Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 10/14 kur. 4-6
  • Jinsi ya Kupata Mafanikio ya Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kupata Mafanikio ya Kweli
  • Amkeni!—2014
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi Unavyoweza Kupata Mafanikio ya Kweli Maishani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Mafanikio ya Kweli Yanapatikana Jinsi Gani?
    Amkeni!—2014
  • Kufanikiwa kwa Gharama Yoyote?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Jinsi Unavyoweza Kufanikiwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2014
g 10/14 kur. 4-6
Charlotte na Timothy

HABARI KUU | MAFANIKIO YA KWELI YANAPATIKANA JINSI GANI?

Jinsi Ya Kupata Mafanikio Ya Kweli

Biblia inawatia moyo watu wawe na maoni yanayofaa kuhusu mafanikio ya kweli. Biblia haisemi kwamba ni watu wachache tu wanaoweza kufanikiwa. Pia, si kama vitabu vinavyowahimiza watu ‘wafuate ndoto zao’ na mambo yatawaendea sawa. Dhana hiyo—ambayo watu wengi wamefundishwa tangu utotoni—huwakatisha tamaa baadaye.

Ukweli ni kwamba, kila mtu anaweza kupata mafanikio ya kweli—lakini inahitaji jitihada. Chunguza kanuni zifuatazo.

  • Sarafu

    BIBLIA INASEMA NINI?

    “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.”—Mhubiri 5:10.

    MAANA YAKE NI NINI? Kuwa na pesa nyingi hakumfanyi mtu aridhike. Mara nyingi huwa ni kinyume. Dakt. Jean M. Twenge anasema hivi katika kitabu chake Generation Me: “Watu ambao malengo yao ni kupata pesa nyingi huwa na wasiwasi na hushuka moyo kuliko wale ambao wanathamini kuwa na uhusiano mzuri na wengine.” Anaongeza hivi: “Utafiti unathibitisha kwamba pesa haziwezi kununua furaha—baada ya kupata vitu unavyohitaji maishani, si lazima upate pesa nyingi ili uridhike.”

    JAMBO LA KUFANYA. Jiwekee lengo lenye kuridhisha zaidi kuliko kutafuta pesa na mali. Yesu alisema hivi: “Mjilinde na kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.”—Luka 12:15.

  • Mtu mwenye kiburi

    BIBLIA INASEMA NINI?

    “Kiburi hutangulia kuanguka, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.” —Methali 16:18.

    MAANA YAKE NI NINI? Kiburi na kujitakia makuu hakuwezi kukusaidia ufanikiwe kikweli. Kitabu kiitwacho, Good to Great kinasema kwamba wasimamizi wa makampuni waliofanikiwa zaidi “ni wenye kiasi na wasiotaka makuu. Kinyume chake, karibu asilimia 66 ya wasimamizi waliotamani sana kutambulika, walisababishia kampuni zao hasara.” Tunajifunza nini? Ukijifikiria kupita kiasi huenda utashindwa, badala ya kufanikiwa.

    JAMBO LA KUFANYA. Badala ya kujitakia makuu, uwe mwenye kiasi. Biblia inasema: “Yeyote akifikiri kuwa yeye ni kitu wakati yeye si kitu, anaidanganya akili yake mwenyewe”—na hayo si mafanikio!—Wagalatia 6:3.

  • Mtu ameshika nyundo

    BIBLIA INASEMA NINI?

    “Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko . . . kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.”—Mhubiri 2:24.

    MAANA YAKE NI NINI? Ukisitawisha mazoea mazuri ya kazi, utafurahia kazi yako. Katika kitabu chake kiitwacho Teach Your Children Well, Dakt. Madeline Levine aliandika hivi: “Ili ufanikiwe kufanya jambo fulani unapaswa kulifanya kwa ustadi, na ili ulifanye kwa ustadi unahitaji bidii na kutokufa moyo.” Hilo linatia ndani kutokata tamaa unapokabiliana na hali ngumu.

    JAMBO LA KUFANYA. Jitahidi kupata ustadi wa kufanya kazi, na unapokabiliana na hali ngumu usikate tamaa. Ikiwa una watoto, wape fursa (kulingana na umri na uwezo wao) ya kutatua matatizo yao. Usifanye haraka kuwasaidia kutatua matatizo yao yote. Vijana huridhika sana—na kupata mazoezi yatakayowasaidia baadaye maishani—wanapositawisha uwezo wa kutokata tamaa.

  • Mbwa

    BIBLIA INASEMA NINI?

    “Mbwa aliye hai ni afadhali kuliko simba aliyekufa.”—Mhubiri 9:4.

    MAANA YAKE NI NINI? Ikiwa umeajiriwa, kazi yako inapaswa kuwa sehemu ya maisha yako, bali si maisha yako yote. Kwa kweli, je, unaweza kusema kwamba una mafanikio ya kweli ikiwa umepata cheo kikubwa kazini lakini afya yako imezorota au familia yako haikuheshimu? Watu wenye mafanikio ya kweli hujitahidi kusawazisha kati ya kazi, afya, na familia zao.

    JAMBO LA KUFANYA. Tunza afya yako. Pumzika vya kutosha. Hakuna faida kufanya kazi kupita kiasi na kupuuza mambo mengine yote kutia ndani afya yako, familia, na marafiki ili tu upate mafanikio.

  • Biblia iliyofunguliwa

    BIBLIA INASEMA NINI?

    “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

    MAANA YAKE NI NINI? Siri ya mafanikio ya kweli ni kusoma Biblia na kutumia yale unayosoma. Kwa kweli, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wamepata mafanikio ya kweli kwa kutanguliza mambo ya kiroho maishani, na hilo limewapunguzia mahangaiko kuhusiana na vitu vya kimwili.—Mathayo 6:31-33.

    JAMBO LA KUFANYA. Jifunze jinsi Biblia inavyoweza kukusaidia kupata mafanikio ya kweli. Ili upate habari zaidi zungumza na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au utembelee Tovuti yetu ya www.jw.org/sw.

“Mwanzoni Sikuwa na Mafanikio Halisi”

Charlotte na Timothy

Timothy na Charlotte walikuwa na nyumba kubwa yenye vyumba vingi. Walikuwa na magari matatu ya kifahari na walitumia pesa nyingi kwenda likizo kila mwaka. Hata hivyo, licha ya mafanikio hayo ya kifedha, waliamua kubadili maisha yao. Mwandishi wa Amkeni! alimhoji Timothy kuhusu kilichofanya wabadili maisha yao.

Mlifanya kazi gani?

Nilifanya kazi ya muziki na uhasibu. Mke wangu Charlotte alikuwa mtaalamu wa tiba na pia alifanya kazi benki. Baadaye, tulifungua sehemu nne za biashara ya kinyozi. Nilionwa kuwa mtu mwenye mafanikio. Kwa kweli, sikufanya kazi sana kwa sababu nilikuwa na wafanyakazi. Hata hivyo, mimi na Charlotte tuliamua kupunguza biashara zetu. Tuliuza mali nyingi.

Kwa nini mlipunguza biashara zenu?

Tuligundua kwamba hatukuwa na mafanikio ya kweli. Msisimuko tuliopata kutokana na kununua vitu vipya ulitoweka haraka, na kutuacha tukiwa tumekata tamaa na wasioridhika.

Mlipataje mafanikio ya kweli?

Kwa sababu mimi ni Shahidi wa Yehova, nilikuwa nimezoea kuhubiri kwa bidii. Ingawa wakati fulani mimi na Charlotte tulitumia saa 70 kila mwezi ili kuhubiri na kuwafundisha wengine Biblia, kazi ya kuhubiri haikuwa muhimu sana maishani mwetu. Kwa hiyo tuliuza biashara zetu na kujitolea kutumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wa walimu wa Biblia. Sasa tunatumikia kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Marekani. Kwa sababu kazi ninayofanya ni sehemu ya utumishi wetu, silipwi mshahara wala kupata sifa. Tunapata mahitaji ya msingi ya maisha. Lakini hilo si jambo kuu maishani mwetu.

Je, unahisi umefanikiwa kuliko mwanzoni?

Naam! Mafanikio yangu ya mwanzoni yalikuwa bandia. Sasa nimeridhika kikweli. Nimeridhika kwa sababu najua kazi yangu inasaidia kufikisha ujumbe wa Biblia kwa watu duniani kote na ujumbe huo unaboresha maisha ya watu.a

a Mashahidi wa Yehova hawalipwi mshahara wanapohubiri au kuwafundisha wengine Biblia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki