Kukomaa kwa Kikristo Ni kwa Lazima Ili Kupata Uzima
“Kesheni, simameni imara katika Imani, fanyeni kiume, mkawe hodari.”—1 Kor. 16:13.
1. Ukuzi unakamatanaje na uhai?
KUKUA ni jambo la kawaida kwa namna zote za kidunia za uhai zilizofanyizwa na zaidi ya chembe moja. Wadudu, ndege, samaki, amphibians (wanyama wawezao kuishi baharini na katika nchi kavu) na mammals (wanyonyeshao watoto wao) wanakuwa na mianzo midogo midogo kisha wanakua mpaka wanafikia kukomaa kwa njia yao iliyowekwa kwa kimungu, ili kulitimiza kusudi ambalo Muumba wao alikuwa nalo katika kuwafanya wawe hai kwa hekima yake isiyo na kikomo. Vile vile, wanadamu hawazaliwi wakiwa watu wazima, kwa kimwili au katika akili. Nasi twatazamia watoto wakue, wafikie hali ya kimwili, ya akili na ya moyoni ya watu wazima wenye madaraka. Kwa wazi, uhai katika mpango wa Mungu wa mambo watia ndani ukuzi.
2. Ni maoni gani yanayofaa juu ya kupata kukomaa kwa kiroho, na kwa sababu gani?
2 Kunao ukuzi wa Wakristo vile vile kutoka utoto wa kiroho kufikia utu mzima wa kiroho, kukomaa kwa Kikristo. Kukomaa huku kwa kiroho siyo mradi usiofikika, wa kuwazia tu, wala si kitu cha kufikiwa na wachache tu. Kama vile kukomaa kwa kimwili kunavyotazamiwa kama pato la kawaida kwa viumbe vilivyo hai, ndivyo na kukomaa kwa kiroho kunavyopaswa kutazamiwa na kutafutwa na kila “mtoto mchanga” wa Kikristo. Kwaweza kupatikana na wote wanaotia jitihada inayotakiwa. Mahali anapokaa mtu, ujuzi, uwezo mbalimbali au hali ya elimu siyo mambo yanayoamua. Mtume Paulo aliwasihi Wakristo ambao walikuwa hawajakuwa watu wazima wa kiroho ‘wasonge mbele hata kukomaa.’ (Ebr. 6:1, NW) Ili wafanye hivyo ilikuwa lazima kwanza wafahamu hali yao ya kiroho ilivyo hasa kisha wajitahidi kufanya maendeleo.
KUTAMBUA KUKOMAA KWA KIROHO
3. Simulia Mkristo asiyekomaa, “wa kimwili.”
3 Kulingana na Biblia, Mkristo asiyekomaa ni “wa kimwili,” yaani, kwa kawaida yeye anatenda kulingana na kanuni zinazofuatwa na wanadamu waliofarikishwa na Mungu na Kristo. Huko nyuma katika karne ya kwanza walikuwako Wakristo hao wasiokomaa katika kundi la Korintho. Paulo hakuweza kuzungumza nao “kama kwa watu wa kiroho,” bali ilimlazimu kusema nao “kama kwa watu wa kimwili, kama kwa watoto wachanga katika Kristo.” Yeye aliwalisha “maziwa” ya ukweli wa Kikristo tu, kwa maana ‘hawakuwa na nguvu za kutosha.’ Kwa sababu ya kuwa “wa kimwili,” wivu, ugomvi na madhehebu zilikuwamo kati yao.—1 Kor. 3:1-4, NW.
4. Twaweza kujiuliza maulizo gani tujue kama tu watu “wa kimwili” au hapana?
4 Je! wo wote kati yetu ndivyo walivyo—wenye kusita-sita, wangali wana maelekeo ya kufuata wanadamu? Je! wengine ni “wa kimwili” au wa kilimwengu katika kuwaza kwao, kwa kawaida wakilaumu-laumu ndugu zao na kazi wanayoifanya kuliko kufanya kazi pamoja nao kwa mapatano chini ya ukichwa wa Kristo? Je! wapo wengine ambao wangali hawajaukuza upendo unaomvuta mtu ajitolee kulijenga kundi la Kikristo? Basi wao wana haja ya kujitahidi wafikie kukomaa kwa Kikristo.
5. Kwa sababu gani mtume Paulo alisihi Wakristo fulani ‘wasonge mbele hata kukomaa’?
5 Vile vile katika karne ya kwanza, Wakristo wengine walikuwa wameshindwa kufanya maendeleo kupita “mambo ya msingi ya matangazo matakatifu ya Mungu.” Ndivyo ilivyokuwa ijapokuwa muda ulikuwa umekwisha pita ambao wangaliweza kuwa wamekua vya kutosha, siyo kuweza kupata imani iliyo imara na iliyokomaa tu, lakini vile vile kuweza kuzipata sifa za kufundisha wengine mambo mengi. Yaangalie maneno makali ya mtume Paulo kwao: “Ijapokuwa inawapasa kuwa waalimu kufikia hapo, ninyi mwahitaji mtu tena wa kuwafundisha tangu mwanzo mambo ya msingi ya matangazo matakatifu ya Mungu; nanyi mmekuwa kama watu wanaohitaji maziwa, siyo chakula kigumu. Kwa maana kila mtu anywaye maziwa halifahamu neno la haki, kwa maana yeye ni mtoto mchanga. Lakini chakula kigumu ni cha watu waliokomaa, cha wale ambao kwa manufaa wamezoezwa uwezo wao wa kufikiri kuweza kupambanua kati ya yaliyo haki na mabaya. Kwa hiyo, kwa kuwa sasa tumeyaacha mafundisho ya msingi juu ya Kristo, ebu na tusonge mbele hata kukomaa, tusiweke msingi tena.”—Ebr. 5:12–6:1, NW.
6. Leo wengine wanawezaje kuwa na haja ya kusihiwa vivyo hivyo?
6 Je! kati yetu wamo wo wote ambao wamekuwa wakishirikiana na kundi la Kikristo miaka mingi na hali hawawezi kufundisha wengine mafundisho ya msingi ya Biblia? Miaka mingi ikiisha kupita ya ushirika na watu wa Mungu, je! wengine wangali na ugumu wa kuacha dhamiri yao itofautishe kati ya yaliyo haki na mabaya? Je! wangali wakitaka wengine wawafanyie maamuzi katika mambo ya dhamiri? Wo wote wanaojikuta wangali wakihitaji maagizo katika mafundisho ya msingi ya Kikristo na maisha wamepaswa bila shaka wawe wakijitahidi kukomaa. Haiwapasi Wakristo kuwa kama wajenzi wasioweza kuendeleza ujenzi wamalizapo msingi, “msingi” kwa habari hii ukiwa ni mafundisho ya msingi juu ya Kristo. Imewapasa wasonge mbele wakalimalize jengo au ujenzi wa juu unaoukalia msingi huo, yaani, mafundisho magumu zaidi juu ya kusudi la Mungu kama linavyofunuliwa kupitia kwa Mwanawe.
7. Kwa sababu gani Mkristo asiyekomaa anayeshindwa kujitahidi akue kwa kiroho yumo hatarini?
7 Mkristo asiyekomaa anayeshindwa kujitahidi awe imara katika imani, asifanye maendeleo zaidi kuliko mambo ya msingi ya Neno la Mungu, yumo katika hatari kubwa. Kwa kweli yeye hana nguvu za kushinda mkazo wa kufanya kosa na kuwaza kwa uongo kwa kilimwengu na kwa hiyo anaweza ‘kusukwa-sukwa kana kwamba na mawimbi’ na kuchukuliwa kwenye msiba. (Efe. 4:14, NW; Ebr. 6:4-8) Wale wanaoendelea kuwa “wa kimwili,” wakiweka wivu moyoni, kijicho na uadui, vile vile wamo hatarini mbele za Yehova Mungu. Maelekeo hayo yamo kati ya matendo ya mwili wenye dhambi yanayoweza kumzuia mtu asipate uzima. Kama vile mtume Paulo alivyoeleza: “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo; katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”—Gal. 5:19-21.
KUFIKIA KUKOMAA KWA KIROHO
8. Ni namna gani ambavyo kufikia kukomaa kwa kiroho kulivyo tofauti na kupata kukomaa kwa kimwili?
8 Lakini mtu awezaje kukoma kuwa “wa kimwili” na kufikia kukomaa kwa kiroho? Tofauti na kukomaa kwa kimwili, ambako kunatokea kwenyewe tu, utu mzima wa kiroho unapatikana kwa jitihada ya unyofu. Inahitaji unyenyekevu na tamaa ya kweli ya kupatanisha maisha ya mtu na mfano uliowekwa kwa Wakristo katika Neno la Mungu. Inatia ndani funzo na kutafakari kuweza kupata ufahamu mwingi wa mapenzi ya Mungu na kusudi, kujifunza kumtegemea yeye kuliko kuwaza kwa kibinadamu. Je! wewe umepata kujitumia hivyo ukifikiria ukuzi wa kiroho? Je! unatenda kulingana na shauri la Maandiko ‘kukesha, kusimama imara katika Imani, kufanya kiume, ukawe hodari’?—1 Kor. 16:13; Ebr. 5:14.
9. Kujifunza Neno la Mungu na kulitumia kuna matokeo gani juu ya “mtoto mchanga” wa Kikristo?
9 Wakati “mtoto mchanga” wa Kikristo anapoendelea kujifunza Maandiko na kuyatumia anayojifunza, maendeleo yake katika ufahamu wa kweli ya Mungu na mafundisho yaliyo magumu zaidi yanafuatana na ukuzi unaolingana katika maoni yake ya kiroho na utu wa Kikristo. Kufikiri kwake na maoni yake na maisha yanakuwa tofauti. Anaona kwamba mapendezi yake na makusudi yanaelekeana na mambo ya kiroho, kwa maana kweli ya Mungu inakuwa na matokeo makubwa na yenye faida maishani mwake. Yeye anafuata onyo kutoka kwa Neno la Mungu ‘kuacha kufuatisha namna ya dunia hii; bali ageuzwe kwa kufanywa upya nia yake, apate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.’—Rum. 12:2.
10. Ni mabadiliko gani yanayotokea wakati Mkristo ambaye ndiyo sasa anakomaa ‘anapofanywa upya nia yake’?
10 Huku ‘kufanya upya nia’ kuna matokeo makubwa katika utu wa Mkristo anayeendelea kukomaa. Mahali pa maoni ya kilimwengu, pamoja na mawazo yake, mkazo wake juu ya mambo ya kimwili na anasa za kilimwengu, panazidi kuchukuliwa na mapendezi ya mambo ya kiroho na ya kufanya mapenzi ya Yehova Mungu. Mahali pa matendo ya mwili, tunda la roho ya Mungu—upendo, furaha, amani, uvumilivu, fadhili, wema, imani, upole na kujiweza—linaonekana zaidi na zaidi. Nguvu mpya au roho yenye nguvu inatenda kazi ndani yake. Yeye analitii shauri la Biblia: “Mpate kuuvua utu wa kale unaofanana na namna ya mwenendo wenu wa zamani na unaoharibika kulingana na tamaa zake za udanganyifu; bali mpate kufanywa wapya katika nguvu yenye kuendesha akili zenu, na kuuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika haki ya kweli na uaminifu.”—Efe. 4:22-24, NW; Gal. 5:19-23.
11. Ni nini “nguvu” inayoendesha akili ya Mkristo aliyekomaa, nayo inamfanya atendeje katika hali zinazohitaji maamuzi ya mambo ya adili?
