Utabiri wa Saa ya Maangamizi hautatimia kwa sababu Mungu anaahidi kwamba hali ya dunia na wanadamu itakuwa nzuri wakati ujao
HABARI KUU | JE, ULIMWENGU UMEPOTEZA MWELEKEO?
Biblia Inasema Nini?
KARNE nyingi zilizopita, Biblia ilitabiri kwamba kungekuwa na hali mbaya duniani. Kwa kuongezea, Biblia ilitabiri kihususa pia kwamba hatimaye wanadamu watakuwa na maisha mazuri wakati ujao. Yale ambayo Biblia inasema hayapaswi kupuuzwa kwa sababu mambo mengi sana ambayo ilitabiri tayari yametimia kikamili.
Kwa mfano, fikiria unabii ufuatao wa Biblia:
“Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine.”—Mathayo 24:7.
“Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.”—2 Timotheo 3:1-4.
Unabii huo unaelezea kuhusu ulimwengu ambao huenda watu fulani wakasema umepoteza mwelekeo. Kwa njia fulani, ulimwengu wetu umepoteza mwelekeo—wanadamu hawana uwezo wa kuudhibiti. Biblia inasema kwamba wanadamu hawana hekima wala uwezo wa kuleta suluhisho la kudumu. Maandiko yafuatayo yanaonyesha jambo hilo:
“Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.”—Methali 14:12.
“Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—Mhubiri 8:9.
“Mwanadamu . . . hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.
Ikiwa wanadamu wangeachwa waendelee kufanya chochote wanachotaka, inaelekea kwamba ulimwengu ungeangamia. Lakini jambo hilo halitatukia! Kwa nini? Kwa sababu Biblia inasema:
Mungu “ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.”—Zaburi 104:5.
“Kizazi kinaenda, kizazi kinakuja; lakini dunia inasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Mhubiri 1:4.
“Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29.
“Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” —Zaburi 72:16.
Mafundisho hayo ya Biblia yanatupatia majibu ya wazi kabisa. Jamii ya wanadamu haitaangamizwa na uchafuzi wa mazingira, ukosefu wa chakula na maji, au ugonjwa fulani wenye kuenea duniani pote. Ulimwengu hautaangamizwa na vita vya nyuklia. Kwa nini? Kwa sababu wakati ujao wa ulimwengu wetu uko mikononi mwa Mungu. Ni kweli kwamba Mungu amewaruhusu wanadamu watumie uhuru wao wa kuchagua. Hata hivyo, watavuna matokeo ya matendo yao. (Wagalatia 6:7) Ulimwengu si kama treni iliyopoteza mwelekeo na inayoelekea kuanguka na kuharibika kabisa. Mungu ameweka mipaka au kikomo kuhusiana na uharibifu ambao wanadamu wanaweza kusababisha.—Zaburi 83:18; Waebrania 4:13.
Lakini Mungu atafanya mengi zaidi. Ataleta “wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Mambo mazuri yaliyozungumziwa katika makala hii ni kionjo tu cha maisha bora ya wakati ujao ambayo mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wamejifunza kuyahusu katika Biblia.
Mashahidi wa Yehova ni kikundi cha ulimwenguni pote cha wanaume na wanawake wa umri mbalimbali kutoka katika makabila tofauti-tofauti. Wanamwabudu Mungu wa kweli anayeitwa Yehova katika Biblia. Hawaogopi mambo yatakayotokea wakati ujao kwa sababu Biblia inasema hivi: “Kwa maana Yehova, Muumba wa mbingu, Yeye Mungu wa kweli, Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu, amesema hivi: ‘Mimi ni Yehova, wala hakuna mwingine.’”—Isaya 45:18.
Makala hii imezungumzia baadhi ya mafundisho ya Biblia kuhusu wakati ujao wa dunia na wanadamu. Unaweza kupata habari zaidi katika somo la 5 la broshua Habari Njema Kutoka Kwa Mungu! iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova na inayopatikana kwenye tovuti ya www.jw.org/sw
Unaweza pia kutazama video yenye kichwa Kwa Nini Mungu Aliumba Dunia? kwenye tovuti ya www.jw.org/sw. (Tafuta kwenye MACHAPISHO > VIDEO)