Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 12/1 kur. 3-7
  • Kipawa cha Kazi Ambacho Mungu Amewapa Watumishi Wake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kipawa cha Kazi Ambacho Mungu Amewapa Watumishi Wake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uhitaji wa Mwanadamu wa Kazi ya Maana
  • Mfanya Kazi Kufurahia Matunda ya Kazi Yake
  • Yesu na Wafuasi Wake—Wafanya Kazi
  • Kazi ya Kuchangamsha Sana Huko Mbele
  • Furahia Kazi Yako
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Jinsi ya Kufurahia Kazi Ngumu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Ona Mema kwa Ajili ya Kazi Yako Ngumu
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Jinsi ya Kusitawisha Maoni Yanayofaa Kuhusu Kazi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 12/1 kur. 3-7

Kipawa cha Kazi Ambacho Mungu Amewapa Watumishi Wake

“Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye.”​—Yohana 17:4.

1. Yesu alifanya nini na kazi aliyotumwa aifanye duniani?

YESU KRISTO, Mwana mzaliwa pekee wa Mungu, ndiye mtumishi mkuu wa Muumba wa mbingu na dunia. Wakati Yehova alipomtuma duniani kwa kusudi la kuondoa lawama juu ya enzi kuu Yake ya ulimwengu wote na kukomboa ulimwengu wa wanadamu, Yesu alistaajabiwa sana, hasa na wanadamu. Jambo hilo lilitukia kama lilivyotabiriwa katika Isaya 52:13, 14: “Tazama, mtumishi wangu atatenda kwa busara, atatukuzwa, na kuinuliwa juu, naye atakuwa juu sana. Kama vile wengi walivyokustaajabia, (uso wake ulikuwa umeharibiwa sana zaidi ya mtu ye yote, na umbo lake zaidi ya wanadamu).” Kazi hiyo isiyofanywa kwa kawaida aliimaliza kwa uaminifu, sawa na vile alivyokiri katika sala aliyompelekea Yehova Mungu, akisema: “Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa nifanye.” (Yohana 17:4) Yeye ni mfano mwema kwa watumishi wote wenzake wa Mungu.

2. Ni katika maana gani sisi tuko katika mfano wa Mungu?

2 Wanaume na wanawake wana uhitaji wa kufanya kazi. Iko hivyo kwa sababu walifanywa kwa njia ya kuihitaji kazi. “Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu,” Yehova Mungu alisema wakati wa kuumba mwanadamu awe mtumishi wake duniani. (Mwanzo 1:26) Kufanana huko si kumlanda Mungu katika hali yo yote ya kimwili, maana yeye ni roho na haonekani na macho ya kibinadamu. Bali, maana yake ni kwamba mwanadamu mkamilifu alipewa sifa fulani-fulani za Mungu, sifa kama vile haki, hekima, upendo na nyingine zinazotenganisha mwanadamu na wanyama wa hali ya chini. Kwamba maoni hayo ni sawa inaonyeshwa na Wakolosai 3:9, 10, NW, ambapo watumishi walio wakf wenzi wa Yesu Kristo wanaambiwa wabadili utu wao, kwa maneno haya: “Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na mjivike wenyewe utu mpya, ambao kupitia maarifa sahihi unafanywa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba.”

3, 4. (a) Maneno ya Biblia ya utangulizi yanamwonyesha Mungu kuwa nini? (b) Ni katika maana gani yeye aliburudika ilipomalizika kazi ya kuumba?

3 Sehemu moja ya “mfano” wa Mungu ni kuwa kwake mfanya kazi. Yehova ana uhuru kamili kabisa wa kutenda atakalo, nalo atakalo kufanya ni kazi. Maneno ya kwanza ya Biblia yanamjulisha kwetu kuwa mfanya kazi asiyechoka: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.” (Mwanzo 1:1) Kazi hiyo haikumweka katika hali ya kuwa hoi asiweze lo lote: “[Yehova], Muumba miisho ya dunia, hazimii, wala hachoki.”​—Isaya 40:28.

4 Kwa hivyo, inaposemwa kwamba alijiburudisha mwishoni mwa siku ya sita ya kuumba haiwezi kuwa na maana ya kwamba alihitaji pumziko la kumpa nafuu kwa kulemewa na kazi: “Katika siku sita Yehova alizifanya mbingu na dunia na siku ya saba akakoma na kuchukua hatua nyingine ya kujiburudisha mwenyewe.” (Kutoka 31:17, New World Translation, maelezo ya chini, chapa ya mwaka wa 1963) Mungu hakupumzika akaacha kazi zote, bali aliiacha hiyo ya kuumba tu. Ilipomalizika aliifikiria tena akaona kwamba ilikuwa nzuri sana, ilikuwa imefikia kiwango chake cha ukamilifu, naye aliburudika na kuridhishwa na kutimizwa kwa kazi hiyo yenye hali bora kabisa. Kuiona kazi nzuri hiyo ikiwa imemalizika kulimfurahisha na kumburudisha Yehova Muumba wa kazi yote hiyo. (Mwanzo 1:31; Yohana 5:17) Kutokana na hayo yote tunaona kwamba watu, ambao walifanywa kwa sura ya Mungu, wanazaliwa wakiwa na uhitaji wa kuburudishwa pia na hisi ya kujisikia wametimiza kazi nzuri, si uhitaji wa kuwa wafanya kazi tu.

Uhitaji wa Mwanadamu wa Kazi ya Maana

5. (a) Mungu anaonyeshwa tena kuwa nini, na kwa hiyo iweje? (b) Kuna maelezo gani machache juu ya kinachofanya watu wazidi kujiona na wajibu wa kufanya kazi?

5 Tena, Yehova ni Mungu wa kusudi na kazi zake ni zenye kusudi. “[Yehova] amefanya kila kitu kwa kusudi lake,” kutia na wanadamu. (Mithali 16:4) Kwa hiyo, ni lazima pia kazi za mwanadamu ziwe na kusudi. “Kujitahidi sana kupata maana katika maisha ya mtu,” anaandika Viktor Frankl daktari wa uchunguzi wa matatizo ya akilini, “ndicho kichochezi kikuu ndani ya mwanadamu. . . . Mimi nathubutu kusema kwamba ulimwenguni hamna kitu ambacho kingesaidia mtu afaulu kuziokoka hata hali zilizo mbaya zaidi, kama vile anavyoweza kusaidiwa na maarifa ya kujua kwamba maisha yake yana kusudi.” Lakini watu wengi wanaona ni jambo la kuchosha kurudia-rudia kazi ile ile ya kusimamia mlolongo (mstari mrefu) wa bidhaa zinazofuatana zinapotengenezwa, kwa maana hawapendezwi na kazi hiyo au hawaionei fahari. Hiyo ni sababu moja kubwa inayofanya watu wakose kujiona kuwa na wajibu wa kufanya kazi—​nyingi za kazi za siku hizi hazitoshelezi uhitaji wa maoni ya akili za watu wa kutaka kuhisi maana ya kazi na kujisikia wametimiza jambo fulani.

6. Mtu yule wa kwanza alipewa kazi gani yenye kusudi?

6 Kwa kuwa kila kilichofanywa na Mungu kilifanywa kwa kusudi fulani, basi mwanadamu naye alifanywa kwa kusudi fulani. Alifanywa kisha akawekwa duniani afanye kazi. Kazi aliyompa Mungu ilikusudiwa iwe ya maana, kazi inayohusu matumizi ya akili na mikono yake kwa njia zenye kutokeza mema. “[Yehova] Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza.” Mwanadamu mkamilifu alipaswa ‘kutawala samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi,’ na ‘Yehova Mungu akafanyiza kutoka katika ardhi kila mnyama wa msituni, na kila ndege wa angani, akamletea Adamu ili aone atawaitaje; kila kiumbe hai, jina alilokiita Adamu likawa ndilo jina lake.’​—Mwanzo 2:15; 1:26; 2:19.

7, 8. (a) Kwa sababu gani kwa kufaa kazi inayofanywa katika utumishi wa Mungu inaweza kuitwa kipawa kutoka kwake? (b) Kwa sababu gani kawaida zinazofuatwa na watu ili kujifurahisha zinakosa kuziba pengo linaloachwa na kazi?

7 Yehova alimpa mwanadamu kazi inayofaa ili apate furaha na uradhi kutokana nayo. Kazi hiyo ingetimiza mapendezi ya maisha yake, iondolee mbali uwezekano wo wote wa kujisikia amechoshwa na kazi au kujisikia hana furaha kwa sababu ya kurudia jambo lile lile moja. Kazi aliyompa ingemfanya aridhike kwa kujisikia ni mtu wa maana. Ingekuwa kazi yenye kujawa na kusudi kwa sababu alipewa kazi hiyo na Muumba wa dunia na ulimwengu wote, Mungu wa kusudi Mweza Yote. Badala ya sifa zile za kimungu kukomeshwa au kuvurugwa au kugandamizwa kwa sababu ya kutokutumiwa, kama inavyotokea mara nyingi katika kazi za kilimwengu, mgawo wa kazi kutoka kwa Yehova uliwapa mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, uhuru wa kutoa maoni yao wenyewe. Hata baada ya mwanadamu kuondoshwa katika bustani ya Edeni na kuambiwa kwamba angefanya kazi “kwa jasho la uso wako,” bado kazi hiyo ingemletea mwanadamu faida.​—Mwanzo 3:19.

8 Uchunguzi mwingi wa kisayansi uliofanywa majuzi unaihakikisha ile kweli ya Kimaandiko ya kwamba mwanadamu aliumbwa awe akifanya kazi. Uchunguzi huo umeonyesha kwamba wengi wa watu wazee-wazee walio na afya nzuri hawataki kustaafu (kuacha kazi), kwamba mara nyingi kustaafu kunafanya mtu aone maisha yakimchosha badala ya kumpa furaha. Wachunguzi wanaamini kwamba kustaafu hufanya watu waliochoshwa na maisha, wenye kujikalia bila la kufanya, waache kutaka kuishi na kwa kweli kunafupisha urefu wa maisha yao. Kufuatia kawaida fulani za kujifurahisha tu hakuzibi kwa njia ya kutosha pengo lililoachwa katika maisha za watu waliostaafu. Kawaida hizo huenda zikawa za kufurahika saa chache kwa juma ili kumpa mtu badiliko la shughuli na kumstarehesha kutokana na kazi yake ya kawaida, lakini zinachosha zinapofuatiwa wakati wote. Haziwezi kutufanya tujisikie kwamba maisha zetu zinatimiza kusudi fulani lenye mafaa. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Moyo wangu ulifurahi kwa sababu ya kazi yangu yote, na hii ilikuwa sehemu yangu katika kazi yangu yote. Mwanadamu hapati jema kupita kula na kunywa, na kuiburudisha [nafsi] yake kwa mema katika kazi yake. Hayo nayo naliona ya kwamba hutoka mkononi mwa Mungu.” Kwa hiyo kazi katika utumishi wa Mungu ni kipawa kutoka kwa Mungu.​—Mhubiri 2:10, 24.

Mfanya Kazi Kufurahia Matunda ya Kazi Yake

9, 10. (a) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba mwanadamu anapaswa kufurahia matunda ya kazi ngumu yake? (b) Ni vilio vya nani anavyovisikia Yehova?

