Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 11/15 kur. 5-9
  • Endelea Kufuatia Miradi ya Kiroho

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Endelea Kufuatia Miradi ya Kiroho
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Kuwa wa Nia Hii ya Akili’
  • Mazoezi Katika Utawa
  • ‘Jinyoshe Mbele’​—Bado Si Wakamilifu
  • Hali Zinatofautiana
  • ‘Kufuatia Mradi’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Songa Mbele Kuuelekea Mradi!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Fuatieni Ujitoaji Kimungu Mkiwa Wakristo Waliobatizwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Nafasi Kubwa Zaidi kwa Vijana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 11/15 kur. 5-9

Endelea Kufuatia Miradi ya Kiroho

“Nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, [niufikilie mradi wa] thawabu.”​—Wafilipi 3:13, 14.

1, 2. Wale waliokuwa wakishindana katika mbio za kale za miguu walitia jitihada ya kadiri gani, na kwa sababu gani? (1 Wakorintho 9:24)

MKIMBIAJI mwema tangu wakati kizuizi kinapoondolewa anafikiria tu juu ya kwenda mbele, anaweka akili yake kwenye mahali pa kumalizia na huitumaini miguu yake imshindie.” Ndivyo mwanahistoria wa karne ya kwanza Lucian alivyoeleza maoni ya wale waliomo katika mbio za miguu. Kila mshipa wa fahamu na msuli ulikazwa ili kuufikia mradi kwanza. Thawabu, mara nyingi ikiwa ni taji la majani, kwa kawaida ilimletea mshindi “sifa bora zaidi” muda wote wa maisha yake, kwa maana kila mtu alikuwa anajua kwamba mshindi huyo “alijikaza kisabuni” mpaka ‘aliposhinda thawabu.’a

2 Akitumia mkimbiaji ili kuonyesha ni nini kinachohitajiwa ili mtu afanikiwe akiwa Mkristo, mtume Paulo aliwaonya kwa upole wale wanaofuatia mradi wa uzima wa milele hivi: “Pigeni mbio namna hiyo, ili mpate [thawabu].” (1 Wakorintho 9:24) Paulo alisema kwamba alikuwa ‘akichuchumilia mbele’ (kama mkimbiaji ambaye mwili wake ulikuwa umeinamishwa mbele, akiwa amejikaza kabisa kabisa ili afike mwisho) na ‘kukaza mwendo aufikilie [mradi] wa thawabu ya mwito [wa juu] wa Mungu.’ (Wafilipi 3:13, 14) Ikiwa “mkimbiaji” Mkristo atapokea thawabu, jambo la kukaziwa, au lengo, la kuelekezea maisha yake yote lapasa kuwa zawadi ya uzima wa milele, wala jambo jingine lo lote halipasi kufuatiwa. Je! ndivyo ilivyo na maisha yako?

‘Kuwa wa Nia Hii ya Akili’

3. Kulingana na Wafilipi 3:13, Wakristo waliokomaa wanapaswa kuonyesha nia gani?

3 Kwa ‘kusahau mambo yaliyo nyuma,’ mtume Paulo alionyesha kwamba thawabu hiyo ndiyo iliyokuwa mradi wake wa maana zaidi. Aliyataja “yaliyo nyuma” kuwa “mavi” au “lundo la takataka.” (New World) Huo ulikuwa usemi wenye nguvu tukifikiria yale ambayo Paulo aliacha nyuma alipoingia katika mbio za uzima. (Ona ukurasa 4) Akitafakari juu ya mfano wake mwenyewe, Paulo alisihi hivi: “Basi, kwa kuwa wengi wetu ni wakomavu, na tuwe na nia hii ya akili.”​—Wafilipi 3:5-8, 15, 17, NW.

4. Ni hatua gani ya kwanza inayopasa kufikiwa na (a) watu wenye kupendezwa ambao hawajabatizwa? (b) watu ambao wamebatizwa karibuni?

