Sura ya 36
Farisayo Mwenye Kujivuna
MAANA yake nini kuwa mwenye kujivuna? unajua?—
Hapa pana mfano. Je! umepata kujaribu kufanya jambo fulani ambalo hulijui sana? Pengine ulijaribu kuupiga mpira. Au labda ulijaribu kuruka kamba. Je! ye yote alipata kusema, “Ha! Ha! Ha! Mimi naweza kufanya vizuri zaidi kukushinda wewe”? Basi, mtu huyo alikuwa akijivuna. Yeye alikuwa akijisifu mwenyewe.
Wewe unaona namna gani wakati wengine wanapofanya hivyo? Unapenda? Basi, unafikiri wengine wangeona namna gani wakati unapojivuna?— Je! ni wema kumwambia mwingine, “Mimi ni mzuri zaidi kuliko wewe”?— Je! Yehova anawapenda watu wanaofanya hivyo?—
Mwalimu Mkuu alijua watu wengine waliofanya mambo kama hayo. Siku moja aliwaambia hadithi. Ilikuwa juu ya Farisayo na mtoza kodi.
Mafarisayo walikuwa waalimu wa dini wenye kiburi. Mara nyingi walitenda kana kwamba walikuwa wenye haki zaidi au watakatifu zaidi kuliko watu wengine. Farisayo wa hadithi ya Yesu alikwenda kwenye hekalu la Mungu katika Yerusalemu kusali.
Yesu alisema kwamba mtoza kodi naye alikwenda huko kusali. Sasa, karibu watu wote ha-wakuwapenda watoza kodi. Waliona kwamba watoza kodi walikosana nao. Na, zaidi ya hilo, watoza kodi wengine hawakuwa waaminifu sikuzote.
Pale hekaluni Farisayo alianza kusali kwa Mungu katika njia hii: ‘Ee Mungu, nakushukuru kwa vile mimi sifanyi dhambi kama watu wengine. Mimi siwapunji watu au kufanya mambo mengine mabaya. Mimi si kama mtoza kodi yule pale. Mimi ni mtu wa haki. Mimi ninakaa bila kula chakula mara mbili kwa juma ili niwe na wakati zaidi wa kufikiri juu yako. Nami ninatoa hekaluni sehemu ya kumi ya vitu vyote ninavyopata.’ Kwa kweli Farisayo yule alifikiri yeye alikuwa mtu wa haki, sivyo?— Tena alimwambia Mungu hili.
Lakini mtoza kodi hakuwa hivyo. Yeye hakujiona kwamba alifaa hata kuja karibu na hekalu la Mungu. Hakuinua hata macho yake kuelekea mbinguni. Basi aliendelea kusimama mbali hali ameinamisha kichwa shake. Alisikitika juu ya dhambi yake. Naye alijipiga-piga kifuani pake kwa kusikitika. Yeye hakujaribu kumwambia Mungu namna alivyokuwa mzuri. Lakini yeye alisali hivi: ‘Ee Mungu, unihurumie mimi mwenye dhambi.’
Ni nani kati ya wanaume hao unafikiri alikuwa akipendeza kwa Mungu? Je! alikuwa Farisayo mwenye kujivuna, yule aliyejiona alikuwa mzuri sana? Au alikuwa mtoza kodi, aliyesikitika juu ya dhambi zake?—
Yesu alisema: ‘Kwa Mungu, mtoza kodi ndiye aliyekuwa mtu wa haki zaidi kuliko Farisayo. Kwa sababu kila mtu anayejaribu kujifanya aonekane kama ni mzuri zaidi kuliko watu wengine atatelemshwa chini. Lakini yeye anayejiweka chini machoni pake mwenyewe atapandishwa.’—Luka 18:9-14.
Je! ulielewa somo ambalo Yesu alikuwa akifundisha?— Alikuwa akionyesha kwamba ilikuwa makosa kufikiri kwamba sisi ni watu wazuri zaidi kuliko watu wengine. Ebu tuone namna somo hili linavyopatana na maisha zetu.
Labda wewe na mtoto mwingine mnaulizwa maulizo fulani katika masomo. Namna gani ikiwa unaweza kujibu upesi, lakini mtoto mwingine hajibu upesi? Kwa kweli, unafurahi wakati unajua majibu. Lakini je! ungekuwa wema kumwambia mwanafunzi mwingine kwamba yeye hana akili?— Je! ni vizuri kujaribu kujifanya uonekane mzuri kwa kumfanya mtu mwingine aonekane mbaya?—
Hivyo ndivyo yule Farisayo alifanya. Alijisifu kwamba yeye alikuwa mtu mzuri zaidi kuliko mtoza kodi. Lakini Mwalimu Mkuu alisema kwamba alikosa.
Ni kweli kwamba mtu mmoja anaweza kufanya jambo fulani vizuri zaidi kuliko mwingine. Lakini je! hiyo maana yake ni kwamba yeye ni mtu mzuri zaidi?—
Ebu fikiri. Ikiwa tunajua mengi, je! tujivune?— Je! ni sisi tuliofanya ubongo wetu?— Sivyo, Mungu Ndiye aliyempa mwanadamu ubongo. Na vitu vyote tunavyojua tunajifunza kutoka kwa mtu mwingine. Labda tulisoma katika kitabu. Au labda mtu fulani alituambia. Hata ikiwa sisi wenyewe ndio tuliofikiria jambo hilo, tulilifanya namna gani? Kwa kutazama mambo ambayo Mungu alikuwa amefanya. Kila kitu tulicho nacho kimetoka kwa mtu mwingine.
Watu wengine wana nguvu. Je! hiyo inawafanya kuwa wazuri zaidi kuliko kila mtu mwingine?— Sio waliofanya miili yao, sivyo? Ni Mungu Ndiye aliyempa mwanadamu mishipa. Na Mungu Ndiye afanyaye chakula kikue ili tuweze kula na kupata nguvu.
Basi, ye yote wa sisi ana sababu ya kujivuna? Je! sisi ni watu wazuri zaidi kuliko watu wengine?— Kuliko kuwaambia wengine namna sisi tulivyo wazuri, kweli imetupasa tuwaambie namna Yehova alivyo mzuri sana, sivyo?— Kwa sababu Ndiye anayefanya iwezekane kwetu kufanya mambo vizuri sana.
Wakati mtu anapojaribu sana, jambo zuri ni kusema jambo fulani litakalomfurahisha. Pengine unaweza hata kumsaidia afanye vizuri zaidi. Hivyo ndivyo wewe ungependa watu wakufanyie, sivyo? Basi, Yesu alisema: ‘Kama vile unavyotaka watu wengine wakufanyie, wafanyie vivyo hivyo.’ Hiyo ni kanuni nzuri kufuata, sivyo?—Luka 6:31.
Tukifanya hivyo, hatutajisifu au kujivuna. Hatutaki tuwe kama Farisayo mwenye kujivuna.
(Kiburi na kujisifu ndiyo mambo ya kuepuka. Soma ambayo maandiko haya yanasema: Mithali 16:5, 18; 1 Wakorintho 4:7; 13:4)