Habari Njema Wanazotaka Usikie
YESU alipokuwa duniani, wanafunzi wake walimjia wakamwuliza: “Ni nini ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Alijibu kwamba kungekuwako vita kati ya mataifa mengi, njaa, magonjwa ya kipuku, matetemeko ya dunia, kuongezeka kwa uasi, walimu wa kidini wasio wa kweli wanaopoteza wengi, wafuasi wake wa kweli kuchukiwa na kunyanyaswa, na kupoa kwa upendo wa kutaka uadilifu. Wakati ambapo mambo hayo yangeanza kutukia, ingeonyesha Kristo angekuwapo bila kuonekana, na kwamba Ufalme wa mbinguni uko karibu. Hizo zingekuwa habari—habari njema! Hivyo Yesu aliongezea maneno haya kuwa sehemu ya ile ishara: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:3-14.
Mambo yenyewe ambayo yametukia katika ulimwengu karibuni ni mabaya, lakini kile ambacho yanamaanisha ni chema, yaani, kuwapo kwa Kristo. Mambo hayo yaliyotajwa juu yalianza kutukia mwaka ule uliotangazwa kotekote wa 1914! Ulionyesha mwisho wa Nyakati za Mataifa na mwanzo wa kipindi cha badiliko kutoka utawala wa kibinadamu kuja kwenye Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu (Milenia).
Zaburi ya 110, mistari 1 na 2, na Ufunuo 12:7-12 zaonyesha kwamba kungekuwapo kipindi cha mabadiliko. Inaonyeshwa humo kwamba Kristo angeketi kwenye mkono wa kulia wa Mungu mbinguni mpaka wakati wa kuwa kwake Mfalme. Ndipo vita mbinguni ingetokeza kufukuzwa kwa Shetani kuja kwenye dunia, kukileta ole duniani, na Kristo angetawala katikati ya maadui wake. Mwisho kamili wa uovu ungekuja kupitia “dhiki kubwa,” ikifikia upeo katika vita ya Har–Magedoni na kufuatwa na Utawala wa amani wa Kristo wa Miaka Elfu.—Mathayo 24:21, 33, 34; Ufunuo 16:14-16.
“Lakini jua hili,” Biblia yasema, “kwamba katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu, wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakithibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya hiyo; na geukia mbali kutoka kwa hawa.”—2 Timotheo 3:1-5.
Huenda watu fulani wakabisha wakisema kwamba mambo hayo yametukia zamani katika historia ya kibinadamu, lakini ukweli ni kwamba hayajawahi kutukia kwa kadiri hii. Kama wanahistoria na wafafanuzi wanavyosema, haujapata kuwako wakati duniani kama ule ambao umekuwapo tangu mwaka wa 1914 na kuendelea. (Ona ukurasa wa 7.) Ole zimeenea zaidi ya zile zilizotangulia. Isitoshe, kwa habari ya sehemu nyingine za ishara ya Kristo ya siku za mwisho, mambo haya ya hakika yapasa kufikiriwa: Kutangazwa duniani pote kwa kuwapo kwa Kristo na Ufalme kumefanywa kwa kiasi kikubwa sana ambacho hakina kifani katika historia. Kunyanyaswa kwa sababu ya kuhubiri hakujapata kuwa na kifani kamwe kama kule ambako Mashahidi wa Yehova wamepata. Mamia ya Mashahidi waliuawa katika kambi za mateso za Nazi. Mpaka leo hii Mashahidi wa Yehova wamepigwa marufuku katika sehemu fulani-fulani, na katika nyingine wanakamatwa, wanafungwa gerezani, wanateswa, na kuuawa. Yote hayo ni sehemu ya ile ishara ambayo Yesu alitoa.
Kama ilivyotabiriwa katika Ufunuo 11:18, ‘mataifa wamekuwa na hasira ya kisasi’ dhidi ya Mashahidi waaminifu wa Yehova, na hiyo inaonyesha kwamba “hasira ya kisasi” ya Yehova mwenyewe italetwa juu ya mataifa hayo. Andiko ilo hilo lasema kwamba Mungu ‘atawaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.’ Haujapata kamwe kuwako wakati mwingine wowote katika historia ya kibinadamu ambapo uwezo wa dunia kuendeleza uhai umekaribia kuharibiwa, kama ilivyo leo. Lakini, sasa ni tofauti! Wanasayansi wengi wameonya kwamba iwapo mwanadamu ataendelea kuichafua dunia, itakuwa isiyokalika. Lakini Yehova “aliiumba ili ikaliwe na watu,” naye atawaondoa wachafuzi hao kabla hawajamaliza kuiharibu dunia.—Isaya 45:18.
BARAKA ZA KIDUNIA CHINI YA UFALME
Huenda wazo la kwamba watu wataishi duniani wakiwa raia za Ufalme wa Mungu likaonekana kuwa la ajabu kwa waamini wengi wa Biblia wanaodhani kwamba watu wote waliookolewa wako mbinguni. Biblia yaonyesha kwamba ni wachache tu wanaoenda mbinguni na kwamba wale watakaoishi milele duniani watakuwa umati mkubwa usiohesabika. (Zaburi 37:11, 29; Ufunuo 7:9; 14:1-5) Unabii wa kitabu cha Biblia cha Danieli waonyesha kwamba Ufalme wa Mungu mikononi mwa Kristo utajaa duniani na kuitawala.
Katika kitabu hicho, Ufalme wa Kristo unafananishwa na jiwe lililochongwa kutoka katika enzi kuu ya Yehova iliyo kama mlima. Lapiga na kuharibu sanamu inayofananisha mataifa ya dunia yenye nguvu, ‘nalo jiwe hilo likawa mlima mkubwa, likaijaza dunia yote.’ Unabii huo waendelea hivi: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:34, 35, 44.
Ufalme huo na lile tumaini linalotegemezwa na Maandiko la uhai wa milele katika dunia iliyosafishwa na kurembwa ndiyo mambo ambayo Mashahidi wa Yehova wanataka kukuambia juu yake. Mamilioni ya watu wanaoishi sasa na mamilioni wengine wengi walio sasa katika makaburi yao watapata fursa ya kukaa humo milele. Ndipo kusudi la awali la Yehova la kuiumba dunia na kuweka ndani yake watu wawili wa kwanza litakapotimizwa, chini ya Utawala wa Kristo Yesu wa Miaka Elfu. Paradiso hiyo ya kidunia haitakuwa yenye kuchosha kamwe. Kama vile Adamu alivyopewa kazi katika bustani ya Edeni, vivyo hivyo jamii ya binadamu itakuwa na mipango itakayohitaji kufikiri kwingi katika kuitunza dunia na mimea na wanyama watakaokuwa juu yake. “Wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”—Isaya 65:22; Mwanzo 2:15.
Maandiko mengi yangeweza kutolewa kuonyesha hali zitakazokuwako wakati ambapo ile sala ambayo Yesu alitufundisha itakapojibiwa: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:10) Lakini, acheni hili litoshe kwa sasa: “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’ Na Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’ Pia, husema: ‘Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’”—Ufunuo 21:3-5.
[Blabu katika ukurasa wa 15]
“Nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,”
LAKINI ‘mwisho utakuja’
[Picha katika ukurasa wa 18]
Uholanzi
[Picha katika ukurasa wa 18]
Nigeria