Sura 94
Uhitaji wa Sala na Unyenyekevu
MAPEMA kidogo, Yesu alipokuwa katika Yudea, alisimulia kielezi kuhusu umaana wa kudumu katika sala. Sasa, katika safari yake ya mwisho ya kwenda Yerusalemu, anakazia tena uhitaji wa kutochoka kusali. Labda Yesu angali katika Samaria au Galilaya anapowasimulia wanafunzi wake kielezi hiki zaidi:
“Katika jiji fulani alikuwako hakimu fulani ambaye hakuwa na hofu yoyote kwa Mungu na hakuwa na staha yoyote kwa mwanadamu. Lakini alikuwako mjane wa kike katika jiji hilo na mjane huyo aliendelea kumwendea, akisema, ‘Hakikisha kwamba mimi napata haki kutoka kwa hasimu wangu katika sheria.’ Basi, kwa kitambo fulani hakimu hakuwa na nia, lakini baadaye alijisemea hivi, ‘Ingawa mimi sihofu Mungu wala sistahi mwanadamu, kwa vyovyote, kwa sababu ya mjane huyu kuendelea kunisumbua, nitahakikisha kwamba anapata haki, ili kwamba yeye asiendelee kuja na kunipiga-piga mpaka akanimalize.’”
Kisha Yesu anafanya utumizi wa hadithi yake, akisema: “Sikieni jambo ambalo hakimu, ingawa si mwadilifu, alisema! Kwa uhakika, basi, je! Mungu hatasababisha haki ifanywe kwa ajili ya wachaguliwa wake wanaompaazia kilio mchana na usiku, hata ingawa yeye ni mstahimilivu kuwaelekea?”
Yesu hadokezi kwamba Yehova Mungu anafanana kwa vyovyote na hakimu huyo asiye mwadilifu. Bali, ikiwa hata hakimu asiye mwadilifu ataitikia kusihi-sihi kwa daima, hakupasi kuwe na shaka kwamba Mungu, ambaye ni mwadilifu na mwema kabisa, atajibu watu wake wasiochoka kusali. Kwa hiyo Yesu anaendelea kusema: “Mimi naambia nyinyi, [Mungu] atasababisha haki ifanywe upesi.”
Mara nyingi watu walio dhalili na maskini hunyimwa haki, hali walio na uwezo mwingi na matajiri hupendelewa mara nyingi. Hata hivyo, si kwamba tu Mungu atahakikisha kwamba waovu wanaadhibiwa ilivyo haki bali atahakikisha pia kwamba watumishi wake wanatendewa haki kwa kuwapa uhai wa milele. Lakini ni watu wangapi wanaoamini kwa uthabiti kwamba Mungu atasababisha haki itendwe upesi?
Akimaanisha imani inayohusiana hasa na nguvu ya sala, Yesu anauliza hivi: “Wakati Mwana wa binadamu atakapowasili, je! kweli yeye atapata imani duniani?” Ingawa swali hili linabaki bila kujibiwa, maana inayodokezwa huenda ikawa kwamba huenda imani hiyo isiwepo sana wakati Kristo atakapowasili katika mamlaka ya Ufalme.
Miongoni mwa wale wanaomsikiliza Yesu wamo baadhi ya watu wanaojihisi kwa uhakika kwamba ni wenye imani. Wanajitegemea wenyewe kwamba ni waadilifu, na wanadharau watu wale wengine. Hata huenda baadhi ya wanafunzi wa Yesu wakatiwa katika kikundi hicho. Kwa hiyo yeye anaelekezea watu hao kielezi hiki:
“Watu wawili walipanda wakaingia hekaluni kusali, mmoja akiwa ni Farisayo na yule mwingine mkusanya kodi. Farisayo alisimama na kuanza kusali mambo haya akijiambia mwenyewe, ‘O Mungu, mimi nakutolea wewe asante kwamba mimi si kama watu wale wengine, wanyakuzi, watu wasio waadilifu, wazinzi, au hata kama huyu mkusanya kodi. Mimi hufunga mara mbili kwa juma, mimi hutoa sehemu ya kumi ya vitu vyote ninavyojipatia.’”
Mafarisayo wanajulikana sana kwa majionyesho yao ya uadilifu mbele ya watu ili wasifiwe nao. Siku zilizo kawaida ya nyakati za kufunga walizojitwika wenyewe ni Jumatatu na Alhamisi, nao wanafuatilia sana kijambo kidogo sana cha kulipa sehemu ya kumi ya hata vimea vya shambani. Miezi michache mapema kidogo, dharau lao kwa watu wa kawaida lilikuwa limedhihirishwa wakati wa Sikukuu ya Tabenakulo waliposema hivi: “Umati huu ambao hauijui Sheria [yaani, fasiri ya Kifarisayo inayotolewa kuhusu Sheria hiyo] ni watu walaaniwa.”
Akiendeleza kielezi chake, Yesu asimulia juu ya mtu ‘mlaaniwa’ wa jinsi hiyo: “Lakini mkusanya kodi akiwa amesimama umbali fulani hakuwa na nia hata ya kuinua macho yake kuelekea mbinguni, bali aliendelea kupiga-piga kifua chake, akisema, ‘O Mungu, uwe na neema kwangu mimi mtenda dhambi.’” Kwa sababu mkusanya kodi ameyakiri kwa unyenyekevu makosa ya kupungukiwa kwake, Yesu anasema: “Mimi nawaambia nyinyi, Mtu huyu alishuka kwenda nyumbani kwake akiwa amethibitishwa kuwa mwadilifu kuliko mtu huyo; kwa sababu kila mmoja ambaye hujikweza mwenyewe atashushiwa heshima, lakini yeye ambaye hujinyenyekeza mwenyewe atakwezwa.”
Hivyo Yesu anakazia tena uhitaji wa kuwa wanyenyekevu. Kwa sababu wanalelewa katika jamii ambamo Mafarisayo wanaojiona kuwa waadilifu ni mashuhuri sana na cheo na daraja hukaziwa sikuzote, haishangazi kwamba wanafunzi wa Yesu wanaathiriwa. Na bado, ni masomo mazuri kama nini ya unyenyekevu ambayo Yesu anafundisha! Luka 18:1-14; Yohana 7:49, NW.
▪ Kwa nini hakimu asiye mwadilifu anampa mjane ombi lake, na ni somo gani linalofundishwa na kielezi cha Yesu?
▪ Yesu atatafuta kuona imani gani awasilipo?
▪ Yesu anaelekeza kwa nani kielezi chake juu ya Farisayo na mkusanya kodi?
▪ Ni mwelekeo gani wa Mafarisayo unaopasa kuepukwa?