4 Wale ambao mtume huyo aliwaeleza hayo walikuwa tayari wamekwisha kuingia katika mbio na walikuwa wamefikia kukomaa kwa Kikristo. Lakini namna gani ikiwa hujabatizwa na hivyo ungali unahitaji kuingia katika mbio hiyo? Basi unahitaji kujitahidi kufikia huo kama mradi wa kwanza, kwa maana wale wasiokimbia hawatapokea zawadi ya uzima wa milele. Hata hivyo, ikiwa ndiyo kwanza tu uanze kukimbia katika mbio ya uzima, basi, mradi wako wapasa kuwa kufikia kukomaa kwa Kikristo. Hiyo ingemaanisha kujitahidi kufikia jumla yote ya kweli ya Kikristo na ‘akili zao kuzoezwa kupambanua mema na mabaya.’​—Waebrania 5:14; 6:1.

5. Ni maulizo gani tunayoweza kutumia ili kutambua nia yetu ya akili kuhusu mradi wa uzima?

5 Hata hivyo maneno ya Paulo, “Kwa kuwa wengi wetu ni wakomavu, na tuwe na nia hii ya akili,” yanaonyesha kwamba hata wale ambao wamekomaa wanahitaji kuichunguza ‘nia yao ya akili,’ kwa maana huenda wengine wakawa na “maelekeo mengine ya akili.” (Wafilipi 3:15, NW) Kwa mfano, ni mambo gani uliyoyaacha nyuma? Je! ungali unayaona kama vile Paulo alivyoyaona? Au kupata mambo ya kimwili na ya heshima sana katika ulimwengu kumechukua wakati na fikira zako zaidi? Bila shaka, lazima Mkristo ajitafutie riziki yake mwenyewe na watu wa nyumba yake. Paulo alikuwa akifanya kazi ngumu ya kutengeneza hema—hilo lilikuwa badiliko kubwa sana kutoka kazi kubwa sana aliyokuwa akifanya hapo kwanza. Lakini sasa “thawabu” ilikuwa ndilo jambo kuu maishani mwake, wala si kazi yake ya kimwili. Je! ndivyo ulivyo?​—Matendo 18:3; 20:33, 34.

Mazoezi Katika Utawa

6. Kulingana na 1 Timotheo 4:7, 10, ni mazoezi gani yaliyo ya lazima ili kufikia mradi wa uzima wa milele?

6 Akimshauri Timotheo, mtume Paulo alielekeza fikira kwenye sifa iliyo ya lazima kwa wote wanaotaka kupata “thawabu.” Bila shaka akiwa anakumbuka muda wa miaka mingi unaohitajiwa na wanariadha wa kufanya mazoezi magumu, yeye aliandika hivi: “Nawe ujizoeze kupata utauwa. . . . Kwa mana twajitaabisha na kujitahidi kwa kusudi hili.”​—1 Timotheo 4:7,10.

7. Utawa ni nini, na tunawezaje kuchunguza kichocheo chetu?

7 Utawa unahusu kuambatana na Yehova kibinafsi. Ni vile tulivyo moyoni, wala si lazima uamuliwe na vitendo vyetu vya kidini vya nje.b Kwa hiyo, kwa ukawaida tunahitaji kuchunguza ni kwa sababu gani tunashiriki katika utumishi mtakatifu. Je! ni kwa sababu ya jinsi ambavyo huenda wengine wakafikiri tusiposhiriki? Je! ni kwa kusudi la kutengeneza sifa yenye kuvutia mbele ya watu? Je! ni kwa sababu tu wazazi wetu wanasisitiza? Au je, ni kwa sababu tunataka kumpendeza Mungu? Nyakati nyingine sisi sote tunahitaji kusukumwa kidogo na wengine. Kipimo cha kibinafsi au mpango fulani wa kitengenezo unaweza kuwa kichocheo, walakini yanayofanywa yapasa hasa kuwa “matendo ya utawa.”​—2 Petro 3:11, NW.

8. Ili kusitawisha utawa, ni nini kinachohitajiwa kuongezea funzo la Biblia?

8 Kwa ‘kulishwa na maneno ya imani’ kupitia funzo la Biblia la kibinafsi na la kundi, mtu anaweza kusitawisha utawa. (1 Timotheo 4:6, NW) Lakini mengi zaidi ya kumaliza kusoma kurasa nyingi yanahitajiwa. Jiulize mwenyewe hivi: Jambo hili linaniambia nini juu ya Yehova? Hili lapasa kuhusuje maisha yangu au maoni yangu juu ya wengine? Je! nitafanya yale niliyojifunza? Wakati gani? Kutafakari huko ni sehemu ya mazoezi yetu kuelekea utawa.

9. Ni jambo gani linaloonyesha uhitaji wa kujizoeza wakati wote utawa ukiwa lengo letu?

9 Mwanariadha, anapojizoeza, wakati wote anachanganua jinsi ya kufanya maendeleo. Tukiwa wakimbiaji katika mbio ya Kikristo twapaswa kuwa waangalifu kutochukua vivi hivi ukuzi wetu wa kiroho. Mwanamke mmoja ambaye alikuwa amehudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova toka utotoni, pamoja na kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani, alipata kufahamu kwamba mambo mengine zaidi ya utendaji huo wa kawaida wa Kikristo yalihitajiwa, kwa sababu baadaye alifanya uasherati. Baada ya kulimaliza tatizo hilo, mwanamke huyo alisema: “Nilikuwa nimedhani kwamba nilikuwa mtu wa kiroho, lakini nikatambua kwamba nilikuwa tu nimefuata kawaida ya kufanya mambo. Baada ya anguko langu la kiroho nilianza kufanya funzo la Biblia kwa kadiri kubwa zaidi na kufanya linihusu mimi mwenyewe. Niliomba msaada wa Yehova. Kwa sababu hiyo nikaanza kukua kiroho, kwa mara ya kwanza nikasitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova.”

10. Macho yenye kuthamini yanawezaje kutuvuta karibu zaidi na Yehova?

10 Vilevile jicho linalothamini linahitajiwa. Kwa mfano ukiisha kufurahia kipande cha tunda tamu sana, unaweza kuwaza hivi: ‘Tuna Baba mwema kama nini aliyetoa tunda hili tamu kweli kweli!’ Au ukiisha kutazama kuchwea kwa jua kwenye kuvutia sana, huenda ukatamka hivi: ‘Baba yetu ni fundi kama nini!’ Katika mambo ya kila siku lifanye liwe zoea la kuuona uangalizi wa Yehova. Kwa njia hiyo utamkaribia zaidi.​—1 Wathesalonike 5:18; Yakobo 4:8.

‘Jinyoshe Mbele’​—Bado Si Wakamilifu

11. Je! Mkristo anapaswa kustarehe kwa sababu ya kuwa katika kweli miaka mingi?

11 Wengine katika kundi la Filipi la karne ya kwanza, huenda wakawa walianza kustarehe, wakiwa na maoni kwamba walikuwa wamefikia kiwango kinachofaa cha hali ya kiroho kwa sababu ya kuwa katika ile kweli kwa muda fulani. Paulo alielekeza fikira kwenye mfano wake mwenyewe, kwa kusema: “Si kwamba [mimi mtume, na Mkristo kwa miaka zaidi ya 25] nimekwisha [kupokea zawadi ya kimbingu], au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! bali [naifuatia] . . . Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika.”​— Wafilipi 3:12, 13.

12. Kwa sababu gani Mkristo anapaswa kuendelea kujitahidi kuvaa utu mpya?

12 Wakati wote maisha ya Mkristo yanakuwa na maendeleo. ‘Maendeleo’ ya wakati wote yanahitajiwa ili kuvaa utu mpya. Udhaifu unaoharibu sifa wapasa kupingwa. (1 Timotheo 4:15; 1 Wakorintho 9:27) Shahidi mmoja alieleza wazi kwamba mara nyingi yeye alikuwa mwenye kiburi na alikuwa akikasirishwa kwa urahisi na wengine. Baada ya kushauriwa, alitambua hilo lingeweza kuhatirisha kupata kwake uzima wa milele. “Halafu nikajikaza mno kuwaza inavyofaa juu ya wengine. Baada ya kujilazimisha mwenyewe kwa muda fulani, jambo hilo likawa rahisi zaidi,” ndivyo alivyokubali mwanamke huyo. “Nilipokasirika, nilikuwa nikisali: ‘Sitaki kuwa mtu wa namna hii, Yehova. Unajua hilo ni tatizo kubwa sana kwangu, kwa hiyo tafadhali nisaidie!’ Naye alinisaidia kweli kweli!” Mradi wake ulikuwa kushinda udhaifu fulani na kuonyesha zaidi matunda ya roho ya Mungu. Yeye alibarikiwa hata akastahili kutumika akiwa misionari. Je! kuna miradi ya namna hiyo unayohitaji kufuatia?​—Wagalatia 5:22-26.

13. Jamaa moja ilifikia mradi gani, na ni nini kilichowachochea?

13 Akitambua kwamba bado ‘hajawa mkamilifu’ au kwamba bado hajapokea zawadi ya uzima wa milele, Mkristo anaendelea kuangalia nia yake kuelekea ile huduma. Wenzi wa ndoa katika Marekani walichunguza hali zao. Wakati huo (nyuma katika mwaka 1958) mke alikuwa mwalimu wa shule ya msingi, na mume alikuwa mkurugenzi wa uuzaji mwenye kulipwa shilingi zaidi ya 400 kwa saa moja. “Halafu tukaanza kufikiri juu ya wengine waliotumikia katika makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova ambao walikuwa wameacha utajiri ili watumikie huko bila kulipwa, ili tu kuwaletea kweli watu kama sisi,” ndivyo aliyosema mke. Kwa kuchochewa na mfano huo, wenzi hao waliuza nyumba yao na, wakiwa na watoto wao wawili, wakahamia mahali ambapo uhitaji wa wahubiri wa Ufalme ulikuwa mkubwa zaidi. Wote waliridhika kufanya kazi za chini ili kutegemeza jamaa yao. Sasa maisha yao yote yalikuwa yanazunguka kuwasaidia wengine, kwa kuwa kila mmoja wao alikuwa anaongoza kwa wastani, mafunzo ya Biblia ya kila juma 15 pamoja na watu wenye kupendezwa baada ya muda mfupi. “Tulipata furaha nyingi mno isiyoweza kamwe kununuliwa na pesa. Na hasa tulipendezwa kuona watoto wetu wakikua wakiwa na upendo uo huo kwa Yehova,” akasema mume.​—Wafilipi 4:12, 13.

14. Ni nini baadhi ya miradi ya kibinafsi ambayo wengine wamejitahidi kufikia?

14 Bila shaka, si kila jamaa inayoweza kuhama hivyo. Walakini hesabu yenye kuongezeka wamefanya marekebisho ili kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri, pengine hata kuwa mapainia wasaidizi au wa kawaida. Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1981 kila mwezi, kwa wastani, watu 151,180 walishiriki katika kazi ya painia—kilele kisichopata kufikiwa wakati mwingine na karibu asilimia 10 zaidi ya mwaka uliotangulia! Wengi wamefanya utumishi wa Betheli au misionari uwe mradi wao. Kwa kuongezwa kwa shule za Gileadi katika Meksiko na katika Jamhuri ya Ujeremani, wengi zaidi wameweza kufikia miradi mipya na iliyopanuliwa katika maisha zao za kibinafsi. Na bado wengine wamefanya kazi kwa bidii ili kusitawisha upendo mwingi kwa ajili ya Yehova katika watoto wao. Watu waliojiweka wakf wamejitahidi kufikia kazi ya mtumishi wa huduma, mzee, au hata mwangalizi asafiriye, kwa kukuza sifa za kiroho zinazohitajiwa.​—1 Timotheo 3:1-13.

15. Wake Wakristo wanawezaje kuwasaidia waume wao waweke mbele kabisa mradi wa uzima?

15 Wake Wakristo wanasaidia kwa kuweka “thawabu” hiyo mbele ya kila kitu. “Sitasahau kamwe aliyosema mke wangu niliposoma kwamba watatu wa wanaume niliozoeza wafanye kazi yangu tulipohama walikuwa wamekuwa mamilionea karibuni,” ndivyo alivyosimulia Shahidi aliyetajwa katika fungu la 13. “Yeye [mke] alisema: ‘Pesa ziko leo na kesho hazipo. Tunayofanya kwa kusaidia watu kwa njia ya kiroho yanaleta faida yenye kudumu.’ Sikuzote yeye alinitia moyo nisiingilie kujitafutia hela nyingi tena. Kwa msaada wake tuliingia katika kazi ya mzunguko watoto wetu walipokua.” Ndiyo, wanawake wanaowategemeza waume wao kwa njia ya kiroho wanaweza kuwasaidia kupata “nia njema kutoka Yehova.”​—Mithali 18:22, NW.

Hali Zinatofautiana

16. (a) Mtume Paulo alipoliambia kundi la Filipi, “Hamkupata nafasi,” inaelekea alimaanisha nini? (b) Tunajuaje kwamba Yehova si asiyeridhika kamwe na jitihada za watumishi wake?

16 Kundi la karne ya kwanza la Filipi lilikuwa limekuwa na ukarimu mwingi sana kwa Paulo, walakini kipindi fulani cha wakati kilipita bila ya wao kutoa kitu cho chote cha kimwili. Kwa sababu gani? “Hamkupata nafasi,” ndivyo alivyoandika Paulo. (Wafilipi 4:10) Pengine nyakati zenye magumu, hali zilizobadilika, au wao kutokujua mahali alipokuwa Paulo ni mambo yaliyowazuia kufanya vile mioyo yao ilivyopenda. Vilevile huenda hali zetu zikapunguza tunayoweza kufanya. Yehova anatambua jambo hilo. Kwa mfano, chini ya sheria ya Musa Yehova alikubali toleo lo lote la hatia ambalo mtu angeweza kutoa, hata kama lilikuwa ni vikombe vinane peke yake vya unga! (Mambo ya Walawi 5:5-11) Aliyotaka Mungu tu ni kwamba dhabihu ziwe bora zaidi.​—Kutoka 23:19; Waebrania 13:15, 16.

17. Ni nini yaliyo mambo makuu katika njia yetu ya mbio ya kufuatia mradi wetu wa mwisho, zawadi ya uzima wa milele?

17 Hata hivyo, je, kweli kweli tunampa Yehova yaliyo bora zaidi? Je’ kila siku tunaweka mbele yetu zawadi bora sana ya uzima wa milele? (Linganisha Waebrania 12:1, 2.) Tunaweza kusaidiwa sana kufanya hivyo tukiwa na miradi ya kiroho ambayo tunajitahidi sana kuifikia tunaposonga mbele. Inakuwa mambo makuu katika njia ya mbio yetu. Kama tulivyoona, mojalapo la mambo hayo makuu ni ubatizo. Je! umekwisha kufikia hatua hiyo? Namna gani ukomavu wa Kikristo—kukubali kikweli jumla yote ya kweli ya Kikristo, kutoshuku tena, kutokuuliza-uliza kwa mashaka, kubisha kila wazo jipya linalotolewa? Na je, umekwisha kujifunza kufanya maamuzi ya kila siku kwa msingi wa kanuni za Biblia? Ikiwa ndivyo, umekwisha kutimiza jambo jingine kuu. Je! matunda ya roho yamekwisha kutia mizizi kabisa katika utu wako? Je! huduma ya shambani ina umaana ule ule kwako sawa na ilivyokuwa kwa mfano wetu, Yesu Kristo? Na namna gani juu ya sababu kwa nini unafanya mambo? Je! wewe unachochewa na utawa wa kweli? Ajapokuwa mzee katika kundi la Kikristo, Timotheo alishauriwa kwamba alihitaji kujizoeza mwenyewe jambo hilo likiwa lengo lake. Je! sisi tunafikia miradi hiyo na kujitahidi kufikia mingine, sikuzote zawadi kuu ya uzima wa milele ikiwa mbele yetu? Je! kweli kweli ‘tunachuchumilia yaliyo mbele’?

18. Tunapokea thawabu gani sasa kwa kusitawisha utawa?

18 Zawadi za jitihada hizo ni nyingi. Kama alivyosema Paulo juu ya utawa, “unayo ahadi ya uzima wa sasa.”​ (1 Timotheo 4:8) Kwa ufupi alieleza uradhi tunaoweza kuwa nao sasa hivi ijapokuwa magumu: “Twajua huzuni, hata hivyo furaha yetu haizimiki. . . . Twawabariki wengine wengi kwa utajiri wa kweli. Hatuna hela, na bado kwa kweli tuna kila kitu kinachostahili.”​—2 Wakorintho 6:10, Phillips.

19. Kwa sababu gani kila mmoja wetu anapaswa kuangalia sana jinsi anavyokimbia akifuatia uzima wa milele?

19 Halafu upesi tutafikia mradi wetu wa mwisho—“Uzima utakaokuwapo baadaye.” Paulo angeweza kusema kwa kutarajia zawadi yake ya kimbingu: “Kwa maana nayahesabu mateso ya wakati huu wa sasa kuwa si kitu kama [kwa kulinganisha na] utukufu ule utakaofunuliwa [ndani yetu].” (Warumi 8:18) Ndiyo, kukakamka kote katika mbio hiyo kutakuwa si kitu kukilinganishwa na baraka za thawabu yenye thamani kubwa mno ya uzima wa milele, ama mbinguni ama duniani. Kwa hiyo kaza macho yako juu ya miradi ya kiroho. Kimbia ukiwa na kusudi la kushinda. Kimbia kama kwamba maisha yako mwenyewe yanategemea hilo—kwa maana yanalitegemea!—Zaburi 37:3, 4, 11, 29.

□ Ni mradi gani wa lazima ambao Mkristo anapaswa kujitahidi kuufikia, na tunapaswa kuwa na “nia ya akili” gani juu ya kuufikia?

□ Tunajizoezaje utawa ukiwa lengo letu?

□ Ni nini baadhi ya miradi ya kwanza tunapojitahidi kufikia mradi wa mwisho wa uzima wa milele?

□ Je! ni kusema Yehova haridhiki kamwe na jitihada zetu katika utumishi wake mtakatifu?

[Maelezo ya Chini]

a Uchunguzi wa mtunga mashairi wa kale Mgiriki Pindar katika kitabu chake Isthmian Odes, I 40-50.

b Neno la awali la Kigiriki, eusebeia, lilitumiwa wakati huo na mwanafalsafa Filo kueleza mtu wa kidini kweli kweli tofauti na mwabudu “bandia” ambaye alionyesha tu vitendo vingi vya kidini vya nje-nje.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kuna miradi ya kwanza katika mwendo wetu wa Kikristo tunapojitahidi sana kufikia mradi wa mwisho wa uzima wa milele

Utawa

Ukomavu

Ubatizo

Huduma Kubwa Zaidi

Matunda Zaidi ya Roho Takatifu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki