Uwe Mwenye Maendeleo
ULIPOJIFUNZA kutumia kanuni za Biblia kwa mara ya kwanza, mawazo yako, usemi wako, na tabia ulizozoea sana zilianza kubadilika polepole. Ulifanya mabadiliko mengi hata kabla ya kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Sasa inaelekea umefanya maendeleo kufikia hatua ya kujiweka wakfu kwa Yehova. Je, hiyo inamaanisha kwamba uache kufanya maendeleo? La hasha. Kubatizwa ni mwanzo tu.
Mwanafunzi Timotheo tayari alikuwa akitumikia akiwa mzee Mkristo wakati Paulo alipomwambia ‘afikirie kwa uzito’ mashauri anayopewa na mapendeleo ya utumishi aliyokabidhiwa—‘avame’ katika mambo hayo—ili ‘kusonga mbele kwake kupate kuwa dhahiri.’ (1 Tim. 4:12-15) Uwe mpya katika kweli au uwe umekuwa Mkristo kwa muda mrefu, kuza tamaa ya kusonga mbele.
Ujuzi na Mabadiliko
Katika Waefeso 3:14-19, tunasoma kwamba mtume Paulo alisali ili waamini wenzake ‘wapate kwa ukamili kuweza kufahamu kiakili . . . upana na urefu na kimo na kina’ cha kweli. Ili wafanikiwe, Yesu alitoa zawadi za wanadamu wafundishe kutaniko na kulirekebisha na kulijenga. Tunaweza ‘kukua’ kiroho tukitafakari kwa ukawaida Neno la Mungu lililopuliziwa na kwa kusaidiwa na walimu wenye uzoefu.—Efe. 4:11-15.
Ukuzi huo unatia ndani ‘kufanywa upya katika kani inayotendesha akili yako.’ Hiyo inahusisha kukuza akili yenye nguvu inayopatana na maoni ya Mungu na Kristo. Inamaanisha kwamba ili ‘uvae utu mpya’ unahitaji kuzingatia daima mawazo yao. (Efe. 4:23, 24) Unapojifunza vitabu vya Injili, je, unayaona masimulizi ya maisha ya Kristo kama mifano ya kuiga? Je, unajaribu kutambua tabia fulani hususa ambazo Yesu alionyesha na kujitahidi sana kuziiga maishani mwako?—1 Pet. 2:21.
Mambo unayotaja katika mazungumzo yanaweza kuonyesha maendeleo yako. Wale ambao wamevaa utu mpya si wadanganyifu, hawasemi maneno machafu, hawana matusi, wala hawasemi maneno yasiyofaa. Badala yake, usemi wao ni “mwema kwa ajili ya kujenga . . . ili huo upate kuwapa wasikiaji lililo la kupendeleka.” (Efe. 4:25, 26, 29, 31; 5:3, 4; Yuda 16) Maneno yao faraghani na kwenye mikutano ya kutaniko yanafunua kwamba kweli inabadili maisha yao.
Ikiwa ‘hurushwi huku na huku kama na mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho,’ huo pia ni uthibitisho wa maendeleo. (Efe. 4:14) Kwa mfano, unatendaje ulimwengu unapokushambulia kwa mawazo mapya, mambo mapya, au aina mpya za vitumbuizo? Je, unashawishiwa kutumia wakati wa kutimiza wajibu wa kiroho kufuatilia mambo hayo? Kufanya hivyo kunaweza kuzuia maendeleo yako ya kiroho. Ni jambo la hekima kama nini kununua wakati wa kufuatia mambo ya kiroho!—Efe. 5:15, 16.
Jinsi unavyowatendea watu wengine pia inaweza kuonyesha maendeleo yako ya kiroho. Je, umejifunza kuwa ‘mwenye huruma kwa njia nyororo, ukisamehe kwa hiari’ ndugu na dada zako?—Efe. 4:32.
Maendeleo yako kwa kufanya mambo kwa njia ya Yehova yanapasa kuwa dhahiri kutanikoni na nyumbani vilevile. Pia yanapasa kuwa dhahiri shuleni, hadharani, na kazini. (Efe. 5:21-6:9) Kama unaonyesha kikamili sifa za Mungu katika hali hizo zote, basi maendeleo yako yanakuwa dhahiri.
Tumia Zawadi Yako
Yehova amemkabidhi kila mmoja wetu uwezo na vipawa. Anatarajia tuvitumie kuwasaidia wengine ili aweze kuonyesha fadhili yake isiyostahiliwa kupitia sisi. Mtume Petro aliandika hivi kuhusu jambo hilo: “Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba walio wema wa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu.” (1 Pet. 4:10) Unatumiaje zawadi yako ya utumishi?
Petro anaendelea kusema: “Ikiwa yeyote asema, acheni aseme kama kwamba ni matamko matakatifu ya Mungu.” (1 Pet. 4:11) Mstari huu unakazia daraka la kusema kwa kupatana kabisa na Neno la Mungu, ili Mungu atukuzwe. Basi njia yetu ya kuzungumza pia na iwe yenye kumtukuza Yehova. Mazoezi yanayoandaliwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi yanaweza kukusaidia kutumia zawadi yako kwa njia hiyo—kumtukuza Mungu kwa njia unayowasaidia wengine. Ukiwa na kusudi hilo, upimeje maendeleo yako katika shule?
Badala ya kufikiria ni sifa ngapi za usemi ambazo umetimiza katika shauri la usemi au kufikiria aina ya migawo ambayo umepewa, fikiria kadiri ambavyo mazoezi hayo yameboresha dhabihu zako za sifa. Shule hutuzoeza kuwa bora katika huduma ya shambani. Basi, jiulize: ‘Je, kweli mimi hutayarisha mambo nitakayosema katika utumishi wa shambani? Je, nimejifunza kupendezwa kibinafsi na watu ninaowahubiria? Je, ninaweka msingi wa ziara za kurudia kwa kuwaachia watu swali kwa ajili ya mazungumzo yajayo? Kama namfundisha mtu Biblia, je, najitahidi kuwa mwalimu bora anayefikia moyo?’
Usione unafanya maendeleo eti kwa sababu tu ya mapendeleo ya utumishi unayopata. Maendeleo yako yanaonyeshwa na jinsi unavyotimiza mgawo wako na wala hauonyeshwi na mgawo wenyewe. Ukipokea mgawo unaohusu ufundishaji, jiulize: ‘Je, kweli nilifundisha kwa ustadi? Je, nilishughulikia mgawo huo kwa njia iliyogusa mioyo ya wasikilizaji?’
Himizo la kutumia zawadi yako linadokeza hali ya kuchukua hatua kabla ya kuulizwa. Je, unachukua hatua ya kuhubiri na wengine katika huduma ya shambani? Je, unatafuta fursa za kuwasaidia wapya, wachanga, au wagonjwa kutanikoni? Je, unajitolea kusafisha Jumba la Ufalme au kusaidia katika njia kadha wa kadha katika makusanyiko? Je, pindi kwa pindi unaweza kuchukua upainia msaidizi? Je, unaweza kutumikia ukiwa painia wa kawaida au kusaidia kutaniko lenye uhitaji mkubwa? Kama wewe ni ndugu, je, unajitahidi kufikia sifa za Kimaandiko za watumishi wa huduma na wazee? Utayari wako wa kusaidia na wa kukubali daraka ni ishara ya maendeleo.—Zab. 110:3.
Jinsi Uzoefu Unavyotusaidia
Ukihisi huwezi kutimiza mambo mengi kwa sababu huna uzoefu katika maisha ya Kikristo, jipe moyo. Neno la Mungu ‘linaweza kumtia mjinga hekima.’ (Zab. 19:7; 119:130; Mit. 1:1-4) Kutumia mashauri ya Biblia hufanya tufaidike na hekima kamili ya Yehova, ambayo ni bora sana kuliko chochote tunachoweza kujifunza kupitia uzoefu pekee. Lakini, tunapozidi kufanya maendeleo katika utumishi wetu kwa Yehova, sisi hupata uzoefu wenye thamani. Tunaweza kuutumiaje uzoefu huo vizuri?
Baada ya kuona mengi maishani, mtu anaweza kushawishiwa kufikiria: ‘Hali hii imewahi kunipata. Najua jambo la kufanya.’ Je, ni hekima kufanya hivyo? Mithali 3:7 linaonya hivi: “Usiwe mwenye hekima machoni pako.” Kwa hakika uzoefu unapasa kufungua akili zetu tunaposhughulika na hali zinazotokea maishani. Na kama tunafanya maendeleo ya kiroho, uzoefu unapasa kukazia akilini na moyoni kwamba tunahitaji baraka za Yehova ili tufanikiwe. Basi maendeleo yetu yanakuwa dhahiri tunapomwendea Yehova mara moja atuongoze katika maisha yetu badala ya kukabili hali za maisha kwa kujitumaini. Maendeleo yetu huonekana tunapokuwa na uhakika kwamba hakuna kitu kiwezacho kutokea bila Yehova kukiruhusu. Pia maendeleo hayo huonekana tunapodumisha uhusiano wenye tumaini na wenye upendo pamoja na Baba yetu wa mbinguni.
Endelea Kujitahidi Kusonga Mbele
Ijapokuwa mtume Paulo alikuwa Mkristo mtiwa-mafuta aliyekomaa kiroho, alitambua kwamba alihitaji ‘kujinyoosha mbele’ ili afikie mradi wake wa uhai wa milele. (Flp. 3:13-16) Je, una maoni kama hayo?
Umefanya maendeleo kwa kadiri gani? Pima maendeleo yako kwa kutazama kadiri ambavyo umejivika utu mpya, umenyenyekea enzi kuu ya Yehova, na kujitahidi kutumia zawadi zako kumheshimu Yehova. Unapofaidika na elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, usemi wako na ufundishaji wako zinapasa kuendelea kudhihirisha sifa zinazoonyeshwa katika Neno la Mungu. Endelea kuzingatia sehemu hizo za maendeleo yako. Ndiyo, zifurahie, na maendeleo yako yatakuwa dhahiri.