Sura ya 12
Je! Unamaliza Unachoanza?
1, 2. Unatakiwa kufanya nini ili upate furaha inayotokana na kutimiza jambo fulani?
FURAHA nyingi ya wanadamu inatokana na kutimiza mambo. Kwa mfano, ukiamua kujifunza kupiga gambusi na kuendelea kufanya hivyo mpaka ujue, ndipo unapopata furaha yake. Lakini ukiacha mara unapoanza, huwezi kupata furaha hiyo na uradhi. Ndivyo na kazi yo yote inayotaka mazoezi na kufundishwa kwa muda mrefu.
2 Walakini, sote tuna maelekeo ambayo inatupasa tuyashinde katika shauri hili la kuendelea na kazi mpaka inapomalizika.
MAGUMU YALIYOMO
3-8. (a) Ni nini linaloweza kusaidia mtu asiwe mwenye haraka-haraka? (b) Ni jambo gani lenye hekima kufanya wakati wo wote kabla hujaanza kazi fulani? Ni shauri la nani lingeweza kukupa faida katika kuamua? (c) Ingekuwa bora kutomaliza unachoanza wakati gani?
3 Kama unavyojua, watoto wadogo hawana uendelevu. Hata katika kucheza, hawakawii kuvutwa upesi na mambo mengine au kuacha kupendezwa na jambo wanalofanya. Lakini mtu anapokuwa mzima, uwezo wa kukaza fikira pamoja unasitawi. Labda wewe mwenyewe umeona ndivyo ulivyo. Inakupasa na inafaa usitawishe sana sifa hii, kwa sababu inakusaidia utimize mengi zaidi maishani.
4 Ili upate kukaza fikira pamoja unatakiwa ushinde tabia nyingine waliyo nayo watu wengi. Tabia hiyo ni haraka haraka. Kumbuka ulipokuwa mtoto mdogo. Kama unavyokumbuka, sikuzote watoto wadogo wanataka mambo yafanyike SASA HIVI! Mara nyingi wanakuwa tayari kuacha wanapojaribu mara chache kufanya jambo fulani wasiweze. Basi, labda unawajua vijana wengi ambao wangali hivyo. Lakini kama unafahamu kwamba mengine kati ya mambo yanayofaa zaidi sana maishani yanataka wakati mwingi na bidii, itakusaidia usiache upesi.
5 Kwa kawaida mtu wa haraka-haraka anaanza kufanya mambo haraka-haraka, bila kufikiri. Kama mithali yenye hekima inavyotuambia: “Mafikili ya wenye bidii yanaelekea utajiri tu: lakini kila mutu anayetenda kwa haraka anaelekea uhitaji.” (Mithali 21:5, ZSB) Kwa hiyo, kabla ya kuanza kazi fulani au kuikubali, hakikisha kwanza kwamba inafaa sana.
6 Inafaa mara nyingine kutomaliza unachoanza. Namna gani ? Kwa sababu labda tangu mwanzo lilikuwa wazo baya. Huenda mradi ulikuwa mbaya, usiopatana na kanuni njema. Au, pengine si mzuri kwako wewe. Je! unastahili kupotezea wakati na bidii ili kuufikia? Je! una sababu nzuri kusadiki kwamba unaweza kuufikia?
7 Yesu alisimulia juu ya mtu aliyeanza kujenga mnara bila kuhesabu fedha kwanza na kama anaweza kumaliza ujenzi au sivyo. Kama Yesu alivyosema, huenda mtu akaanza msingi kisha akaona hawezi kuendelea zaidi ya hapo na kuwafanya watazamaji wacheke na kusema hivi: “Mtu huyu alianza kujenga, akawa hana nguvu za kumaliza.” (Luka 14:28-30) Kwa hiyo, ukitaka kumaliza unachoanza, hesabu fedha kwanza.
8 Linganisha faida na hasara. Waombe wengine maoni yao, zaidi wazazi wako. Pata faida ya ujuzi wao; wamefanya makosa na wanaweza kukuepusha na makosa hayo. Biblia ni chanzo kikubwa sana cha kupatia shauri lenye hekima na lenye kufaa. Imetoka kwa Mungu na inatoa mambo yaliyowapata watu kwa muda wa maelfu ya miaka iliyopita. Kwa mfano, mfalme Sulemani alifanya karibu yote ambayo mtu anafanya katika kutafuta anasa kutokana na mali. Anatuambia yaliyotokea: Kulikuwa “kufuatia upepo” tu. Kwa hiyo, kwa nini kufuatia jambo la bure kama hilo? —Mhubiri 2:3-11, NW.
EPUKA KUWA MTU WA KUACHA
9-12. (a) Ukiisha kuchagua mradi, sababu gani inafaa kupanga namna utakavyoufikia? (b) Unapopata majaribu, uyaoneje? (c) Sababu gani ni jambo la maana sana kutokuzoea kuwa mtu wa kuacha? (Luka 9:62)
9 Ukiisha sadiki kwamba mradi wako unafaa kweli kweli, ni jambo la maana vilevile kupanga namna ya kuufikia. Vijana wengi hawamalizi wanachoanza kwa sababu wanavunjika moyo. Huenda magumu au vizuizi visivyotazamiwa vikatokea. Au wanaona kwamba waliloanza kufanya ni gumu zaidi kuliko walivyodhani. Halafu nini sasa?
10 Hali hiyo inafunua utu wako. Kama unaacha magumu yakujaze mawazo yasiyo na matumaini mazuri, utakosa nguvu ya kuendelea kufanya. Ni kama mithali ya Biblia inavyosema: “Je! umejionyesha kuwa mwenye kuvunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako ni chache.” (Mithali 24:10, NW) Basi, itazame hali hiyo kama jaribu, badala ya kuvunjika moyo. Lishinde kwa bidii zaidi—kufikiri zaidi, kwa nguvu na wakati zaidi. Majaribu yaweza kufanya maisha yapendeze kama huyaogopi. Unakuwa hodari na mwenye busara kwa kushinda. Ndipo unapoweza kuanza kufanya kazi za wakati ujao ukiwa na hakika na furaha kubwa zaidi.
11 Basi epuka kusitawisha mazoea ya kuacha ati kwa sababu jambo linakuwa gumu. Bila hivyo, utaelekea kuacha wakati mwingine mambo yatakapokuwa magumu. Unaweza kuzuia maisha yasiendelee kuwa ya bure na yenye makusudi yasiyotimizwa kwa kuzuia mazoea hayo yasianze.
12 Wengine watakutumaini na kukuheshimu ukijionyesha kuwa mtu asiyeacha kwa vyepesi. Timotheo Mkristo wa karne ya kwanza “alishuhudiwa vizuri na ndugu” katika miji miwili mbalimbali alipokuwa bado kijana. (Matendo 16:2, ZSB) Ndiyo sababu mtume Paulo alimchagua awe mwenzi wa kusafiri naye. Timotheo alikuwa na mapendeleo ya pekee, ya kusafiri katika sehemu nyingi za Milki ya Rumi pamoja na mtume. Alipokwisha kutumikia kwa uaminifu muda wa miaka karibu kumi na miwili, mara nyingine katika hatari, alipewa daraka kubwa alilotimiza ijapokuwa afya yake mbaya. Ndiyo, Timotheo aliweza kutegemewa kuendelea na mgawo wake na kuumaliza. Alikuwa mtu wa kutumainiwa. Lakini ili astahili kutumainiwa hivyo, wakati mwingi na uendelevu ulitakiwa.
MSINGI WA KUENDELEA
13, 14. (a) Tumefaidika namna gani na uendelevu wa Nuhu katika kujenga safina? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa mtume Paulo wa uendelevu? (2 Timotheo 4:16, 17)
13 Kama unataka kufanya jambo fulani kwa sababu ni jema au kwa sababu wataka sana umpendeze Mungu, atakusaidia ulitimize. Kwa mfano, mkumbuke Nuhu. Ile safina ambayo yeye na wanawe walijenga ilikuwa jengo kama sanduku lenye orofa tatu na urefu zaidi ya futi mia moja (metres 122). Haikuwa kazi ya kufanywa siku moja au mbili. Lakini kwa sababu alifanya kazi mpaka ikamalizika, Nuhu na jamaa yake waliokoka gharika, na sisi wazao wake tuko hai leo.
14 Tena, mkumbuke mtume Paulo. Alikuwa mfano kweli kweli wa mtu ambaye hakuacha kulipokuwa na magumu. Mgawo wake wa kazi aliuona kuwa wenye kufaa kuvumilia namna zote za taabu ili aumalize. Alikuwa na moyo wa kupatwa na mapigo, kupigwa kwa mawe, kufungwa gerezani, kufanya kazi yenye taabu, kukesha bila kulala usingizi, kuona kiu, kuona njaa, kupatwa na baridi na kukosa mavazi, kupatwa na hatari kutoka kwa wenye kuchukia kweli na kutokana na wahalifu wa kawaida, vilevile kutokana na wanyama-mwitu na dhoruba alipokuwa akisafiri katika nchi kavu na baharini. Kwa sababu hakuacha, aliweza kusema kwamba ‘alikuwa amevipiga vita vizuri, akaumaliza mwendo, akailinda imani.’ Kwa msingi gani? Si kwa sababu ya kujitegemea, bali kama Paulo mwenyewe alivyosema: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” Tena kama alivyoandika: “Tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda.” (2 Timotheo 4:6-8; Wafilipi 4:13; Warumi 8:35-39) Je! wewe hungesema alikuwa mtu anayestahili kuigwa?
15. (a) Kwa sababu gani sote twahitaji kupatana na watu wengine? (b) Ni nini litakalotusaidia tusiwe wepesi wa kukasirikia wengine wanapotukatisha tumaini?
15 Ili ufurahie uzima inakupasa vilevile upatane na wengine, wapate kushirikiana nawe na kukuheshimu. Kama wewe ni mtu wa kukasirishwa upesi na watu, mwenye kuanza urafiki kisha kuuvunja mara kunapotokea kutopatana kidogo, huliwezi hilo. Jichunguze mwenyewe. Je! mara nyingine unawatendea wengine vibaya hata wanakasirika? Je! hilo linakufanya ujikasirikie? Basi kwa nini uwe mwepesi wa kukasirika au kuchukia wengine kwa sababu labda mara nyingine wanaweza kukukatisha tumaini? Tumia wakati mwingi ulio lazima kutatua matatizo kwa uvumilivu. Ni nani asiyeweza kuifahamu hekima ya mithali hii: “Asiye mwepesi kwa kukasirika ana ufahamu mwingi, lakini mwenye roho ya haraka anatukuza upumbafu”?—Mithali 14:29, ZSB.
16. Kusitawisha kwetu uendelevu kunapasaje kupata utimizo wa tumaini letu la Kikristo?
16 Faida za uendelevu ni nyingi na zastahili kufanyiwa bidii. Utapata mapendeleo na faida nyingi kwa kujionyesha kuwa mtu anayeanza kazi na kuzimaliza. Kwa habari ya wale wanaomfuata, Yesu alisema hivi: “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.” (Mathayo 24:13) Sisi kama Wakristo, tuko katika mashindano ya mbio. Zawadi kubwa itakayotolewa ni uzima wa milele. Utaipata zawadi hiyo ikiwa unasitawisha uwezo wa kuendelea bila kufikiria magumu, umalize unayoanza tu.