Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g16 Na. 2 kur. 8-9
  • Kumsaidia Mtoto Anapobalehe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumsaidia Mtoto Anapobalehe
  • Amkeni!—2016
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • CHANGAMOTO
  • MAMBO UNAYOPASWA KUJUA
  • MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA
  • Ninaweza Kukabilianaje na Kubalehe?
    Vijana Huuliza
  • ‘Kwani Nina Shida Gani?’
    Amkeni!—2004
  • Kwa Nini Mwili Wangu Unabadilika?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Mwili Wangu Unapatwa na Nini?
    Amkeni!—1990
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2016
g16 Na. 2 kur. 8-9
Baba akizungumza na mwana wake

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA

Kumsaidia Mtoto Anapobalehe

Baba na mwana wanatazama ishara barabarani inayoonyesha barabara inayotoka utotoni kwenda kubalehe na kuelekea utu uzima

CHANGAMOTO

Ni kama juzi tu ulimbeba mtoto wako akiwa mchanga. Lakini sasa anakaribia utineja. Ingawa bado yeye ni mtoto, yuko kwenye njia panda ya ukuzi inayoitwa kubalehe.

Unaweza kumsaidiaje mwana au binti yako kukabiliana na kipindi hicho kigumu na chenye kuchanganya cha kubalehe?

MAMBO UNAYOPASWA KUJUA

Hakuna umri hususa wa kubalehe. Kijana anaweza kuanza kubalehe akiwa kati ya umri wa miaka minane hadi miaka 17. Kitabu Letting Go With Love and Confidence kinasema: “Umri wa kubalehe hutofautiana sana.”

Kubalehe humfanya kijana aache kujiamini. Matineja huhangaishwa sana na jinsi wengine wanavyowaona. “Nilikuwa na wasiwasi mwingi kuhusu watu wanavyoniona na jinsi ninavyotenda,” anakumbuka kijana mmoja anayeitwa Jared.a “Nilipokuwa na wengine, nilijiuliza ikiwa wananiona kuwa mtu wa ajabu.” Kujiamini kunaathiriwa hata zaidi chunusi zinapojitokeza. “Nilihisi kana kwamba uso wangu unashambuliwa!” anasema Kellie aliye na umri wa miaka 17. “Nililia na kuona kuwa sura yangu ni mbaya.”

Wanaobalehe mapema hukabili changamoto za pekee. Changamoto hizo huwapata hasa wasichana, kwa sababu huenda wakadhihakiwa pindi matiti yanapojitokeza na wanapopata umbo la kike. Kitabu A Parent’s Guide to the Teen Years kinasema: “Pia, kuna hatari ya kuwavutia wavulana wenye umri mkubwa zaidi ambao wana uzoefu zaidi kuhusu mambo ya ngono.”

Kubalehe hakumaanishi ukomavu. Methali 22:15 inasema hivi: “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana.” Kubalehe hakubadili ukweli huo. Huenda kijana akaonekana kwa nje kuwa mtu mzima, lakini hilo “halifunui chochote kuhusu uwezo wake wa kufanya maamuzi kwa hekima, kujiendesha kwa busara, kujizuia, wala hakuonyeshi kwamba amekomaa kwa njia nyingine yoyote,” kinasema kitabu You and Your Adolescent.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Mweleze mapema kuhusu kubalehe. Mjulishe mtoto wako mambo ya kutarajia, hasa kuhusu kupata hedhi (kwa wasichana) na kuhusu kutokwa na shahawa usiku (kwa wavulana). Tofauti na mengine, mabadiliko hayo hutokea ghafla, hivyo yanaweza kumchanganya na kumwogopesha kijana. Unapozungumzia mambo hayo, yaeleze kwa njia inayofaa. Mweleze kwamba kubalehe ni kipindi cha mabadiliko muhimu yanayomsaidia kuwa mtu mzima.—Kanuni ya Biblia: Zaburi 139:14.

Usieleze mambo kijuujuu tu. Kijana anayeitwa John anakumbuka hivi: “Wazazi wangu walipozungumza nami kuhusu kubalehe, hawakuwa wazi. Afadhali wangenieleza mambo waziwazi zaidi.” Alana, mwenye umri wa miaka 17, anahisi hivyo pia. Anasema hivi: “Mama yangu alinisaidia kuelewa mabadiliko katika mwili wangu, lakini afadhali angenitayarisha kukabiliana na hisia zangu.” Tunajifunza nini? Ingawa huenda likawa jambo lenye kuaibisha, zungumza na mtoto wako kuhusu mabadiliko yote yatakayompata anapobalehe.—Kanuni ya Biblia: Matendo 20:20.

Uliza maswali yanayoanzisha mazungumzo. Ili iwe rahisi zaidi, anza kwa kuzungumzia jinsi wengine wanavyokabiliana na kubalehe. Kwa mfano, unaweza kumwuliza binti yako hivi, “Je, tayari wanafunzi wenzako wanazungumzia kupata hedhi?” “Je, wengine wanawadhihaki wasichana ambao wamebalehe mapema?” Unaweza kumwuliza hivi mwana wako, “Je, watoto wengine wanawakejeli wale wanaochelewa kubalehe?” Matineja wanapozungumzia jinsi kubalehe kunavyowaathiri wengine, huenda ikawa rahisi zaidi kwao kueleza wazi hisia zao na mambo wanayokabili. Wanapofanya hivyo fuata ushauri huu wa Biblia: ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.’—Yakobo 1:19.

Msaidie mtoto wako awe na “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.” (Methali 3:21) Kubalehe si kipindi cha mabadiliko ya kimwili na kihisia tu. Ni kipindi ambacho mtoto wako anakuza uwezo wa kufikiri ambao utamsaidia kufanya maamuzi mazuri atakapokuwa mtu mzima. Tumia wakati huu vizuri kumfundisha mtoto wako viwango vinavyofaa.—Kanuni ya Biblia: Waebrania 5:14.

Usikate tamaa. Vijana wengi husita kuzungumza na wazazi wao kuhusu kubalehe, lakini hilo lisikupumbaze. Kitabu You and Your Adolescent kinasema hivi: “Hata ikiwa mtoto anajifanya kuwa hapendezwi, amechoshwa, amechukizwa, au hasikilizi huenda akawa anakariri kila neno unalosema.”

a Majina katika makala hii yamebadilishwa.

MAANDIKO MUHIMU

  • “Nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha.”—Zaburi 139:14.

  • “Sikuepuka kuwaambia ninyi lolote kati ya mambo yenye faida.” —Matendo 20:20.

  • “Watu wakomavu . . . nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.”—Waebrania 5:14.

“Wazazi wangu walinisaidia sana nilipokuwa nikibalehe, hasa mama yangu. Alinieleza kila kitu bila haraka. Nilijua vizuri mambo ambayo yangetukia na mambo ya kutarajia, hivyo mabadiliko hayo hayakunishtua. Na zaidi ya hilo, mama alihakikisha ninajihisi huru kuzungumza naye. Wazazi walifanya iwe rahisi kwangu kuzungumza nao.”—Marie, mwenye umri wa miaka 16.

“Wazazi wangu walijali hisia zangu. Kwa mfano, walijua kwamba niliabika sana kwa sababu ya hali hiyo, kwa hiyo walijitahidi kuheshimu faragha yangu. Pia, hawakuwatangazia wengine mambo niliyokuwa nikipitia. Na walizungumza nami kuhusu mabadiliko hayo kabla yanipate.”—Joan, mwenye umri wa miaka 18.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki