Sura ya 23
Baraka ya Kazi
UNGEPENDELEA kufanya jambo gani, kazi au mchezo?— Ni kweli sote tunajifurahisha kucheza. Lakini kweli ingekuwa vizuri ikiwa tungecheza wakati wote?— Umepata kufikiri ingekuwaje ikiwa hakuna ambaye angefanya kazi wakati wo wote?—
Fikiria chakula ambacho unakula. Unajua kinatoka wapi?— Karibu chote kinamea juu ye mimea na miti. Lakini ikiwa hakuna ambaye angeiangalia na kuchuma matunda na mboga, ungekula nini? Je! si vizuri kwa vile watu wanafanya kazi hata unakuwa na chakula?—
Tazama huku na huku katika nyumba unamoishi. Je! una kitanda pa kulala?— Kuna viti vya kukalia na meza vile vile?— Je! wewe hauna furaha kwa vile mtu fulani alifanya kazi akatengeneza vitu hivi?—
Mwalimu Mkuu alionaje juu ya kazi? Ache tuone.
Hata alipokuwa mtoto alifanya kazi katika kiwanda cha seremala. Alitengeneza vitu kwa mbao. Yusufu alikuwa seremala, na alimlea Yesu kama mtoto wake mwenyewe. Ndiyo sababu Biblia inamwita Yesu “mwana wa seremala.” Katika siku hizo mtoto wa kiume angejifunza kazi zile zile ambazo baba yake alifanya.— Mathayo 13:55.
Pengine mwanzoni ilikuwa vigumu kwa Yesu. Lakini kwa mazoezi, akajifunza kufanya kazi vizuri. Yesu vile vile akawa seremala.—Marko 6:3.
Unafikiri kazi hii ilimpendeza Yesu?— Ungefurahi ikiwa ungeweza kutengeneza meza nzuri na viti na vitu vingine vya kutumia watu?— Biblia inasema ni vizuri mtu “kuzifurahia kazi zake.” Kazi inakupa furaha ambayo huwezi kupata kwa mchezo. Si vibaya kucheza, lakini si vizuri kucheza wakati wote.—Mhubiri 3:22.
Yesu hakufanya kazi kama seremala maisha yake yote. Yehova Mungu alimpa kazi ya pekee ili afanye duniani. Unajua ilikuwa kazi gani?— Yesu alisema: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu . . . ; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” Ndiyo, Mungu alimpa Yesu kufanya kazi ya kuhubiri.—Luka 4:43.
Yesu alionaje juu ya kufanya kazi hii? Je! alitaka kuifanya?—
Yesu alisema: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.” Unapenda kwa kadiri gani kula chakula ambacho unapenda sana?— Hii inakupa wazo la namna Yesu alivyoipenda sana kazi ambayo Mungu alimpa.—Yohana 4:34.
Mungu alitufanya sisi tuwe na furaha wakati tunapojifunza kufanya kazi. Anasema kwamba ni zawadi ambayo amempa mtu apate “kufurahia kazi yake ngumu.” Basi, ukijifunza kufanya kazi wakati wewe ni mchanga, maisha yako yote yatakuwa yenye kufurahisha zaidi.—Mhubiri 5:19, NW.
Hiyo haina maana kwamba mtoto mchanga aweza kufanya kazi ya mtu mkubwa, bali sote twaweza kufanya kazi fulani. Baba yako anafanya kazi kila siku ili tuwe na chakula na nyumba mwa kuishi. Unajua ni kazi ya namna gani ambayo baba yako anafanya?— Yeye hafanyi kazi kwa ajili yake mwenyewe tu. Yeye anafanya kazi kwa faida ya jamaa nzima. Naye mama yako anafanya kazi ya kutupikia vyakula. Anasafisha nyumba yetu na kufua nguo zetu.
Kuna kazi gani uwezayo kufanya itakayokuwa baraka kwa jamaa nzima?— Unaweza kusaidia kutandika meza, kupangusa sahani, kufagia chumba chako na kuokota vitu vyako vya kuchezea. Labda hata sasa unafanya mengine ya mambo haya. Je! kweli kazi hiyo ni baraka?—
Ebu tuone namna kazi kama hiyo ni baraka. Vitu vya kuchezea vyapaswa virudishwe mahali pake ukimaliza kucheza. Sababu gani ungesema hilo ni la maana?— Inasaidia kufanya nyumba kuonekana malidadi. Tena ni jambo la maana kwa sababu inaweza kuzuia ajali. Ikiwa huokoti vitu unavyochezea, pengine mama yako atakuja siku moja akiwa na vitu vingi katika mikono yake na kukanyaga kimoja. Huenda akajikwaza akaanguka akaumiza kichwa chake. Huenda ikawa lazima aende hata hospitali. Je! isingekuwa vibaya sana?— Basi, wakati unaondoa vitu unavyochezea ukiisha kucheza, ndiyo baraka kwetu sote.
Kuna kazi nyingine ambayo watoto wanayo tena. Ninafikiria kazi ya masomo. Katika masomo mnajifunza kusoma. Wakati unajua kusoma, kuna mambo mengi yenye kupendeza uwezayo kujifunza. Utaweza hata kujisomea mwenyewe kitabu cha Mungu mwenyewe, Biblia. Basi, unapofanya vizuri kazi yako ya masomo, kweli ni baraka, sivyo?—
Kuna watu wengine wanaojaribu kuepuka kazi. Pengine unamjua anayefanya hivyo. Lakini kwa kuwa Mungu alitufanya sisi tufanye kazi, yatupasa tujifunze kujifurahisha kazi.
Hapa pana mambo fulani yawezayo kusaidia. Unapokuwa na kazi ya kufanya, jiulize mwenyewe: Sasa, sababu gani lazima jambo hili lifanywe? Unapojua jambo fulani ni la maana, ni vyepesi kulifanya. Na kwamba kazi ni kubwa au ndogo, ifanye vizuri. Ukifanya hivyo, unaweza kufurahia kazi ya mikono yako. Ndipo utakapojua mwenyewe kwamba kweli kazi ni baraka.
(Biblia yaweza kusaidia mtu awe mfanya kazi mzuri. Soma ambayo Biblia inasema katika Wakolosai 3:23; Mithali 10:4; 22:29; Mhubiri 3:12, 13, 22.)