Sura ya 9
Kulea Watoto tangu Uchanga
1-4. Kuna ushuhuda gani unaoonyesha kwamba mtoto mchanga anao uwezo mkubwa wa kujifunza?
AKILI za kitoto kichanga kilichozaliwa sasa hivi zimelinganishwa na ukurasa usioandikwa kitu. Kwa kweli, alama nyingi zilitiwa katika akili za kitoto kichanga hata kilipokuwa bado katika tumbo la uzazi la mama yake. Nazo tabia fulani za utu zinaandikwa bila kufutika ndani yake kwa kurithi. Lakini kuna nafasi kubwa ajabu ya kujifunza tangu wakati wa kuzaliwa na kuendelea. Badala ya kuwa ukurasa mmoja, ni kama vitabu vinavyongojea kuchapwa.
2 Wakati wa kuzaliwa, uzito wa ubongo wa kitoto kichanga ni robo moja ya uzito ule ambao kitakuwa nao kikiwa mtu mzima. Lakini ubongo unakua haraka sana hivi kwamba kwa muda wa miaka miwili tu unakuwa wenye uzito kamili kiasi cha vile atakapokuwa mtu mzima! Akili zinakua haraka. Wachunguzi wanasema kwamba akili za mtoto zinakua haraka sana wakati wa miaka ya kwanza minne ya maisha kama zinavyokua wakati wa miaka kumi na mitatu inayofuata. Kwa kweli, wengine wanaeleza kwamba “mawazo ambayo mtoto anajifunza kabla ya siku yake ya tano ya kuzaliwa, ni kati ya mambo yaliyo magumu zaidi atakayopata wakati wo wote.”
3 Mawazo hayo ya msingi kama vile kuume na kushoto, juu na chini, kujaa na hali tupu, na vilevile kadiri za ukubwa na uzito, yote hayo yanaonekana kuwa mambo ya kawaida sana kwetu. Lakini inampasa mtoto ajifunze hayo na mawazo mengine mengi. Wazo la usemi lapaswa litiwe na kuimarishwa katika akili za kitoto kichanga.
4 Wengine wanaona lugha kuwa “labda jambo la akili ni gumu kuliko yote ambayo mwanadamu ametakiwa kutimiza.” Ikiwa umepata kujaribu sana kujifunza lugha mpya, bila shaka utakubali hivyo. Lakini wewe umeona faida ya kujua namna lugha inavyotenda kazi. Kitoto kichanga hakijui hayo, hata hivyo akili zake zinaweza kufahamu wazo la lugha na kulitumia. Si hayo tu, watoto wenye miaka ya uchanga wanaoishi katika nyumba au katika maeneo ambamo lugha mbili zinatumiwa, wanaweza kusema lugha hizo mbili bila taabu—hata kabla ya kuanza kwenda shuleni! Basi, ziko akili zinazongojea kusitawishwa.
WAKATI WA KUANZA NI MARA HIYO!
5. Ni upesi kadiri gani kulea mtoto kumepaswa kuanza?
5 Akimwandikia Timotheo mtumishi mwenzake, mtume Paulo alimkumbusha kwamba alikuwa ameyajua maandiko matakatifu “tangu utoto.” (2 Timotheo 3: 15) Mzazi anayejua uhitaji wa akili wa mtoto wa kujifunza, ni mzazi mwenye hekima. Vitoto vichanga ni vyenye kuchunguza sana, vinatumia macho na masikio yote. Kwamba wazazi wanajua hivyo au hawajui, watoto ni wenye bidii katika kujifunza habari, wanaiweka akilini mwao, wakiiongeza na kukata mashauri. Kwa kweli, wazazi wasipokuwa waangalifu, huenda kwa muda mfupi kitoto kichanga kikajifunza kwa njia ya ajabu sana namna ya kuwaongoza kulingana na vile kinavyotaka. Basi, onyo hili la upole linalotolewa katika Neno la Mungu linatumika tangu kuzaliwa na kuendelea: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Bila shaka, mafundisho ya kwanza ni juu ya upendo pamoja na utunzaji mwingi wa upendo na shauku. Lakini pamoja na hayo, ni lazima kuweko kukaripia kunakotumiwa kwa upole lakini kwa uthabiti (imara).
6. (a) Inafaa zaidi kusema na mtoto kwa usemi wa namna gani? (b) Maulizo mengi ambayo huenda mtoto akatokeza yaonweje?
6 Sema na kitoto, si katika “usemi wa kitoto” bali katika usemi wa mtu mzima unaofahamika, na huo ndio unataka ajifunze. Mtoto mdogo anapojifunza kusema atakusumbua kwa maulizo mengi kama: ‘Kwa sababu gani mvua inakunya? Mimi nilitoka wapi? Wakati wa mchana nyota zinakwenda wapi? Unafanya nini? Sababu gani hili? Sababu gani lile?’ Maulizo yanatokea bila mwisho! Yasikilize, kwa maana maulizo ni kati ya vyombo bora zaidi ambavyo mtoto anatumia ili ajifunze mambo. Kuzuia maulizo kunaweza kuzuia maendeleo ya akili.
7. Maulizo ya mtoto mchanga yanaweza kujibiwaje kwa njia inayofaa zaidi, na kwa sababu gani?
7 Lakini ukumbuke, kama mtume alivyokumbuka, kwamba “nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga.” (1 Wakorintho 13: 11) Yajibu maulizo hayo kwa kadiri uwezavyo, lakini kwa kueleweka na kwa ufupi. Mtoto anapouliza, ‘Sababu gani mvua inakunya?’ hataki jibu gumu na lenye maneno mengi. Jibu kama hili. ‘Mawingu yanalemewa na maji kisha maji hayo yanaanguka,’ laweza kutosha. Mtoto ana muda mfupi wa kusikiliza; upesi anakwenda kwenye mambo mengine. Kwa hiyo kama vile unavyompa mtoto maziwa mpaka anapofanya maendeleo ya kupata vyakula vigumu, vivyo hivyo mpe habari nyepesi mpaka atakapoweza kufahamu maarifa yenye mambo magumu.—Linganisha Waebrania 5:13, 14.
8, 9. Ni jambo gani ambalo lingeweza kufanywa ili kumfundisha mtoto kusoma hatua kwa hatua?
8 Mtoto anapaswa ajifunze mambo hatua kwa hatua. Kama tulivyokwisha kutaja, Timotheo aliyajua Maandiko tangu utoto. Kwa wazi mambo ya kwanza kabisa ambayo alikumbuka tangu utoto ni pamoja na mafundisho aliyopewa kutoka Biblia. Bila shaka hayo yalitolewa hatua kwa hatua, kama vile baba au mama leo angeanza kumfundisha mtoto ajue kusoma. Msomee mtoto wako. Wakati yeye angali kitoto kichanga, mpakate (mshike mapajani), na mkono wako ukiwa umewekwa kumzunguka umsomee kwa sauti yenye kupendeza. Atajisikia kuchangamka na hali ya usalama na furaha, na kusoma huko kutafurahisha, hata kama anafahamu machache tu. Labda baadaye, unaweza kumfundisha herufi za A, B, C, D mpaka Z, labda ukifanya kama mchezo. Kisha upange maneno, na mwishowe yafanye maneno hayo kuwa sentensi. Tena kufanye kujifunza kufurahishe kadiri iwezekanavyo.
9 Kwa mfano, mume na mke walikuwa wakisoma kwa sauti pamoja na mtoto wao mwenye umri wa miaka mitatu, wakimweleza mtoto kila neno ili apate kufuata wakati walipokuwa wakiendelea kusoma. Walikuwa wakisimama penye maneno fulani, naye mtoto akataja maneno kama vile “Mungu,” “Yesu,” “mtu,” “mti.” Polepole yale maneno aliyoweza kusoma yaliongezeka, na alipokuwa mwenye umri wa miaka minne alikuwa akisoma karibu maneno yote. Kusona kunafuatana na kuandika, kwanza herufi moja moja, kisha maneno kamili. Mtoto anafurahi sana akiandika jina lake mwenyewe!
10. Sababu gani ni jambo la hekima kumsaidia kila mtoto asitawishe uwezo wake mwenyewe?
10 Kila mtoto ni tofauti, na anao utu wa peke yake, naye amepaswa asaidiwe kukua kupatana na uwezo wake na majaliwa (vipawa) yake aliyorithi. Ukimfundisha kila mtoto asitawishe nguvu na uwezo wake aliorithi, hataona lazima ya kuonea wivu mambo ambayo watoto wengine wanatimiza. Yafaa kila mtoto apendwe na kuonwa peke yake kuwa ana faida. Unapomsaidia mtoto ashinde maelekeo mabaya, usijaribu kumlazimisha mtoto afuate mfano fulani uliotangulia kukusudiwa. Badala yake, mwongoze atumie vizuri zaidi tabia za utu wake kwa faida yake mwenyewe.
11. Kwa sababu gani si jambo la hekima kumlinganisha mtoto mmoja isivyofaa na mwenzake?
11 Mzazi anaweza kusitawisha roho ya kushindana kwa choyo kwa kuonyesha ama ukubwa ama udogo wa mtoto mmoja akilinganishwa na mwenzake. Ijapokuwa wakati wa uchanga watoto wadogo wanaonyesha ishara za choyo walichozaliwa nacho, mwanzoni hawana mawazo ya cheo, ya ukubwa, na ya kujiona kuwa bora. Ndiyo sababu Yesu aliweza kutumia mtoto mdogo awe mfano wa kuondoa roho mbaya ya kutaka makuu na kutamani sana cheo ambayo wanafunzi wake walionyesha pindi fulani. (Mathayo 18:1-4) Kwa hiyo, epuka kumlinganisha mtoto mmoja isivyofaa na mwenzake. Huenda mtoto huyo akadhani kwamba hiyo inaonyesha anakataliwa. Kwanza ataudhika, na akiendelea kutendewa hivyo, inaelekea kwamba atakuwa na uadui. Kwa upande mwingine, mtoto anayeonyeshwa kuwa mkubwa (bora) kuliko mwenzake anaweza kuwa mwenye kiburi na hiyo inaweza kutokeza hali ya kuchukia wengine. Kama mzazi, upendo wake na ukubali wako haupaswi hata kidogo kutegemea namna mtoto mmoja anavyolingana na mwenzake. Hali tofauti inapendeza. Jamii ya wapiga muziki wana vyombo vya muziki vya namna nyingi vipate kuongeza namna tofauti na uzuri, hata hivyo vyote vinapatana. Nyutu zilizo tofauti zinaongezea mpango wa jamaa hali nzuri na yenye kupendeza, hata hivyo upatano hautaharibiwa wakati wote wanapofuata kanuni za haki za Muumba wao.
MSAIDIE MTOTO WAKO APATE KUKUA
12. Ni mambo gani ya hakika juu ya watu wazima yanayoonyesha kwamba mtoto anahitaji uongozi unaofaa?
12 Neno la Mungu linasema kwamba ‘kuelekeza hatua za mwanadamu si katika uwezo wake.’ (Yeremia 10:23) Wanadamu wanasema anao uwezo huo. Kwa hiyo wanakataa uongozi wa kimungu, wanakubali uongozi wa kibinadamu, wanaingia katika taabu hii na taabu hii, na mwishowe kuonyesha kwamba Mungu ni wa kweli. Yehova Mungu anasema kwamba kuna njia inayoonekana kuwa sawa machoni pa mwanadamu, lakini mwisho wake ni njia ya mauti. (Mithali 14:12) Kwa muda mrefu wanadamu wamefuata njia ambayo imeonekana kuwa sawa kwao, nayo imeongoza kwenye vita, njaa, magonjwa na mauti. Ikiwa njia inayoonekana kuwa sawa kwa mtu mzima na mwenye ujuzi, mwisho wake unakuwa mauti, basi mwisho wa njia inayoonekana kuwa sawa kwa mtoto mdogo unawezaje kuwa tofauti? Ikiwa si juu ya mwanadamu anayetembea kuelekeza hatua zake, mtoto mdogo anayejifunza kutembea anawezaje kuelekeza njia yake ya uzima? Muumba anampa mzazi na mtoto maongozi kupitia kwa Neno Lake.
13, 14. Wazazi wanaweza kufundishaje watoto, kupatana na shauri la upole linalopatikana katika Kumbukumbu la Torati 6:6, 7?
13 Mungu anawaambia wazazi hivi: “Maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Maagizo yamepaswa yatolewe nyakati zo zote, wakati wo wote nafasi zinazofaa zinapotokea. Ikiwa jamaa inakula kiamshakinywa pamoja, hata ijapokuwa huenda kwa wengi asubuhi ikawa wakati wa haraka wa kujitayarisha waende kazini au shuleni, toleo la shukrani juu ya chakula litaelekeza mawazo kwa Muumba nalo laweza kutia mambo mengine yenye faida ya kiroho kwa jamaa. Huenda nafasi ikaruhusu maelezo fulani yatolewe juu ya kazi zitakazofanywa siku hiyo au juu ya shule na shauri jema juu ya kushindana na magumu yanayoelekea kutokea. Wakati “ulalapo,” unaweza kuwa wakati wenye furaha kwa watoto wadogo ikiwa wazazi wanawaangalia zaidi. Hadithi za wakati wa kulala zinaweza kupendeza sana watoto, nazo zaweza kuwa njia nzuri ya kufundisha. Biblia imejaa habari inayohitaji ufundi tu na uchangamshi wa wazazi ili kuifanya imfurahishe sana mtoto. Mambo yaliyotukia katika maisha yako mwenyewe yatapendeza watoto wako kwa njia ya pekee, tena yanaweza kukazia mafundisho fulani yaliyo mema. Ijapokuwa huenda ikaonekana kuwa vigumu kuona hadithi mpya utaona kwamba njia za kupashana habari pamoja na watoto wako zitapatikana zaidi ili zitumiwe wakati huo wa ziada. Kusali pamoja na watoto wakati wa kulala kunaweza kusaidia vilevile kuimarisha njia ya mapema ya kupashana habari na Yeye awezaye kuwaongoza na kuwalinda sana.—Waefeso 3:20; Wafilipi 4:6, 7.
14 Po pote ulipo, “uketipo katika nyumba yako” au “utembeapo njiani,” unazo nafasi za kumfundisha mtoto wako njia zenye kupendeza na zenye kufaa. Kwa watoto, mengine ya hayo yaweza kutolewa kwa namna ya mchezo fulani. Mume na mke walisimulia hivi namna hilo lilivyoleta matokeo ya kusaidia watoto wakumbuke mambo waliyojifunza kwenye mkutano ili wayatumie katika funzo la Biblia:
‘Jioni moja tulichukua mtoto wa kiume mwenye umri wa miaka sita, ambaye kwa kawaida hasikilizi sana katika mikutano. Tulipokuwa tukienda kwenye jumba, nilimwambia hivi: “Na tucheze mchezo fulani. Tutakaporudi nyumbani, tutaona ikiwa tunaweza kuzikumbuka nyimbo zilizoimbwa na mengine kati ya mambo makuu yaliyozungumzwa katika mkutano.” Tulipofika nyumbani, tulistaajabu. Mtoto huyo wa kiume wa mwisho, ambaye kwa kawaida hasikilizi sana, alipewa nafasi ya kwanza azungumze naye akakumbuka mengi kati ya mambo yaliyozungumzwa. Kisha watoto wetu wakaongeza maelezo yao na mwishowe sisi watu wazima wawili tukatoa maelezo. Badala ya kuwa kazi ngumu, walifurahia.’
15. Mtoto anaweza kutiwaje moyo atengeneze vizuri zaidi mambo yake anayofanya?
15 Mtoto anapoendelea kukua, atajifunza kusema mawazo, kuchora vitu, kufanya kazi fulani, kupiga muziki fulani katika kinanda. Anataka kutimiza jambo fulani. Kwa njia hiyo kazi yake inakuwa njia ya kujiendeleza mwenyewe. Ni kazi ambayo yeye mwenyewe amefanya. Ukitazama na kusema ‘Umefanya vema,’ mtoto anafurahi sana. Ukitafuta jambo fulani katika kazi yake unaloweza kusifu kwa unyofu wa moyo, naye atatiwa moyo. Ukimwambia kwamba umefanya vibaya sana, naye ataelekea kukosa furaha na kuvunjika moyo. Uliza juu ya sehemu fulani ya kazi hiyo ikiwa lazima, lakini ulizo hilo lisiwe kama linaonyesha kwamba kazi yake haifai. Kwa mfano, badala ya kuchukua picha ambapo amechora na kuzichora upya, labda unaweza kuonyesha uchoraji mzuri zaidi katika kipande kingine cha karatasi. Kufanya hivyo kunamruhusu ageuze mchoro wake ikiwa anataka. Kwa kumtia moyo ajitahidi, unatia moyo ukuzi wake; kwa kumlaumu vikali, huenda ukamvunja moyo au kuzuia tamaa yake ya kuendelea kujaribu. Ndiyo, kanuni iliyo katika Wagalatia 6: 4, NW inaweza kuwapasa watoto vilevile: “Na achunguze ili none namna kazi yake mwenyewe ilivyo, na hapo ndipo yeye peke yake atakapokuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe, wala si kwa kulinganishwa na mtu mwingine.” Sana sana, mtoto anapojitahidi mara ya kwanza, anapaswa atiwe moyo. Ikiwa kazi hiyo ni nzuri kwa kadiri ya umri wake, isifu! Ikiwa si nzuri, sifu jitihada yake, umtie moyo ajaribu kuifanya tena. Ingawaje, hakutembea mara ya kwanza alipojaribu hivyo.
NAWEZA KUELEZAJE NGONO?
16. Kulingana na yale ambayo Biblia inasema, ni majibu gani ambayo yamepaswa yatolewe kwa maulizo ya mtoto juu ya ngono?
16 Ukijibu maulizo ya mtoto wako, unamtia moyo apashane habari na wewe. Lakini ndipo unapoulizwa ghafula (bila kutazamia) juu ya ngono. Je! unajibu waziwazi au unatoa jibu la kudanganya, kama vile kusema kwamba ndugu yako au dada yako mchanga alinunuliwa katika hospitali? Je! utatoa habari ya kweli au utawaacha watoto wapate majibu yasiyofaa, hata yenye makosa, labda katika njia ya matusi, kutoka kwa watoto wenye umri wa kuwapita? Biblia ina habari zinazotaja mambo mengi kidogo yanayohusiana na ngono au viungo vya uzazi. (Mwanzo 17:11; 18: 11; 30:16, 17; Mambo ya Walawi 15:2) Alipokuwa akiwaagiza watu wake juu ya makusanyiko ambapo Neno lake lilipaswa lisomwe, Mungu alisema hivi: “Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto . . . wapate kusikia na kujifunza.” (Kumbukumbu la Torati 31:12) Kwa hiyo watoto wadogo wangesikia habari zo zote hizo, kwa makini, kwa heshima, wala si kwa kusikia mazungumzo ya watoto wenzao.
17-19. Maelezo juu ya ngono yanaweza kuelezwaje hatua kwa hatua?
17 Kwa kweli, si lazima iwe vigumu kueleza ngono kama wazazi wengi wanavyowaza. Watoto wanajua habari ya miili yao mapema sana, wakichunguza sehemu zake mbalimbali. Mtajie mtoto sehemu hizo hivi: mikono, miguu, pua, tumbo, matako, mboo, kuma. Mtoto mdogo haoni haya, isipokuwa wewe ukivifanya viungo hivyo vya mwili kuwa vitu vya siri ambavyo ni mwiko kuvitaja. Jambo linaloogopesha wazazi ni kwamba wanadhani itawapasa kueleza kila kitu, maulizo yakiisha kuanza. Kwa kweli, maulizo yanatokea kidogo kidogo, wakati mtoto anapofikia umri mbalimbali wa kukua kwake. Wakati umri mbalimbali unapofikiwa, itakupasa tu umpe maneno yanayofaa kutumiwa na maelezo mbalimbali yaliyo mepesi sana.
18 Kwa mfano, siku moja ukiulizwa hivi, ‘Watoto wachanga wanatoka wapi?’ Unaweza kujibu kwa vyepesi tu kwa kusema kama hivi: ‘Wanakua ndani ya matumbo ya mama ma.’ Kwa kawaida, hili ndilo linalotakiwa tu kwa sasa. Huenda baadaye mtoto wako akauliza hivi, ‘Mtoto mchanga anatokaje?’ ‘Kuna mlango wake wa pekee wa kutokea.’ Na kwa kawaida hilo litamtosha kwa sasa.
19 Huenda wakati mwingine baadaye likatokea ulizo hivi, ‘Kitoto kichanga kinaanzishwaje?’ Labda jibu lako laweza kuwa hivi: ‘Baba na mama wanataka kuwa na mtoto. Mbegu kutoka kwa baba inakutana na yai lililo ndani ya tumbo la uzazi la mama kisha kitoto kichanga kinaanza kukua, kama vile mbegu katika udongo inavyokua na kuwa ua au mti.’ Kwa hiyo, ni hadithi inayoendelezwa, kila sehemu yake ikiwa inamtosha mtoto kwa wakati huo. Huenda baadaye mtoto akauliza hivi, ‘Mbegu ya baba inaingiaje ndani ya tumbo la uzazi la mama?’ Labda unaweza kusema tu hivi: ‘Unajua namna mtoto wa kiume alivyo. Ana mboo. Mtoto wa kike ana mlango katika mwili wake ambamo mboo inaingia sawasawa. Mbegu hiyo inapandwa. Watu wameumbwa hivyo ili vitoto vichanga vianzishwe na kukuzwa ndani ya mama zao, na mwishowe kitoto kichanga kinatokea.’
20. Sababu gani inafaa wazazi ndio wawaeleze watoto wao mambo ya ngono?
20 Bila shaka hiyo ndiyo njia bora ya kumweleza mtoto kweli kuliko kutoa hadithi za uongo, au kuvifanya viungo hivyo vya mwili kuwa vitu vya siri ambavyo ni mwiko kabisa kuvitaja wala kuzungumza habari zake. (Linganisha Tito 1:15) Ni afadhali vilevile mtoto kusikia mambo hayo ya hakika kutoka kwa wazazi wake, wanaoweza kutoa maelezo pamoja na sababu zinazoonyesha kwa nini vitoto vichanga vimepaswa vizaliwe kwa kufaa na watu waliooana peke yao, wanaopendana na ambao wamelikubali daraka la kumpenda na kumtunza mtoto mchanga. Jambo hilo linayafanya mazungumzo hayo yawe katika hali nzuri na ya kiroho, badala ya kujulikana kuwa machafu kabisa.
KUTOA MASOMO YA MAANA SANA YA MAISHA
21. Ni kwa sababu ya maelekeo gani katika watoto inafaa sana wazazi wawekee wazao wao mfano mwema?
21 Wakati mmoja Yesu alifananisha watu wa wakati wake na “watoto wanaokaa sokoni, wanaowaita wenzao, wakisema, Tuliwapigia filimbi, wala hamkucheza ; tuliomboleza, wala hamkulia.” (Mathayo 11:16, 17) Michezo ya watoto ilikuwa kama ya watu wazima pamoja na sikukuu na mazishi yao. Kwa sababu ya maelekeo ya asili ya mtoto kutaka kuiga watu, mfano wa wazazi unatimiza daraka lenye nguvu katika kulea mtoto.
22. Ni matokeo gani ya mwenendo wa wazazi yanayoweza kuwa juu ya watoto wao?
22 Kitoto chako kichanga kinajifunza kwako tangu wakati wa kuzaliwa—si kwa jambo unalosema tu, bali kwa namna unavyolisema, kwa namna ya sauti unayotumia katika kuzungumza: na kitoto chenyewe, na mwenzi wako na watu wengine. Kinatazama namna wazazi wanavyotendeana, wanavyotendea washiriki wengine wa jamaa na wanavyowatendea wageni. Mfano wako katika mambo hayo unaweza kuanza kutoa masomo yaliyo ya maana sana kuliko mtoto wako anavyojifunza kutembea au kuhesabu au kujifunza herufi za ABC. Unaweza kuweka msingi wa maarifa na ufahamu unaoongoza kwenye furaha za kweli katika maisha. Mfano huo unaweza kumfanya mtoto awe mwelekevu wa kupashana habari za kanuni za haki wakati atakapokuwa na umri wa kutosha kujifunza kwa kusema na kwa kusoma.
23, 24. Ikiwa wazazi wanataka watoto wafuate kanuni fulani, wao wenyewe inawapasa wawe tayari kufanya nini?
23 ”Mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; mkaenende katika upendo,” hayo ndiyo maneno ya mtume yenye kutia moyo Wakristo. Kabla hajasema hayo, alionyesha yaliyotakiwa katika kumfuata Mungu, akisema: “Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya; tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi. Hivyo mfuateni Mungu kama watoto wanaopendwa . . . ” (Waefeso 4:31, 32; 5:1, 2) Ikiwa sauti ambazo kitoto kichanga kinasikia, au matendo ambayo kinaona, yanatoa mafundisho kwa hasira, kama vile kusema kwa sauti kuu yenye kuchukiza, manung’uniko-manung’uniko, kiburi au hamaki, alama ambayo si vyepesi kufutwa inafanyizwa. Ikiwa wewe unaonyesha wote fadhili na huruma, ikiwa mwenendo wako ni mwema na kanuni zako ni njema, basi mtoto wako ataelekea kukuiga katika hilo. Tenda kama unavyotaka watoto wako watende, uwe kama unavyotaka watoto wako wawe.
24 Haiwapasi wazazi wawe na kanuni za namna mbili, namna moja ya kusema, nyingine ya kutenda, namna moja ya kufuatwa na watoto wao, na nyingine ni yao wenyewe. Kuna faida gani kuwaambia watoto wako wasiseme uongo, ikiwa wewe mwenyewe unasema uongo? Ukivunja ahadi zako ulizoahidiana nao, je! unaweza kuwatazamia kutimiza ahadi zao wanazoahidiana nawe? Ikiwa wazazi hawaheshimiani, wanawezaje kutazamia watoto wao kujifunza kuheshimu? Ikiwa mtoto hasikii hata wakati mmoja baba yake au mama yake akionyesha unyenyekevu, anawezaje kuwa mnyenyekevu? Hatari nzito inayoweza kutokea mzazi akitoa wazo la kuonyesha kwamba yeye yuko sawa nyakati zote, ni kwamba huenda mtoto huyo akadhani kwamba kila jambo ambalo mzazi anafanya ni sawa —hata mzazi anapofanya mambo yenye makosa na kuonyesha tabia yenye dhambi. Kusema bila kufanya ni kama Mafarisayo wanafiki (wadanganyifu), ambao Yesu aliambia hivi: “Yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi.” Basi, wazazi, ikiwa hamtaki watoto wenu wawe Mafarisayo wadogo katika jamaa yenu, msiwe Mafarisayo wakubwa!—Mathayo 23:3.
25. Watoto wamepaswa wafundishweje juu ya upendo?
25 Kwanza, watoto wanajifunza upendo kwa kuutazama ukionyeshwa, kisha wanajifunza kutoa upendo huo kwa kuupokea. Upendo hauwezi kununuliwa. Huenda wazazi wakawapa watoto wao zawadi nyingi sana. Lakini kwanza upendo ni jambo la kiroho, la moyoni wala si jambo linalonunulika, nazo zawadi peke yake haziwezi hata kidogo kuwa badala ya upendo wa kweli. Kujaribu kununua upendo ni kuuondolea thamani yake. Zaidi ya zawadi za kimwili, jitoe mwenyewe, toa wakati wako, nguvu zako, upendo wako. Utapokea kadiri iyo hiyo. (Luka 6:38) Kama 1 Yohana 4:19 isemavyo juu ya upendo wetu kwa Mungu: “Sisi twapenda kwa maana yeye alitupenda sisi kwanza.”
26, 27. Watoto wanaweza kufundishwaje furaha inayotokana na kutoa?
26 Watoto wanaweza kujifunza kutoa kwa kupokea. Wanaweza kusaidiwa kujifunza furaha za kutoa, za kutumikia, za kugawia wengine vitu. Wasaidie wajue kwamba kuna furaha katika kutoa—kukupa wewe, kuwapa watoto wenzao, kuwapa watu wazima. Mara nyingi watu wazima hawataki kupokea zawadi kutoka kwa watoto, wakidhani kwa makosa kwamba kuonyesha upendo ni kuwaacha watoto wakae na zawadi ambazo wangetaka kutoa. Mtu mmoja alisema hivi:
“Wakati mtoto alipokuwa akinipa peremende, nilikuwa nikikataa. Nilidhani nilikuwa mwenye fadhili kwa kufanya hivyo, yaani, kukataa kupokea kitu ambacho nilijua akipenda sana sana. Lakini nilipokataa kupokea nikimwachia ale peke yake, sikuiona furaha niliyofikiri mtoto huyo angeonyesha. Ndipo nilipofahamu kwamba kumbe nilikuwa nikikataa ukarimu wake, nikikataa zawadi yake, na kumkataa yeye. Tokea hapo nilianza kupokea sikuzote zawadi hizo, ili nimjulishe furaha za kutoa.”
27 Wazazi katika jamaa moja walitaka wamsaidie mtoto wao mdogo wa kiume awe kama wale wanaosimuliwa katika Biblia katika 1 Timotheo 6:18, “tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine.” Basi, walipokuwa wakihudhuria funzo la Biblia, walikuwa wakichukua fedha ambazo wangetaka kutoa mchango na kumpa mtoto wao wa kiume, wakimwacha atumbukize katika kisanduku cha michango. Jambo hilo lilisaidia kumwonyesha kwa mkazo ubora wa kusaidia mambo ya kiroho na kusaidia kutoa mahitaji yo yote ya kimwili yanayoweza kuhusiana nayo.
28, 29. Watoto wanaweza kufundishwaje maana ya kuomba radhi! (msamaha) kwa makosa yao?
28 Kama vile watoto wanavyoweza kujifunza kupenda na kuwa wakarimu ikiwa mafundisho mema yanafuatana na mfano mwema, vivyo hivyo wanaweza kujifunza kuomba radhi (msamaha) inapofaa. Mzazi mmoja alisema hivi: “Ninapowakosea watoto wangu, ninakiri kosa hilo kwao. Ninawaambia kifupi sana kwa nini nilikosea na kukubali kwamba nilikosa. Kwa njia hiyo, inakuwa vyepesi zaidi kwao vilevile kukiri makosa yao kwangu, wakijua kwamba mimi si mkamilifu, nami nitafahamu.” Linaloonyesha mfano wa maoni hayo ni kisa (jambo) kilichotukia wakati mgeni alipokuwa akitembelea jamaa moja, naye baba alikuwa akimjulisha mgeni huyo watu wa jamaa yake. Mgeni huyo alieleza hivi:
“Nilijulishwa wote waliokuwapo, kisha mtoto mdogo wa kiume mwenye furaha akaingia chumbani. Baba akasema, ‘Na huyu ni mwana wetu wa mwisho, huyo mwenye shati lenye kupakwa uchafu.’ Ile furaha ya mwana huyo ikapotea, akageuka uso wake, ukawa wenye kuchukizwa. Baba alipoona hali hiyo ya kuudhika ikiwa karibu kutokeza machozi, alimvuta mtoto huyo upesi kwake akasema, ‘Haingenipasa kusema hivyo; nasikitika.’ Mtoto huyo alipiga kwikwi kidogo, kisha akaondoka chumbani, lakini alirudi upesi, akiwa mwenye furaha nyingi hata zaidi—naye alikuwa amevaa shati safi.”
29 Bila shaka vifungo vya upendo vinatiwa nguvu na unyenyekevu huo. Ndiyo, baadaye mzazi anaweza kumweleza mtoto namna ya kuwa na maoni yaliyosawazika juu ya magumu ya maisha, makubwa na madogo. Anaweza kusaidia watoto wake wajifunze kutokuyaona mambo madogo kwa uzito mno, waweze kujichunguza wenyewe wala wasitazamie hata kidogo wengine kuwa wakamilifu kama wao wasivyotaka watazamiwe kuwa hivyo.
TOA KANUNI BORA
30-32. Sababu gani inawafaa sana wazazi waanze mapema sana kusaidia watoto wao wajue kanuni bora maishani?
30 Leo wazazi wengi hawajui sawasawa zilizo kanuni bora za maisha kwa sababu hiyo, watoto wengi hawapewi kanuni bora hata kidogo. Wazazi fulani hawana hata hakika kama wanayo haki ya kutengeneza nia za watoto wao. Ikiwa wazazi hawatengenezi nia za watoto wao, watoto wengine, jirani, sinema na televisheni zitatengeneza. Kutopashana habari kwa wazazi na watoto, uasi wa vijana, dawa za kulevya, adili mpya na uasherati—yote hayo yanaogopesha sana wazazi. Lakini kweli ni, utu wa mtoto umekwisha kusitawi tayari kabla magumu hayo hayajatokea katika maisha yake.
31 Uchunguzi ulioripotiwa katika gazeti moja la kisayansi unasema kwamba “sehemu kubwa ya utu wa kila mtu inaimarishwa kabla ya kuanza kwenda shuleni. Bila shaka inajulikana na watu wengi kwamba watoto ambao bado kuanza kwenda shuleni ni rahisi sana kuongozwa, tena ni rahisi kuwafanya watii. . . . Walakini, tumepata kuona kwamba nia na matukio ambayo wamepatwa nayo katika utoto wao, mara nyingi yanaimarisha mienendo ya kufuata yenye kuendelea muda mrefu na ambayo mara nyingine haiwezi kugeuzwa.”
32 Mifano mibaya inaweza kugeuzwa, lakini mchunguzi mwingine anaeleza yanayotukia ikiwa miaka bora inaachwa ipite bure tu: “Mtoto anaendelea kuwa rahisi kuongozwa wakati wa miaka yake ya kuanza saba, lakini kadiri unavyozidi kukawia, ndivyo inavyozidi kuwa vigumu sana kugeuza hali yake—nao uwezekano huo wa kumgeuza unazidi kuwa mdogo sana kila mwaka unaofuata.”
33. Ni mawazo gani yaliyo ya maana sana kuliko yote ambayo watoto wamepaswa wafundishwe?
33 Inawapasa watoto wadogo wajifunze mawazo mengi ya msingi, lakini mawazo yenye maana kubwa kuliko yote ni yale ya mambo yaliyo ya kweli na yaliyo uongo, yaliyo sawa na yasiyo sawa. Akiwaandikia Wakristo Waefeso, mtume Paulo aliwasihi wapate maarifa sahihi, akisema, “tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu. Lakini tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo.” (Waefeso 4:13-15) Wazazi wakikawia kusaidia watoto wao wasitawishe kupenda kweli na unyofu, kupenda yaliyo haki na yaliyo mema, watoto wataachwa bila ulinzi juu ya makosa na mabaya. Miaka hiyo ya kabla ya kuanza kwenda shuleni inamalizika hata kabla wazazi hawajajua. Usiache miaka hiyo ipite bure tu; itumie pamoja na watoto wako ile michache ya kwanza, miaka yenye maana, miaka ambayo tabia za watoto zinafanyizwa, uwape kanuni bora. Huenda ukajiepusha na huzuni inayotokea katika miaka ya baadaye.—Mithali 29:15, 17.
34. Sababu gani kanuni zilizo imara ni za maana, nacho chanzo kilicho bora kuliko yote cha kanuni hizo, ni nini?
34 “Tamasha ya ulimwengu huu inabadilika,” akaandika mtume aliyeongozwa na Mungu, na ndivyo zilivyo bila shaka kanuni za kimwili, za maono ya moyoni na za adili. (1 Wakorintho 7:31, NW) Mambo ya ulimwengu leo yanaelekea sana kubadilika. Ni lazima wazazi wafahamu kwamba, wakiwa wanadamu, nao vilevile wanaweza kushindwa upande huo. Ikiwa wanataka sana watoto wao wawe na hali njema na furaha wakati ujao, wazazi wataelekeza watoto wao kwenye kanuni zilizo imara kweli kweli. Wanaweza kufanya hivyo kwa kukaza katika akili za watoto wao tangu uchanga na kuendelea kwamba, ulizo lo lote linaloweza kutokea, tatizo lo lote linalohitaji kutatuliwa, Biblia Neno la Mungu lililoandikwa, ndiyo ya kutegemea ili wapate majibu ambayo ni yenye kukata maneno na yenye kufaa zaidi. Hata ikiwa huenda nyakati nyingine hali zikafanya maisha yaonekane kuwa yenye kutatiza au yasiyo na matumaini, Neno hilo litaendelea kuwa ‘taa ya miguu yao, na mwanga wa njia yao!’—Zaburi 119:105.
35. Kulea watoto wako ni kwa maana sana kadiri gani?
35 Ndiyo, huu ndio wakati wako wenye nafasi bora ya kuanza kutia katika watoto wako kanuni bora zinazoweza kuwategemeza katika maisha yao yote. Hakuna kazi ya maisha iliyo bora wala kazi yo yote iliyo ya maana sana kuliko kulea watoto wako. Wakati wa kuanza ni mara wanapozaliwa, katika uchanga wao!
[Picha katika ukurasa wa 117]
Kufanye kujifunza kufurahishe