Sura ya 3
Kuwa Mwanamume
1-6. Ni mambo gani ya ajabu yanayoonyesha namna tunavyokua mpaka tunapozaliwa? Je! kuna ye yote anayestahili kusifiwa kwa sababu ya hayo yote? (Zaburi 139:13-18)
TWAWEZA kufaidika tukitazama namna kila mmoja wetu alivyopata mwanzo wake. Fikiri: Miaka michache iliyopita ulikuwa kiyai kidogo zaidi ya nukta hii (.). Ulianza kukua katika tumbo la uzazi la mama yako kutokana na mwanzo huo mdogo sana. Mwishowe mwili wako ulikamilika ukawa na ubongo, macho, masikio, na viungo vingine vingi vya ajabu. Ukuzi huo wa ajabu ulitokeaje?
2 Wazazi wako sio waliofikiria namna umbo lako lingekuwa. Lakini, ilitukia wakati mbegu ya uzazi ya baba yako ilipoungana pamoja na yai dogo sana katika tumbo la uzazi la mama yako. Kwa muda kidogo, umbo lako lilifanyizwa ndani ya ile mbegu ndogo sana iliyoungana na yai la mama mpaka ukawa binadamu mwingine mzima!
3 Habari yote iliyohitajiwa ili upate kuumbwa inapatikana katika umajimaji (DNAa) wa mbegu hiyo ya mama iliyoungana na ile ya baba yako. DNA ndiyo asili ya maelfu mengi sana ya viungo vidogovidogo vilivyomo katika kila mbegu ya uzazi, navyo viungo hivyo vidogovidogo vinaunganishwa na mafungu 23 ya viini vinavyoitwa chromosomes. Kila mbegu imejaa habari nyingi sana hata ingejaa chumba kizima cha vitabu ikiwa ingeandikwa katika usemi wa wanadamu. Lakini labda jambo la kustaajabisha hata zaidi ni vile kila mbegu mpya ya mwili inavyopitishiwa habari zote hizo. Kwa hiyo kila mbegu ina habari zote zilizokuwamo katika yai la kwanza la mama yako lililoungana na mbegu ya baba!
4 Labda utauliza hivi: Ile DNA inawezaje kutumia habari inayotaka peke yake ili kufanyiza sehemu nyingi mbalimbali za mwili wa mtu inapotaka tu? Kwa mfano, inawezaje kuchagua maagizo yale tu yanayohitajiwa ili kufanyiza jicho? Na inapofanyiza jicho, inazuiaje habari zote za kufanyizwa kwa masikio yako, figo, ini, na viungo vinginevyo?
5 Ni ajabu. Wanadamu wameshindwa kujua. Ni kazi ya Muumba mkuu! Kwa sababu ya kupata habari juu ya mwili wa mwanadamu, mwandikaji mmoja wa Biblia alimwambia Mungu hivi: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.” (Zaburi 139:14) Je! ndivyo unavyoona?
6 Ile chembe ndogo sana iliyoungana na shahawa za baba, kisha wewe ukaanza kukua, iligeuka kwa muda wa miezi tisa tu kuwa kitoto kizima, mwungano wa ajabu wa maelfu ya milioni za chembe. Hutakua tena haraka hivyo! Lakini miaka kama kumi na mitatu au kumi na minne ukiisha kuzaliwa, unaanza kipindi kingine cha kukua haraka. Wakati huo unaanza kuacha uvulana uwe mwanamume.b Kipindi kizima hicho cha mageuzo, kinachojulikana kama kipindi cha kubalehe, kinaendelea muda wa miaka fulani. Kinamalizika unapokomaa mwili, kwa kawaida kati ya umri wa miaka 20 na 23. Hiki ni kipindi chenye magumu mengi katika maisha yako, lakini ni chenye maana sana sana. Ndicho kipindi kinachoonyesha namna maendeleo yako yatakavyokuwa wakati ujao.
MAGEUZO YA MWANZO WA KUBALEHE
7-12. (a) Wakati wa kubalehe, ni mageuzo gani yanayompata mwanamume? Je! kuna sababu yo yote ya kuwa na wasiwasi juu ya mageuzo hayo? (b) Kijana wa kiume anaweza kujua namna gani wakati viungo vyake vya uzazi vimekua hata anaweza kuzaa watoto?
7 Ubalehe unaanza katika umri ambao dalili (alama) za kuweza kuzaa zinaonekana. Kwa wavulana, umri huu unakadiriwa kuanza na miaka kumi na minne, na miaka kumi na miwili kwa wasichana, lakini haiwi namna ile ile sikuzote. Labda wewe ulianza kubalehe ukiwa na umri wa miaka kumi na mmoja au kumi na miwili, au labda sasa una umri wa miaka kumi na mitano au kumi na sita na bado hujaanza kubalehe. Lakini si ajabu kubalehe mapema au kuchelewa kubalehe, kwa hiyo usiwe na wasiwasi. Ni magumu gani unayoweza kutazamia wakati wa kubalehe?
8 Kwanza, labda utakuwa na sura mbaya na kasoro fulani fulani za mwili. Sababu yake ni kwa vile mifupa yako inarefuka na minofu yapaswa itanuke pamoja nayo. Kwa kupanuka hivyo sehemu nyingine za mwili zinakua haraka na nyingine polepole. Walakini, maumbo yanayotokea yatakwisha. Usiwe na wasiwasi, hata hivyo inafaa sana uwe mwangalifu usijiumize kwa kupatwa na mabaya.
9 Mishipa ya sauti ni kati ya zile sehemu za mwili zinazotanuka. Urefu wa ziada unaongeza unene wa sauti. Lakini huenda wakati wa kurefuka sauti yako ikawa nyembamba na kali nyakati nyingi usizotazamia. Tena hilo ni gumu jingine la kubalehe. Basi, inapokuwa hivyo na wengine wanacheka, wewe cheka nao, na haya itakwisha upesi.
10 Mageuzo hayo ya mwili yanaletwa na viungo vyako vya kupitishia maji mwilini, kutia na kifuko cha kikoromeo, viungo vilivyo karibu na figo na mifuko ya mbegu za uzazi (makende). Vinafanya mageuzo mengine. Geuzo moja ni kukua kwa mavuzi kando-kando ya viungo vya uzazi (katika kinena) , na vilevile makwapani na kifuani pako. Watu wengine wana mavuzi mengi na wengine machache, lakini wingi wa mavuzi hauonyeshi kwamba wewe ni mwanamume hodari. Nywele zinaanza kutokea usoni vilevile. Ijapokuwa hivi ni vinywele-nywele tu, unakaribia kunyoa ndevu.
11 Labda mageuzo yanayowasumbua mara nyingi sana wavulana wanaokaribia kuwa wanaume wazima ni yale ya viungo vya uzazi. Viungo hivyo vinakuwa vikubwa mwanzoni mwa ubalehe na kuanza kufanya kazi vilevile. Katika Mambo ya Walawi 15:16, 17, Biblia inataja “shahawa.” Ikiwa wazazi wako hawakuzungumza mapema jambo hili nawe, labda utakasirika utakapoona mara ya kwanza unatokwa shahawa. Ni nini kinachofanya shahawa zitoke?
12 Unapokuwa mtu mzima na kuweza kuzaa watoto, mboo yako inaanza kutoa umajimaji mweupe unaoitwa shahawa. Ni umajimaji ulio mzito zaidi ya maji na ndani yake mna mamilioni ya mbegu ndogo sana za uzazi. Yo yote ya mbegu hizi inaweza kuungana na yai la mwanamke iwe mimba na mwisho kuwa mtoto. Mara kwa mara mwili wako utatoa shahawa hizi. Kwa kawaida zinatoka wakati uko usingizini unapoota ndoto.
KUSUDI LA NGONO
13-15. (a) Mungu alifanya mpango wa ngono kwa kusudi gani? Ni kwa sababu gani aliweka sheria za ngono? (Waebrania 13:4) (b) Ni nani wanaofaa wakupe habari za kweli juu ya ngono? (Mithali 6:20)
13 Muumba wetu alifanya mpango wa ngono uwe njia ambayo kwa hiyo mwanamume anaweza kumwonyesha mwanamke upendo mwingi wazae watoto wao. Lakini Mungu aliweka sheria juu ya ngono, akaeleza kwamba ngono zifanywe na mwanamume na mwanamke tu waliofunga ndoa pamoja. Sababu yake ni kwa vile Mungu alikusudia kila mtoto anayezaliwa awe na baba na mama wa kumlea. Kwa hiyo, ni makosa machoni pa Mungu ikiwa watu wasiofunga ndoa pamoja wanafanya ngono.
14 Lakini watu waliofunga ndoa pamoja, ngono ni njia nzuri sana ya kuonyeshana upendo. Mume analala karibu sana na mke wake hata mboo yake inaingia vyepesi katika kuma ya mke wake. Kufanya hivyo kwaweza kuwapa raha nyingi. Wakati wa kufanya ngono, zile shahawa za mume zinatoka mwilini mwake kupitia kwa mboo yake mpaka kuingia katika kuma ya mke wake. Shahawa hizo zinatembea katika kuma, na ikiwa katika mke mna yai lililokomaa, mbegu ya mume wake inaweza kuungana nalo na kuwa kitoto. Basi, unaona kwamba Mungu alifanya viungo vya uzazi vitimize kusudi lenye heshima, yaani, kupitisha uhai kwenye vizazi vingine. Ndiyo sababu viungo hivi vya uzazi vyafaa vitumiwe kulingana na sheria za Mungu.
15 Njia inayofaa kujibiwa maulizo yako juu ya kubalehe ni kuwauliza wazazi wako, zaidi baba yako. Baba yako amekwisha kupatwa na kila jambo ambalo limekupata, tena zaidi. Baba yako anaweza kukupa habari nzuri na ya kweli itakayokusaidia na kukuletea furaha kuliko unavyoweza kuambiwa na vijana wengine juujuu tu na kwa upuzi. Ikiwa baba yako hawezi kukupa habari au shauri la Neno la Mungu, ingekufaa sana ujue Neno la Mungu linavyosema. Wazee katika kundi la Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.
KUJIONYESHA UNASTAHILI HUPEWA MADARAKA
16-18. (a) Ni katika njia gani wazazi wako wamekutia moyo ujitegemee kidogo? Maoni yako juu ya mapendeleo hayo yatageuzaje nafasi zako za wakati ujao? (b) Ni kwa sababu gani vijana wengi wanajiunga na “wahuni”? Huenda kufanya hivyo kukawaongoza wapi? (1 Wakorintho 15:33)
16 Ni kawaida kutaka kujionyesha namna ulivyo, yaani, kujiona wewe ni mtu tofauti unapokaribia kuwa mwanamume mzima. Ni jambo la kawaida vilevile kutaka kujitegemea kidogo. Bila shaka wazazi wako wataanza kukuweka tayar kwa wakati utakapoweza kujitegemea. Namna gani?
17 Bila shaka ni kwa kukupa polepole madaraka na mapendeleo zaidi ya kushiriki kuamua utakayofanya. Labda watakuruhusu uchague mwenyewe masomo unayopendelea zaidi kujifunza shuleni au pengine watakuruhusu ufanye kazi ya kibarua. Pengine utaruhusiwa ujinunulie vitu vyako mwenyewe. Lakini lo lote ambalo wazazi wako wataona lafaa kufanya katika habari hii, itakuwa juu yako kujionyesha unastahili kupewa madaraka. Ukitenda kitoto au kuwa mwenye “kichwa kikubwa,” labda wataona yafaa waache kukupa mapendeleo zaidi mpaka utakapojionyesha kuwa mwanamume anayestahili.
18 Kutaka kujionyesha namna ulivyo na kujitegemea kidogo kunafuatana na tamaa nyingine za asili. Utaona uhitaji wa kuheshimiwa na wengine kwa namna ulivyo na unayoweza kufanya. Vijana wengine wanataka kutimiza tamaa yao ya kujionyesha walivyo na kutambuliwa na watu kwa kujiunga au kuwa “wahuni.” Lakini kwa kawaida wahuni hao wana mwenendo wao wenyewe, na sikuzote mwenendo huo unawaongoza kufanya mabaya na hata uhalifu (ubaya) mkubwa mara nyingine kama ushuhuda unavyoonyesha. Labda jambo kubwa zaidi linalotia vijana katika matata ni urafiki mbaya.
19, 20. Sababu gan1 uhusiano (ushirika) mzuri na wazazi wako ni wa maana sana? Ni nini kingeweza kuuharibu? (Mithali 23:24, 25)
19 Wakati wa kipindi hiki cha maisha ndipo unapoanza kufahamu namna sura yako itakavyokuwa utakapokuwa mwanamume mzima. Lakini imekupasa vilevile uanze kufikiria zaidi na zaidi namna sura yako ya ndani itakavyokuwa, ile ambayo Biblia inaita “mutu wa moyo, asiyeonekana.” (1 Petro 3:4, ZSB) Umri huu sio wakati wa kujiacha ujitenge na wazazi wako na wengine katika jamaa ukitaka kujitegemea zaidi. Mageuzi unayopata wakati wa kubalehe, na tamaa nyingine za ghafula unazoona na kujifunza kuzizuia, zinakufanya uhitaji zaidi upendo na uongozi wao wa kukuimarisha.
20 Basi, kuliko kujitenga na wazazi wako, wakaribie zaidi ili ujifunze kwao kadiri uwezavyo unapokaribia sasa kuwa mtu mzima. Hutasikitika kwa kufanya hivyo. Vilevile utawafurahisha sana na kuwafanya wakufurahie wewe mtoto wao wa kiume.
[Maelezo ya Chini]
a DNA ni jina linalotumiwa badala ya deoxyribonucleic acid.
b Sura inayofuata inazungumza juu ya mageuzo ya, usichana kuwa mwanamke mzima.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Mbegu ndogo sana inageuka kuwa mtoto kwa muda wa miezi tisa tu