Sura ya 45
Namna ya Kumwambia Mungu, ‘Mimi Nakupenda’
JE! WEWE wajua kwamba mtu fulani alikupenda hata ulipokuwa hujazaliwa?— Basi, sisi tulijua ungezaliwa. Bila shaka, hatukujua wakati huo ungekuwa namna gani. Bado ulikuwa ukikua ndani ya mama yako. Lakini baba yako na mama yako walikwisha kuanza kufanya mambo mengi kuonyesha walikupenda.
Ndiyo sababu kulikuwako tayari nguo upate kuvaa mara ulipozaliwa. Na kulikuwako kitanda kidogo upate kulalia.
Na, lo! namna baba yako na mama yako walivyofurahi wakati mwisho walipokuona! Wakati huo walikupenda. Na wanakupenda wewe sasa, tena sana sana. Unampenda baba na mama yako, vile vile, sivyo?
Lakini sasa mimi ninafikiria mtu mwingine ambaye naye alikupenda ulipokuwa hujazaliwa. Unamjua ni nani?— Ni Yehova Mungu. Kwa kweli, Mungu alitupenda sisi sote tulipokuwa hatujazaliwa. Je! unajua namna tunavyojua alitupenda?—
Kwa sababu hapo zamani Mungu alimtuma Mwana wake atutolee sisi uhai wake. Tena, Mungu anakusudia kufanya dunia kuwa bustani nzuri ambapo tutaweza kuishi milele katika furaha, ikiwa tunataka.
Hii inakufanya wewe uone namna gani juu ya Mungu?— Inanifanya mimi kumpenda sana sana. Mimi nataka nimtumikie maisha yangu yote. Wewe je?—
Lakini tunaweza kumwambia Mungu hivyo namna gani?— Yesu alijua namna ya kumwambia Mungu hivyo. Sikiliza wakati ninapokusimulia aliyofanya.
Siku moja alikwenda kwenye Mto Yordani. Yohana Mbatizaji alikuwako huko. Yesu na Yohana wakatembea katika maji. Maji yalifika viunoni mwao. Unajua jambo ambayo walitaka kufanya?—
Yule mtu aliweka mkono mmoja mgongoni mwa Yesu. Akamweka Yesu kabisa chini ya maji kisha mara moja akamwinua tena. Alimbatiza. Kwa sababu gani alifanya hivyo? Yesu alimwomba yule mtu afanye hivyo. Lakini kwa sababu gani? Unajua?—
Yesu alifanya hivyo ili Mungu ajue kwamba Yesu alitaka kumtumikia yeye maisha yake yote, ndiyo, milele. Lakini je! Mungu alitaka Yesu awekwe chini ya maji kwa njia hiyo?— Ndiyo. Tunajua namna gani?—
Kwa sababu wakati Yesu alipotoka katika maji alisikia sauti kuu kutoka mbinguni ikisema: ‘Wewe ni Mwana wangu ambaye napenda. Napendezwa sana na wewe.’—Marko 1:9-11.
Kutoka hapa Yesu alifanya nini?— Basi, yeye alianza kuzunguka akisema juu ya Mungu kwa kila mtu ambaye angesikiliza. Aliwaambia juu ya ufalme wa Mungu. Aliwaambia namna wangeweza kuishi milele.
Wanaume wengine na wanawake waliamini ambayo Mwalimu Mkuu aliwafundisha. Lakini hawakufurahi. Unajua ni kwa sababu gani?—
Kwa sababu walifikiria mambo mengi mabaya ambayo walikuwa wamefanya. Walijua kwamba Mungu hakupendezwa na mambo hayo. Walijua Biblia ilisema mambo hayo yalikuwa mabaya. Sasa walitaka wawe kama Yesu wampendeze Mungu. Basi, unajua walichofanya?—
Waliomba wabatizwe kama Yesu alivyokuwa amebatizwa. Walitaka wamwambie Mungu kwamba walimpenda na kwamba walitaka wamtumikie maisha yao yote.
Sisi tunaweza kufanya mamoja leo. Bila shaka, wewe sasa bado unakua. Lakini hutatumia maisha yako yote ukikua tu, sivyo?— Sivyo kabisa. Siku fulani utakuwa mtu mzima. Wakati huo utafanya nini?—
Je! utakuwa kama Yesu? —Je! utafanya ambalo wanaume na wanawake waliomwamini Yesu walifanya? Je! utabatizwa? Ukifanya hivyo, utakuwa ukimwambia Mungu kwamba unampenda. Utakuwa ukimwambia kwamba unataka kumtumikia maisha yako yote. Bila shaka mimi natumaini utafanya hivyo. Na Mungu atapendezwa sana ikiwa unafanya hivyo.
Wakati mtu anapokuwa mtu mzima, kuna mambo mengi ambayo anaweza kufanya. Watu wengine ambao ni wazima wanaishi na jamaa zao. Wanafanya kazi na kupata fedha, na wananunulia jamaa zao vitu. Wananunua mavazi, chakula, vyombo vya nyumbani, hata motokaa. Hivi ni vizuri. Lakini je! hii ndiyo njia ya kumwambia Mungu kwamba wanampenda? Je! hii ndiyo njia ya kumwambia Mungu kwamba wanataka wamtumikie maisha yao yote?—
Wengi kati ya watu hawa hawataki hata kusikiliza wakati mtu mwingine anajaribu kusema kwao juu ya Biblia. Huenda hata hawasomi Biblia. Wengine kati yao hawasemi mara nyingi juu ya Mungu au juu ya Mwalimu Mkuu, hata kwa watoto wao. Labda wengine kati yao hata hawamshukuru Mungu kwa chakula wanachokula, au kusema naye katika sala usiku. Kweli hawampendi Mungu, sivyo?— Wewe usingetaka ukue na kuwa kama wao, sivyo? Lo! hiyo ingekuwa huzuni.
Mwalimu Mkuu alisema juu ya Mungu kwa namna zote za watu, kutia na watoto wadogo. Alijifurahisha kusema juu ya Mungu na juu ya mambo mazuri ambayo Mungu atawafanyia wale wanaompenda. Alisema kweli alipomwambia Mungu: ‘Baba, mimi nakupenda na nataka nikutumikie milele.’ Jifunze kwa kadiri uwezavyo juu ya Mwalimu Mkuu sasa wakati bado uko mtoto. Mayo wako na ujae upendo kwa Yehova Mungu. Ndipo usemi wako vile vile, utakuwa wa kweli utakapomwambia Mungu: ‘Mimi nakupenda na nataka nikutumikie milele.’
(Maandiko mengine ambayo unaweza kusoma yanayoonyesha namna tunavyoweza kuonyesho upendo wetu kwa Mungu ni: Mathayo 6:24-33; 24:14; 1 Yohana 2:16-17;1:3.)