Je! Ni Sawa Kuwa na Rafiki wo Wote Bila Kujali Walivyo?
Mambo ya hakika ambayo vijana wanataka kujua
KUWA na rafiki ni mojawapo la mambo yanayoshiriki sana katika kuleta furaha ya maisha. Watu wanaojitenga wenyewe na kuwaepa wengine hawana furaha kwa kweli wakati wo wote. Je! mna nini katika urafiki kinachoongeza sana furaha yetu?
Kufanya jambo fulani pamoja na rafiki kunaelekea kuzidisha furaha yetu ya mambo yenye kupendeza ya maisha na matendo. Huenda ukakumbuka namna, katika mifano ya Yesu, mchungaji aliyempata kondoo wake aliyepotea na mwanamke aliyeipata shilingi yake iliyopotea walivyowaita kila mmoja rafiki zake, wakisema, “Furahini pamoja nami.” (Luka 15:6, 9) Ndiyo, kwa kawaida twataka kufurahia mambo mema pamoja na rafiki, nayo furaha yetu yaelekea kuzidi mara mbili kama matokeo.
Kwa upande mwingine, mambo yasipokuwa mazuri sana kwetu nasi twajisikia kuhuzunika, rafiki mwema aweza kufanya mengi kuipunguza huzuni yetu. Mara nyingi rafiki wanaweza kusaidia sana taabu inapokaribia, wakituonya juu ya hatari au wakitusaidia kuiepuka, wakitupa nguvu zaidi katika nyakati zenye hatari. Kama vile Mithali 17:17 inavyosema: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.”
Andiko hilo linatilia mkazo sifa ambayo kwa kutokeza inaonyesha rafiki za kweli: uaminifu. Kuwa rafiki kwa kweli kunamaanisha zaidi ya ‘kutenda kwa urafiki’ tu. Rafiki wa kweli ni mwaminifu kwako na kwa faida zako bora. Je! ndivyo walivyo rafiki zako?
Leo, watu kwa jumla wanaelekea kupendezwa zaidi katika kumshinda jirani yao kuliko katika kumsaidia jirani yao. Ndivyo ilivyo kati ya vijana hata kama vile ilivyo kati ya wazee. Hata kati ya wanaoitwa ‘rafiki’ mara nyingi iko roho ya kushindana, si ya uaminifu. Urafiki mwingi unaendelea maadamu hakuna anayeombwa kufanya mageuzi fulani ama kujinyima faida fulani ya kichoyo. Katika ulimwengu huu wenye kushindana, si vyepesi kupata rafiki ya kweli. “Kunao rafiki wanaoelekea kuangamizana,” Mithali 18:24, NW, inatuambia, “lakini yuko rafiki aambatanaye zaidi kuliko ndugu.”
Biblia inaonyesha kwamba Daudi, mwana wa Yese, alikuwa na rafiki fulani wafaao kweli kweli. Zaidi ya mara moja hawa waliokoa uhai wake. Huenda ukakumbuka namna, nyuma ya ushindi wa Daudi wa shujaa Mfilisti mkubwa sana Goliathi, alivyompata Yonathani kama rafiki mwema, mwana wa Mfalme Sauli. Yonathani angeweza kumchukia Daudi kama adui kwa ajili ya kiti cha enzi cha Israeli, kiti cha enzi ambacho Yonathani huenda alitumainia kurithi kutoka kwa babaye, Mfalme Sauli. Mahali pake, Yonathani alijua kwamba kibali cha Mungu kilikuwa juu ya Daudi, na “nafsi ya Yonathani yenyewe ikaambatana na nafsi ya Daudi, naye Yonathani akaanza kumpenda kama nafsi yake mwenyewe.” (1 Sam. 18:1, 3, NW) Mahali pa kuwa mwenye kijicho kwa Daudi, Yonathani alimpenda kwa ajili ya uhodari wake na imani katika Yehova Mungu. Na zaidi ya mara moja Yonathani alihatirisha uhai wake na akavumilia hasira kali ya babaye (lakini isiyo haki) kusudi amlinde rafiki yake.—1 Sam. 19:1-20:17, 24-40.
Vile vile waweza kusoma juu ya rafiki ya nyumaye ya Daudi aliyeitwa Hushai, ambaye, kama “rafiki yake mfalme,” alikuwa mmoja wa rafiki wakubwa wa Daudi wakati wa ufalme wake. Namna ambavyo Hushai alihatirisha uhai wake ayazuie mapatano mabaya ya Absalomu, mmojawapo wa wana wa Daudi, ni habari ya kusisimua ya kuangaliwa.—Tazama 2 Samweli 15:10-37; 16:16–17:16.
Pengine wewe vile vile unao rafiki kama hawa. Lakini, ikiwa sivyo, je! wawezaje kuwapata? Itachukua jitihada kweli kweli, lakini bila shaka inaistahili.
KUTAFUTA RAFIKI WAFAAO
Kuna usemi kwamba ‘njia ya pekee ya kupata rafiki ni kuwa mmoja.’ Mna ukweli mwingi katika maneno hayo. Nyakati nyingine watu wanajiona peke yao na kujisikia ‘kutotiwa’ katika mambo na vijana wengine ambao huenda wakawaheshimu. Au huenda wamekuwa na rafiki lakini ‘wakawapoteza.’ Huenda wakajiona kuchukizwa kwa sababu hii. Lakini urafiki ni jambo la watu wawili.
Kwa hiyo ni vema kujiuliza wenyewe, Mimi nafanya nini ili niwe mwenye urafiki kwa wengine? Mimi napendezwa na wengine kwa kadiri gani kwa unyofu na bila choyo nami nafanya nini ili niongeze furaha yao na hali njema yao? Je! ni sifa gani ninazositawisha ambazo zingewafanya wengine waone wangependa kuushiriki urafiki wangu mara nyingi zaidi?
Namna ambavyo unajaribu kutafuta rafiki kwa jumla itaamua namna ya utakaowapata. Wengine wanajaribu kupata rafiki kwa kutumia fedha juu yao au kwa kuwakaribisha washiriki anasa za mali nyingine za kimwili—kinanda na rekodi, vifaa vya michezo au vitu vinginevyo. Kweli, hii yaweza kuvuta wengine kwako, kama vile kitabu cha Mithali kinavyosema kwamba “tajiri ana rafiki wengi” na kwamba “kila mtu ni rafiki yake atoaye tunu.” (Mit. 14:20; 19:6) Watu wengi wanatenda kwa urafiki wakati ambapo mtu anatumia fedha yake kwa wingi mno. Lakini fedha imalizikapo ndivyo na ‘rafiki’ hao.
Nyakati nyingine si fedha ama mali za kimwili tuwezazo kutumia kujaribu ‘kununua’ urafiki. Twaweza kufanya hivyo vile vile kwa kusifu-sifu isivyostahili au kwa kumpatia mwingine kila wazo na mapendezi, tukijiacha wenyewe tutumiwe na mtu huyo kwa ajili ya faida zake za kichoyo. Lakini rafiki wafaao hawawezi ‘kununuliwa’ kwa njia hizi. Rafiki ye yote awezaye kununuliwa hastahili bei yenyewe—bila ya kujali udogo wake. Rafiki za kweli wanavutwa kwako na uliyo nayo kwa habari ya sifa zifaazo—si na wawezayo kupata kutoka kwako.
Kwa hiyo, ni vizuri kuwa na nia ya kirafiki kuelekea watu kwa jumla; lakini ikiwa wataka rafiki za kweli imekupasa uwe mwenye kuchagua juu ya wale unaokubali kama rafiki wakubwa. Daudi alikuwa mwenye kuchagua. Yeye anasema: “Amsingiziaye [rafiki] yake kwa siri, huyo [nanyamazisha]. Mwenye macho ya kiburi na moyo wa majivuno, huyo sitavumilia naye. . . . Hatakaa ndani ya nyumba yangu mtu atendaye hila. Asemaye uongo hatathibitika mbele ya macho yangu.” (Zab. 101:5-7) Kwa sababu gani ni muhimu sana kwa vijana leo kuwa wenye kuchagua rafiki wakubwa?
SABABU GANI KUCHAGUA NI KWA LAZIMA
Ni kanuni ya msingi ya ukamatano wa watu wote kwamba unaelekea kuwa namna wale walio karibu yako walivyo ukishirikiana nao muda mrefu vya kutosha. Kuna mithali ya Kispain inayosema: “Niambie wewe unatembea na nani nami nitakuambia namna ulivyo.” (Dime con quién andas y te diré quién eres.) Uchaguzi wako wa rafiki unaeleza mengi juu ya namna ya mtu utakaye kuwa. Rafiki zako wakubwa lazima watakuwa na matokeo ‘yenye kugeuza’ juu ya utu wako.
Je! wewe unachagua rafiki walio na sifa za uaminifu na adabu, wenye huruma na walio na heshima kwa Mungu na Neno lake na walio na uhodari kufanya yaliyo haki?
Au je! wewe wavutwa na vijana ambao ni kama watu aliowaepuka Daudi, wale wanaojifikiria wenyewe sana na wanaowasingizia wengine, wanaojivuna juu ya kuweza kuwa ‘wajanja mno’ kupita wengine kwa kutumia njia za werevu, na ambao, mahali pa uhodari wa kweli, wana uwazimu tu unaowafanya wajihatirishe kwa ujinga bila ya kusudi lo lote la kweli na bila ya kutazamia lengo lo lote lifaalo? Huenda wakajitia katika ufisadi, au kuiba au kutumia dawa zenye kulevya kisha kujisifu kwamba ‘hawashikwi.’ Kama wakijaribu kukutega uambatane nao, je! wanaweza kwa haki kuitwa “rafiki”?
Kumbuka, mkiwa rafiki wakubwa wa watu hao ama itawalazimu mwambatane nao katika wanayofanya ama mkosane nao. Kukosana nao labda kutauvunja ‘urafiki.’ Kwa sababu gani? Kwa sababu, ijapokuwa vijana hao mara nyingi wanapenda kufanyia wengine mzaha, wao wenyewe kwa kawaida hawawezi kukubali karipio; wanalichukia. Mithali 9:8 inasema juu ya mtu wa namna hiyo kisha, kwa kutofautisha, inaongeza, “Mkaripie mwenye hekima, naye atakupenda.” (Tazama vile vile Mithali 15:12.) Rafiki za kweli wanaweza kusemezana kwa unyofu na kusaidiana kuendelea na kujirekebisha na kujitia nguvu wenyewe katika mambo ambamo wao ni dhaifu. Mwandikaji wa kale anasema: “Marhamu na manukato huufurahisha moyo; kadhalika utamu wa rafiki ya mtu utokao katika kusudi la moyo wake.” (Mit. 27:9) Wakati unapokuwa na rafiki mwema kweli kweli anayefikiri sawasawa na kuzungumza sawasawa, ni karibu kama kuwa na akili ya pili ya kutumia kwa faida yako.
Vijana wengi sana leo, kwa sababu ya kutokuwa na imani katika Neno la Mungu na tumaini linalolitoa, wanatwaa nia ya “na tule, na tunywe, maana kesho tutakufa.” Ndivyo watu wengi walivyoona waliohukumiwa kupigana na wanyama-mwitu katika uwanja wa kuchezea wa Efeso wa kale katika Asia Ndogo. Wao hawakuwa na tumaini katika Yehova Mungu wala tumaini lo lote katika ufufuo wa uzima katika taratibu mpya ya Mungu. Kama kijana kwa kweli ndiyo sasa unapoanza katika maisha. Kwa hiyo, je! wewe wataka kuikubali filosofia ya wafungwa waliolaaniwa na kuifanya hiyo nia yako kuelekea maisha? Nyuma ya kusimulia maoni hayo ya ‘kuishi kwa ajili ya leo’ tu, mtume Paulo anaendelea kusema: “Msidanganyike. Mashiriki mabaya yanaharibu mazoea mema.” (1 Kor. 15:32, 33, NW) Ukitafuta urafiki mkubwa wa vijana wanaofikiria mambo ya sasa tu, bila shaka watayaharibu matumaini yako na jitihada za kuelekea kupata wakati ujao wenye furaha kweli kweli. “Asiyemcha Mungu humpoteza jirani yake kwa kinywa chake; bali wenye haki watapona kwa maarifa.”—Mit. 11:9.
Nyakati nyingine huenda kijana aseme kwamba yeye anashirikiana na mtu mwingine mwenye sifa na mazoea yasiyo mema akiwa na maoni ya ‘kumsaidia huyo.’ Kutaka kusaidia wengine ni jambo jema. Lakini ukiambatana nao katika kutafuta anasa ya kichoyo, je! unawapa msaada wa kadiri gani? Ingawaje, kama ungemwona mtoto katika kiziwa cha matope, je! ungechukua sabuni na kuitia katika kiziwa na kujaribu kumsafisha mtoto kwayo? Ungejichafua mwenyewe tu kama matokeo. Ingekupasa kwanza ujaribu kumtia mtoto moyo atoke katika kiziwa cha matope mbele ya kutumainia kufanya lo lote juu ya kumsafisha akiwa karibu.
Kwa kweli, kumkubali kijana mwenye mazoea mabaya kama rafiki yako mkubwa mara nyingi kutakuwa na matokeo mabaya juu ya mtu huyo (vile vile juu yako). Kwa sababu gani? Kwa sababu kunaweza kumtia huyo moyo aendelee katika njia ile ile, akiona kwamba, ijapokuwa yale anayoyafanya, ungali waona urafiki wake mkubwa wakubalika. Je! usingekuwa msaada mkubwa zaidi kuzuia mashirika yako kwenye nyakati uwezapo kumsaidia mtu huyo kwa kweli kwa kutoa shauri jema kutoka katika Neno la Mungu na kwa kumkaribisha yeye afuatane nawe kwenye mahali ambapo shauri hilo linazungumzwa na kuelezwa?
RAFIKI WALIO WA MAANA KUPITA WOTE
Juu ya yote, imekupasa ufikirie kwa uzito juu ya namna ushirika na watu wenye mazoea yasiyo mema uwezavyo kuugeuza ukamatano wako na Yehova Mungu na Kristo Yesu. Huenda mtu akasema, ‘Lakini mimi mwenyewe siyafanyi hayo mambo mabaya.’ Labda sivyo—haikosi bado. Lakini ikiwa wewe huyapendi ama kuyakubali mambo mabaya anayoyafanya mtu huyo, basi kwa sababu gani wewe waupenda urafiki wake mkubwa? Je! watu wasingehesabiwa haki kwa kufikiri unayakubali mazoea ya mtu huyo na je! wasingehesabiwa haki kwa kukupa wewe sifa inayofanana?
Katika Yakobo 4:4 twaambiwa kwamba ‘ye yote atakaye kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.’ Kanuni hiyo yaweza kutumika kwa ukamatano wetu na mtu ye yote mmoja na vile vile kwa ukamatano wetu na ulimwengu wa wanadamu uliotengwa mbali na Mungu. Tukizikubali njia za kilimwengu katika mtu fulani au kuupendelea urafiki wa huyo kuliko ule wa kijana ambaye kwa kweli anataka kumpendeza Mungu, basi je! hatujionyeshi wenyewe kuwa ‘rafiki za ulimwengu’?
Ikiwa kwa kweli unataka furaha sasa na wakati ujao, kwa vyo vyote ujifunze kuona ubora wa urafiki wa Mungu na Mwanawe kupita ule wa wengine wote. Kwa maelfu ya miaka sasa Mungu amekuwa akiuonyesha urafiki wake kuwaelekea wale wanaopenda haki, akiyakuza makusudi yake ya ajabu awaletee uzima wa milele katika hali zenye furaha kweli kweli. Mwanawe amefanya kazi pamoja naye na, alipokuwa duniani, aliuhakikisha upendo wake mwaminifu juu ya watu wenye mioyo ya haki. Yeye aliwaambia wanafunzi wake: “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo.”—Yohana 15:13, 14.
Tofauti na wengi wanaoweza kujifanya kuwa rafiki zako, Yehova Mungu na Mwanawe hawatachoshwa nawe wala kukuacha kwa sababu unapatwa na shida. Ukiweka tumaini lako katika wao utaona kwamba nyakati zako za taabu zitakuwa ambapo msaada wao na tegemezo vyapatikana zaidi.
Je! kwa kweli wewe waona ubora wa Rafiki hawa wakubwa? Basi onyesha hivyo kwa kutafuta rafiki kama wao duniani. Utafute rafiki waaminifu wanaoukubali na watakaoutimiza wajibu aliouandika mtume Yohana aliposema: “Katika hili tumelifahamu pendo, kwa kuwa yeye [Yesu] aliutoa uhai wake kwa ajili yetu; imetupasa na sisi kuutoa uhai wetu kwa ajili ya hao ndugu.” (1 Yohana 3:16) Kwa kila hali, wao watakuwa namna ya rafiki wanaostahiliwa. Watakusaidia kupata uzima milele katika taratibu mpya ya Mungu.