Sura ya 25
Wale Waliochagua Mahali Bora
SIKUZOTE watu wengine wanajitakia wenyewe vitu bora. Watachukua vitu hivi wakati mwingine ye yote hajavipata. Umepata kuona hili?— Mimi nimeona.
Kwa mfano, chakulani nimeona sahani kubwa ikipitishwa. Ilijaa vipande vya mikate. Sahani ilipokuwa ikipitishwa, kila mtu kwa uangalifu alitazama vipande aone kama alichagua kikubwa kuliko vyote. Unafikiri ni vizuri kufanya hivyo?—
Kuna jambo jingine ambalo nimeona likitukia. Baba na mama wamechukua watoto wao kwenda nao kuamkia rafiki. Walipoingia katika nyumba ya rafiki, watoto walikimbilia kuketi penye viti vya starehe zaidi sana. Je! hivi ni vizuri?—
Mwalimu Mkuu alipokuwa duniani jambo fulani lilitukia. Alialikwa karamuni nyumbani kwa Farisayo mwenye sifa. Kulikuwa na wageni wengi walioalikwa. Wageni walipoingia kwa chakula, Yesu aliona kwamba walichagua mahali ambapo ni bora mezani. Walitaka mahali pa heshima. Ungependa kusikia ambayo Yesu aliwaambia?—
Aliwasimulia hadithi. Ilikuwa na shauri jema kwa wageni hao, na ina shauri fulani jema kwetu leo.
Yesu akasema: ‘Huenda mtu fulani akakualika kwenye karamu kubwa ya arusi. Unapokwenda, usichague kuketi mahali pa heshima zaidi sana. Kwa maana huenda tena mtu fulani mwenye sifa zaidi amealikwa. Ndipo aliyekualika pengine atakuja kwako na kusema, “Mpishe huyu!” Ndipo utaona haya wakati wengine wote wanakutazama ukienda mahali pa chini zaidi sana.’
Yesu alitaka kuonyesha wageni jambo jema kufanya. Basi akaendelea kuwaambia:
‘Unapoalikwa arusini nenda kaketi mahali pa nyuma. Ndipo labda yeye ambaye amekualika atakuja na kusema, “Rafiki yangu, njoo huku mbele zaidi.” Ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote wakati unasogea mahali ambapo ni bora.’—Luka 14:1-11.
Ulifahamu maana ya hadithi ya Yesu?— Na tuchukue mfano, tuone ikiwa ulifahamu. Tuseme ikiwa tungekwenda kula nyumbani kwa mtu fulani. Je! ungechagua mahali ambapo ni bora wakati ungekuwa tayari kuketi? Au ungemwachia mwingine mahali ambapo ni bora?— Unafikiri Yesu angetaka ufanye nini?
Chukua mfano mwingine. Wazia unapanda bas yenye kujaa tele watu. Je! ukimbilie kuketi, na kumwacha mzee asimame? Je! Yesu angetaka ufanye hivyo?—
Pengine mwingine atasema kwamba tunalofanya si kitu kwa Yesu. Lakini unaamini hilo?— Wakati Yesu alipokuwa karamuni hiyo nyumbani kwa Farisayo, aliwatazama watu walipokuwa wakichagua viti vyao. Je! hufikiri anapendezwa tena na lile tunalofanya leo?— Kwa vile sasa Yesu yuko mbinguni hakika ana uwezo bora wa kututazama.
Wakati kila mtu anapojaribu kupata mahali ambapo ni bora, inaweza kuleta matata. Mara nyingine hii inatukia wakati watoto wanapopanda motokaa pamoja. Mara mlango wa motokaa unapofunguliwa, wanakimbilia kukaa penye viti bora, vile vilivyo karibu na dirisha. Na mara hiyo kunakuwa na ugomvi. Wanakasirikiana kwa sababu kila mtu anataka mahali ambapo ni bora.
Hili laweza kutukia tena wakati watoto wanapokwenda kucheza mpira. Hata wakati bado kuanza mchezo huenda wakagombana juu ya nani atakuwa wa kwanza. Je! si vibaya sana mambo haya kutukia?—
Kutaka sikuzote kuwa wa kwanza kwaweza kuleta matata mengi. Hata kulileta matata kati ya mitume wa Yesu. Ulijua hilo?—
Yesu alikuwa amewapa wote shauri jema. Yesu aliwaambia kwamba watawala wa mataifa wanapenda kuwa wakubwa na wenye sifa. Wanataka kila mtu awatii wao. Lakini Yesu aliwaambia wafuasi wake wasiwe hivyo. Lakini, Yesu akasema: “Mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote.”—Marko 10:35-45.
Unajua analofanya mtumwa? Anawatumikia wengine, kuliko kuacha wengine wamtumikie. Anakaa mahali pa chini zaidi sana, si pa kwanza. Anatenda kama mdogo, si mtu mkubwa. Na kumbuka Yesu alisema kwamba anayetaka kuwa wa kwanza imempasa atende kama mtumwa kwa wengine.
Sasa, unafikiri hilo lina maana gani kwetu?— Je! mtumwa angegombana na bwana wake juu ya nani atakaa penye kiti kilicho bora?— Au je! angegombania nani atakayekula kwanza?— Yesu alionyesha kwamba sikuzote mtumwa anakuwa nyuma ya bwana yake. Je! sivyo imetupasa tufanye vile vile?— —Luka 17:7-10.
Ndiyo, ni njia ya Kikristo tuwe nyuma ya wengine. Hivi ndivyo Mwalimu Mkuu alifanya. Na tukifuata mfano wake tutakuwa wenye kupendeza kwa Mungu.
(Maandiko zaidi kututia moyo tuwe nyuma ya wengine yanapatikana katika Warumi 12:3 na Wafilipi 2:3, 4.)