Matukio Hayo Yote Yanamaanisha Nini?
YESU KRISTO alisema: “Umalizio wa mfumo wa mambo” ungekuwa na vita, upungufu wa chakula, tauni, na matetemeko ya nchi.—Mathayo 24:1-8; Luka 21:10, 11.
Tangu mwaka wa 1914 maisha ya watu yameharibiwa na mashambulizi ya kigaidi ambayo yameenea kotekote na vita kati ya mataifa na kati ya makabila mbalimbali. Vita hivyo vimesababishwa na viongozi wa kidini wanaoingilia siasa.
Ijapokuwa kuna maendeleo ya kisayansi katika uzalishaji wa chakula, bado mamia ya mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanakumbwa na upungufu mkubwa wa chakula. Kila mwaka, mamilioni ya watu hufa njaa.
Tauni, yaani kuenea kwa magonjwa ya kuambukiza ni sehemu ya ishara aliyotoa Yesu. Baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, homa ya Kihispania iliwaua watu zaidi ya 21,000,000. Tofauti na tauni za kale zilizotukia mahali pamoja tu, homa hiyo iliathiri mataifa yote ulimwenguni kutia ndani visiwa vya mbali. Sasa UKIMWI unawaathiri watu wengi duniani pote, na tauni kama vile kifua kikuu, malaria, upofu wa mtoni, na ugonjwa wa malale zinaendelea kuwaathiri watu katika nchi zinazositawi.
Inasemekana kwamba makumi ya maelfu ya matetemeko ya nchi yenye vipimo mbalimbali hutokea kila mwaka. Ingawa kuna vifaa na mbinu bora za kutoa habari kuhusu matetemeko ya nchi, misiba inayosababishwa na matetemeko ya nchi katika maeneo yenye watu wengi huripotiwa kwa ukawaida.
Biblia ilitabiri hivi pia: “Ujue jambo hili, ya kwamba katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake; nawe geukia mbali kutoka kwa hao.”—2 Timotheo 3:1-5.
Je, wewe hukubali kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo”?
Je, umeona kwamba kwa kadiri kubwa watu hujipenda wenyewe, hupenda pesa, na wana kiburi?
Ni nani anayeweza kubisha kwamba watu wengi ulimwenguni hujifikiria tu, hawana shukrani, hawataki kufanya makubaliano, na si washikamanifu?
Je, unajua kwamba idadi ya watoto wasiotii wazazi inazidi kuongezeka na kuna ukosefu mkubwa sana wa upendo ulimwenguni pote?
Bila shaka unatambua kwamba tunaishi katika ulimwengu ambao unapenda raha kupindukia lakini haupendi wema. Hivyo ndivyo Biblia inavyoeleza mitazamo ya watu katika “siku za mwisho.”
Je, tunahitaji uthibitisho zaidi ili kutambua nyakati tunamoishi? Yesu pia alitabiri kwamba katika nyakati hizi, habari njema ya Ufalme wa Mungu ingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa. (Mathayo 24:14) Je, inahubiriwa?
Gazeti Mnara wa Mlinzi linalozungumzia Biblia na linalotangaza habari njema ya Ufalme wa Yehova huchapishwa kwa ukawaida katika lugha nyingi kuliko gazeti lingine lolote.
Kila mwaka, Mashahidi wa Yehova hutumia mabilioni ya saa wakiwahubiria wengine kuhusu Ufalme wa Mungu.
Hivi sasa, vichapo vya Mashahidi wa Yehova vinavyozungumzia Biblia huchapishwa katika lugha 400 hivi, kutia ndani lugha zinazozungumzwa na watu wachache katika maeneo ya mbali. Mashahidi wa Yehova wamehubiri habari njema katika mataifa yote; wamehubiri pia katika visiwa vingi na maeneo madogo sana ambayo yanapuuzwa na wanasiasa. Katika nchi nyingi, wanaendesha programu ya kawaida ya elimu ya Biblia.
Kwa kweli, habari njema ya Ufalme wa Mungu inahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa, si ili kuugeuza ulimwengu, bali kutoa ushahidi. Watu kila mahali wanapewa nafasi ya kuonyesha ikiwa watamjali yule aliyeumba mbingu na dunia na ikiwa wataheshimu sheria zake na kuwapenda wanadamu wenzao.—Luka 10:25-27; Ufunuo 4:11.
Hivi karibuni, Ufalme wa Mungu utawaharibu waovu wote na kuifanya dunia kuwa paradiso.—Luka 23:43.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Ni Siku za Mwisho za Nini?
Si siku za mwisho za wanadamu. Biblia inaahidi kwamba wale wanaofanya mapenzi ya Mungu wataishi milele.—Yohana 3:16, 36; 1 Yohana 2:17.
Si siku za mwisho za dunia. Neno la Mungu linaahidi kwamba dunia inayokaliwa itadumu milele.—Zaburi 37:29; 104:5; Isaya 45:18.
Badala yake, hizi ni siku za mwisho za mfumo huu wa mambo wenye jeuri, usio na upendo na za wale wanaoshikilia njia zake.—Methali 2:21, 22.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]
Je, Kweli Biblia Ni Neno la Mungu?
Manabii wa Biblia waliandika hivi tena na tena: ‘Yehova amesema hivi.’ (Isaya 43:14; Yeremia 2:2) Hata Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alikazia kwamba ‘hakusema kwa kujitungia mwenyewe.’ (Yohana 14:10) Biblia yenyewe inasema hivi waziwazi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.”—2 Timotheo 3:16.
Shirika la Muungano wa Vyama vya Biblia lilisema kwamba hakuna kitabu kingine kimechapishwa katika lugha nyingi kama Biblia—lugha zaidi ya 2,200. Hakuna kitabu kingine kimesambazwa kwa kadiri kubwa hivyo—kwa sasa zaidi ya nakala bilioni nne zimesambazwa. Je, hutarajii ujumbe wa Mungu kwa wanadamu wote uenee hivyo?
Ili kupata uthibitisho zaidi kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu, soma kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
Utafaidika sana ukisoma Biblia na kutambua kwamba kwa kweli ni Neno la Mungu.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
Ufalme wa Mungu Ni Nini?
Ni serikali ya pekee iliyoanzishwa na Mungu wa kweli, Yehova, Muumba wa mbingu na dunia.—Yeremia 10:10, 12.
Biblia inasema kwamba Yesu Kristo ndiye aliyepewa na Mungu mamlaka ya kutawala. (Ufunuo 11:15) Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha kwamba alikuwa amepewa mamlaka kubwa na Mungu. Alitumia mamlaka yake kudhibiti nguvu za asili, kuponya magonjwa, na hata kuwafufua wafu. (Mathayo 9:2-8; Marko 4:37-41; Yohana 11:11-44) Unabii wa Biblia ulioongozwa na roho takatifu ulitabiri kwamba Mungu angempa pia “utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye.” (Danieli 7:13, 14) Serikali hiyo inaitwa Ufalme wa mbinguni kwa sababu Yesu Kristo anatawala sasa akiwa mbinguni.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Habari njema inahubiriwa duniani pote