11 Wakati utu wa kale unapovuliwa na nguvu mpya au roho yenye nguvu inapoendesha akili, Mkristo anakuwa amefikia kukomaa. Hapo kwanza nguvu yenye kuendesha akili yake ndiyo iliyotokezwa na mambo yaliyofundishwa na yakaonwa ulimwenguni. Mambo haya yaliyotiwa akilini yalikuza ndani yake namna fulani za kufikiri na nia ya moyoni. Hivyo, wakati aliposikia jambo lililohitaji uamuzi wa adili, nguvu hii iliyomo akilini mwake ilimwelekeza kwenye upande wa kilimwengu. Lakini, kama Mkristo aliyekomaa, yeye anayo nguvu mpya au roho inayomsukuma kutenda. Kama matokeo ya funzo lake la kawaida na lenye kujawa na sala la Neno la Mungu la kweli na utendaji wa roho ya Mungu, nguvu hii yenye kuendesha inamwelekeza kwenye upande wa haki. Kwa hiyo, wakati anapopelekewa jambo linalotia ndani uamuzi wa adili, akili yake inaelekezwa na hii “nguvu” mpya au nia yenye nguvu kwenye mwendo wa haki, wa kiroho. Hivyo anahifadhi ukamatano mwema na Yehova Mungu naye aweza kuendelea kuwa na uhakika wa kupata thawabu ya uzima wa milele.
12. Ni nini daraka la wazee katika kusaidia washiriki wa kundi wapate kukomaa?
12 Mojawapo ya nia za msingi za kundi la Kikristo, pamoja na ‘vipawa vyake katika wanadamu,’ wazee watumikiao kama wachungaji na waalimu, ni kusaidia wote wafikie kukomaa, wawe imara sana katika kweli ya Kikristo na waishi kupatana nayo. Kwa habari hii, yaangalie maneno ya mtume Paulo katika Waefeso 4:11-15, NW: “Yeye [Yesu Kristo, kichwa cha kundi la Kikristo] alitoa wengine kama mitume, wengine kama manabii, wengine kama wahubiri wa injili, Wengine kama wachungaji na waalimu, kwa kusudi la kuwatengeneza watakatifu upya, kwa ajili ya kazi ya huduma, kwa ajili ya kuujenga mwili wa Kristo, mpaka sote tuufikie umoja katika imani na katika maarifa yaliyo sahihi ya Mwana wa Mungu, tukawe mtu mzima, kufikia kadiri ya maendeleo ya utimilifu wa Kristo; ili kwamba tusiwe watoto wachanga tena, tukisukwa-sukwa kana kwamba na mawimbi na kuchukuliwa huku na huko na kila upepo wa mafundisho kwa njia ya hila ya wanadamu, kwa njia ya ujanja katika kufanya kosa. Lakini tukisema kweli, na tukue kwa upendo katika mambo yote katika yeye ambaye ndiye kichwa, Kristo.” Kwa hiyo, zaidi ya funzo la kipekee na matumizi ya Neno la Mungu, itikio kwa mafundisho ya wazee wa Kikristo yenye msingi wa Biblia laweza kusaidia sana katika kufanya maendeleo hata kukomaa.
HATARI KWA WAKRISTO WALIOKOMAA NA WALE AMBAO NDIYO SASA WANAKOMAA
13. (a) Je! yawezekana kwa Mkristo aliyekomaa kuwa asiyekomaa? (b) Ni nini kinachoweza kumpata Mkristo aliyekomaa asipouangalia mwenendo wake?
13 Wanapokwisha kukomaa, lazima Wakristo wajihadhari wasije wakaharibika au wakawa waasi, Kama vile ambavyo mtu hawezi kuwa mtoto kwa kutenda kitoto, ndivyo na Mkristo aliyekomaa asivyokuwa asiyekomaa kwa kufanya matendo mabaya. Lakini anaweza kupotoka na kupoteza hali yake yenye kibali na Mungu. Kwa hiyo, yawapasa Wakristo wote wayakumbuke maneno yaliyoongozwa na roho ya Mungu: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.”—1 Kor. 10:12.
14. Imewapasa Wakristo wawe watoto wachanga kwa njia gani na wakati ule ule wawe kama watu wazima?
14 Lazima tujihadhari tusiuache ulimwengu uongoze kuwaza kwetu, utie mashaka ndani yake na kutufanya tutende kipumbavu. Biblia inatuonya sisi: “Msiwe watoto katika akili zenu; lakini katika uovu mgeuzwe watoto wachanga, bali katika akili zenu mkawe watu wazima.” (1 Kor. 14:20) Bila shaka Wakristo hawana haja ya kujua namna ya kutenda mabaya, wala haiwapasi kujaribu kujua. Linapokuwa shauri la kufanya shughuli za udanganyifu na wengine, kutenda kama mnafiki, au kufuatia mashirika ya ufisadi au yaliyopotoshwa, inawapasa Wakristo kuwa kama watoto wachanga, safi na wajinga. Na hali imewapasa wawe kama watu wazima walio imara kwa yaliyo haki na siyo kuvutwa kwa vyepesi kwa maneno ya kujipendekeza katika kutofautisha kati ya yaliyo haki na mabaya.
15. “Mashirika mabaya” yanaweza kuwa ya namna gani, na kwa sababu gani hata Mkristo aliyekomaa anaweza kupotoshwa nayo?
15 Kuwaza kuchafu na kwa ufisadi kwa kilimwengu kwaweza kukamharibu hata Mkristo aliyekomaa. Hakuna mtu asiyeweza kushawishika. Lazima wote wapigane na maelekeo yenye dhambi ya mwili na kuepuka mambo yanayochochea tamaa za kimwili. Kwa hiyo, ni hekima kulitii shauri kutoka kwa Neno la Mungu: “Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” (1 Kor. 15:33, NW) Hiyo yamaanisha kuepuka ushirika wa wale wasio na imani, watu wenye maelekeo maovu au tamaa au mwenendo uliopotoshwa—waasherati, wazinzi, wanaume wenye kulalana na wenzao na wanawake wenye kufanya vivyo hivyo, walevi na wakatili. Je! hii vile vile isingetia na kuwaondoa katika mawazo ya mtu kwa kutotafakari juu ya watu wa namna hizo, kwa kutosoma juu yao ujifurahishe, kwa kutokuwatazama katika televisheni ujifurahishe au katika sinema? Vivyo hivyo, matumizi ya usemi wa kishenzi na kufanya mizaha ya matusi na kusimulia hadithi za namna hiyo, ambazo walimwengu wengi wanaziona kuwa mwenendo “wa watu wazima,” yanaweza kudhoofisha Wakristo waliokomaa na kuwadhuru wale wanaojaribu kufikia kukomaa kwa Kikristo. Mambo hayo yamepaswa yaepukwe, kama vile Neno la Mungu linavyoshauri: “Uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi.”—Efe. 5:3, 4; 4:29-31; Kol. 3:5-10.
16. (a) Ni nia gani ya mambo ya kimwili ya kilimwengu ambayo lazima tujihadhari nayo? (b) Kwa sababu gani kujua mambo ya kimwili hayadumu hakutoshi kuweza kushindana na pupa ya fedha?
16 Pupa ya ulimwengu isiyoisha ya fedha na mapato ya kimwili ni jambo jingine ambalo lazima lizuiwe. Lakini, kufahamu utajiri wa mambo ya kimwili haudumu hakutoshi kuweza kushindana na pupa hii. Watu wengi ulimwenguni wanajua sana nao wanakubali kwa hiari kwamba fedha haiwezi kununua mambo yaliyo ya muhimu hasa zaidi ya mahitaji makubwa ya maisha—furaha, afya njema, ufahamu wa kibinadamu. Na hali wanafuatia miradi ya kimwili kwa pupa. Kama Mkristo akiiruhusu roho hii imnase, yaweza kuhatirisha kuthamini kwake mambo ya kiroho bila ya yeye kujua. Yaweza hata kuiharibu imani yake. Biblia inasema hivi: “Shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.”—1 Tim. 6:10.
17. Ni nini ambacho lazima kifanywe ili tujizuie tusije tukaharibiwa na kuhangaikia masumbufu ya maisha au na tamaa ya utajiri?
17 Ili tuzuie hili lisije likatupata, lazima tuendelee kuwaza juu ya ubora mwingi zaidi wa utajiri wa kiroho. Haitupasi tuache hangaiko lisilofaa la mahitaji ya maisha lituondolee matumaini yenye kufariji kwamba Yehova Mungu anawaangalia watu wake. Yesu Kristo alitoa uhakikisho huu: “Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote [chakula, mavazi na mahali pa kukaa]. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe.” (Mt. 6:32-34) Ndiyo, imetupasa turidhishwe na mahitaji ya maisha. Utawa wetu unatuwezesha kufurahia afya ya kiroho na uradhi nao watoa ahadi ya uzima wa milele.—1 Tim. 4:8; 6:6-8.
18. (a) Ni mashaka ya namna gani ambayo huenda yakatokea akilini mwa Wakristo waliokomaa na wale ambao ndiyo sasa wanakomaa? (b) Mashaka hayo yanaweza yakawa na matokeo gani juu ya Mkristo?
18 Mashaka vile vile yanaweza kuwadhuru Wakristo waliokomaa na vile vile wale ambao ndiyo sasa wanakomaa. Nyakati nyingine yawezekana hata Wakristo waliokomaa wasielewe shauri fulani la Maandiko. Kama wakiacha hili liwaondolee amani yao ya akili na uradhi, wanaweza kwa vyepesi kuondoshwa katika jambo lililo la maana hasa, yaani, kumtumikia Yehova Mungu kwa uaminifu. Nyakati nyingine wengine wanaleta makisio yao wenyewe juu ya maelezo ya maandiko fulani. Kwa kuwa kundi la watu wa Mungu leo haliyakubali maelezo hayo kama kweli, wao wanaanza kulalamika na kutia mashaka juu ya kama Yehova anasaidia watu wake kweli. (Linganisha Yohana 6:53, 66-69; Luka 12:42-44.) Tena wengine wanatia mashaka mengi mno juu ya hali au matendo ya waamini fulani wenzao. Wanaanza kuwatazama wanadamu wasiokamilika, kulihukumu kundi zima kuwa ndivyo lilivyo na karibuni wanapoteza furaha yao katika kufundisha wengine kweli. Wanaanza kutia mashaka kwamba wale ambao walifurahia ushirika wa kiroho pamoja nao si watu wa Mungu waliojitoa hasa.—Linganisha Wakolosai 3:13, 14.
19. N’nini kinachoweza kufanywa ikiwa mtu anaanza kuwa na mashaka juu ya kundi la Kikristo?
19 Mashaka ya namna hii yakitokea akilini mwako, waweza kufanya nini? Mwombe Yehova Mungu hekima kwa unyenyekevu. Waweza kuendelea kuwa na uhakika wa kwamba yeye atakupa hekima inayohitajiwa kushindana na hali yo yote yenye kujaribu. Kama vile mwanafunzi Yakobo alivyoandika: “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.” (Yak. 1:5) Vile vile, jifaidi na msaada unaoweza kutolewa na wazee katika kundi la mashahidi wa Yehova wa Kikristo. Kwa kuzungumza na mtu fulani mwenye ufahamu mwema wa Neno la Mungu, mara nyingi utaona kwamba maelezo yake yenye maana yatakusaidia upate tena furaha katika utumishi wako kwa Mungu.
20. Imewapasa Wakristo waliokomaa na ambao ndiyo sasa wanakomaa wafanye nini kwa sababu wanatazamia uzima wa milele?
20 Kwa hiyo, basi, iwapo wengine hawajafikia kukomaa kwa Kikristo, na ‘wasonge mbele’ wakufikie, wakijihadhari na maongozi yasiyofaa ya ulimwengu. Ikiwa sisi tumekwisha kuwa Wakristo waliokomaa, “na tuenende katika lilo hilo,” tusijiachilie tupotoke. Na tukutumie kukomaa kwetu kwa faida, ‘tukifanya kiume, tukawe hodari,’ tukisaidia wengine ambao wangali hawajaufikia mradi wa kukomaa kwa Kikristo, kusudi kwamba sote pamoja tuweze kuufikia mradi wetu wa mwisho—kibali cha Mungu hata uzima wa milele.—Flp. 3:12, 14-16; Gal. 6:1, 2; 1 Kor. 16:13, 14.