Sura ya 11
Yesu Anatufundisha Kusali
WEWE unasema kwa Yehova Mungu?— Yeye anataka useme kwake. Unaposema kwa Mungu, hii inaitwa sala.
Mara nyingi Yesu alisema kwa Baba yake mbinguni. Mara nyingine alitaka awe peke yake aliposema kwa Mungu. Wakati mmoja, Biblia inasema “alipanda mlimani faraghani, kwenda kuomba. Na kulipokuwa jioni, alikuwako huko peke yake.”—Mathayo 14:23.
Unaweza kwenda wapi ukasali kwa Yehova peke yako?— Labda unaweza kusema kwa Mungu peke yako mbele ya kwenda kulala usiku. Yesu alisema: “Wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako.” Je! unasali kwa Mungu kila usiku mbele ya kulala?— Ni vizuri kufanya hivyo.—Mathayo 6:6.
Yesu tena alisali wakati watu wengine walipokuwa na yeye. Alipokuwa na mikutano pamoja na wanafunzi wake, Yesu alisali. Unaweza kwenda kwenye mikutano ya Kikristo ambapo sala inatolewa. Kwa kawaida penye mikutano hii mtu mzima ndiye atasali. Sikiliza kwa uangalifu anayosema, kwa sababu anasema kwa Mungu kwa ajili yako. Ndipo utaweza kusema “Amina” kwa sala.
Unajua maana yake kusema “Amina” mwishoni mwa sala?— Maana yake unaipenda sa-la. Maana yake unakubaliana nayo, na waitaka iwe sala yako vile vile.
Vile vile Yesu alisali wakati wa chakula. Alimshukuru Yehova kwa chakula chake. Je! sikuzote unasali mbele ya kula vyakula vyako?—
Ni vizuri kwetu kumshukuru Yehova kwa chakula mbele ya kuanza kula. Labda baba yako ndiye atatoa sala wakati mnapokula pamoja. Lakini ukila peke yako namna gani? Au ikiwa unakula pamoja na watu wasiomshukuru Yehova je!— Basi lazima utoe sala yako mwenyewe.
Je! ni lazima kusali kwa sauti kuu sikuzote?— Hapana. Yehova aweza kusikia sala yako hata ukisali moyoni mwako. Basi unaweza kutoa sala ya kimya kwa Yehova wakati uko pamoja na watu wasiosali kwa Mungu. Kwa mfano, labda utatoa sala ya kimya unapokula chakula cha mchana katika masomo.
Je! ni lazima uinamishe kichwa chako unaposali? Je! ni lazima upige magoti yako? Unaonaje?—
Mara nyingine Yesu alipiga magoti yake aliposali. Nyakati nyingine aliinua kichwa chake kuelekea mbinguni aliposali. Tena alisema juu ya kusali kwa Mungu hali umesimama.
Basi hii inaonyesha nini? Je! sikuzote ni lazima uwe na kikao kile kile unaposali?— Kikao si jambo kubwa. Lakini nyakati nyingine ni vizuri kuinamisha kichwa chako. Nyakati nyingine labda hata utataka upige magoti kama alivyofanya Yesu. Lakini, kumbuka, twaweza kusali kwa Mungu wakati wo wote mchana au usiku naye atatusikia.
Jambo la maana katika sala ni kwamba tunaamini Yehova anasikiliza kweli. Unaamini Yehova anakusikia?—
Imetupasa tuseme nini katika sala zetu kwa Yehova?— Niambie: Unaposali, unasema kwa Mungu juu ya nini?—
Yehova anatupa mambo mengi mazuri, na ni vizuri kumshukuru kwa mambo hayo, sivyo?— Tunamshukuru yeye kwa chakula tunachokula. Lakini umepata kumshukuru kwa anga la buluu, miti na maua mazuri?— Alivifanya hivyo navyo.
Siku moja wanafunzi wa Yesu walimwomba awafundishe kusali. Na Mwalimu Mkuu akawaonyesha mambo yaliyokuwa ya maana zaidi sana kuombea. Unayajua ni mambo gani haya?— Chukua Biblia yako na kufungua Mathayo sura ya 6. Katika mistari 9 mpaka 13 tunaona ambayo watu wengi wanaita “Sala ya Bwana.” Na tusome pamoja.
Hapa tunajifunza kwamba Yesu alituambia tusali juu ya jina la Mungu. Alisema tusali jina la Mungu litakaswe au lionwe takatifu. Jina la Mungu ni jina gani?— Biblia inatuambia kwamba ni Yehova, nasi imetupasa tupende jina hilo.
Pili, Yesu alitu-fundisha kusali ufalme wa Mungu uje. Ufalme huu ni wa maana sana kwa sababu utaleta amani kwenye dunia na kuifanya paradiso.
Tatu, Mwalimu Mkuu alisema tusali mapenzi ya Mungu yatimizwe duniani kama yalivyotimizwa mbinguni. Maana yake imetupasa tufanye mapenzi ya Mungu.
Yesu tena alitufundisha kusali kwa chakula tunachotaka kwa siku hiyo. Na akasema imetupasa tumwambie Mungu kwamba tunasikitika wakati tunapofanya mabaya. Imetupasa tumwombe Mungu atusamehe. Lakini wakati yeye hajatusamehe, yatupasa tusamehe wengine wakitutenda mabaya. Je! unafanya hivyo?
Mwisho, Yesu alisema, imetupasa tusali kwamba Yehova Mungu atulinde na mwovu, Shetani Ibilisi. Basi, haya yote ni mambo mazuri ya kuombea kwa Mungu.
Imetupasa tuamini kwamba Yehova anasikia sala zetu na imetupasa tuendelee kumshukuru, zaidi ya kumwomba yeye atusaidie. Yehova apenda kutusikia tukisali kwake. Yeye anafurahi wakati tunaposema kweli katika sala na wakati tunapomwomba mambo mazuri. Naye atatupa mambo haya. Je! unaamini hivyo?—
(Shauri jema zaidi juu ya sala linapatikana katika 1 Petro 3:12, 1 Yohana 5:14 na Warumi 12:12.)