Kugeuka Kutoka Usichana Kuingia Katika Utu Uke
Mambo ya hakika ambayo vijana wanataka kujua
MWISHOWE wakati wa masika unapita na wa hari kuingia; nyuma ya hapo miti yenye maua inakuwa miti yenye kuzaa matunda. Kwa hiyo, vile vile, ndivyo vijana wa kike wanavyokuwa wanawake wachanga kama kawaida. Ni mageuzi makubwa kama yalivyo kutoka utoto uchanga kuingia katika ujana.
Kama vile tumba linapofunguka, likionyesha wazi ua lilivyo, kwa hiyo, vile vile, wakati huu upitapo, ndivyo itakavyoonekana wazi zaidi wewe utakuwa mwanamke wa namna gani. Ujapokuwa upekuzi waweza kuwa wenye nguvu nyingi ndani yako, itakupasa kungoja uone. Lakini kuna mengi uwezayo kufanya kushiriki kuleta matokeo yenye furaha katika ukuzi huu.
Kwa kawaida wakati wa kubalehe mpaka kupevuka unaanza katika karibu umri wa miaka kumi na mmoja kwa vijana wa kike na huenda ukaendelea mpaka karibu umri wa miaka kumi na saba au kumi na minane. Ni wakati ulio na furaha zake na magumu. Sehemu upatayo kutoka kila mojawapo ya hali hizi yaweza kukutegemea wewe sana. Kujua na kufahamu mambo fulani yenye msaada kwaweza kukufaa sana.
MAGEUZI YA MWILINI NA SABABU YAKE
Moja ni namna mwili wako unavyogeuka na sababu yake. Wakati wa miaka yako ya kubalehe, si kwamba tu unakuwa mrefu zaidi, ukiongezea urefu wako labda inchi tano au sita, lakini vile vile unakuwa mzito zaidi, ukiongeza karibu ratli 35. Kwa kawaida, miaka fulani utakua sana, wakati ambapo kadiri yako ya kukua katika urefu na uzito itakuwa ya kasi sana. Sasa, huenda ukawaona vijana wengine wa kike wa umri wako wakikupita kwa ghafula, au huenda ukajiona mwenyewe ukiwapita wao kwa kasi. Bila ya kujali ilivyo, hakuna haja ya kuwa na wasiwasi juu ya jambo hili. Kila mtu ana wakati wake wa ukuzi huu wa kasi. Kwa kawaida vijana wa kike wanaingia katika ukuzi huu wa kasi mwaka mmoja au miwili mapema kuliko vijana wa kiume. Kwa kweli, kuna wakati ambapo huenda vijana wa kike waelekee kuwa warefu zaidi kuliko vijana wa kiume wa umri ule ule. Lakini vijana wa kiume wanawafikia, kwa kuwa ukuzi wao unaendelea kwa muda mrefu zaidi kuliko ule wa vijana wa kike, kwa kawaida vijana wa kiume wanakuwa warefu zaidi—na wenye nguvu zaidi.
Nyakati nyingine ukuzi huu wa kasi unaonekana zaidi katika sehemu moja ya mwili kuliko katika nyingine. Huenda nyayo zako au mikono ikaelekea kuwa mirefu zaidi kwa njia ya kuhuzunisha ikilinganishwa na sehemu nyingine yote ya mwili wako. Lakini, nyuma ya hapo, sehemu nyingine yote ya mwili inaanza kukua nayo mambo yanakuwa sawa, kwa kawaida kurefuka kwa kiwiliwili nacho kifua kikiongezeka mwishowe. Mistari ya uso inageuka, kwa kawaida ikiwa myembamba zaidi, kidevu kinakuwa kilichochongoka zaidi na pua ndefu zaidi. Wakati ule ule sehemu nyingine za mwili zinaanza kutokeza mafuta mafuta yanayoipa sura umbo la mviringo la mtu wa kike.
MATAYARISHO KWA AJILI YA DARAKA KUBWA KATIKA MAISHA
Lakini ukuzi mwingine unatukia mnamo kubalehe kwa watu wa kike. Ndio mwanzo wa ambayo mkewe Yakobo Raheli aliyaita “mambo ya kike,” mwezi. (Mwa. 31:34, 35) Katika maana fulani, ni wakati wenye kusisimua—unaonyesha kwamba umefikia mwanzo wa utu uke. Vitu fulani vilivyomo katika damu vyenye kuchochea viungo vingine mwilini vimeanza kufanya kazi. Vinachochea vifuko vya mayai vilivyomo tumboni vianze kutoa chembe za mayai, kwa njia isiyo ya kawaida kwanza, lakini nyuma ya hapo karibu mara moja kila majuma manne. Wakati chembe ya yai inapotolewa inashuka kuingia katika tumbo la uzazi au mji wa mimba, ambao umechochewa kutokeza tabaka ya pekee ya kupokea yai likitungwa mimba. Yai linapokaa bila ya kuzaa, wakati fulani nyuma ya hapo tabaka hii inaondoshwa. Hii ndiyo inayoleta mwezi, kutolewa kwa damu kwa wakati wake, maji maji na takataka kadiri fulani ya matengenezo ya chembe. Kwa hiyo, ingawa hii huenda ikafuatana na maumivu fulani au masumbuo, ni utaratibu wa kawaida nao haupaswi usababishe wasiwasi usiofaa.
Utaratibu huu unaanza wakati gani? Mwanzo wake unatofautiana kwa mtu na mwingine. Ingawa katika nchi nyingi wastani ni karibu miaka kumi na mitatu, huenda kijana mmoja wa kike akaanza mapema hata akiwa na umri wa miaka kumi (wengine hata mapema zaidi), hali huenda mwingine asianze mpaka amekuwa mwenye umri wa miaka kumi na sita au hata nyuma ya hapo. Vivyo hivyo, muda wa mwezi huenda ukatofautiana kutokea siku tatu hata tano.
Pamoja na haya viuno vinapanuka, nayo maziwa (matiti) yanaanza kusitawi. Maendeleo haya mengi, mengine yanayoonekana, mengine yasiyoonekana, yote ni matayarisho kwa ajili ya kazi yenye madaraka mawili katika maisha ambayo Muumba wa wanadamu amewawekea wanawake—ile ya kuwa mke na mama. Kadiri ambavyo vijana wa kike wanavyozidi kupanuka viunoni haisaidii kuufanya uzazi wa mtoto mwepesi tu lakini vile vile kuufanya ubebaji wa watoto wadogo kuwa mwepesi. Wakati wa mimba mafuta mafuta yanayotolewa katika mwili wa mwanamke ni akiba inayoweza kutolewa anapolisha watoto wasiozaliwa au watoto waliozaliwa majuzi, na wakati wanapozaliwa matiti yanaanza kutoa maziwa.
YANATOKEA MADARAKA ZAIDI
Mapendeleo waliyopewa wanawake na Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu, yanafuatana na daraka la kuheshimu na kutenda kwa kupatana na kusudi la Muumba. Mvutano wa wanaume na wanawake ambao Mungu ameuweka katikati yao unakamatana sana na uzazi. Mwili wa kijana wa kike unapokua hivi kwamba anakuwa na uwezo wa kuzaa watoto, anatoa mvutano wenye nguvu zaidi kuelekea wanaume waliofikia hatua ya kuzalisha watoto. Lakini mvutano huu waweza kutumiwa vibaya. Kwa hiyo, ni kitu gani kinachopaswa kukumbukwa ili ufuate mwendo ufaao, ule utakaohakikisha baraka ya Mungu na kibali na kushiriki kukuletea furaha yako ya wakati ujao yenye kuendelea?
Katika kitabu cha Biblia cha Wimbo ulio Bora twapata maneno yenye kupendeza kwa wazi yaliyosemwa na kaka za mwanamwali wa Shulami. Kwanza, mmoja anatajwa kama akisema: “Kwetu sisi tuna umbu mdogo, wala hana maziwa; tumfanyieje umbu letu, siku atakapoposwa?” Yaani, wangemfanyia dada yao kitu gani wakati ambapo angeacha kuwa asiye na maziwa, ambapo angekuwa mkubwa na sasa mtu fulani akamposa? Kaka mwingine alijibu, akisema: “Kama akiwa ni ukuta, tumjengee buruji za fedha; na kama akiwa ni mlango, tumhifadhi kwa mbao za mierezi.” (Wim. 8:8, 9) Hii maana yake nini?
Kwa wazi usemi wao wa mfano ulimaanisha kwamba kama dada yao alikuwa imara kama “ukuta” wao wangemthawabisha kwa kupendezwa na kumheshimu. Angewezaje kufanya hivyo? Kwa kuonyesha nia imara ya kuendelea kuwa safi, akionyesha nguvu katika kuzuia majaribio yo yote ya kumtia katika mwenendo wa ufisadi. Wakati ambapo angefaa kwa ndoa, angejionyesha mwenyewe kuwa imara na mwaminifu katika kushikamana na kanuni za haki. Kwa upande mwingine, kama angekuwa kama “mlango” unaomfungukia ye yote anayeusukuma kidogo, hata mtu asiyefaa, basi ingewalazimu kuchukua hatua za kumzuia, yaani, ‘kumfungia’ kama mtu asiyepaswa kuaminiwa kwa habari ya wanaume. Vile vile angeweza kuwa kama mlango wenye kujifunga na kujifungua katika upendano wake, kwanza akipumbazika na mtu huyu kisha na yule.
Mwanamwali Mshulami, sasa akiwa ni mwanamke aliyekomaa mwenye maziwa, alilishinda jaribu hili na kuweza kuwaambia kaka zake: “Mimi nalikuwa ukuta, na maziwa yangu kama minara; ndipo nikawa machoni pake [yaani, machoni pa aliyemtazamia kuwa mumewe] kama mtu aliyeipata amani.”—Wim. 8:10.
Hata wewe una jaribu kama lile mbele yako unapokaribia utu uke. Ikiwa wataka kufurahia amani ya kweli ya akili, moyo na dhamiri na kujilinda mwenyewe na magumu yenye kuharibu amani, imekupasa utumie kujizuia na kuonyesha nguvu kwa ajili ya yaliyo haki. (Zab. 119:165) Je! uvutie fikira kwa makusudi kwenye sehemu zile za mwili wako zinazokamatana na umama kwa kuvaa marinda mafupi yanayokushika, mablausi au fulana zenye kubana? Hiyo ingekuwa na matokeo yenye kuchochea nyege kwa wanaume. Halafu?
Basi, je! utakuwa na imara na nguvu za kukataa urafiki utakaoulizwa kwa sababu ya kukazia kwenye sehemu hizo za mwili? Na, hata ingawa unaonyesha maendeleo ya kimwili, je! unayo maendeleo ya akili na moyoni ambayo ungeyahitaji kwa ndoa na umama? Paka anakuwa tayari kupata vipaka akiwa mwenye umri wa miezi kumi na miwili na kwa njia ya silika aweza kufanya kazi nzuri ya kuvitunza vipaka vyake. Lakini wanadamu si viumbe vya silika kama wanyama. Wanadamu wanajifunza mambo zaidi kuliko yale wanayoyarithi, nako kujifunza kunachukua wakati. Kujaribu kuuharakisha utaratibu huu kungekuwa kama kuyafungua majani ya tumba la waridi kwa lazima mbele ya wakati wake kufika. Kufanya hivyo kungeliharibu ua tu na kuharibu uzuri wo wote ambao lingekuwa nao wakati ujao. Vile vile, kumbuka kwamba ndoa siyo kuwa bibi-arusi tu. Inamaanisha vile vile kuwa mtunza nyumba, mpishi na mwosha nguo, ambapo kuwa mama kunahitaji subira nyingi na uvumilivu katika uangalifu kwa watoto bila ya kukata tamaa—yote haya katika nyakati zifaazo na zisizofaa, katika ugonjwa na katika afya.
Mbali na hayo, hata ingawa huenda kijana wa kike ajisikie yu tayari kwa ndoa na kazi na magumu yanayofuatana nayo, je! yeye anataka kujaribu kuvuta mume wa namna gani? Ikiwa kijana wa kiume anavutwa ati na ambavyo kijana wa kike anaonekana aweza kutoa kwa njia ya kutosheleza nyege, je! ataelekea kuwa mume mzuri? (Linganisha 2 Samweli 13:1-9.) Mahali pa kujaribu kuvuta kwa msingi huo, je! isingekuwa bora kutafuta urafiki wenye kuendelea juu ya msingi wa ambavyo wewe ulivyo kama mtu—akilini mwako na moyoni? Waweza kufanya hivyo kwa kukuza nia na tabia za utu zenye kuvuta kwa wengine. Vile vile kwa mambo kama mazungumzo yako, kwa kuonyesha maoni mazuri, yenye uchangamfu katika maisha, kwa kuonyesha kwamba unaona ubora wa mambo kama vile uaminifu, adabu, kiasi, fadhili, kutokuwa na choyo.
Waweza kuhakikisha unasema kweli katika hili kwa kukataa kuziondosha sifa hizi njema kwa ajili ya dakika chache za raha ambayo ingekuondolea ubora wako katika kukadiri kwako mwenyewe na kule kwa wengine unaowaheshimu, kuwapenda na kuwatunza. Zaidi kwa kuonyesha kwamba una miradi ifaayo kweli katika maisha, kwamba wataka ‘kumkumbuka Muumba wako siku za ujana wako wa utu uke,’ waweza kuwapata kama rafiki watu ambao urafiki wao utatunuka sikuzote kwa maana unakuletea furaha ya kweli.—Mhu. 12:1; 1 Tim. 2:9, 10.
KUJITAHIDIA USAWA WA MAONI YA MOYONI
Mageuzi ya kimwili ya kubalehe yana matokeo ya moyoni yasiyokusudiwa. Hata kama vile kijana wa kike mchanga awezavyo kujisikia mwenye nguvu nyingi dakika moja na mwenye uchovu dakika ifuatayo, ndivyo vile vile na maoni yake ya moyoni yanavyoweza kuelekea kutanga-tanga sana na mara nyingi bila ya kukusudia. Huenda vipindi vya ukunjufu na furaha vikafuatwa haraka na vipindi vya huzuni. Huenda ukajikuta unashangaa kama wewe ni mtu wa kawaida au unageuka uwe mtu wa namna gani. Zaidi katika jamii za kisasa za kazi, pamoja na kugeuka kwao kwa mambo yaliyo bora, vijana wa kike wenye kubalehe wanatiishwa na mkazo na wasiwasi.
Ingekuwa vyepesi kushindwa na ulegevu huu, kurudi nyuma, kufikiria yako mwenyewe, au kuwa mwenye kujitegemea sana na mwenye kudai haki zako. Vijana wengine wa kike wanashindwa kujizuia wasionyeshe jeuri, hasira za ghafula au usemi usio na adabu; wengine wanaanza kujifanya namna wasivyo, namna ya kijuujuu tu. Lakini hii haisaidii; inazidi tu kuharibu mambo. Kwa kuwa sasa unatoka utotoni, ndio wakati wa kufanya jitihada yako mwenyewe yenye fikira uyasitawishe matunda ya roho ya Mungu—upendo, furaha, amani, uvumilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.—Gal. 5:22, 23, NW.
Vile vile, sitawisha tabia zinazosaidia kuleta imara. Mahali pa kukiacha chumba chako kiwe kichafu-chafu, kifanye chenye utaratibu na malidadi. Jitahidi kuwa wa kawaida katika tabia za kulala na kula; mwili wako wenye kukua unauhitaji msaada wote uwezao kuupa. Kadiri ambavyo unaweza kufanya katika mambo haya, ndivyo utakavyojisikia kuwa imara, na hii itasaidia kusawazisha maono yako ya moyoni.
Kwa vyo vyote usiache kipindi hiki cha mageuzi kikufanye usiwategemee wazazi wako. Wao wanaweza kuutoa msaada imara unaopaswa kutegemewa nawe ili kuushika usawa wako mnamo kipindi hiki cha mageuzi. Ingawa unatiishwa na mkazo wa kuchunguza-chunguza—mkazo kutoka kwa wengine wa umri wako kuwa kama wao—kumbuka kwamba wao wenyewe wanageuka. Ndiyo sababu mambo yanayowapendeza leo huenda yasiwapendeze hata kidogo kesho. Kuhangaikia mno namna wanavyokufikiria kutazidisha tu magumu yako. Ndiyo sababu, vile vile, unapokuwa na maulizo ya kipekee ya ndani sana, wazazi wako ndio chanzo kilicho bora zaidi cha habari. Wao wanaweza kukupa jibu lenye maelezo zaidi, lililosawazika kupita ambalo lingeweza kutolewa na kijana ye yote aliyemo katikati ya kipindi cha kubalehe na kupevuka.—Mit. 6:20-23; 19:20, 21.
Kama vile manyunyu ya mapema yanavyofuatwa na maua mazuri, ndivyo na wewe ukijifunza kushinda matata bila ya kuhangaika, utakavyoipata njia ya imara na matumaini. Ijapokuwa yakupasa uhangaikie kujiweka mwenyewe mzima na safi kwa kimwili (kwa ulaji mzuri na utunzi wa afya wa kawaida), imekupasa ukazie fikira sana—si namna ulivyo kwa nje—bali namna ulivyo kwa ndani. Uzuri wa “roho ya upole na utulivu” inayotokezwa na ‘utu wa moyoni wa siri’ ndio utakaokufanya mwenye kuvuta kweli kweli—machoni pa Mungu na wanadamu.—1 Pet. 3:3, 4.
Usihangaike basi ama kuona uchungu kwa sababu ya umbo lako la kimwili ama sura, kana kwamba wakati wako wote ujao unategemea hili. Watazame watu wazima kukuzunguka—watu unaowapenda na kuwaheshimu. Je! wengi, pengine karibu wote, si wenye sura ya kawaida? Uzuri wa kimwili sio ufunguo wenyewe kwa furaha ya wakati ujao.
Na hivi ni sawa na kwa kijana wa kike aliye na urembo wa kimwili. Yampasa afahamu kwamba wanawake wengi warembo wanapotoka wakiishi maisha zisizo na maana yo yote, na mara nyingi za ufisadi. (Linganisha Mithali 6:24, 25; Ezekieli 16:15.) Na namna ilivyo kweli kwamba, “Kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe, kadhalika mwanamke mzuri asiye na akili.” (Mit. 11:22) Ndiyo, “upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili; bali mwanamke amchaye [Yehova], ndiye atakayesifiwa.”—Mit. 31:30.
Basi, na ugeuke kuwa mzuri katika sifa zenye kuendelea zilizo bora kweli kweli. Kwa maana hizi zinaongoza, si kwenye kufurahia maisha hakika sasa tu, bali kwenye uzima wa milele katika taratibu mpya ya uzuri usiokwisha na ukamilifu.