Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 2/15 kur. 10-11
  • Mtoto Wako Anapokuuliza Kuhusu Kifo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mtoto Wako Anapokuuliza Kuhusu Kifo
  • Amkeni!—2015
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KIKWAZO
  • Msaidie Mtoto Wako Akabiliane na Huzuni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Kulea Watoto tangu Uchanga
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako
    Amkeni!—2007
  • Mtoto Anapotaka Kujiua
    Msaada kwa Ajili ya Familia
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2015
g 2/15 kur. 10-11
Baba akizungumza na mtoto wake

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA

Mtoto Wako Anapokuuliza Kuhusu Kifo

KIKWAZO

Mtoto wako mwenye umri wa miaka sita anakuuliza hivi: “Kuna siku utakufa?” Huenda ukashangazwa na swali hilo na kujiuliza: ‘Je, mtoto wangu ana umri wa kutosha kuelewa maana ya kifo? Nawezaje kumweleza?’

MAMBO UNAYOPASWA KUJUA

Watoto hufikiria kuhusu kifo. Hata wengine huigiza kama watu waliokufa katika michezo yao. Kwa hiyo, si vibaya kuzungumzia kifo na mtoto wako, na anapokuuliza swali kuhusu kifo uwe tayari kumjibu. Unapozungumza waziwazi kuhusu kifo, unamsaidia mtoto wako kujua jinsi ya kukabiliana na kifo kinapotokea.

Kuzungumza kuhusu kifo hakutamfanya mtoto wako apate mawazo mabaya. Badala yake, kutamsaidia kuondoa hofu. Hata hivyo, utahitaji kumsaidia awe na maoni yanayofaa. Kwa mfano, wataalamu fulani wanasema kwamba watoto wengi wenye umri wa chini ya miaka sita hawaoni kifo kuwa mwisho wa uhai. Kwenye michezo yao, mtoto anaweza kuigiza amekufa na muda mfupi baadaye akawa hai tena.

Lakini, wanapoendelea kukua watoto huanza kuelewa kwamba kifo ni jambo zito. Hali hiyo inaweza kuwafanya waulize maswali mengi na hata kuwa na wasiwasi na kuogopa, hasa ikiwa aliyekufa ni mtu wanayemjua. Kwa hiyo, ni muhimu uzungumze nao kuhusu jambo hili. Marion Haza, mtaalamu wa magonjwa ya akili anasema hivi: “Mtoto ataanza kuwa na wasiwasi kuhusu kifo ikiwa atahisi haruhusiwi kuzungumzia jambo hilo nyumbani.”

Usihangaike sana kuhusu jinsi utakavyosema. Kulingana na utafiti mmoja, watoto hupenda “kusikia ukweli unaosemwa kwa fadhili.” Uwe na uhakika kwamba mtoto wako hatauliza swali hadi unapokuwa tayari kumweleza ukweli.

JAMBO UNALOWEZA KUFANYA

Tumia fursa mbalimbali kumweleza mtoto wako kuhusu kifo. Ikiwa mtoto wako ataona ndege aliyekufa kando ya barabara au mnyama wa kufugwa nyumbani akifa, tumia maswali rahisi kumsaidia aeleze hisia zake. Kwa mfano, unaweza kumwuliza hivi: “Unafikiri mnyama aliyekufa anateseka? Anahisi baridi au njaa? Unajuaje ikiwa mnyama au mtu amekufa?”—Kanuni ya Biblia: Mhubiri 3:1, 7.

Mwambie ukweli. Ikiwa mtu anayemjua au mtu wa ukoo amekufa, epuka kumwambia maneno ya mafumbo kama vile: “Ameenda zake au ameondoka.” Maneno kama hayo yanaweza kumfanya mtoto wako afikiri kwamba mtu aliyekufa atarudi nyumbani hivi karibuni. Badala yake, mweleze ukweli. Kwa mfano, unaweza kumwambia hivi: “Bibi (nyanya) alipokufa, mwili wake uliacha kufanya kazi. Hatuwezi kuzungumza naye, lakini hatutamsahau.”—Kanuni ya Biblia: Waefeso 4:25.

Kwa sababu mtoto anaweza kufikiri kwamba kifo ni kama ugonjwa wa kuambukiza, mwambie sivyo ilivyo

Mfariji mtoto wako. Huenda akafikiri kwamba matendo au mawazo yake yalisababisha kifo cha mtu. Badala ya kumwambia kwamba hakusababisha kifo hicho, unaweza kumwuliza hivi: “Kwa nini unafikiri kwamba wewe ndiye uliyesababisha?” Msikilize kwa makini, na usipuuze hisia zake. Pia, kwa sababu mtoto anaweza kufikiri kwamba kifo ni kama ugonjwa wa kuambukiza, mwambie sivyo ilivyo.

Mruhusu mtoto wako ajieleze. Mwambie mtoto wako kuhusu watu wa familia waliokufa hata ambao hawajui. Unaweza kumsimulia mambo mazuri kuhusu shangazi, mjomba, au babu aliyekufa zamani. Unapozungumza waziwazi kuhusu watu hao, unamsaidia mtoto wako kujua kwamba anaweza kuwafikiria na kuzungumza kuwahusu. Lakini usimlazimishe mtoto wako kuzungumza. Wakati mwingine unahitaji kungoja muda unaofaa zaidi ili kuzungumzia jambo hilo.—Kanuni ya Biblia: Methali 20:5.

Sura ya 34 na 35 kwenye kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu zinaweza kumsaidia mtoto wako kujua yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu kifo. Tafuta kwenye MACHAPISHO > VITABU NA BROSHUA

MAANDIKO MUHIMU

  • “Kuna . . . wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” —Mhubiri 3:1, 7.

  • “Semeni kweli kila mmoja wenu.”—Waefeso 4:25.

  • “Shauri moyoni mwa mtu ni kama kilindi cha maji, lakini mtu mwenye utambuzi ataliteka.”—Methali 20:5.

MAMBO YA KUZINGATIA

Ikiwa mtu amekufa, unaweza kumsaidia mtoto wako asiwe na hofu kupita kiasi kuhusu kifo kwa kuhakikisha anaelewa mambo yafuatayo:

  • Si kwamba na yeye atakufa.

  • Ikiwa siku moja utakufa, hatabaki peke yake; watu wengine wa familia watamtunza.

  • Mtu akifa hateseki.

  • Mtu aliyekufa hatasahauliwa. Unaweza kumwambia hivi: “Hutamwona nyanya (bibi), lakini unaweza kumkumbuka kwenye mawazo yako.”

Kumbuka kwamba kunyamaza tu hakutamwondolea wasiwasi mtoto wako. Badala yake, kutamfanya aendelee kuwana wasiwasi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki