Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 11/1 kur. 23-27
  • Kukazania Ukomavu wa Kikristo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukazania Ukomavu wa Kikristo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ukuzi wa Kiroho Ni wa Lazima
  • Ukomavu wa Kikristo—Ni Nini?
  • Kueni kwa Upendo
  • Kukomaa kwa Kikristo Ni kwa Lazima Ili Kupata Uzima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Dhihirisha Maendeleo Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Je, Wewe Ni Mkristo “Aliyekua Kabisa”?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Songa Mbele Kuelekea Ukomavu—“Ile Siku Kuu ya Yehova Iko Karibu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 11/1 kur. 23-27

Kukazania Ukomavu wa Kikristo

“Kwa kusema kweli, na tukue kwa upendo katika mambo yote ndani ya yeye aliye kichwa, Kristo.”​—WAEFESO 4:15, New World Translation.

1, 2. (a) “Uzao wa tumbo ni thawabu” kwa njia gani? (b) Inatazamiwa nini kwa watoto waliotoka kuzaliwa?

MTOTO mwenye afya anayejitupa-tupa ni furaha kweli kweli. Watu wengi wanavutiwa na vituko vyake. Yeye ni chanzo cha msisimuko na furaha isiyo na mwisho, ko kote anakoenda anakaziwa fikira. Ni jambo la kufahamika kwamba wazazi wanampenda kama ‘fahari na furaha’ yao ijapokuwa taabu yote na mvurugo wote anaoleta. Kweli kweli, “uzao wa tumbo ni thawabu.”​—Zaburi 127:3.

2 Lakini, hata mtoto apendeke namna gani, inakuwaje asipoonyesha dalili yo yote ya ukuzi? Akibaki katika hali hiyo baada ya miezi mingi au labda baada ya miaka mingi ya kutunzwa kwa upendo na wazazi, basi kwa wazi kuna taabu fulani kubwa. Kweli kweli, ukuzi umekuja kuhusiana na uhai; tunatazamia vyote vilivyo hai vikue. Ni ushuhuda wa uwezo wa uumbaji wa Yehova na hekima yake.​—Luka 2:52.

Ukuzi wa Kiroho Ni wa Lazima

3. Ni ukuzi gani uliotabiriwa na Yesu, na ni utimizo gani unaoonekana?

3 Kwa kutimiza unabii wa Yesu, ukuzi wa aina nyingine unatokea. Ulimwenguni pote, “mavuno” ya kiroho yanaendelea. (Mathayo 9:37) Kwa mfano, wakati wa mwaka wa utumishi wa 1985, nchi zaidi ya sita ziliripoti wastani za wahubiri wa Ufalme zaidi ya 100,000. Miaka mitatu tu kabla, mwaka 1981, ni nchi mbili tu zilizokuwa na hesabu hiyo. Katika miaka sita ya mwisho, mashahidi wapya wa Yehova 827,144 walibatizwa na makundi mapya zaidi ya 5,000 yakaundwa. Yehova ameharakisha kazi yake.​—Isaya 60:22.

4. Matokeo ya ukuzi wa ulimwenguni pote kati ya watu wa Yehova yamekuwa nini?

4 Tarakimu hizo zinaonyesha kwamba karibu kila watu watatu wanaoshirikiana kwa ukawaida na watu wa Yehova na kushiriki kazi ya kuhubiri leo walibatizwa katika miaka sita iliyopita. Je! wewe ni mmoja wao? Ikiwa ndivyo, umekuwa chanzo cha furaha kubwa kwa wale waliokusaidia ujifunze ukweli, kwa marafiki wako wote Wakristo, na kwa Baba yako wa kimbingu, Yehova Mungu. (Mithali 27:11) Kama ile hatua ya kwanza anayochukua mtoto, hatua uliyochukua ya kujiweka wakfu kwa Yehova ilikuwa tukio lenye kusisimua. Ilionyesha mwendo wa kusonga mbele, wenye kuendelea katika upande wako. Ilikuwa ishara ya ukuzi.

5. Kila mtu mmoja mmoja anapaswa kujiuliza maswali gani? Ni nini kinachoweza kusaidia kupata majibu yake?

5 Imekuwaje tangu wakati huo? Kwa uangalizi wa upendo wa Wakristo wenzako, je, wewe unaonyesha ushuhuda wenye kuendelea wa ukuzi wa kiroho? ‘Nijueje?’ huenda ukauliza. Kumbuka aliyosema mtume Paulo juu ya ukuzi: “Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto [“tabia za mtoto,” NW].” (1 Wakorintho 13:11) Kwa hiyo si kupita kwa wakati tu bali kuacha “tabia za mtoto” ndiko kulimfanya awe mtu aliyekomaa. Hizo ni tabia gani?

6, 7. (a) Eleza ‘tabia moja ya mtoto’ na hatari ambayo inatokeza. (b) Tabia hiyo inaonyeshwaje? Matokeo yanaweza kuwa nini?

6 Jambo moja kuhusu watoto ni kwamba wanakaza fikira kwa muda mfupi sana. Ingawa wanataka kujua kila jambo linalowazunguka, wao wanabadili-badili maoni wakati wo wote, ni vigeugeu, na hawatulii. Kwa wazi, ye yote anayebaki katika hali hiyo yumo katika hatari kubwa ya kiroho. Anaelekea ‘kutupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, katika njia za udanganyifu,’ kama alivyosimulia mtume Paulo katika Waefeso 4:14.

7 Mawimbi na pepo zaweza kutokea haraka hali moja na vile zinavyoisha mara moja. Leo, inapopangwa mambo yawe yasiyofaa tena, mielekeo na mitindo inakuja na kwenda. Mambo yaliyokuwa yakionwa kuwa ya lazima muda mfupi tu uliopita yamekuwa ya kizamani kabisa na yakasahauliwa. Iwe ni katika habari ya tafrija, mavazi na kujipamba, au jambo jingine lo lote, ni jambo lisilo la hekima kama nini​—na la kitoto​—kuvutwa na tamaa ya kutaka sikuzote kila jambo la karibuni au kuwa nalo, halafu upesi linakuwa la kizamani na tunakatishwa tamaa upesi. Katika mambo ya kiroho, matokeo ya ukosefu huo wa imara yanaweza kuwa yenye msiba.​—Linganisha Yakobo 1:6-8.

8. Ni ‘tabia’ gani nyingine ya watoto wa kiroho, na inatokeza hatari gani?

8 ‘Tabia nyingine ya mtoto’ ni kwamba watoto wana wazo dogo sana juu ya yaliyo mema na mabaya, yaliyo sahihi au kosa. Hali moja na hiyo, watoto wa kiroho wangali ‘hawajazoezwa kupambanua mema na mabaya,’ na ndiyo sababu mtume Paulo aliwasihi Wakristo wenzake ‘wakaze mwendo ili wafikilie utimilifu (‘kukomaa,’ NW); kutoweka msingi tena.’ (Waebrania 5:14; 6:1) Wale ambao ni watoto wa kiroho wanahitaji kupewa uhakikisho daima kwamba walichokubali kuwa ukweli ndicho ukweli hasa, na waliyofundishwa kufanya ndiyo hasa wanayopaswa kufanya. Wanahitaji msaada hata katika mambo yaliyo ya msingi. Ama sivyo wanavurugwa akili kwa urahisi, kushuka moyo, na kushindwa na mashaka yanayoweza kuharibu imani yao.

9. Ni kwa sababu gani tunapaswa kukazania kukomaa kwa Kikristo?

9 Je! umepata kuona kwamba sikuzote watoto wanafanya wanayoona watu wazima wakifanya? Bila shaka, kwao huo ni mchezo. Kwa wazi, sehemu ya mchezo huo ni kuweza kufanya wanayotaka bila kulazimika kukubali daraka linaloambatana na kufanya hivyo. Ingawaje hayo ndiyo maisha ya mtoto. (Ona Mathayo 11:16, 17.) Lakini ukuzi na usitawi unaambatana na daraka na jukumu. Hilo ni jambo la kukazaniwa ambalo mtoto anapaswa kusaidiwa alikubali. Kadiri ambayo anakubali hilo itaamua, kwa sehemu kubwa, kufaulu au kushindwa kwake katika maisha ya baadaye. Katika hali ya kiroho, ni jambo la maana hata zaidi kwamba kila mmoja wetu afikirie kwa uzito kukazaniwa kwa ukomavu wa Kikristo. Je! wewe una nia, hata shauku, ya kukubali daraka linaloambatana na kuwa mtu wa kiroho aliyekua kabisa, aliyekomaa? Au je, wewe unaambaa-ambaa tu, ukiachia wengine mzigo wa daraka lako?​—Wagalatia 6:4, 5.

Ukomavu wa Kikristo—Ni Nini?

10. Ni kwa sababu gani Paulo aliwasihi Wakristo Waebrania ‘wakaze mwendo kufikia kukomaa’?

10 Mtume Paulo alipowasihi Wakristo ‘wasonge mbele ili wafikilie kukomaa,’ alikuwa akifikiria nini? (Waebrania 6:1, NW) Habari inayozunguka inaonyesha kwamba hapo kwanza Paulo alikuwa na mengi ya kuwaambia Wakristo Waebrania juu ya “kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki,” Yesu Kristo. Lakini alihisi kwamba hawakuwa tayari kwa jambo hilo kwa sababu aliyokuwa akifikiria yalikuwa “ni shida kuyaeleza.” (Waebrania 5:10, 11) Badala yake, aliwakumbusha hivi: “Nanyi mmekuwa mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu. Kwa maana kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.”​—Waebrania 5:12-14; linganisha Yuda 3.

11. Kukomaa kunamaanisha nini?

11 Basi, je, hiyo inamaanisha kwamba kukomaa ni kuwa tu na maarifa ya mambo ya kindani ya Biblia? Ingawa kukomaa kwa Kikristo kunatia ndani maarifa na kuielewa Biblia, mengi zaidi yanahusika. Kuelewa maneno yaliyotumiwa na mtume Paulo kutatusaidia tuone jambo hilo waziwazi zaidi. Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “kukomaa” ni te·lei·oʹtes, na neno la sifa “mkomavu” limetafsiriwa kutoka teʹlei·os. Maneno hayo yanahusiana na teʹlos, ambalo linamaanisha “mwisho.” Kwa hiyo kitabu Expository Dictionary of New Testament Words cha W. E. Vine, kinaeleza kwamba kukomaa (teʹlei·os) “kunamaanisha kufikia mwisho wake, kutimilika, kamili, kamilifu.” Kwa hiyo, Mkristo aliyekomaa ni yule ambaye amefikia mwisho au mradi fulani. Mradi huo ni nini?

12. Kulingana na Waefeso 4:11-13, kukomaa kunatia nini ndani?

12 Mtume Paulo, katika Waefeso 4:11-13, alieleza kwamba Kristo Yesu, akiwa kichwa cha kundi la Kikristo, ametoa maandalizi mengi ili kusaidia “watakatifu” wafikie mradi huo, yaani, “sisi sote [tuufikie] umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo.” Hapa, kuwa mkomavu, au kuwa mtu mkamilifu (Kigiriki, teʹlei·os), kunahusiana si kuwa tu na “maarifa sahihi” (‘kufahamu,’ UV) bali pia na “umoja wa imani” na kujipatanisha wenyewe kulingana na kimo kilichofikiwa na Kristo.

13. Kwa sababu gani hakuwezi kuwa kukomaa kwa Kikristo pasipo “umoja wa imani”?

13 “Umoja wa imani” unamaanisha muungano. Kabla mtu hajajifunza juu ya ile “imani moja,” huenda akawa na mawazo na maoni yake mwenyewe juu ya jinsi mambo yanavyopasa kufanywa, juu ya yanayofaa na yasiyofaa, na kadhalika. (Waefeso 4:4, 5) Akiruhusu mawazo hayo yaendelee, ataliona kuwa jambo gumu sana kukua kiroho. Wakati mmoja Paulo aliwaita Wakristo katika kundi la kale la Wakorintho “watoto wachanga katika Kristo” na “watu wenye tabia ya mwilini” kwa sababu walitenganishwa na “husuda na fitina,” wengine wakidai kumfuata Paulo, wengine Apolo. (1 Wakorintho 3:1-4) Kwa hiyo, ni jambo rahisi kuona kwamba “umoja wa imani,” unaambatana na kukomaa kwa Kikristo. Hakuwezi kukawa moja bila lile jingine. Kwa hiyo tunapaswa kujiuliza hivi: Je! tumeacha njia zetu za kufikiri za kilimwengu za kwanza? Je! tunaona umaana wa umoja wa mawazo na matendo pamoja na watu wa Yehova? “Umoja wa imani” ni kitu cha lazima katika ukomavu wa Kikristo.​—Waefeso 4:2, 3.

14. Kukomaa kunahusiana na nini kingine?

14 Kukomaa kwa Kikristo pia kunahusiana na kuwa na “cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo.” Hiyo maana yake ni nini? Paulo anaendelea kusema kwamba wale wanaofikia kimo hicho si watoto tena, hawaendelei ‘kutupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, ‘kwa ujanja’ ambao kwa hila wanatunga kosa. Badala yake, wana maarifa sahihi ya ukweli. Wamekua katika upendo wa Kristo, na wanaonyesha sifa za kimungu nyinginezo, kama vile hekima, uadilifu, na uwezo. (Waefeso 4:13, 14; Yohana 15:12, 13; 1 Wakorintho 1:24, 30; 2:7, 8; Mithali 8:1, 22-31) Ingawa sisi, tukiwa wanadamu wasiokamilika, huenda tusiweze kufikia kabisa ‘kimo cha Kristo,’ hakika tunaweza kumfanya awe Mfano wetu wa kufuatwa, tukijiwekea wenyewe mwisho, au mradi, wa kusitawisha aina ile ile ya utu wa kimungu. (Wakolosai 3:9) Kwa kadiri tunavyojitahidi kufikia mradi huo tunakuwa wakomavu.

Kueni kwa Upendo

15. Ni nini hatua ya kwanza katika kutafuta kufikia kukomaa?

15 Tukiwa tumekwisha kufikiria maana ya usemi “ukomavu wa Kikristo,” tunahitaji kujua jinsi tunavyoweza kuufikia. Kama tulivyokwisha kuona, andiko la Waebrania 6:1 linaonyesha kwamba katika kutafuta kupata ukomavu wa Kikristo kuna msingi fulani ambao juu yake tunapaswa kujenga. Hilo likiisha kufanywa, jitihada zaidi zaweza kuelekezwa kwenye kukaza mwendo kufikia ukomavu. Kwanza kati ya vitu mbalimbali vinavyofanyiza msingi huo ni “kuzitubia kazi zisizo na uhai.”

16. Tunapaswa kutubia ‘kazi gani zisizo na uhai’? Kwa sababu gani?

16 Kwa wazi, “kazi zisizo na uhai” zingetia matendo ya mwili wenye dhambi, ambayo, kama hayazuiwi, yataongoza kwenye kifo. Tunakuja kutambua kwa urahisi makosa ya moja kwa moja kama vile uasherati, uchafu, mwenendo usio wa adili, ibada ya sanamu, na ibada ya mashetani kuwa dhambi, na tunayepuka. Lakini matendo ya mwili, “kazi zisizo na uhai,” pia yanatia ndani mambo ambayo huenda wengine wakaita tabia za kiutu kama vile uadui, ugomvi, wivu, hasira [vishindo vya hasira, NW], fitina, faraka, uzushi, na husuda. (Wagalatia 5:19-21) Tabia hizo za kiutu zisipovuliwa na mahali pake pachukuliwe na “utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli,” haielekei sana kwamba mtu atafanya maendeleo yo yote akafikie ukomavu wa Kikristo.​—Waefeso 4:22-24.

17. Ni mambo gani mengine yanayoweza kuhesabiwa kuwa “kazi zisizo na uhai”?

17 Licha ya matendo ya mwili, “kazi zisizo na uhai” tunazopaswa kuvua zinatia ndani pia matendo na mambo ambayo yamekufa kiroho, yasiyofaa kitu, na yasiyozaa matunda. Yaweza yakawa ni mipango ya kuchuma pesa, ya kujitajirisha haraka. Yaweza ikawa ni mipango ya mambo makubwa na yenye kumaliza wakati ya kuwa na elimu ya juu, au yaweza kuwa ni matengenezo ya kilimwengu ya kuleta mabadiliko katika ujamii, amani, na kadhalika. Huenda mambo hayo yote yakaonekana yana faida fulani kama yalivyo, lakini mambo hayo ni “kazi zisizo na uhai” kwa sababu yanaweza kuleta kifo cha kiroho kwa wale wanaojiingiza ndani yake. Wote wanaopendezwa na kufikia ukomavu wa Kikristo wanapaswa ‘kutubia’ au kujiepusha na kuzifuata hizo “kazi zisizo na uhai” na kufuata onyo la Yesu la kuendelea kutafuta “kwanza ufalme wake, na haki [ya Mungu].”​—Mathayo 6:33.

18, 19. (a) Katika Waefeso 4:15 (Zaire Swahili Bible), ni nini maana ya ‘kuisema kweli’? (b) Kufanya hivyo kunahusianaje na kukomaa kwa Kikristo?

18 Iweje ujenzi ukiisha kufanywa juu ya msingi huo? Paulo anashauri hivi: “Lakini tukisema kweli katika mapendo tupate kukua katika maneno yote ndani yake aliye kichwa, ndiye Kristo.” (Waefeso 4:15, ZSB) Kwanza, tunaona Paulo anataja uhitaji wa ‘kusema kweli.’ Usemi huo kwa wazi unatia mengi zaidi ya kusema tu; kwa kweli unamaanisha ‘kudumisha ukweli.’ (Kingdom Interlinear) Tafsiri nyingine zinaufasiri kwa kusema “ishini kulingana na ukweli”; “fuateni ukweli kwa upendo nyakati zote​—mkisema kwa ukweli, mkishughulika kwa ukweli, mkiishi kwa ukweli”.​—Waefeso 4:15, The Jerusalem Bible; The Living Bible.

19 Kwa hiyo, kufuatia ukomavu wa Kikristo kunataka kwamba tudumishe, au tushikilie, ukweli kwa jinsi tunavyoishi, kusema, kutenda, na kushughulika na wengine. Hiyo maana yake ni kutumia katika mambo yetu ya kila siku maarifa ya Biblia ambayo tumepata na kwa njia hiyo tuje kuwa kati ya wale “ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” (Waebrania 5:14) Je! wewe unafanya hivyo? Je! unawaza kulingana na kanuni za Biblia kila wakati unapokabili uamuzi wa kufanya? Je! wewe unakazania kuwa Mkristo aliyekomaa, anayeshikilia ukweli kwa maneno na kwa matendo, au je, unapendelea tu kubaki ukiwa mtoto wa kiroho, asiye na madaraka na ukiwa huru kufuatia tamaa na mapendezi yako mwenyewe?

20, 21. (a) Upendo unahusikaje katika ukuzi wa kufikia ukomavu? (b) Ni maulizo gani yaliyobaki kuzungumzwa kirefu?

20 Paulo anasema: ‘Katika upendo na tukue hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo.’ (Waefeso 4:15) Hapa, Paulo anataja jambo kuu​—himizo. Kwenye 1 Wakorintho 13:1-3 anaonyesha kwamba kazi ambazo zingaliweza kuwa za thamani zinakuwa zisizo na faida kabisa zikifanywa pasipo himizo linalofaa. Kwa hiyo ni lazima tuchunguze kusudi letu la kila jambo tunalofanya. Je! linafanywa ili tuonwe na wengine, kuwavutia ili wafikiri sisi tumekomaa? Au, je, badala yake linafanywa kwa sababu ya kumpenda Mungu na kupenda jirani yetu? Upendo unapokuwa himizo letu ‘tutakua katika yote,’ tuwe Wakristo waliosawazika, wenye kutegemeka, waliokomaa, wenye kumtambua kwa ukamili “yeye aliye kichwa, Kristo.”

21 Ingawa kujitahidi kufikia kukomaa kwa Kikristo ni mradi unaostahili, huo sio mwisho. Mtu akiisha kufikia mradi huo, je, kuna jambo jingine zaidi analopaswa kufanya? Namna gani wale ambao wamekuwa katika ukweli kwa miaka kadha na wamekwisha kufikia mradi wa ukomavu wa Kikristo. Tutachunguza hayo katika makala itakayofuata.(itaendelezwa)

Je! Wewe Unaweza Kueleza?

◻ Nyingine kati ya “tabia za mtoto” ni gani, nazo zinatokeza hatari gani?

◻ “Umoja wa imani”na“kimo cha Kristo” yanahusianaje na kukomaa?

◻ Ili kufikia kukomaa kwa Kikristo, ni ‘kazi gani zisizo na uhai’ tunazopaswa kuacha?

◻ Mtu ‘anakuaje katika upendo’?

[Blabu katika ukurasa wa 24]

KATIKA MIAKA SITA ILIYOPITA

​—Mashahidi wapya 827,144 walibatizwa

​—Makundi mapya zaidi ya 5,000 yaliundwa

​—Kati ya wale ambao sasa wanashiriki katika kazi ya kuhubiri, mmoja kwa kila watatu alibatizwa katika wakati huo

[Blabu katika ukurasa wa 24]

Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1985, nchi zaidi ya sita zilikuwa na wastani ya wahubiri wa Ufalme zaidi ya 100,000

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wengi leo wanaichagua huduma badala ya kufuatia mambo ya kutafuta mali

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki