Sura ya 4
Kuwa Mwanamke
1-3. Ni nini linaloweza kumfanya msichana asumbukie ukuzi wake wa kimwili wakati wa kubalehe? Lakini ni nini linalotukia mwishowe?
MWISHOWE masika yanakwisha, kiangazi chaja. Mwishowe miti yenye kuchanua maua inageuka kuwa miti yenye kuzaa matunda. Ndivyo wasichana wachanga wanavyogeuka kuwa wanawake wazima. Kama vile hali ya ua inavyoonekana likiisha kufunguka, ndivyo na hali yako ya kuwa mwanamke inavyoonekana wazi zaidi kikiisha kupita kipindi hiki cha kubalehe. Kuna mambo mengi unayoweza kufanya wakati wa ukuzi huu ili upate matokeo yenye kufurahisha.
2 Unakuwa mrefu kidogo wakati huo wa miaka ya kubalehe, ukiongezea kimo chako inchi kama tano au sita hivi (sentimita 12 kufika 15). Vilevile unakuwa mzito kidogo. Kama kawaida, itakuwako miaka fulani utakapoona unakua haraka sana na unaongeza uzito. Labda utaona wasichana wengine wa umri wako wakivuvumka (wakikua haraka sana) kukushinda wewe, au labda wewe unawashinda. Usiwe na wasiwasi kwa sababu wengine wanakua haraka kukushinda au wewe unawashinda. Kila mtu ana wakati wake wa kukua haraka sana. Kwa kawaida, wasichana wanatangulia wavulana mwaka mmoja au miwili katika kipindi hiki cha kukua haraka sana. Kwa kweli, kuna wakati wasichana wanapoweza kuwa warefu kushinda wavulana wenye umri ule ule. Lakini wavulana wanakuja kulingana nao, na kama ilivyo kawaida, mwishowe wavulana huwa warefu na wenye nguvu kushinda wasichana kwa vile wanavyochukua muda mrefu kukua kuliko wasichana.
3 Kwanza, mara nyingine sehemu moja ya mwili inakua haraka kushinda sehemu nyingine wakati wa kipindi hiki cha ukuzi wa haraka sana. Pengine miguu au mikono yako inaweza kuonekana kuwa mirefu sana ikilinganishwa na sehemu nyingine za mwili wako. Lakini mwishowe, sehemu nyingine za mwili zinaendelea kukua na kusawazika. Kwa kawaida, kurefuka kwa kiwiliwili na kupanuka kwa kifua kunatokea mwishowe. Maumbo ya uso yanageuka. Wakati ule ule sehemu nyingine za mwili zinaanza kunenepa ili mwanamke awe na umbo zuri.
MAGEUZO MENGINE YA MWILI
4-6. (a) Ni ‘mambo gani ya kike’ yanayoanza wakati wa kubalehe? Mageuzo hayo ya mwili yana sababu gani? (b) Ni mageuzo gani mengine ya mwili yanayotukia vilevile wakati huu, na kwa sababu gani?
4 Lakini yanatukia mageuzo mengine wakati wa kubalehe kwa mwanamke. Huo ndio mwanzo wa yale ambayo Raheli, mwanamke anayetajwa katika Biblia, aliyaita “mambo ya kike,” yaani, hedhi (kuingia mwezini). (Mwanzo 31:34, 35) Hiki ni kipindi chenye kufurahisha sana, kwa maana kinaonyesha kwamba umeifikia hali ya kuwa mwanamke. Zile sehemu zenye kutoa umajimaji ndani ya mwili wako zimeanza kufanya kazi. Zinaamsha vifuko vya mayai (ovaries) vianze kutoa mayai, kwanza bila mpango mzuri, lakini tokea hapo inakuwa kila baada ya juma nne. Linapotolewa, yai hilo linatelemka katika tumbo lako la uzazi (chumba cha mtoto) lililokwisha kuamshwa litoe tabaka ya pekee ya kupokelea yai hilo ikiwa limeungana na shahawa za mwanamume. Chembe hiyo ya uzazi isipoungana na mbegu ya mwanamume, mwishowe tabaka hii inaondolewa kama kitu kisichotakiwa. Hii ndiyo inayotokeza hedhi (kuingia mwezini), kile kipindi cha kutokwa damu ya mwezi, umajimaji na ngozi-ngozi. Ijapokuwa kuingia mwezini kunafuatana na maumivu au usumbuo, ni hali ya kawaida wala si jambo la kusumbukia sana.
5 Vipindi hivi vya mwezini vinaanza wakati gani? Watu wanatofautiana mwanzo wa kuingia mwezini. Ijapokuwa katika nchi nyingi wastani ya vipindi hivi ni karibu na umri wa miaka kumi na mitatu, huenda msichana akaanza kuingia mwezini mapema sana akiwa mwenye umri wa miaka kumi au hata mapema zaidi ya umri huo, hali huenda mwingine aanze akiwa mwenye umri wa miaka kumi na sita au hata baadaye. Vilevile, muda wa kutokwa damu ya mwezi unaweza kutofautiana tangu siku tatu mpaka tano.
6 Wakati mageuzo hayo ya kutoka utoto kuwa mwanamke mzima yanapotokea, vilevile nyonga zako zinapanuka na matiti (maziwa) yako yanaanza kukua. Mageuzo yote hayo yaliyo mengi, mengine yakiwa wazi na mengine yasiyo wazi, ni matayarisho ya kutimiza daraka lenye sehemu mbili katika maisha ambalo Muumba wanadamu amewawekea wanawake, yaani, kuwa mke na kuwa mama watoto. Nyonga pana zaidi wanazokuwa nazo wasichana zinasaidia iwe vyepesi zaidi wakati wa kuzaa na vilevile kubeba watoto wadogo. Yale mafuta yaliyo katika mwili wa mwanamke yanayotokea wakati wa kuchukua mimba ni akiba inayoweza kutumiwa anapolisha watoto wasiozaliwa bado au wale ambao wamezaliwa hivi karibuni, na wakati wa kuzaa matiti yanaanza kuwa na maziwa.
KUVUTIA ZAIDI WANAUME
7-10. (a) Kukua kwa mwili wa msichana kunampaje daraka zaidi la mwenendo wake? (b) Daraka hili linaonyeshwaje katika Wimbo Ulio Bora kwa kulinganisha msichana fulani na “ukuta” na “mlango”?
7 Yale mapendeleo ambayo Yehova Mungu Muumba wanadamu aliwapa wanawake yanafuatana daraka la kuheshimu na kufuata kusudi la Muumba. Ule uvutano ambao Mungu aliweka kati ya wanaume na wanawake unakamatana sana na uzazi. Wakati mwili wa msichana unapokua kiasi cha kuweza kuzaa watoto, anavuta wanaume zaidi ambao wamefikia vilevile hali ya kuweza kuzaa watoto. Lakini uvutano huu unaweza kutumiwa vibaya. Basi, ni jambo gani unalohitaji kukumbuka ili uweze kufuata mwendo mzuri utakaokuletea furaha ya milele wakati ujao na kupata baraka ya Mungu?
8 Tunaona maneno yenye kupendeza yaliyosemwa bila shaka na kaka za msichana Mshulami, katika kitabu cha Biblia, Wimbo Ulio Bora. Kwanza, mmoja alisema hivi: “Kwetu sisi tuna [dada] mdogo, wala hana maziwa; tumfanyieje [dada yetu], siku atakapoposwa?” Yaani, wangemfanyiaje dada yao wakati angekuwa na matiti (maziwa), wakati angekuwa mwanamke mzima na sasa angetaka kuchumbiwa? Kaka yake mwingine alijibu, akisema hivi: “Kama akiwa ni ukuta, tumjengee buruji za fedha; na kama akiwa ni mlango, tumhifadhi kwa mbao za mierezi.” (Wimbo Ulio Bora 8:8, 9) Hii maana yake nini?
9 Inaelekea usemi wao wa mfano ulikuwa na maana ya kwamba kama dada yao angekuwa imara kama “ukuta” wangempa zawadi nzuri na kumheshimu. Angewezaje kuwa imara kama ukuta? Kwa kukaza moyo sana aendelee na mwenendo mtakatifu, kwa kuonyesha nguvu za kupinga vishawishi vyo vyote vya kumtia katika mwenendo wa uasherati. Angejionyesha kuwa imara na mwaminifu akifuata sana kanuni za haki wakati angestahili kuolewa. Lakini, kama angekuwa kama “mlango” unaofunguka wakati mtu anapousukuma kidogo, hata mtu asiye safi, hapo ingewapasa wachukue hatua za kumzuia kwa vile hawezi kuaminika kwa habari ya wanaume. Vilevile angekuwa kama mlango unaofunguka kisha asionyeshe mapenzi, akimpenda huyu, kisha anamkataa na kumpenda mwingine.
10 Yule msichana Mshulami, akiwa sasa mwanamke mzima mwenye matiti (maziwa), alishinda jaribu hili akaweza kuwaambia kaka zake hivi: “Mimi nalikuwa ukuta, na maziwa yangu kama minara; ndipo nikawa machoni pake [yaani, machoni pa mchumba wake] kama mtu aliyeipata amani.”—Wimbo Ulio Bora 8:10.
11-14. (a) Ni kwa sababu gani kuvaa mavazi mafupi au yenye kubana sana kunamletea msichana magumu yasiyotakiwa? (b) Wewe kama msichana, ungetaka zaidi umvute kijana mwanamume kwa sababu gani hasa?
11 Vilevile wewe, unalo jaribu la kushinda wakati unapokaribia kuwa mwanamke mzima. Ukitaka kufurahia amani ya kweli ya akili, ya moyo na ya dhamiri, na kujilinda usipate matatizo yanayoharibu amani, ni lazima ujiweze na kushikamana sana na yaliyo haki. Je! uonyeshe wazi zile sehemu za mwili wako za umama kwa kuvaa mavazi mafupi yanayoacha matiti wazi au yenye kubana sana? Kufanya hivyo kungeamsha nyege za wanaume. Halafu?
12 Je! utakuwa imara na mwenye nguvu za kuzuia mikazo yote inayoweza kusababishwa na sehemu hizo za mwili zinazoachwa wazi? Ijapokuwa unaonyesha kukomaa kimwili, je! umekomaa kiakili na kimoyoni, upate kuwa tayari kuolewa na kuwa mama? Paka anakuwa tayari kuzaa watoto akiwa mwenye umri wa miezi kumi na miwili na aweza kuangalia vizuri watoto wake maana anajikuta amekwishajua kufanya hivyo bila kufundishwa. Lakini wanadamu si kama wanyama wanaotenda bila kufundishwa. Inawapasa wanadamu wajifunze mambo mengi kuliko kurithi tu, na kujifunza kunataka wakati mwingi. Kufanya haraka kungekuwa kama kujaribu kulazimisha maua yachanue kabla ya wakati wao. Kufanya hivyo kungeharibu ua na uzuri wo wote unaoweza kuonekana wakati ujao. Vilevile ukumbuke kwamba ndoa si kuwa bibi-arusi tu. Inamaanisha vilevile kuwa mtunza nyumba, mpishi na mfua nguo, na kuwa mama kunataka saburi na kuvumilia sana watoto katika nyakati nzuri na nyakati mbaya, wakati wa magonjwa na wakati usio wa magonjwa.
13 Zaidi ya hayo, ijapokuwa msichana anaona amekuwa tayari kuolewa, anataka kujaribu kuvuta mume wa namna gani? Ikiwa kijana wa kiume anavutwa kwa sababu ya ngono ambazo msichana anaweza kumfurahisha nazo tu, je! kweli ni mume mwema? Je! si afadhali kutafuta urafiki unaodumu kwa sababu ya vile ulivyo katika akili na moyo wako kuliko kujaribu kuwa na urafiki wa kuvutwa na ngono? Unaweza kufanya hivyo kwa kusitawisha tabia zenye kupendeza wengine. Vilevile unaweza kufanya hivyo kwa mazungumzo yako, kwa maoni yako mazuri ya maisha yenye uchangamshi, kwa kuonyesha kwamba unaona ubora wa uaminifu, kiasi, adabu, fadhili na kupenda wengine.
14 Unaweza kuonyesha kwamba unafuata haya kwa kutokuacha sifa nzuri hizi ufurahie kwa muda kile ambacho kingekufanya uache kujiheshimu na kuheshimiwa na wengine unaoheshimu, kusifu na kupenda sana. Unaweza kuwa rafiki ya watu walio na urafiki ambao sikuzote utauona kuwa bora sana na unaoweza kukuletea furaha ya kweli ukiwa hasa na miradi ya maisha ambayo ni yenye kufaa sana, kwamba wataka ‘kumkumbuka Muumba wako siku za usichana wako.’—Mhubiri 12:1.
MAONI YANAYOFAA JUU YA SURA
15, 16. (a) Ijapokuwa ni kawaida kutia sana sura yako urembo, ni nini kitakachoongeza zaidi furaha yako ya wakati ujao? (b) Eleza maana ya Mithali 11:22 kulingana na kawaida ya maisha ya kila siku. Vilevile Mithali 31:30.
15 Ni kawaida ya wasichana kutia sana sura zao urembo. Lakini usifanye urembo kupita kiasi, wala usichukie umbo au sura yako kama kwamba wakati wako wote ujao unategemea hilo. Watazame watu wazima karibu nawe—watu unaopenda na kusifu sana. Je! wengi wao au karibu wote si watu wenye sura za kawaida? Uzuri wa sura silo jambo kubwa sana la kumpatia mtu furaha ya wakati ujao.
16 Na hili ni sawa na msichana mwenye urembo wa kimwili. Imempasa afahamu kwamba mwishowe wanawake wengi warembo wanakuwa na maisha yasiyo na maana, na mara nyingi maisha ya umalaya. Ni kama mithali ya Biblia inavyosema: “Kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe, kadhalika mwanamke mzuri asiye na akili.” (Mithali 11:22) Ndiyo, ni kama Biblia inavyosema tena kwamba, “huenda urembo ukadanganya, na uzuri ukawa wa bure; lakini mwanamke anayemwogopa Yehova ndiye anayejipatia sifa.”—Mithali 31:30, NW.
HUFIKIA USAWA WA MAONO YA MOYONI
17-19. (a) Ni mageuzo gani ya maono ya moyoni ambayo msichana aweza kupata wakati wa kubalehe? Ni nini kinachoweza kumsaidia apate usawa wa moyoni? (Wagalatia 5:22, 23) (b) Ni tabia gani zinazoweza kusaidia mtu awe imara vilevile?
17 Huenda kipindi cha kubalehe kikaleta mageuzo ya maono ya moyoni. Kama vile wakati mmoja msichana mdogo anavyoweza kujiona ana nguvu nyingi na wakati mwingine ajione amechoka sana, ndivyo na maono yake ya moyoni yanavyoelekea kutofautiana sana. Huenda vipindi vya kuchangamka na vyenye furaha vikafuatana upesi na vipindi vya kutochangamka na vyenye huzuni. Labda utadhani una kasoro usijue utakuwa mtu wa namna gani. Wasichana wanaobalehe wanapatwa na wasiwasi na mashaka zaidi katika jamii ya watu wa kisasa wenye maendeleo na mitindo yenye kugeuka-geuka.
18 Ingekuwa vyepesi kushindwa na hali hii yenye ukosefu wa imara na kuwa mtu mwenye kujitenga na mwenye kujifikiria mambo yake mwenyewe, au kugeuka kuwa mwenye kujitegemea na mwenye kujidai sana. Wasichana wengine wanaonyesha ukatili na kuwa wenye hasira-hasira au maneno yasiyo ya adabu. Wengine wanajidai bure tu na kuwa wenye akili chache. Lakini ni bure kufanya hivi; kunaifanya hali kuwa mbaya zaidi. Kwa vile sasa unaacha utoto, huu ndio wakati wa kujitahidi sana kusitawisha matunda ya roho ya Mungu, yaani, upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole na kujiweza.
19 Sitawisha tabia zinazoleta hali ya kuwa imara vilevile. Mahali pa kuacha chumba chako kiwe chenye kuvurugana, kipange kwa utaratibu na kwa mpango mzuri. Jitahidi kujizoeza kulala na kula bila kuchelewa; mwili wako unaokua wahitaji msaada wote unaoweza kuupa. Kwa kadiri unavyoweza kufuata mambo haya, ndivyo utakavyojiona kuwa mtu mtulivu na mwenye imara, na hili litakusaidia kutuliza maono yako ya moyoni.
20, 21. (a) Unapotaka kuuliza mau1izo juu ya maisha, ni kwa sababu gani utapata habari yenye kutegemeka zaidi kwa wazazi wako kuliko kwa vijana wengine? (b) Ni nini hasa, kitakachokufanya uwe mtu mwenye kupendeza sana?
20 Usiruhusu hata kidogo kipindi hiki chenye mageuzo kikutenge na wazazi wako. Wanaweza kukusaidia na kukuimarisha ili usawazike wakati wa kipindi hiki chenye mageuzo. Unapokazwa sana na wengine wenye umri wako ili uwe kama wao, fahamu kwamba hata wao wanaona mageuzo hayo kama wewe. Ndiyo sababu linalowapendeza leo huenda lisiwapendeze kesho hata kidogo. Kusumbukia mno wanavyokufikiria kutazidisha magumu yako tu. Ndiyo sababu unapokuwa na maulizo ya mambo yako mwenyewe, wazazi wako ndio wanaofaa zaidi kukupasha habari hizo. Wanaweza kukupa jibu kamili na lenye kusawazika kuliko wanashule wenzako.
21 Kama vile manyunyu ya kwanza ya mvua yanavyofuatana na maua mazuri, ndivyo utakavyoona njia ya kuwa imara na hakika ukijifunza kuyashinda magumu bila kuhangaika. Ijapokuwa imekupasa ufikirie sana kutunza afya yako na usafi wa mwili wako (kwa kula chakula kizuri na kufuata sikuzote kanuni za afya) , si lazima ufikirie mno hali yako ya nje, bali hali yako ya ndani. Kujipamba kwa “roho ya upole na utulivu” inayofanyizwa na ‘utu wa moyo wako usioonekana’ ndiko kutakakokufanya upendeze sana machoni pa Mungu na wanadamu.—1 Petro 3:3, 4.
[Picha katika ukurasa wa 28]
Je! wewe ni kama mlango . . .
[Picha katika ukurasa wa 29]
. . . au kama ukuta?
[Picha katika ukurasa wa 32]
Je! wewe unahangaikia sura kupita kiasi?