9 Yehova hataki mwanadamu anyimwe matunda ya kazi yake ngumu. “Yampasa mkulima mwenye taabu ya kazi kuwa wa kwanza wa kupata fungu la matunda,” akaandika mtume Paulo. Mahali pengine aliieleza kanuni hiyo ya kimungu kwa urefu, akisema: “Ni nani apandaye mizabibu asiyekula katika matunda yake? Au ni nani achungaye kundi, asiyekunywa katika maziwa ya kundi? Je’ ninanena hayo kwa kibinadamu? Au torati nayo haisemi yayo hayo? Kwa maana katika torati ya Musa imeandikwa, Usimfunge kinywa ng’ombe apurapo nafaka. Je! hapo Mungu aangalia mambo ya ng’ombe? Au yamkini anena hayo kwa ajili yetu? Naam, yaliandikwa kwa ajili yetu; kwa kuwa alimaye nafaka ni haki yake kulima kwa matumaini; naye apuraye nafaka ni haki yake kutumaini kupata sehemu yake.”​—2 Timotheo 2:6; 1 Wakorintho 9:7-10.

10 Hata wanyama wenye kufanya kazi walipaswa washiriki matunda ya kazi yao ngumu. Ikiwa Yehova analinda faida za hayawani wasiojua mengi, si zaidi sana wafanya kazi wa kibinadamu! Kwa kweli, yeye anaonyesha wazi nia yake ya kufanya hivyo: “Angalieni, ujira wa wakulima waliovuna mashamba yenu, ninyi mliouzia kwa hila, unapiga kelele, na vilio vyao waliovuna vimeingia masikioni mwa [Yehova] wa majeshi.”​—Yakobo 5:4.

Yesu na Wafuasi Wake—Wafanya Kazi

11. Yesu alikuwa na maoni gani juu ya kazi, na kwa sababu gani lazima sisi tuyathamini maoni yake ya kazi?

11 Yesu ni mfanya kazi mwenzi wa Baba yake wa kimbinguni Yehova. “Baba yangu anatenda kazi hata sasa,” yeye alisema, “nami ninatenda kazi.” (Yohana 5:17) Yeye anafanya kazi ambayo Yehova alimgawia. Kwa nia ya kupenda na kwa kujitolea anaifanya kazi hiyo na kuonyesha anafurahia kuifanya. Anaiona kuwa yenye kujenga, yenye kushibisha na kuburudisha sawa na chakula. Hakika ndivyo ilivyo, kwa maana wakati mmoja wanafunzi wake walipomhimiza ale, yeye aliwajibu hivi: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.” (Yohana 4:34) Furaha ya kujisikia ametimiza jambo fulani ilikuwa ikimburudisha mwishoni mwa kazi, hivyo ikafukuzia mbali uchovu wo wote aliokuwa nao na kumpa uradhi na uchangamshi mwingi. Wale wanaojisema kuwa Wakristo wanapaswa wauthamini sana mwendo huu na nia ya Kristo Yesu. Kwa sababu gani? Kwa sababu Biblia inaonyesha kwamba Kristo ‘aliwaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.’​—1 Petro 2:21.

12, 13. (a) Ni mfano gani unaoonyesha inafaa kupongeza wafanya kazi wazuri, na watu hao walipewa thawabu gani? (b) Mtumwa asiyeleta faida alifanywa nini? (c) Malikizo yanakuwa na kusudi gani?

12 Kwa kutumia mfano Yesu alionyesha kwamba kazi yenyewe inampa mtu thawabu ya furaha. Mtu mmoja alikuwa anataka kwenda safari. Akawaita watumwa wake na kugawanya bidhaa zake kati yao kulingana na uwezo wa kila mmoja wenye kutofautiana na wa wenzake. Baada ya kutokuwapo kwa muda mrefu alirudi kufanya hesabu nao. Aliyepewa talanta tano alizifanya maradufu, aliyepewa mbili akazifanya maradufu, lakini mwenye kupewa talanta moja hakuitumia hata. Je, wale wafanya kazi wawili wenye bidii walithawabishwa namna gani? Je, ni kwa kupewa likizo? La, bali kazi zaidi! Bwana wao alisifu kila mmoja wa hao, akisema: “Vema, mtumwa mwema na [mwaminifu]”! kisha akaongezea hivi: “Ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako.” Bwana alipata furaha yake kutokana na kazi hii, na kwa kupewa nyingi zaidi waifanye, wale watumwa wenye bidii waliingia zaidi sana katika furaha yake. Lakini namna gani yule mtumwa mvivu? Iliamuliwa hivi: “Mnyang’anyeni talanta hiyo, mpeni yule aliye nazo talanta kumi.” —Mathayo 25:14-30.

13 Sasa mtumwa huyo mvivu alikuwa na nafasi ya kujikalia bure tu kilofa. Lakini je, alikuwa na furaha? La, mwisho wake ulikuwa “kilio na kusaga meno”! Ili tuwe na furaha tunahitaji kuwa na kazi yenye mafaa. Walakini, tunahitaji pia vipindi vya pumziko. Sisi si kama Yehova. Sisi huchoka. Lakini likizo likiisha kuturudishia nguvu zetu za kimwili na za fahamu na kuinua tena uchangamfu wetu, tunakuwa tayari kufanya kazi zaidi—ndiyo, tunakuwa na hamu nyingi ya kurudia kazi. Ndivyo inavyokuwa isipokuwa kama kazi yenyewe haipendezi na inafuata kawaida ile ile nyakati zote, bila kumpa mwenye kuifanya kusudi na maana, na ndivyo kazi nyingi za kilimwengu zilivyo leo.

14. Mwendo wa kufuatia mali mno una faida ya kudumu?

14 Lakini zaidi ya kuwako kazi zisizopendeza zinazopunguza wajibu wa kufanya kazi, watu wengi siku hizi wananaswa na mtego wa utafutaji mwingi mno wa mali. Hata watafute, je, mali zinazokusanywa na kuyazidi mahitaji yale ya lazima zina faida gani ya kudumu? Ni kama wana-siku-hizi wanavyosema, “Hutakwenda nazo, utaziacha.” Sulemani alitoa maana ya maneno hayo kwa mkazo zaidi: “Alivyotoka tumboni mwa mamaye, atakwenda tena tupu-tupu kama alivyokuja; asichume kitu cho chote kwa ajili ya kazi yake, hata akichukue mkononi mwake. Hiyo ndiyo balaa mbaya sana, ya kwamba kama vile alivyokuja, vivyo hivyo atakwenda zake; naye amefaidiwa nini mwenye kujitaabisha kwa ajili ya upepo?”​—Mhubiri 5:15, 16.

15. Wengine wananaswa na mtego wa mambo gani mengine ya bure tu?

15 Wengine wanajitia katika jambo jingine la bure tu: kufanya kazi ili wawe na kile ambacho fulani-wa-fulani anacho. Au, sana-sana, wawe na mali nyingi kuliko huyo fulani-wa-fulani. “Mimi nimejifunza pia kwa nini watu hutia bidii sana wafaulu,” akasema Sulemani. “Ni kwa sababu wanaona kijicho juu ya vitu ambavyo jirani zao wanavyo.” Au, “Maana yake ni ushindani mkali wa mmoja kuelekea mwingine.” (Mhubiri 4:4, Today’s English Version; NW) Hakika maisha na kazi za waovu ni bure tu, ni utupu: “Mtakuwa kama mwaloni ambao majani yake yakauka, na kama bustani isiyo na maji. Na mtu hodari atakuwa kama makumbi, na kazi yake kama cheche ya moto; nao watawaka pamoja, wala hapana atakayewazima.”​—Isaya 1:30, 31.

Kazi ya Kuchangamsha Sana Huko Mbele

16. Ni kazi gani ya kuridhisha iliyo huko mbele kwa ajili ya wanadamu watiifu?

16 Kazi haitaendelea siku zote tu kuwa ufuataji wa upepo kwa watu duniani. Itakuwa yenye kusudi na maana kama ile ambayo hapo awali mwanamume na mwanamke wa kwanza walipewa katika Edeni. Kusudi la Yehova la kutaka dunia iwe paradiso yenye kuenea kila mahali ikitunzwa na wanadamu waadilifu litatimizwa. (Isaya 55:11) Ufalme wa Mungu utaitawala dunia ya namna hiyo yenye kujawa na watu waadilifu ukisimamiwa na Kristo. Maisha katika mfumo mpya huo hayatakosa kamwe upendezi, kwa sababu kutakuwa na kazi nyingi sana za kufanya—si kazi ile ya bure tu na yenye utupu ya ulimwengu huu inayoifanya juma nzima ya kazi iwe kukuru-kukuru yenye kuchosha na kufanya watu wajisikie hawataki kurudi kazini siku ya Jumatatu. La, itakuwa kazi ya kupendeza na kusisimua sana ya kuifanya dunia iwe na hali za kuvuta macho, kutawala wanyama kwa upendo, kulea watoto, na kuelimisha wanadamu wafufuliwa, mpaka dunia itakapojawa na jamii ya watu waadilifu kisha iwe na mambo mengine mengi ya kufurahisha tusiyoyajua. Ndipo watu wenye shughuli nyingi ‘watakapofurahia kazi ya mikono yao na kuitumia kwa ukamili.’​—Isaya 65:22.

17. Ni nini kinachoonyesha kwamba maisha hayatatuchosha kwa kurudia-rudia mambo ya-a-a-le yale tu kwa sababu ya kuwa tumejifunza na kuyamaliza mambo yote kabisa?

17 Zaidi ya kuwa na kazi za mikono kutakuwako matatizo ya kushughulisha akili zenye ukamilifu, kufanya watu watumie kwa ukamili uwezo wao wa kufikiri. Hakuna hata siku moja ambayo wanadamu watajua mambo yote, “kwa jinsi mwanadamu asivyoweza kuvumbua kazi ya Mungu anayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho.” “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! hukumu zake hazichunguziki, wala njia zake hazitafutikani’” (Mhubiri 3:11; Warumi 11:33) Sikuzote kutakuwa na mambo yenye utatizi na mafumbo ya kuchunguzwa na kufukuliwa sana. Ingawa watumishi wa Yehova wataishi milele, hata umilele wenyewe hautawapa nafasi inayotosha waweze kuyajua mambo yote yanayohusu dunia na ulimwengu wote wa vitu vilivyoumbwa na Yehova.

18. Ni jambo gani ambalo lazima kwanza tufanye ndipo tuweze kuishiriki karama ya kazi tutakayopewa na Mungu katika dunia ya paradiso?

18 Walakini, kabla hatujakabidhiwa kazi hiyo ya kuchangamsha sana, kuna kazi ambayo lazima tuifanye sasa ili tuwe na uhakika wa kuufikia wakati huo unaokuja tuwe sehemu ya dunia hiyo ya paradiso. Kujifunza kwetu sasa kazi hiyo iliyo ya lazima ni shauri linalohusu kufa au kupona.

◻ Kwa sababu gani watu wana uhitaji wa kufanya kazi?

◻ Ni katika maana gani Yehova alipumzika baada ya kuzifanya mbingu na dunia?

◻ Hapo awali Mungu alimpa mwanadamu kazi gani yenye kusudi aifanye?

◻ Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba kazi inafaidi mwanadamu hata akiwa katika hali ya sasa ya kutokukamilika?

◻ Ni nini kinachoonyesha kwamba wanadamu waliumbwa ili wafurahie matunda ya kazi ngumu zao?

◻ Yesu alionyesha nia yake kuelekea kazi kwa njia gani?

◻ Ni kazi gani nzuri iliyo huko mbele kwa ajili ya watumishi wa Mungu?

[Picha katika ukurasa wa  5]

Mungu alimpa mwanadamu kazi ya maana

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki