisha maendeleo katika kuthamini mambo ya kiroho. Wakati unakuja katika maisha ya mtoto anapotazamiwa kuacha maoni na njia za kitoto. Juu ya maono yake mwenyewe, mtume Paulo aliandika hivi: “Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto.” (1 Kor. 13:11) Je! wewe, kama mtoto, unaondoa tabia za mtoto mchanga kidogo kidogo? Je! unajichukulia madaraka nyumbani, ukisaidia uwezapo ili kupunguzia wazazi wako kazi? Je! unatafuta nafasi za kufanya mambo? Au, hata sasa ni lazima uwe ukiulizwa-ulizwa usaidie jambo fulani kisha kuitikia kwa manung’uniko? Je! waonyesha akili katika kujijenga kwa kiroho? Je! unasoma Biblia na vitabu vinavyosaidia katika kujifunza na kutayarisha mikutano ya kundi unapokuwa peke yako? Je! namna unavyotumia wakati yaonyesha kwamba unaamini ‘kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo na kwamba utauwa hufaa kwa mambo yote’? (1 Tim. 4:8) Je! unafahamu kwamba utii kwa wazazi wako ni haki na ni njia kubwa ambayo katika hiyo waweza kumpendeza Mungu?​—Efe. 6:1; Kol. 3:20.

25. Watoto wanawezaje kuonyesha maendeleo katika kuwa watii kwa wazazi?

25 Utii kwa wazazi siyo shauri la kufanya tu yale wanayoyasema bali vile vile watia ndani na kujipatanisha na yale unayoyajua yatailetea jamaa sifa njema. Kwa kweli ina maana ya kujitiisha kwa maagizo na mashauri ya baba yako na mama, kupatana na mapenzi ya Mungu. Unaweza ukajiuliza hivi: Wakati ninapotoka nyumbani, je! natoa ushuhuda wa kwamba natoka katika nyumba ya Kikristo? Je! maendeleo yangu ya kiroho yanaonekana wazi katika adabu njema, hali yenye heshima kwa watu wazee na walio na mamlaka na kwa kuwa imara upande wa yaliyo haki​—shuleni, katika ujirani na penginepo? Je! nashirikiana na wazazi wangu wa Kikristo ninapochagua mavazi nitakayoyavaa mwenyewe? Au najaribu kuchagua mitindo isiyo ya adabu na ya kupita kadiri kisha kujaribu kulazimisha wazazi wangu wachukue mambo ninavyotaka mimi?

26. Linapokuwa shauri la kufanya maendeleo katika maisha ya Kikristo, imewapasa wengine waweze kuona nini ndani yetu?

26 Bila ya kujali kama unaishi peke yako au u sehemu ya jamaa, kama umekwisha fikia kukomaa kwa Kikristo au unajitahidi ukaufikie mradi huo, maendeleo yamepaswa yaonyeshwe wazi katika roho au nguvu kuu inayokuvuta wewe ufanye mapenzi ya Mungu. Imewapasa wengine waweze kuona kwamba kushikamana na Neno la Mungu kumekufanya wewe mwanamume bora au mwanamke, mke na mama bora, mume na baba bora, mwana au binti bora. Nyumba ya Kikristo imepaswa kuwa mahali penye furaha, amani na upendo, badala ya kugombana na kupigiana kelele. Imepaswa kuwa malidadi, safi na yenye kutunzwa vizuri. Je! ndivyo nyumba yako ilivyo? Bila ya ushuhuda ufaao wa ukuzi wa kiroho katika maisha za wale walio watumishi wa Mungu, kuhubiri kwetu hakuna maana. Dini yetu, ibada yetu, inaamuliwa ilivyo hasa na matokeo inayoyatokeza ndani yetu na katika maisha zetu za kila siku.​—Kol. 3:8-14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki