Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yy sura 8 kur. 58-65
  • Wataka Rafiki za Namna Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wataka Rafiki za Namna Gani?
  • Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUTAFUTA RAFIKI WANAOFAA
  • SABABU GANI NI LAZIMA UCHAGUE VIZURI
  • RAFIKI WALIO WAKUBWA KULIKO WOTE
  • Je! Ni Sawa Kuwa na Rafiki wo Wote Bila Kujali Walivyo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Tunawezaje Kuchagua Marafiki Wazuri?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Chagua Marafiki Wanaompenda Mungu
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Chagua Marafiki Wako kwa Hekima
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
Pata Habari Zaidi
Kupata Faida Zote za Ujana Wako
yy sura 8 kur. 58-65

Sura ya 8

Wataka Rafiki za Namna Gani?

1-5. (a) Rafiki wanawezaje kukuongezea furaha ya maisha? (b) Ungeeleza namna gani rafiki wa kweli alivyo? (Mithali 18:24)

KUWA na rafiki wa kweli kunaongeza sana furaha ya maisha. Watu wanaopenda kuwa peke yao bila kuwa na wengine hawana furaha sana. Ni nini kinachofanya urafiki uwe wenye furaha zaidi?

2 Kufanya jambo fulani pamoja na rafiki kunafurahisha sana. Wakati mmoja Yesu alisimulia habari ya mchungaji aliyemwona kondoo wake aliyekuwa amepotea na habari ya mwanamke aliyeona shilingi (fedha) yake iliyokuwa imepotea. Kila mmoja wa hawa wawili aliwaita rafiki, akisema, “Furahini pamoja nami.” (Luka 15:6, 9) Ndiyo, ni kawaida yako kutaka kushiriki mambo mema pamoja na rafiki, na kwa sababu hiyo furaha yako inaongezeka. Je! hujapata kuona hivyo?

3 Lakini, mambo yasipokuwa mazuri nawe unahuzunika, rafiki mwema anaweza kukufariji sana. Rafiki wanaweza kukusaidia sana wakati wa taabu. Wanaweza kukuonya hatari na kukusaidia uiepuke, tena wanaweza kukutia moyo wakati mambo yanapokuwa magumu. Labda utakubaliana na vile Mithali 17:17 inavyosema: “Rafiki [wa kweli] hupenda sikuzote; na [ni] ndugu [ambaye] amezaliwa kwa siku ya taabu.”

4 Andiko hilo lakazia sifa inayoonyesha sana wale walio rafiki za kweli, yaani: Ushikamanifu. Kuwa rafiki si kujifanya kama rafiki tu. Rafiki wa kweli kweli anashikamana nawe na kukutendea mema. Je! rafiki zako wako hivyo?

5 Leo, watu wengi wanataka sana kushinda jirani yao kuliko kumsaidia. Mara nyingi kuna roho ya kushindana kuliko roho ya ushikamanifu hata kati ya wale wanaoitwa “rafiki.” Urafiki mwingi unaendelea mradi tu mmoja wa hawa wawili haombwi ageuke wala kuacha kujipenda kwa faida ya mwingine. Si vyepesi kumwona rafiki wa kweli katika ulimwengu huu wenye mashindano.

6-8. Yonathani na Hushai walionyeshaje kuwa rafiki za Daudi?

6 Mfano mzuri katika Biblia unaoonyesha mtu aliyekuwa na rafiki wanaofaa kweli kweli ni Daudi. Labda umepata kusikia namna Daudi alivyopata urafiki mzuri na Yonathani mwana wa Mfalme Sauli alipokwisha kumshinda Goliathi, adui mkubwa mno. Kama Yonathani angalikuwa mwenye wivu, angaliweza kumchukia Daudi na kumfikiria kama mtu anayetaka kuchukua kiti cha enzi cha Israeli. Badala ya kufanya hivyo, Yonathani alifahamu kwamba Mungu alimpendelea Daudi, nayo “nafsi ya Yonatana iliambatana na nafsi ya Daudi, Yonatana akamupenda kama nafsi yake mwenyewe.” (1 Samweli 18:1, ZSB) Yonathani alimpenda kwa sababu alikuwa hodari na alimwamini Yehova Mungu. Bila shaka Yonathani vilevile alikuwa na uaminifu ule ule kwa Mungu. Hauwezi kuwako msingi bora kuliko huo wa kufanyiana urafiki.

7 Unaweza kusoma tena habari ya rafiki mwingine wa Daudi jina lake Hushai, aliyekuwa mmoja wa washiriki wakubwa wa Daudi wakati wa ufalme wake. Ni habari inayopendeza sana kusoma namna Hushai alivyoweka maisha yake katika hatari ili azuie usaliti uliopangwa na Absalomu, mmoja wa wana wa Daudi.—Tazama 2 Samweli 15:10-37; 16:16-17:16.

8 Labda una rafiki walio kama hao. Ikiwa huna, unaweza kuwapata namna gani? Itakupasa ujitahidi sana, lakini inafaa sana kufanya hivyo.

KUTAFUTA RAFIKI WANAOFAA

9-13. (a) Mtu anawezaje kupata rafiki wanaofaa? Sababu gani ni upumbavu kutaka kupata rafiki kwa kutoa au kushiriki nao mali? (b) Ni watu wa namna gani ambao inafaa kuepuka wasiwe rafiki sana kama inavyoonyeshwa katika Zaburi 101:5-7?

9 Ni kweli kwamba inakupasa uwe rafiki kama wataka kuwa na rafiki. Mara nyingine wengine wanataka sana kuwa na rafiki kwa sababu wametengwa na vijana wapendwa wao. Au labda wamepata kuwa na rafiki kisha wakawakosa. Wanahuzunika sana kwa sababu hiyo. Pengine hawajui kwamba urafiki ni wa watu wawili.

10 Basi yafaa tujiulize: Nafanya nini nionyeshe wengine urafiki? Napendezwa na wengine bila choyo kwa kadiri gani, tena nafanya nini ili niongeze furaha yao na faida yao? Ni sifa gani ninazositawisha ambazo zingefanya wengine waone wangetaka sana niwe rafiki yao?

11 Rafiki zako wategemea sana unavyojaribu kuwapata. Wengine wanajaribu kuwa na rafiki kwa kuwapa fedha, au kwa kuwakaribisha wafurahie mali, kama kinanda na sahani za santuri au chombo cha michezo. Ni kweli kufanya hivi kunaweza kuvuta wengine waje kwako. Mithali yasema hivi, “Tajiri ana rafiki wengi,” na kwamba “kila mutu ni rafiki yake anayetoa zawadi.” Ndiyo, watu wengi wanaonyesha urafiki wakati mtu anapotumia sana fedha zake. Lakini wakati fedha zinapokwisha, “rafiki” hao wanakwisha papo vilevile.—Mithali 14:20, UV; 19:6, ZSB.

12 Rafiki wanaofaa hawawezi ‘kununuliwa’ kwa mali wala kwa kubembelezwa wala kwa kukubali matakwa ya wengine. Rafiki ye yote anayeweza kununuliwa hafai hata kidogo hata awe amenunuliwa kwa bei gani. Rafiki za kweli wanavutwa na hali yako, tabia zako, hawavutwi na kitu wanachoweza kupata kwako.

13 Basi, ijapokuwa ni vizuri kuonyesha watu urafiki, ni lazima uchague wale unaotaka wawe rafiki zako wakubwa na unaotumaini sana ikiwa unataka rafiki za kweli. Daudi alichagua rafiki wa namna hiyo. Anasema hivi: “Mwenye macho ya kiburi na moyo wa majivuno, huyo sitavumilia naye. Macho yangu yatawaelekea waaminifu katika nchi, hao wakae nami. . . . Hatakaa ndani ya nyumba yangu mtu atendaye hila.” (Zaburi 101:5-7) Ni kwa sababu gani ni jambo bora sana vijana leo wachague wale wanaotaka wawe rafiki zao wakubwa?

SABABU GANI NI LAZIMA UCHAGUE VIZURI

14-16. (a) Rafiki za mtu wanaweza kumfanyia nini? Onyesha mfano. (b) Urafiki utakuwaje ukimwambia mwenzako kwamba hukubaliani naye?

14 Kawaida ya urafiki ni kwamba ukishirikiana na jirani kwa muda mrefu sana unaelekea kuwa kama wao. Unaonyesha namna ulivyo sasa na utakavyokuwa wakati ujao kwa namna unavyochagua rafiki zako. Rafiki zako wakubwa watakugeuza bila shaka.

15 Je! unachagua wale ambao ni wanyofu na wenye adabu, wale wenye huruma, wanaomheshimu Mungu na Neno lake na walio hodari kutenda yaliyo mema, wawe rafiki zako? Au unavutwa na watu wanaojisifu kuwa wanaweza kuwashinda wengine, ambao si wenye uhodari wa kweli, bali wanajitia katika hatari ili wajionyeshe tu? Je! wako tayari kujaribu kufanya uasherati, au kuiba au kutumia dawa za kulevya kisha wanajisifu kwamba hawawezi kukamatwa? Wakijaribu kukuvuta uwafuate katika kufanya jambo linaloweza kukuumiza, je! kweli wanaweza kuitwa “rafiki”?

16 Kumbuka, kama wewe ni rafiki sana wa watu hao, inakupasa uwafuate au ukosane nao. Pengine kukosana nao kutamaliza “urafiki” huo. Kwa sababu gani? Kwa sababu wataona kukosana nao ni kama kuwalaumu au kuwakaripia. Kwa kawaida watu hao wanapenda kuwacheka wengine, lakini wao wenyewe hawataki kukaripiwa. Mithali 9:8 inazungumza juu ya mtu wa namna hiyo kisha inaongeza hivi kwa kumtofautisha na mwingine: “Mkaripie mwenye hekima, naye atakupenda.” Rafiki za kweli wanaweza kuonyeshana makosa bila kuogopana na kusaidiana wafanye maendeleo au kuondoa makosa yao ikiwa lazima. Ukiwa na rafiki mwema sana anayefikiri mambo mazuri na kusema kweli, una hazina yenye bei kupita hazina zote. Rafiki za kweli ni kama almasi—mawe yenye bei sana yasiyopatikana vyepesi. Tofauti sana na hilo, rafiki za uongo ni kama mawe ya kawaida tu—yanayopatikana kila mahali.

17-19. (a) Jambo gani lingekupata kama ungefanya urafiki na mtu asiyeamini Mungu wala Biblia? (Mithali 11:9; Mwanzo 34:1, 2) (b) Ikiwa unataka sana kumsaidia mtu huyo, ni njia gani bora ya kumsaidia?

17 Kwa sababu ya kutokuamini kuwako kwa Muumba au Neno lake, vijana wengi leo wana moyo ule wa “tule na kunywa, kwa maana kesho tutakufa.” Ndio uliokuwa moyo wa watu wa zamani waliohukumiwa kupigana na wanyama-mwitu katika uwanja wa michezo. Hawakuamini Yehova Mungu wala uwezo wake wa kuwapa tena uzima wale walio waaminifu kwake. Sasa ndiyo unaanza kuishi kama kijana. Basi, wataka kufuata maoni hayo juu ya maisha, ya wafungwa hao waliohukumiwa? Akiisha kusimulia maoni haya ya ‘kuishi kwa ajili ya leo’ tu, mtume Paulo aliendelea kusema: “Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” (1 Wakorintho 15:32, 33, NW) Fikiria ukweli wa hayo. Ukitaka kushirikiana sana na watu wanaofikiria mambo ya sasa tu, ujue bila shaka kwamba wataharibu matumaini na bidii zako za kupata wakati ujao wenye kuendelea na wenye furaha.

18 Huenda mara nyingine kijana akasema kwamba anashirikiana na mtu mwingine mwenye mwenendo na sifa mbaya ili amsaidie. Ni jambo jema kutaka kusaidia wengine. Lakini unawapa msaada gani ikiwa unawafuata katika raha zao za kichoyo? Kwa mfano, ukimwona mtoto katika matope, je! ungeweka sabuni katika matope kisha ujaribu kumsafisha mtoto? Bila shaka kwa kufanya hivyo wewe mwenyewe ungechafuka. Kwanza ungejaribu kumtia mtoto moyo atoke katika matope kabla ya kutumaini kumsafisha ukiwa karibu sana naye.

19 Kwa kweli, kukubali mtu mwenye mazoea mabaya awe mshiriki wako mkubwa kutamharibu sana mtu huyo (vilevile na wewe mwenyewe). Kwa sababu gani? Kwa sababu ushirika huo unaweza kumtia moyo aendelee kuwa hivyo, akidhani unaweza kumwunga mkono sikuzote katika njia hiyo. Je! huoni ni afadhali kushirikiana na mtu huyo wakati unapoweza kumsaidia tu kwa kumpa shauri jema na kumkaribisha aende pamoja nawe mahali shauri hilo linapoelezwa?

RAFIKI WALIO WAKUBWA KULIKO WOTE

20. Tunawezaje kujifanya adui za Mungu kwa namna tuna-vyochagua rafiki zetu?

20 Zaidi ya yote, imekupasa ufikiri sana namna kushirikiana na watu wenye tabia mbaya kunavyoweza kuharibu uhusiano (mapatano) wako na Mungu na Mwanawe. Kweli hii inaelezwa katika Yakobo 4:4 hivi: ‘Ye yote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.’ Kanuni hiyo yaweza kupasa urafiki wetu na mtu ye yote katika ulimwengu kama inavyopasa urafiki na ulimwengu mzima. Ikiwa tunazikubali tabia mbaya za mtu fulani au twapendelea kushirikiana na huyo kuliko na watu wanaotaka sana kumpendeza Mungu, je! hatujionyeshi kuwa ‘rafiki za ulimwengu’?

21-23. (a) Mtu ambaye rafiki zake ni Mungu na Kristo anapata faida gani? (Warumi 8:35, 38, 39) (b) Tunawezaje kuonyesha kwamba twawataka sana wawe rafiki zetu?

21 lkiwa unataka sana furaha sasa na wakati ujao, jaribu sana kujifunza kuona ubora wa kuwa rafiki ya Mungu na Mwanawe. Mungu amekuwa akiwaonyesha urafiki wale wanaopenda haki sasa kwa muda wa maelfu ya miaka, akifunua makusudi yake ya ajabu awaletee uzima wa milele katika hali zenye furaha kweli kweli. Alipokuwa duniani, Mwana wa Mungu aliwaonyesha watu wenye mioyo mizuri upendo wake wenye kushikamana. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo.”—Yohana 15:13, 14.

22 Tofauti na wengi wanaoweza kujifanya kwa uongo kuwa rafiki zako, Yehova Mungu na Mwanawe hawatakuacha kwa sababu unapata taabu. Ukiwatumaini utaona kwamba watakusaidia na kukutegemeza kweli kweli katika nyakati zenye taabu.

23 Je! kweli unawafurahia sana na kuwatamani Rafiki hawa wakubwa sana? Basi onyesha hivyo kwa kutafuta rafiki washikamanifu wanaokubali na watakaofuata wajibu ulioandikwa na mtume Yohana aliposema: “Huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si nzito.” (1 Yohana 5:3) Rafiki hao watakuwa ndio rafiki wa kuwa nao wakati wa taabu na usio wa taabu.

[Balbu katika ukurasa wa 60]

Ni lazima uwe rafiki ili uwe na rafiki.

[Picha katika ukurasa wa 62]

Rafiki za kweli ni kama almasi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki